Featured Post

JINSI YA KUANZISHA CHAMA CHA USHIRIKA

 Zao la korosho ambalo linachangia uchumi katika mikoa ya Kusini mwa Tanzania.

USHIRIKA ni dhana ya kuleta maendeleo kwa kushirikiana. Dhana hii imefanikiwa kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii katika kipindi cha miaka kadhaa iliyopita. Kutokana na changamoto mbalimbali zilizoikumba sekta hii ya ushirika watu wengi wamekosa imani na vyama hivi na baadhi ya vyama vimeshindwa kufanya kazi vizuri.

Hata hivyo, kwa sasa imani kwa vyama vya ushirika imeongezeka na vyama vingi vinaendelea kuundwa hasa vile vya kuweka na kukopa, yaani SACCOS.
Uanzishwaji wa vyama vingi vya ushirika kwa sasa unatokana na elimu watu wengi waliyoipata kuhusu Ushirika na watu kuelewa kuwa changamoto zilizoko ndani ya ushirika zinatatulika.
Ushirika dhamira yake ni nzuri na kama itafanya kazi vizuri ni njia nzuri ya kuleta mabadiliko kwa watu wengi.

Ushirika ni nini?
Ushirika maana yake ni muungano wa watu ambao wanafanya kazi pamoja kwa hiari ili kufanikisha mahitaji yao ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kupitia shughuli ya biashara inayomilikiwa kwa pamoja na kudhibitiwa kidemokrasia.
Ushirika unazingatia maadili ya kujisaidia wenyewe, jukumu binafsi, demokrasia, usawa na mshikamano.
Wanachama wa Ushirika wanaamini katika misingi ya uaminifu, uwazi, uwajibikaji kwa jamii na kuwajali wengine.
Muundo wa Ushirika kwa ujumla unategemea uimara wa chama cha msingi cha Ushirika, hivyo kuna umuhimu wa kuhakikisha vyama imara vya msingi vinaanzishwa.
Kwa kuzingatia hayo, msisitizo usiwekwe kwenye uanzishwaji wa vyama vikuu vya Ushirika, lakini kuwepo na uwezeshaji wa wanachama katika vyama vya msingi kwa lengo la kuunda chama imara cha msingi.
Kukiwa na chama imara cha msingi, chama hiki kinaweza kuunda chama kikuu kilicho imara.
Leo la kuwa na vyama imara vya msingi litatimia kama kutakuwa na jjuhudi za makusudi kuimarisha vyama vya msingi vilivyopo.
Vyama hivi vinaweza kuimarika kunapokuwa na kuongezeka kwa wanachama, uwajibikaji wa viongozi na demokrasia katika maamuzi yanayohusu chama.
Kwa kuzingatia hiyo, Vyama vya Ushirika nchini vitakuwa imara na faida kwa wanachama.

MIKUTANO YA UCHAGUZI WA KAMATI YA KUUNDA CHAMA
Watu wanaopenda kuunda chama cha Ushirika kiwe cha msingi, umoja wa kibiashara au shirika, chama kikuu, muungano wa vyama vikuu au shirikisho, watakuwa chini ya uenyekiti wa Ofisa Ushirika aliyeteuliwa na Mrajis kwa madhumuni ya kuchagua kamati ya kuunda chama.
Kamati ya kuunda chama haitakuwa na wajumbe chini ya idadi ya wanachama wanaotakiwa kuunda chama.
Kila kamati ya kuunda chama itamchagua Mwenyekiti na kuteua Katibu na itatunza kumbukumbu za shughuli zake.

Kazi za kamati ya kuunda chama:
  1. Kufikiria kwa makini aina ya chama kinachotarajiwa kuundwa na kuweka madhumuni yake.
  2. Kukadiria idadi ya wanachama watakaojiunga na ukubwa wa shughuli zitakazofanyika.
  3. Kwa msaada wa Ofisa Ushirika na ambapo ni lazima mtu yeyote mwenye ujuzi, kufanya uchambuzi wa uhai wa kiuchumi wa shughuli  zitakazofanywa na chama kinachotarajiwa kuundwa.
  4. Kuandaa taarifa ya uwezekano wa kufanya kazi kwa ajjili ya kuitumia kwa Mrajis.
  5. Kuandaa orodha ya wanachama wanaotazamiwa na kiasi cha hisa au michango inayotarajiwa.
  6. Kuandaa masharti yanayofaa ya chama kinachotarajiwa wakishauriana na Ofisa Ushirika.
  7. Kufanya shughuli nyingine kama itakavyolazimu kwa ajili ya kuomba kuandikishwa kwa chama hicho kinachotarajiwa.

