Featured Post

DKT. MABULA: KUWENI NA MIPANGO ENDELEVU KUEPUKA UBOMOAJI NYUMBA


Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk. Angeline Mabula akisalimiana na Msajili wa Bodi ya Usajili Wataalamu Mipango Miji Hellen Mtutwa alipokwenda kufunga Mkutano wa tano wa Bodi jana jijini Dodoma, kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi Welbert Kombe.

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk. Angeline Mabula akifunga mkutano wa tano wa Bodi ya Usajili Wataalamu wa Mipango Miji jijini Dodoma Jana.
Sehemu wa washiriki wa Mkutano wa tano wa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Mipango Miji  uliofanyika jijini Dodoma. (Picha zote na Hassan Mabuye wa Wizara ya Ardhi)



Na Munir Shemweta, Dodoma
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk Angeline Mbaula amewataka wataalamu wa mipango miji kuwa na mipango endelevu  na kabambe katika miji na halmashauri zote nchini ili kuwa na miji iliyopangika na kuepuka ubomoaji nyumba za wananchi unaosababishwa na uelewa mdogo wa sheria na taratibu za mipango miji..
Aliwataka wataalamu wa mipango miji kuwajibika ipasavyo katika kutekeleza majukumu yao   kuepesha wananchi kuvunja sheria unaosababishwa na wataalamu kutowaeleza ambapo alisema si kila mwananchi anayevunja sheria za ujenzi mjini anafanya makusudi bali wengine hawajui sheria na taratibu na kuhitaji kuelezwa.
Akizungumza wakati wa kufunga mkutano wa tano wa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Mipango Miji  jijini Dodoma jana, Dk Mabula alesema maeneo mengi ya miji wataalamu wanahangaika na kazi ya kurasimisha jambo ambalo siyo suluhisho la upangaji miji bali ni kujaribu kuweka viraka katika vazi lililochakavu.
Akigeukia suala la kuwepo maeneo mengi yasiyopangwa, kupimwa na kumilikishwa Dk. Mabula alisema eneo hilo linaibua changamoto mbalimbali kwa jamii ikiwemo ongezeko la  makazi holela maeneo ya mijini, kukua kwa miji isiyo na mpangilio mzuri pamoja na kukithiri kwa migogoro ya ardhi nchini na kuwashauri wataalamu hao wa Mipango mijini nchini kuwafuata wananchi waliko kwa ajili ya kutatua kero zao.
Alizitaka halmashauri ambazo muda wa mipango yake kabambe imeisha kuhakikisha  zinahuisha mipango hiyo ili kuwa endelevu kwa minajili ya kuweka miji salama na ikiwa imeandaliwa miundo mbinu muhimu kwa mustakabali wa maendeleo ya miji na taifa kwa ujumla.
Aidha, Dk. Mabula ametaka maeneo ambayo reli ya SGR inapita ni vyema halmashauri za maeneo husika kuanza kufanya upangaji mapema ili reli itakapoanza maeneo yote yawe yamepangwa, yamepimwa na yamemilikishwa na uendelezaji umefanyika ili kuinua uchumi kwa maeneo husika na kutosubiri wajanja wakaanza kuvamia.
Katika maazimio yake yaliyosomwa na Msajili wa Bodi ya Usajili wa Wataalamu Mipango Miji Hellen Mtutwa, Washiriki walikubaliana Chuo Kikuu cha Ardhi kwa kushirikiana na Bodi ya Usajili Wataalamu Mipango Miji kuandaa muongozo utakaowawezesha Watendaji wa Kata na Vijiji kuwa wasimamizi wa mipango  miji kwenye maeneo yao ili kuepuka ujenzi holela na miji isiyopangwa.
Aidha, Washiriki walikubaliana urasimishaji wa makazi ufanayike katika maeneo yote ya nchi na siyo baadhi ya maeneo na wataalamu mipango miji kuhakikisha wanaandaa andiko la mradi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya upangaji miji badala ya kusubiri serikali pekee.
Mkutano huo wa Bodi ya Usajili Wataalamu Mipango Miji uliokuwa ukijadili matatizo na changamoto zinazowakabili Wataalamu wa taaluma za Mipango Miji katika shughuli  zao na kuweka  mikakati ya kukabiliana nazo na kushirikisha wataalamu 260 kutoka Serikali na Sekta Binafsi pamoja na Makampuni yanayojishughulisha na mipango miji.

Comments