Featured Post

UNATAKA KUCHIMBIWA KISIMA KWA MKOPO KWA AJILI YA UMWAGILIAJI? SOMA HAPA…



Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini Blog
SHIRIKISHO la Vyama vya Ushirika nchini (TFC) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali lina mpango wa kuwachimbia visima virefu wananchi ili kuwawezesha kuendesha kilimo cha umwagiliaji nchini.

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirika wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC Ltd), Bw. Henry Mwatwinza Mwimbe, ameieleza MaendeleoVijijini kwamba, lengo la mpango huo ni kuwafanya wakulima kote nchini kuendesha kilimo cha uhakika na endelevu badala ya kutegemea mvua za msimu peke yake.
“Kilimo ndio uti wa mgongo wa uchumi wa taifa letu na katika kutekeleza kauli mbiu ya Tanzania ya Viwanda ni lazima malighafi zipatikane kupitia kilimo, hivyo tumeona ni vyema kwa kushirikiana na wadau mbalimbali tuanzishe mpango huu ambao siyo tu utamkomboa mkulima, bali utaongeza hata pato la taifa kutokana na uzalishaji wake,” alisema Mwimbe.
MaendeleoVijijini inatambua kwamba, kupitia mpango huo hata mikoa inayotajwa kuwa ni nusu-jangwa hasa ya Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga na Simiyu inaweza kugeuka kijani kibichi kupitia kilimo cha umwagiliaji.
Uchunguzi wa MaendeleoVijijini umebaini kwamba, vyanzo vya maji vipo vya kutosha, yakiwemo maji ya ardhini, lakini wakulima wengi hawana uwezo na nyenzo za kuchima visima ama mabwawa ili kuwawezesha kuwa na maji ya uhakika ya kuendeshea kilimo hicho.
“Mpango huu ukifanikiwa maeneo mengi nchini, hata yale ambayo yametelekezwa kwa sababu ya ukame, yatatumika kwa kilimo na kwa maana hiyo hali ya uchumi ya kaya, jamii na taifa itakua ili kutekeleza Malengo Endelevu ya Dunia pamoja na Mpango wa Taifa wa Maendeleo kuelekea mwaka 2025,” aliongeza Mwimbe.
Hata hivyo, amesema kwamba, ikiwa mipango itakwenda vyema, wanakusudia uchimbaji wa visima hivyo uanze mwaka 2018 ili hadi kufikia mwaka 2019 wananchi waanze kujikita kwenye kilimo hicho cha umwagiliaji.
Mwimbe amesema kwamba, anaamini mikoa mingi inaweza kushughulika na kilimo cha mazao ya kila aina ikiwa tu uhakika wa maji utakuwepo.
MaendeleoVijijini inatambua kwamba, eneo la Kardesh-barnea katika Israel, ambalo lilikuwa jangwa, kame na lililojaa mawe, hivi sasa ndilo linalobeba uchumi wa kilimo wa taifa hilo katika Mashariki ya Kati kutokana na kilimo cha umwagiliaji, teknolojia ambayo kama itatumika nchini Tanzania inaweza kubadili taswira ya mikoa kama Tabora, Shinyanga, Simiyu, Singida, Dodoma na Manyara ambayo ni nusu-jangwa.

Nani wanastahili?
Ili wakulima hao waweze kuchimbiwa visima, kwa mujibu wa Mwimbe, ni lazima wazingatie masharti haya yafuatayo:

MASHARTI YA KUCHIMBIWA KISIMA KWA MKOPO KWA AJILI YA KILIMO CHA UMWAGILIAJI KWA VYAMA VYA USHIRIKA TANZANIA BARA.
                                                                                      
1.       Muombaji ni lazima awe Chama cha Ushirika kilichosajiliwa Tanzania Bara.
·         Kwa sheria ya vyama vya ushirika iliyopo.
·         Kina wanachama wanaojishughulisha na kilimo cha mazao mbalimbali ya muda mfupi (mwezi 1 hadi miezi 6).
·         Kiwe na ardhi inayomilikiwa na chama (kwa ushahidi wa maandishi mfano Hati ya Ardhi(Kiserikali au kimila).
·         Wanachama wote wakubaliane kudhaminiana mkopo huu miongoni mwao ili ikitokea mmojawapo anashindwa kurejesha basi wanaobaki watabeba mzigo huo.
2.      Chama hicho lazima kiwe mwanachama hai wa TFC au kiwe mwanachama wa chama cha upili (UNION) ambacho ni mwanachama hai wa TFC.
3.      Wanachama wakubali kulipa 15% ya gharama za kisima kabla ya kazi ya kuchimba kuanza.
·      Hii itajumlishwa katika marejesho ya mkopo yatakayofanywa.

4.      Uchimbaji utafanyika baada ya kupatikana kwa taarifa inayohusu upatikanaji wa maji katika eneo husika (Itakayofanywa na TFC kwa gharama za chama husika).
5.      Udongo wa shamba husika utapimwa ili kujua aina ya mazao yanayoweza kustawi na kushauri ipasavyo juu ya nini cha kufanya ili kuiwezesha ardhi kustawisha zao au mazao yanayotakiwa kulimwa.
6.      Mazao yanayotakiwa kulimwa ni ya muda mfupi (miezi 1-4) tangu kupandwa hadi kuvunwa kwa kipindi chote cha mkataba ambapo mkopo unaendelea kurejeshwa. Mabadiliko ya mazao ya kulimwa yanaweza kufanyika wakati wowote baada ya deni kulipwa.
7.      Marejesho ya mkopo yatafanyika kupitia mauzo ya mavuno yanayopatikana katika kila msimu wa mavuno.
8.     Muda wa marejesho ya mkopo hautazidi miaka mitatu (miezi 36) tangu kuanza kwa msimu wa kilimo.
9.      Marejesho ya mkopo yatakuwa kupitia benki ya NMB au Mitandao ya Simu kwa utaratibu utakaotolewa baada ya kuingia mkataba wa kuchimbiwa kisima.
·         (Kuna uwezekano wa kupata mkopo kutoka benki kwa chama ambacho kinaendesha kilimo cha umwagiliaji hasa ikiwa tayari kina kisima cha maji).

Kwa taarifa zaidi:
Wasiliana: +255 656 331974 au +255 716 775334. Barua-pepe: maendeleovijijini@gmail.com.


Comments