KUANDIKISHWA KWA CHAMA
Kila  chama kinachoomba kuandikishwa lazima kikubaliane na kifungu cha 24 cha Sheria na kitapeleka maombi kwa Mrajis kwa kutumia fomu zilizoagizwa na kanuni.
Kila maombi ya kuandikisha chama cha Ushirika yatatiwa sahihi ipasavyo kwa niaba yake na watu waliochaguliwa na kamati kuunda chama. Maombi yanatakiwa kuambatana na:
  1. Muhtasari wa mkutano uliothibitishwa wenye azimio la kuunda chama.
  2. Nakala nne za masharti ya chama yaliyokubalika.
  3. Nakala nne za taarifa ya uwezekano wa kufanya kazi kwa mradi kama ilivyotajwa katika Kifungu cha 6 cha Kanuni.

Mrajis atakaporudisha maombi atarudisha kwa chama:
  1. Nakala moja ya masharti pamoja na maombi ya kuandikisha chama yaliyotiwa muhuri maalumu pamoja na cheti cha kuandikishwa.
  2. Nakala moja ya taarifa ya uwezekano wa kufanya kazi au uchambuzi wa mradi ulioidhinishwa kwa kupiga muhuri.
  3. Nakala moja ya bajeti ya mapato na matumizi ikiwa ni makisio ya kwanza ya chama hicho.

MRAJIS ANAWEZA KUONGEZA MASHARTI MENGINE KABLA YA KUANDIKISHWA
Ili kuweza kuamua kama chama kinachotarajiwa kuandikishwa kina uhai wa kiuchumi ama vinginevyo, Mrajis anaweza kuagiza moja au zaidi ya mahitaji yafuatayo kabla hajakiandikisha chama:
  1. Kwamba taarifa za ziada zitolewe kuonyesha kama chama kinachokusudiwa kuundwa kinatimiza mahitaji ya kiuchumi au kijamii na uwezekano wa kufikia/kutimiza madhumuni yake.
  2. Kwamba maombi ya kuandikishwa yanaungwa mkono na wanachama wengi ambao wanatarajia kuwa wanachama siku za usoni.
  3. Kwamba mtaji wa kutosha unatolewa na waombaji waanzilishi kwa ajili ya kuanzisha chama na watu wengine wanaotarajia kujiunga na chama na kwamba mtaji huo unatosha kuanzisha shughuli za chama.
  4. Kwamba mipango inafanyika kwa ajili ya kuwaelimisha na kushauri hasa kuhusu kanuni na shughuli za Ushirika na mashumuni ya chama kwa wanachama waanzilishi na watu wengine wanaotarajiwa kuwa wanachama siku za usoni.
  5. Kwamba kuna uwezekano mkubwa wa upatikanaji wa maofisa watakaomudu kuongoza na kuelekeza shughuli za chama kinachotarajiwa na kutunza kwa usiri kumbukumbu za vitabu vya hesabu kama ilivyoagzwa na Mrajis chini ya Sheria ya Vyama vya Ushirika na ikibidi maofisa wapatiwe mafunzo ya ziada kama Mrajis atakavyoona inafaa.

TAARIFA ZA KUKATAA KUANDIKISHA CHAMA
Endapo Mrajis atakataa kukiandikisha chama atatoa masharti yake, sababu zake za uamuzi huo kwa maandishi.

HAKI NA WAJIBU WA WANACHAMA
Wanachama katika chama cha ushirika watakuwa ni:
  1. Watu waliojiunga wakati wa kuomba chama kiandikishwe (waannzilishi).
  2. Watu walioingizwa uanachama kufuatana na masharti ya chama.
  3. Watu waliofikia umri wa miaka 18 na wenye akili timamu na ambao wanafanya biashara au shughuli zinazohusiana na madhumuni ya chama na wana mahitaji ambayo chama kinatazamia kukidhi na wana uwezo wa kulipa viingilio na kununua hisa.
  4. Watu ambao hawajafikia umri wa miaka 18 lakini wametimiza umri wa miaka 15 wanaojulikana kama watoto wanaweza kujiunga na chama cha Ushirika kufuatana na kifungu kidogo cha 3 na 4 cha Kifungu cha 15 cha Sheria ya Vyama vvya Ushirika.

HAKI ZA WANACHAMA
Wanachama watakuwa na haki zifuatazo:
  1. Haki ya kupiga na kupigiwa kura, kuhudhuria mikutano, kushiriki katika uongozi wa chama na haki ya kuitisha mikutano kwa mujibu wa masharti ya chama.
  2. Hakuna mwanachama wa chama cha Ushirika atakayetumia haki za uanachama mpaka awe amelipa kiingilio, hisa na madeni mengine chamani.
  3. Kila chama kitaweka ukomo wa idadi ya wanachama kufuatana na shughuli zake kwa mujibu wa Kifungu cha 15 na 23 (2) cha Sheria ya Vyama vya Ushirika.
  4. Hakuna kampuni iliyounganishwa au iliyoandikishwa chini ya Sheria ya Makampuni na hakuna kampuni ambayo haikuunganishwa au kikundi cha watu kilichoandikishwa kitakuwa na haki ya kuwa mwanachama wa chama cha Ushirika kilichoandikishwa isipokuwa kwa kibali cha maandishi kutoka kwa Mrajis kwa masharti kuwa:
a)                 Kampuni hiyo au kikundi hicho kimeonyesha nia ya kutumia huduma zitolewazo na chama, na Mrajis ameridhika na hatua hiyo.
b)                 Uanachama wa kampuni hiyo au kikundi hicho utakubaliana na sheria, kanuni na masharti ya chama cha Ushirika.
c)                  Chaka kitafaidika kutokana na huduma zitolewazo na kampuni hiyo.

