- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
NA ALOYCE NDELEIO
“Lazima tufange kazi kwa maendeleo yetu badala ya kusbiri
fedha kutoka nje, inashangaza wananchi
wanasubiri kumwagiwa fedha, utasikia, neema yaja, heshima ya nchi ni
kujitambua, kujitegemea.”
Hivyo ni kauli y Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu , Benjamin
William Mkapa wakati akizindua kitabu,
Global Poverty (The Case for sub-Sahara
Africa), kilichoandikwa na aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Marten
Lumbanga na kuongeza, “Hakuna wa kutumwagia
kwa ajili ya maendeleo yetu bali yataletwa kwa watu kufanya kazi kwani
heshima ya nchi ni kujitegemea.”
Aidha Balozi Lumbanga
alisema “Kwa bahati nzuri nchi nyingi za
Afrika zinajitambua kuwa ni maskini na
kazi inayoendelea ni kuondokana na
umaskini, maendeleo yanaonekana.”
Hivyo si mara ya kwanza kwa Rais Mstaafu Mkapa kutoa maoni yake hayo kwani hivi karibuni alisema nchi za Afrika
hazitajikomboa kiuchumi kama zitaendelea kutegemea na kushabikia misaada kutoka
kwa nchi wahisani na badala yake zitumie rasilimali na biashara zao wenyewe ili
zifike mbali zaidi ya zinavyodhani.
Kauli hiyo aliitoa kwenye kongamano la lililowashirikisha
pia Marais Wastaafu Olusegun Obasanjo wa Nigeria na Festus Mogae wa Botswana
likiwa lilikuwa limeandaliwa na Taasisi ya Uongozi jijini Dar es Salaam.
Hoja inayojitokeza katika maoni hayo yanathibitisha kile
kinachoelezwa kuwa misaada inayotolewa
na nchi zilizoendelea ipo katika
mifumo kadhaa, kiuchumi, kijamii na
kibinadamu na imekuwa ndio kipaumbele cha nchi hizo tangu kipindi kilichofuata
baada ya uhuru wa nchi nyingi za
Afrika miaka ya 1960.
Asasi zisizo za serikali
kwa mamia elfu zimekuwa
zikijaribu kuifanya dunia kuwa sehemu nzuri ya kuishi zikiwa zinapambana na
magonjwa ya kutisha, kutoa misaada ya chakula na maji, kutoa walimu na mambo
mengine mengi.
Misaada inayotolewa kwa ajili ya waathirika wa janga la
asili huwa na ufanisi katika kupunguza maumivu ambayo yanakuwepo kwa wakati huo
wa tukio na hata hivyo huwa sio suluhisho la kudumu na haisaidii kutoa jukwaa
imara kwa nchi iliyokumbwa na janga
katika mazingira endelevu.
Hivyo nchi tajiri zimekuwa zinatoa misaada, sawa, na hali
kadhalika kuwepo kwa watu wanaoendelea kukampeni kuhusu upatikanaji wa misaada,
lakini misaada hiyo kutoka nje haioneshi
kuchangia katika hatua za maana za kupambana na umaskini miongoni mwa nchi
maskini.
Tangu miaka ya 1950 utamaduni wa maendeleo ya kiuchumi
umekuwa unahodhiwa na wazo kuwa kiwango kikubwa cha misaada ni suluhisho la
kuziba pengo lililopo miongoni mwa nchi zinazoendelea, lakini kiuhalisia umekuwepo uthibitisho unaoonesha kuwa
mtiririko mkubwa wa misaada hiyo huishia kuleta madhara zaidi kuliko
kuneemesha.
Uchambuzi wa kukua kwa uchumi katika nchi za Asia katika
miongo kadhaa iliyopita ambazo zimekuwa zikipokea kiwango kidogo cha misaada
ikilinganishwa na Afrika ni kielelezo kizuri kwamba misaada haisaidii.
