Featured Post

TEHAMA VIJIJINI NI RADIO


  
NA ALOYCE NDELEIO
Dunia hivi sasa inatawaliwa na mageuzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na hata hivyo moja ya njia inayoonekana kuwa  inatawala katika kuhabarisha katika maeneo ya vijijini ni redio hali  inayoonyesha kuwa  mageuzi yake hayajazifikia jamii nyingi na hususani maskini.

Jenga taswira tu kuwa umepata safari (kwa wale wanaoishi mijini) kwenda vijijini lakini katika mazingira ya kawaida imekuwa ni utaratibu wa kawaida kupata habari  au taarifa mbalimbali za matukio kila siku kupitia  vyombo vya habari.
Aidha yapo matukio nyeti ambayo ukiwa mjini  ni rahisi kuyapata lakini  unapowasili kwenye makazi mapya vijijini unakwama kuyapata matukio hayo  pamoja na mengine kwa njia rahisi kama ilivyozoeleka mjini.
Kadhalika unabaini ni vigumu kuyapata magazeti kwa kuwa hayafiki maeneo hayo kwa wakati mwafaka na mara nyingine hufika kwa kuchelewa na hivyo kuifanya habari kuwa imeshapitwa na wakati.
Pia unabaini kuwa kutokana na kipato duni cha jamii ya eneo husika asilimia kubwa ya watu wa eneo hilo hawamudu kununua magazeti, na wenye magazeti  hawaoni haja ya kuyapeleka huko, likionekana jua siku hiyo kuna mtu  ametoka  mjini.
Hali hiyo inakufanya ufikie hitimisho kuwa  njia mbadala na muafaka ya kupata  habari ni redio peke yake, inahabarisha juu ya matukio mbalimbali yanayoendelea  ndani ya nchi na duniani  kwa ujumla na hata kutoa burudani.
Njia hiyo ya redio unaiona inasadifu kiuchumi kwa kuwa asilimia kubwa ya wanajamii wa vijijini wanamudu kununua betri na wanaweza kuzitumia kwa muda mrefu.
Hapa ndipo linapojitokeza jambo moja muhimu kuwa linapozungumzwa suala la Tehama miongoni mwa jamii nyingi za nchi maskini  kwa asilimia kubwa kinachoweza kuzungumzwa ni redio.
Kigezo muhimu kinachofanya hali hiyo kuwa hivyo ni kutokana na sababu kuwa  hata kama redio hiyo haimilikiwi na familia ni dhahiri matangazo yake  yanafika au kusikilizwa na  jirani zaidi ya mmoja. Hivyo upashanaji wa habari husambaa kwa njia ya kupeana  taarifa au kusimuliana.
Hali ya aina hii hubainisha  kuwa seti za televisheni  na magazeti kwa baadhi ya jamii hizo huonekana kwa nadra pamoja na dhana kuwa teknolojia kwa walio na hali ya uchumi nafuu na kipato chao kinaruhusu na ambao ni wachache.
Hali kadhalika utabaini kuwa katika maeneo mengi ya vijijini hakuna umeme kwa hiyo nishati mbadala inayoweza kutumika ni betri ambazo pia hupatikana  kwa urahisi kwenye maduka yaliyo vijijini.
Asilimia 80 ya jamii inaishi maeneo ya vijijini kupata seti za televisheni ni vigumu lakini redio ni jambo la kawaida kama zilivyo baiskeli  ambazo pia ni moja ya njia muhimu za usafiri, uchukuzi na mawasiliano.
Hapa ndipo unapotokeza msamiati ‘nakalando’ miongoni mwa jamii za mashariki  mwa Uganda ambalo linamaanisha mtu kuzungumza bila kuonekana  hali ambayo jamii hiyo inafananisha na kuzungumza na mizimu.
Hali hiyo ni kwa kuwa njia hiyo ilijulikana kwa wale waliokuwa na imani zinazohusiana na mizimu kuwa kusikiliza redio ni kusikiliza mizimu kwa kuwa anayezungumza haonekani machoni mwa wasikilizaji, hivi sasa ni jina la utani kwa redio.
Kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) ni kwamba watu  milioni 65 walikuwa wanapata matangazo ya redio mwaka 1996 idadi ambayo ni sawa na wastani wa redio moja kwa watu kumi.
Hali kadhalika kwa mujibu wa mtafiti binafsi Helen Hambly, wa mradi wa utafiti wa kuunganisha kilimo na redio vijijini idadi hiyo ya redio itaongezeka kutokana na kuwepo aina nyingi za redio tena za uhakika kutoka China na India ambazo zinafurika katika masoko ya Afrika, na hususan katika kipindi hiki cha biashara ya soko huria.