HAKI ZA WATOTO
  1. Mtoto anaweza kuwa mwanachama ilimradi wazazi au mlezi wa mtoto wana taarifa kuhusu shauku yake ya kuwa mwanachama na atafungua hesabu ya hisa au kiingilio na kununua hisa kama itakavyokuwa.
  2. Ambapo mzazi au mlezi amearifiwa kuhusu hesabu ya hisa au amana zinazomilikiwa na mtoto na hakuna vikwazo vyovyote vilivyowekwa na chama katika hesabu hiyo, mtoto huyo anaweza kuongeza amana hizo na anaweza kupunguza fedha hizo kutoka katika hesabu hizo au kuzitumia kwa njjia yoyote ile kama itakavyoonekana inafaa bila ya kibali cha mzazi au mlezi wake.
  3. Mtoto ambaye anatumia huduma za chama kufuatana na kifungu kidogo cha (2, 3) na (4) cha Kifungu cha 15 cha Sheria atakuwa na haki ya uanachama isipokuwa hatakuwa na haki ya kupiga kura.
  4. Kwa masharti kwamba kipengele hiki cha kanuni hakitahusu chama cha Ushirika cha shule.

Kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Ushirika Na. 6 ya 2013, watu 20 wanaweza kuanzisha ushirika wa mazao na 50 wanaweza kuanzisha ushirika wa akiba na mikopo (SACCOS).
Hata hivyo, kadiri idadi ya watu inavyoongezeka ndivyo chama kinavyokuwa na fursa kubwa zaidi ya kujenga mtaji, mfuko wa kukopeshana, kuzalisha mazao kwa wingi na kupanua soko au wateja wanaohudumiwa.
Baada ya wananchi kwa hiari yao wenyewe, kuamua kuanzisha Chama cha Ushirika watatoa taarifa kwa Ofisa Ushirika wa eneo husika aje kutoa mwongozo au maelekezo ya uanzishwaji wa chama. 

Zifuatazo ni hatua za kuanzisha chama cha Ushirika:

1. Mkutano mkuu wa uanzilishi.
Kikundi au wananchi huitisha mkutano mkuu wa uanzilishi ambapo Afisa ushirika ndiye anakuwa mwenyekiti wa mkutano huo. Malengo makuu ya mkutano huo ni, kutoa ufafanuzi wa maana ya ushirika, faida za ushirika, nia ya uanzilishi wa chama, mgawanyo wa faida, haki na wajibu wa wanachama.

2. Uchaguzi wa bodi ya uanzilishi.
Wanachama huteua bodi ya uanzilishi ambayo huundwa na wanachama 5-9, ambao watakuwa na majukumu yafuatayo:
·                     Kushirikiana na afisa ushirika kutayarisha masharti (Katiba) na Sera mbalimbali za chama cha ushirika.
·                     Kutayarisha taarifa ya uwezo wa kiuchumi wa chama (kidadishi uchumi)
·                     Kuandaa mpango biashara
·                     Kuandaa makisio ya mapato na matumizi ya chama ya mwaka wa kwanza
·                     Kuhamasisha wananchi wengi zaidi kujiunga, kukusanya viingilio, kupokea fedha za Hisa, Akiba na Amana.
·                     Kutafuata ofisi ya chama na kununua vitendea kazi.
·                     Kuajiri mtunza vitabu/karani
·                     Kufanya mambo mengine muhimu ya uanzishwaji wa chama.
3. Kuwasilisha maombi ya usajili wa chama kwa Mrajis Msaidizi kupitia kwa Ofisa Ushirika wa Wilaya.
4. Mkutano mkuu wa kwanza.
Mkutano mkuu wa chama utaitishwa katika kipindi cha miezi miwili baada ya kupata usajili kwa madhumuni ya kukabidhiwa hati ya usajili kutoka kwa OfisaUshirika na mambo mengineyo.

Kwa maelezo zaidi na ushauri kuhusiana na uanzilishi na uendeshaji wa chama cha ushirika wasiliana na blogu hii kwa simu +255 656 331974 au Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirika wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC) simu namba +255 716 775 334. Au barua-pepe: maendeleovijijini@gmail.com.


Comments