Featured Post

SERIKALI KENYA YAFUTA LESENI YA KIPEDA KUTOKANA NA UHABA WA MAFUTA



NAIROBI, KENYA
TUME ya kudhibiti nishati nchini Kenya imefuta leseni ya muungano wa wafanyabiashara wanoagiza mafuta KIPEDA ambao tume huyo inailaumu kwa kuvuruga uchumi.
Inailaumu kwa kuongoza ususiaji wa bidhaa za petroli hatua ambayo imechangia kushuhudiwa uhaba wa mafuta nchini Kenya.

Zimeshuhudiwa foleni ndefu kwenye mji mkuu Nairobi na viunga vyake wakati wenye magari wanasubiri kuongeza magari yao mafuta.
Vyombo vya habari vinasema kuwa wauzaji na wasafirishaji mafuta wamekuwa wakisusia katika jitihada za kuishinikiza serikali ifute kodi mpya. Uhaba wa mafuta umeshuhudiwa sehemu tofauti za nchi.
Hii inajiri huku shinikizo zinazidi kumuandana Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta za kumtaka aweke sahihi mswada wa uchumi mwaka 2018 wenye mabadiliko ya kufuta kodi mpya iliyowekwa kwa bidhaa za mafuta.
Kodi hiyo ya asilimia 16 ilitangazwa na wizara ya fedha, licha ya mswada uliopitishwa na bunge ambao ulitupilia mbali kodi hiyo kwa miaka miwili.
Chama cha watengezaji bidhaa nchini Kenya kimeonya kuwa hatua hii itaathiri ajenda kuu nne za rais na wanataka ifutwe.
Wakenya wengi wamekuwa wakielezea hasira zao kutokana na hali inayojiri huku wengine wakilazimika kufunga foleni ndefu katika vituo vya kujaza mafuta mjini Nairobi na katika maeneo mengine nchini wakitafuta bidhaa hiyo inayoonekana kuwa adimu.
Hivi ndivyo baadhi walivyokuwa wakizungumza katika mitandao ya kijamii.
Kutoka na kodi hiyo mpya ya asilimia 16 kwa bidhaa za mafuta sasa lita moja ya petroli itauzwa takriban shilingi 127.80 mjini Nairobi kutoka shilingi 113 huku mafuta ya dizeli yakiuzwa shilingi 115 na mafuta taa shilingi 97. 
Lakini pia bei hizo zitakuwa juu sehemu zilizo mbali na Nairobi na hasa magharibi mwa nchi na chini kidogo kwenye mji wa Mombasa na sehemu zilizo karibu.
Musalia Mudavadi mwanasiasa wa upinzani nchini Kenya ambaye wakati mmoja alihudumu kama waziri wa fedha, anasema kuwa hali ambayo Kenya imejipata kwa sasa imetokana na hatua ya serikali kukopa kwa njia ya kasi.
Anasema kodi ambazo serikali hutosa bidhaa za mafuta mara zinapowasili nchini Kenya husababisha bei ya lita moja ya mafuta kuongezeka maradufu hali ambayo imeathiri sana mwananchi.
Mudavadi anasema kuwa ile mikopo ambayo serikali inachukua kwa sasa muda wake ya kuanza kuilipa ni mfupi na riba yake ni ya juu zaidi labda kwa kati ya asilimia saba na nane.
"Dalili moja ni vile wameanza kutosa ushuru kwa bidhaa za mafuta, mishahara ya walimu imechelewa, mishahara ya wafanyakazi wengine wa sekali imechelewa, tumeona wafanyabiashara wengine mali yao ikiuzwa kwenye minada kwa sababu labda walifanya kazi na serikali na hawakuwalipwa kulinganana vile walifanya kazi, " Mudavadi anaongeza kusema.
Anasema suluhu ya haraka ni kwa waziri wa fedha kurudi bungeni na kuhakikisha kuwa miradi mipya imesimamishwa kwa kuwa wale watakaoumia zaidi ni wananchi, na pia tatizo la ufisadi lipiwe vita.
Pia katika suala la utunzi wa mazingira Mudavadi amesema kuwa kupanda ya bei ya bidhaa za mafuta itachangia katika ukataji miti kwa kuwa sasa watu hawatakimu gharama ya juu ya bidhaa kama mafuta ya kuwasha jiko, na jivyo itachangia ukataji miti kwa kuni za kupikia ambapo matokeo yatakuwa ni athari kwa mazingira.
Baadhi ya wakenya ambao wamezungumza na BBC hasa wale wanaondesha biashara za uchukuzi wa magari, wamesema kuwa tangu kodi ya asilimia 16 kwa bidhaa za mafuta ianze kutekelezwa, mambo yamekuwa tofauti kwa kuwa sasa wanatumia maradufu pesa walizokuwa wanahitaji awali kuwawezesha kuweka magari yao mafuta.
Gharama hiyo yote imeelekezwa kwa wasafiri kwa kuwa nauli ya usafiri nayo imeongezea angalau na wenye magari nao wapate kundelea na biashara zao.
Kuna hofu kuwa huenda bei ya bidhaa muhimu nayo ikapanda kwa kuwa kawaida jinsi imekuwa, muda tu bei ya bidhaa za mafuta inapopanda, huchochea kupanda bei ya bidhaa muhimu za kukithi mahitaji ya mwanachi wa kawaida, jambo ambalo huchangia tena kupanda kwa gharama ya maisha.
BBC

Comments