Ripoti ya hivi karibuni ya Benki ya Dunia inaonesha kuwa
miongoni mwa watu milioni 700 waliondolewa kutoka kwenye lindi la umaskini kati
ya mwaka 1980 na 2010, watu milioni 627 kati ya hao ni kutoka China. Hiyo
inamaanisha kuwa watu milioni 73 ni kutoka
sehemu nyingine duniani.
Kwa maneno mengine ni kwamba asilimia 89.6 walitoka China,
hivyo kutoa kiashiria kilicho wazi
kwamba misaada kutoka nje si suluhisho dhidi ya umaskini.
Kimsingi utoaji wa misaada ulionekana kama njia ya
kutokomeza umaskini uliokithiri lakini kuanzia miaka ya 2000 nadharia ya
msukumo mkubwa imekuwa ndio mada
inayozua mjadala ikihusu matokeo hasi ya misaada ambayo inaonekana kuziacha
nchi zinazoendelea katika hali mbaya kuliko zilivyokuwa.
Kwa kuliangalia eneo la Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara,
juhudi zote zilizokwishafanyika zinajionesha wazi, lakini kwa kuangalia takwimu
za misaada ya nje katika bajeti kwa nchi nyingi, kiwango cha kupiga hatua kimebadilika
ghafla na kuonekana kuwa ni cha chini ikilinganishwa na fedha nyingi ambazo zimeshapokea.
Kwa ujumla Afrika inapokea takribani dola bilioni 50 za
misaada ya kimataifa kwa mwaka.
Hata hivyo, badala ya kuboresha kwa kasi hali ya maisha ya
watu milioni 600 wanaoishi chini ya mstari wa umaskini, misaada hiyo imewafanya
walio matajiri kuwa matajiri zaidi.
Taswirahiyo inaonesha kuwa walio maskini kuwa maskini zaidi
na hivyo kukwamisha ukuaji wa uchumi, na hali kadhalika kuchochea mzunguko wa rushwa.
Misaada Rasmi ya Maendeleo (ODA) ni utoaji rasmi wa fedha
ambazo zinagawiwa miongoni mwa nchi zinazoendelea zikilenga kukuza maendeleo ya
kiuchumi na ustawi wa nchi hizo.
Fedha hizo ambazo humwagwa kwa nchi hizo zinatoka si tu kwa
serikali moja kwenda kwa serikali nyingine ikiwa ni programu ya msaada, bali
pia hutoka katika programu za maendeleo kimataifa
zinazoratibiwa na Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF)
ambao huwa ni wawezeshaji kati ya serikali zinazotoa na zile zinazopokea.
Misaada ya nje haina tofauti na kushamirisha rushwa na
utegemezi. Hii inamaanisha kuwa misaada inaimarisha wigo wa rushwa miongoni mwa
nchi zinazopokea na ambako tayari rushwa imesambaa.
Kwa mujibu wa Transparency International (TI) ni kwamba kwa
bahati mbaya hali hiyo ndiyo
iliyotamalaki miongoni mwa nchi nyingi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara
ambazo zinapokea kiwango kikubwa cha misaada.
Nchi hizo zina kiwango kidogo cha ufanisi katika maeneo
mengi ya utawala bora hususani katika
suala la rushwa.
Hali hiyo inaonesha kwamba
misaada ya nje inasukuma kiasi cha rasilimali zilizopo kuwa mikononi mwa
makundi maalumu ya viongozi, ambao wanakuwa maswahiba wa watendaji wa serikali.
Hili liko wazi kwani wapo viongozi ambao ni wadokozi na ambao hufumbia mcho
vimelea vya rushwa.
Hakuna uwiano sawa katika usambazaji wa misaada miongoni mwa
idadi ya watu au matumizi yake katika kukuza uchumi na kusaidia watu maskini
badala yake zimekuwa zikitumika kununulia vifaa vya kijeshi, kuanzisha au
kuendesha miradi ya anasa isiyo na faida, manunuzi ya uongo au kughushi katika
manunuzi hayo n.k.
