Featured Post

GLORY NA MARTHA KUTOKA NGANZA WAIBUKA VINARA WA TUZO YA YST 2020

 

Glory Kirochi na Martha Machumu kutoka Shule ya Sekondari ya Wasichana Nganza iliyopo jijini Mwanza, wakiwa wameshikilia kikombe walichokabidhiwa baada ya kuibuka washindi wa  tuzo ya wanasayansi chipukizi inayotolewa na Taasisi ya Young Scientists Tanzania (YST), Agosti 2, 2020. (Picha kwa hisani ya YST).                 

Na Mwandishi Wetu

Glory Kirochi na Martha Machumu kutoka Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Nganza iliyopo jijini Mwanza, ndio vinara wa Tuzo ya Wanasayansi Chipukizi inayotolewa na Taasisi ya Young Scientists Tanzania (YST), kwa mwaka 2020.

Glory na Martha wamenyakua tuzo hiyo kutokana na wazo lao la kubuni Namna ya Kuzalisha Chakula cha Mifugo kwa kutumia teknolojia ya Hydroponic Fodder inayokidhi mazingira ya ukame.

Kutokana na ushindi huo, Glory na Martha wamejinyakulia kikombe kikubwa, ngao, medali za dhahabu na fedha taslimu Sh. 1,350,000, huku pia wakipata ufadhili wa masomo ya chuo kikuu kupitia taasisi ya Karimjee Jivanjee.

Nafasi ya pili imechukuliwa na Albert Mhagama na Stella Kasalla kutoka Shule ya Kisimili mkoani Arusha katika ambao walipata kikombe, ngao, medali za fedha pamoja na fedha taslimu Sh. 900,000.

Katika mashindano hayo ya 10 tangu kuanzishwa kwa taasisi ya YST, wanafunzi Yvonne Rio na Dorris Kilonzo kutoka Shule ya Sekondari Rugambwa iliyoko mkoani Kagera, walinyakua Tuzo ya Kumbukumbu ya Hatim Karimjee kutokana na mradi wa Kuboresha Usalama wa Ndani ya Gari, ambapo pia walipata fedha taslimu shilingi milioni moja, ngao na medali.

Kwa upande mwingine, Lameck Obeid na Dennis Ndahaje kutoka Shule ya Sekondari ya Katubuka iliyopo Kigoma walipata ufadhili wa masomo baada ya kubuni mradi wa ‘Siri kwa nini Wanafunzi Wanaotoka Familia Duni Wanashindwa Kufikia Malengo ya Elimu’.

Kwa mwaka 2020 tuzo hizo zimetolewa kwa njia ya mtandao kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona.

Akizungumza katika utoaji wa Tuzo hizo kutoka jijini Dar es Salaam Agosti 2, 2020, Mwanzilishi mwenza wa YST, Dkt. Gozbert Kamugisha, amesema ugonjwa wa Covid-19 umesababisha changamoto kubwa ikiwemo kuharibu kuharibu mawasiliano na maonesho ya sayansi.

“Kutokana na hali hii, tulilazimika kubadilisha mifumo yetu na kutumia njia za kidigitali kuwafikia wanafunzi na majiji kukagua kazi hizo na kufanya maamuzi kupitia mtandao,” amesema Kamugisha.

Kwa kawaida, maonesho hayo hufanyika kila mwaka kwa lengo la kuongeza chachu kwa wanafunzi kupenda masomo ya sayansi, huku wakibuni miradi mingi katika sayansi ya jamii, teknolojia na kadhalika.

Hata hivyo, Dkt. Kamugisha amesema wanayo mengi ya kujivunia katika kipindi cha miaka 10 tangu kuanzishwa kwa YST, ambapo katika kipindi hicho wameweza kuzifikia shule nyingi na kuleta mabadiliko makubwa katika nyanja ya sayansi na teknolojia.

“Kwa kweli jamii imehamasika sana, na kupitia kupitia maonesho haya ya sayansi, wanafunzi wamekuwa wakibuni miradi mbalimbali ya kisayansi ambayo inaweza kutoa suluhu kwa jamii kulingana na dhana halisi ya maisha,” alisema Dkt. Kamugisha.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Karimjee Jivanjee ambao ndio wadhamini wakuu wa maonesho hayo, Yusufu Karimjee, amesema hadi kufikia mwaka 2019 jumla ya wanafunzi 29 waliofanya vizuri katika maonesho ya YST wanafadhiliwa masomo yao ya elimu ya juu.

“KJF tunaamini katika kuwawezesha vijana kupata elimu, ndio maana tunawasaidia wanasayansi chipukizi kuonesha vipaji na ubunifu ili kuleta maendeleo Tanzania,” amesema Yusufu.

Katika mashindano ya mwaka 2020, takriban mada 600 ziliwasilishwa kutoka shule mbalimbali za Tanzania Bara na Visiwani.

