Featured Post

JENERALI MSTAAFU AWAVISHA VYEO VIPYA VIONGOZI WAPYA TANAPA

Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA Dk. Allan Kijazi akishuhudia uvishwaji wa cheo kwa Naibu Kamishna wa  Uhifadhi na Maendeleo wa TANAPA William Mwakilema uliofanywa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania TANAPA, Jenerali Mstaafu George Waitara.

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii
Mweyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Shirika la Hifadhi za Taifa ,Jenerali (Mstaafu) George Waitara amezindua mfumo mpya wa utendaji kazi ndani ya Hifadhi za Taifa unaopeleka madaraka zaidi katika ngazi ya Kanda nne kuu zilizoundwa ili kuboresha utendaji kazi unaoendana na mfumo mpya wa jeshi -usu.
Uzinduzi huo ulienda sambamba na zoezi la utoaji vyeo vipya vilivyoidhinishwa na bodi ya wadhamini kwa viongozi wa shirika ambao ni Naibu Kamishna wa Uhifadhi wawili, Makamishna wa Uhifadhi wa kanda wanne, Makamishna Wasaidizi Waandamizi 14, Makamishna wasaidizi 22 pamoja na Maafisa Wakuu na Waandamizi saba.
Muundo mpya unahusisha Kanda ya Kaskazini yenye Hifadhi za Arusha, Tarangire, Ziwa Manyara, Kilimanjaro na Mkomazi ,Kanda ya mashariki inayojumuisha Hifadhi za Saadan, Mikumi na Udzungwa, Hifadhi za Ruaha na Kitulo na Katavi zitakuwa chini ya usimamizi wa  kanda ya Kusini.
Kanda ya Magharibi itasimamia Hifadhi za Taifa za Gombe, Mahale, Kisiwa cha Saanane, Kisiwa cha Rubondo, Serengeti pamoja na Hifadhi mpya za Burigi, Kimisi, Biharamulo, Ibanda na Rumanyika.
Hafla hiyo pia imeendana na zoezi la kuwatunuku vyeti wahitimu 217 wa mafunzo yaliyochukua miezi sita kwa awamu mbili yakihusisha Maafisa wa Uhifadhi pamoja na waajiriwa wapya.
Lengo kuu la mafunzo hayo ni kuwawezesha wahitimu kufanya kazi  kwa mfumo wa kijeshi -usu katika kuboresha utendaji kazi na majukumu ya usimamizi thabiti wa maliasili zilizopo hifadhini kwa kuwajengea wahitimu uwezo wa kimwili ,kisaikolojia,kimaadili na uzalendo.

Comments