Hali kadhalika fedha hizo za misaada zinatumiwa na viongozi
ambao wanakuwa na sera chache na wanataka kufikia malengo yao ya kisera kwa
kasi, ikiwa ni pamoja na kuongeza ukubwa wa serikali kwa kuajiri watumishi
(ambao hawachangii chochote katika mfumo au maendeleo na mara nyingine kuajiri
watumishi hewa) ikiwa ni njia ya kupunguza kiwango cha ukosefu wa ajira.
Madhara kwa upande wa utegemezi ni kwamba nchi ambazo
zimekuwa zikipokea kiwango kikubwa cha fedha zimekuwa hazikuzi biashara za
ndani kwa sababu zinakuwa na fedha za
‘bure’ mikononi mwao. Hali hiyo inazuia
aina yoyote ya kuboresha maendeleo ya binadamu na hata pato la nchi.
Hoja inayoibuka ni kwamba kwanini misaada inaendelea
kutolewa? Kimsingi inaonesha kama vile wanasiasa wa nchi zilizoendelea wapo
kama wanaangalia na kuwalinda wenzao wa nchi zinazopokea misaada.
Mkakati wa kimaslahi na kisiasa wa wahisani unaonesha kuwa
hatua za kutoa misaada ni muhimu zaidi kuliko kujali suala la utawala bora miongoni mwa mataifa yanayopokea.
Hali hiyo inazifanya nchi za Afrika kutopiga hatua ya
maendeleo huku zikiwa zinaongozwa na viongozi wadokozi. Historia ya ukoloni
nayo inachangia kwa kiwango kikubwa katika mchakato wa misaada.
Ufaransa kwa mfano huwa inatoa kiwango kikubwa cha misaada
kwa nchi zilizokuwa makoloni yake ikiwa ni kama kufuta madhara ya mambo
waliyoyafanya hapo zamani.
Australia na nchi za Nordic huwa zinawatenga, tofauti na
Ufaransa au Uingereza nchi hizo hutoa misaada yake tu kwa nchi zilizo na
kiwango kidogo cha rushwa. Hii inatokana na sababu kuwa hazikuwa na makoloni
hivyo zinakuwa huru dhidi ya mashinikizo ya kisiasa.
Kama rejea ni kwamba Kamisheni ya Uchumi ya Ulaya (EEC)
ambayo hivi sasa ni Umoja wa Ulaya (EU) iliwahi kuzitenga nchi za Ureno,
Ugiriki na Hispania kabla ya kuwa wanachama wake na hivyo kuwaruhusu kuwa wanachama wake baada ya kuwa na serikali
za kidemokrasia.
Hilo lilionekana ni sawa na huenda IMF na WB wanaweza
kufanya jambo kama hilo kwa sababu hadi sasa hawajazitenga nchi zinazopokea
misaada na ambazo rushwa miongoni mwake imetamalaki.
Hata hivyo hoja nyingine ni kwamba je, uchumi wa nchi za
Afrika unaweza kurudi katika mkondo sahihi? Kama misaada inakuwa haifanyi kazi
basi kuna haja ya kufanya marekebisho.
Kama watendaji hao wa dunia hataweza kusaidia basi angalau
wasiache mambo yakazidi kuharibika. Sera mpya na hamasa zinaweza kuwekwa pamoja
kuonesha hatua kuliko kushindwa. Misaada inatakiwa ibadilishwe iwe ni biashara. Ikimaanisha kuwa misaada
hiyo itolewe katika mfumo wa biashara.
Wananchi wa Afrika wanatakiwa kujengewa uwezo hivyo kwamba
wanakuwa waundaji wa ujasiriamali unaostawi, ili wamudu kuishi kwa kutumia shughuli zao. Sera sahihi na zilizokamilika pamoja na usimamizi mzuri wa
masuala ya uchumi ni muhimu zaidi kuliko
misaada kwa nchi zinazoendelea.
Taasisi thabiti na imara
zinaepuka misaada kwa kuwa inageuka kuwa laana. Hivyo lazima iwepo
misaada katika kuboresha utawala bora
kabla ya kutolewa msaada wa kifedha kwa sababu bila serikali thabiti,
misaada ya kifedha haitaweza kufanikisha matamanio ya malengo.
Comments
Post a Comment