Matangazo ya redio, mazingira
Haiyumkiniki kuwa pamoja na kuhabarishwa mambo mbalimbali jamii za vijijini zingepiga hatua zaidi iwapo matangazo na habari zinazorushwa zingehusiana na jitihada za kujikomboa kutoka kwenye lindi la umaskini unaozikabili sehemu hizo.
Mtafiti Hambly anafahamisha kuwa hali hiyo inawezekana kwa kutumia teknolojia ya kuanzisha vituo vya redio vijijini ambavyo vinajulikana kama vituo vya redio  vya ndani ya ‘mkoba’ kwa gharama ya dola za Marekani 3,000 sawa na takribani  milioni 6.0/-.
Anadokeza kuwa vifaa vya redio ya aina hiyo vimefungwa hivyo kwamba  vinaweza kurusha matangazo yake hadi masafa ya kilometa 50 kwa kutumia jenereta ambayo inatumia nishati ya jua.
Hambly ambaye ni mwanasosholojia wa mazingira na mwandishi wa vipindi vya redio vinavyohusu kilimo anabainisha kuwa walengwa katika vituo vya redio  za vijijini  ni wakulima, hivyo  nafasi hiyo  inaweza kutumiwa  ili kuwahabarisha  kuhusu kilimo endelevu.
Utafiti wa mwanasosholojia huyo uliodhaminiwa na Shirika la Misaada la Kimataifa la Canada (CIDA) na ambao umefanywa kwa ushirikiano na wataalamu wa  Kitengo cha Taasisi ya Maendeleo vijijjini ya Chuo Kikuu wa Guelph na Mtandao wa Redio Kilimo  kwa nchi zinazoendelea  (DCFRN) na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kilimo na Chakula (FAO).
Washiriki wengine katika utafiti  huo ni Mpango  wa Redio za vijijini  kwa nchi za Camerooon, Ghana, Mali na  Uganda  anaendelea kuarifu kuwa  dhana nzima iliyoelekezwa kwenye utafiti ni namna ya kuwasaidia  watangazaji kufanya kazi  na watafiti na wakati huo  huo  kuyachukulia mazingira ya vijijini  kufikisha ujumbe  kwa walengwa  ambao ni wahitaji  wa matokeo ya tafiti za kilimo.
Hata hivyo anafahamisha kuwa jambo lililojitokeza  kwenye utafiti huo ni kwamba watangazaji wa Afrika  wanahitaji mafunzo, vyanzo vizuri vya habari  na fursa ya kuwa pamoja na watafiti wa kilimo.
Kwa upande mwingine Mkurugenzi wa Mtandao Redio za Kilimo, Nancy Bennet anasema kuwa watangazaji wanaweza kutumia habari zinazohusu wakulima ambao labda wameshajenga  uzoefu na wanyama wanaowafuga kama vile kuzungumza na kuku wanaowafuga ili kuvuta hadhira ya wasikilizaji lakini jukumu la mtangazaji wa vijijini ni kubwa, gumu na zito.
Anatoa mfano kuwa miaka kumi iliyopita Mali ilikuwa na vituo vya redio za vijijini 20 lakini hivi sasa vipo vituo zaidi ya 150 vyote vikiwa vinafanya kazi katika programu za jamii ambazo zinatoa taarifa za hali ya hewa, hali ya ukame na taarifa za tahadhari za kuwepo kwa janga la njaa.
Anabainisha kuwa njia za zamani za mawasiliano ya redio zinatoweka na nafasi yake inachukuliwa na teknolojia mpya kama vile redio za intaneti na njia zingine ambazo maudhui yanayotakiwa  yanaweza kuwafikia walengwa.
Hali kadhalika mipaka kati ya vituo vya redio binafsi na redio za umma imekuwa inabadilika ambapo anatolea mfano kuwa vituo vingi vya redio za serikali kwa sasa vimekuwa vinaendeshwa kibiashara na kwa upande wa vituo binafsi kuwa vinaegemea zaidi ushirikishwaji wa jamii.
Mfano hai wa redio za aina hiyo upo nchini Uganda ambapo miaka mitano iliyopita ilikuwepo redio moja tu lakini teknolojia ya kisasa pamoja na mfumo huria wa utangazaji kumewezesha kuwepo redio zaidi ya 70 baadhi zikiwa zinaendeshwa kwa mfumo wa jumuiya na utangazaji wake ukiwa unalenga matukio ndani ya jamii na hata mchango wa wanawake katika uelewa wa teknolojia  ya asili.
Mkurugenzi huyo anadokeza kuwa anabainisha kuwa  uthibitisho  kutoka  kwa wabia wa mradi wa ISNAR ni mapendekezo  yao  kuwa redio  zinaweza  kufanikisha  kuwaunganisha wakulima na tafiti  hali kadhalika zinaweza kusaidia  ubunifu  ambao utawasaidia masikini wa vijijini.
Anaarifu kuwa wanasayansi katika sekta ya kilimo wanaanza kuona redio kama njia mojawapo ya kuwezesha kufanikisha ubunifu wao wa kitaalamu moja kwa moja vijijini.
Anasema kuwa kimsingi ni kwamba jambo linalofanyikas ni kuchupa kutoka juu ya mifumo ya asili ya kilimo ambayo imesahaulika kifedha na hata kiutendaji.
Anaarifu, ‘Wanasayansi nao wameanza kubaini kwamba redio huwasilisha mambo yao muhimu. Hata hivyo hadi sasa baadhi ya watafiti bado wanaamini kwamba jukumu la kufikisha ujumbe au matokeo ya utafiti wao kuwa la mtu mwingine.’
Anaendelea kuarifu kuwa watafiti wanahitaji kuhusishwa na inatakiwa mawasiliano yawe katika mikondo miwili na si kitendo cha habari kuwa kwenye mtiririko wa upande mmoja tu.
Redio za jamii vijijini zinaonesha njia ambayo jamii ya maeneo husika inaweza kuhabarishwa na jamii  hiyo yenyewe kuhabarisha pia  kuhusu miundombinu ambayo wanasayansi na wakala wengine wanaweza kutumia kuboresha mazao ya kilimo na ufugaji na huduma nyingine za kijamii.

Comments