Katika Zawadi za Vipengele (Category Awards):

Teknolojia na Sayansi ya Kompyuta:

Washindi wa kwanza ni Fatma Hassan Saleh na Najma Khamis Malik kutoka Shule ya Sekondari Benbella – Unguja, washindi wa pili ni Innocent Jisena Revocatus na Morice James Kurusanga kutoka Shule ya Sekondari Kibaha; na washindi wa tatu ni Beastus Banelt Majubu na Darwin Stephano Twalale kutoka Shule ya Sekondari ya Wavulana Bwiru ya jijini Mwanza.

Sayansi ya Kilimo:

Washindi wa kwanza ni Spencer Salvatory Minja na Masalu Ernest Masalu kutoka Shule ya Wavulana Kibiti; washindi wa pili ni Rehema Herman Chonde na Abdurazaki Yusuphu Saidi kutoka Mitengo Sekondari – Mtwara; na washindi wa tatu ni Simon Jimmy Kayumba na Alfred Godfrey Katonkola kutoka Kipande Sekondari – Rukwa.

Sayansi ya Baiolojia:

Washindi wa kwanza ni  Elvira Godfrey Kalulu na Maria Anthonia Richard Kapinye  kutoka Pandahill Sekondari – Mbeya; washindi wa pili ni Gracejacqueline Helmas Karatta na Regina Patrick Sawa kutoka Kisimiri Sekondari – Arusha; na washindi wa tatu ni Charles Barnabas Bugeshi na Mujuni Boniphace Mutasingwa kutoka Ilboru Sekondari – Arusha.

Sayansi ya Jamii:

Washindi wa kwanza ni Mary Satiel Mshana na Herman Aidan Ngogo kutoka Mawelewele Sekondari – Iringa; washindi wa pili ni Gloria Martin Mwakalembusya na Calister Michael Sanga kutoka Kisimiri Sekondari – Arusha; na washindi wa tatu ni Gloria Ibrahim Mbonde na Zawadi  Mohamed Mkai kutoka Kikuyu Sekondari – Dodoma.

Sayansi ya Fizikia, Kemia na Hisabati:

Washindi wa kwanza ni Abdul-majid Salum Moh'd na Mathna Khamis Abdul-rahman kutoka Lumumba Sekondari – Unguja; washindi wa pili ni Elian Deogratius Rutazaa na Salma Said Chammah kutoka St. Peter Claver Sekondari – Dodoma; washindi wa tatu ni Moza Rashid Said na Nassbah Mohamed Khalfan kutoka Kiembe Samaki A Sekondari – Unguja.

Sayansi ya Mabadiliko ya Tabianchi na Mazingira:

Washindi wa kwanza ni Zainab Omar Hussein na Swabra Zahor Vuai kutoka Benbella Sekondari – Unguja; Faith Zictor Madulu na Irene Deudatus Mbeleka kutoka Msalato Girls Sekondari – Dodoma; na washindi wa tatu ni Ivan John Nyaindi na Michael Gido Jengela kutoka Marian Boys Sekondari – Pwani.

Tuzo Maalum:

Speedy Print Award:

Washindi ni Rahma Hamza Ally na Winfrida William Achiro kutoka Mtwara Girls Sekondari.

National Institute For Medical Research Award:

Washindi ni Bazilio Yesaya Kaonde na Mpoki Pius Peter kutoka Kizwite Sekondari – Rukwa.

Muhimbili University Of Health And Allied Sciences Award:

Washindi ni Mathias Kasuku na Kenyata T. Kenyata kutoka Rungwa Sekondari – Katavi.

University Of Dar Es Salaam Award:

Washindi ni Lilian Mugeta Magudira na Razer Omary Semunyu kutoka Tabora Girls Sekondari – Tabora.

First Car Rental Award:

Washindi ni Fatma Shomari Mbwana na Upendo Helbert Mwalongo kutoka Loleza Sekondari – Mbeya.

Realising Education For Development Award:

Washindi ni Mabula Guliga Gamaya na Edbily Ndenga Nickson kutoka Bariadi Sekondari – Simiyu.

Regional Coordinator Award:                

Washindi ni Zainabu Juma Shamte na Nurath Mohamedi Makota kutoka Mkonge Sekondari – Lindi.

The YST Teacher Award:

Mshindi ni Emmanuel Athumani Peter kutoka Kisimiri Sekondari – Arusha.

YST Hatim Karimjee Perpetual Trophy:

Washindi ni Ivonne Emmanuel Urio na Doris Cliff Kilonzo kutoka Rugambwa Sekondari mkoani Kagera kwa wazo lao la “Improving A Cars Safety - A Car Black Box”.

Special Education Scholarships:

Washindi ni Lameck Silas Obeid na Denis Cosmas Mpahaje kutoka Kabutuka Sekondari – Kigoma.

Comments