Featured Post

MFUMO WA IKOLOJIA WA MIOMBO UNAHITAJI USIMAMIZI ENDELEVU



NA MWANDISHI WETU
Jumuia ya kimataifa hivi karibuni ilizitaka nchi jirani kuunganisha nguvu ili kuokoa pamoja na kuwepo kwa usimamizi endelevu wa misitu kwenye mfumo wa ikolojia wa Miombo/Mopane ndani ya Afrika kutokana na sababu kuwa mfumo huo asilia ndio unaoonesha kufungamana kwa binadamu na misitu.
Kutokana na kutambua umuhimu na tishio linaloukabili mfumo wa ikolojia wa Miombo Tanzania ilitoa angalizo kwa  jumuia ya kimataifa kupitia Maendeleo ya Ubia  kwa kuunganisha juhudi zake  kuokoa mfumo wa ikolojia kwa Tanzania, Zambia  na sehemu zote za Jumuia ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).

Makubaliano ya kuratibu uhifadhi na usimamizi wa mfumo wa ikolojia wa Miombo/Mopane kati ya Serikali ya Zambia na Tanzania, ulisainiwa na serikali kupitia Wizara ya maliasili na Utalii ambapo ilisema kuwa tishio linaloukabili mfumo huo lisipodhibitiwa kutasababisha hasara kwa jamii kwa kuwa ni mfumo unabeba sehemu kubwa ya maisha ya viumbe hai.
Ilielezwa kuwa katika kipindi cha miaka ya karibuni ujangili wa maliasili  na usafirishaji haramu wa  bidhaa za maliasili kutoka Afrika  umeongezeka kwa kasi na kwamba hali hiyo inaleta tishio si tu kwa  idadi ya rasilimali hizo bali pia kwa mifumo ya uchumi, siasa na ikolojia.
Jambo lililo wazi ni kwamba uondoaji haramu wa maliasili  ndani au nje ya maeneo yaliyohifadhiwa kama itaendelea bila kukomeshwa  kutasababisha madhara kwa sekta ya utalii si tu kwa Tanzania  bali pia kwa mataifa mengine ya Afrika.
Ilibainishwa kuwa mitandao ya kuhamasisha na kuondoa maliasili ndani na nje ya  nchi umeendeleza usafirishaji wa bidhaa za maliasili  na hivyo kufanya iwe vigumu kwa nchi moja peke yake kuingilia kati kudhibiti. Hivyo kutokana na hali hiyo Tanzania ilitoa wito kwa nchi jirani na jumuia ya kimataifa  kuungwa mkono katika kukabiliana na jukumu hili muhimu.
Iliarifiwa kuwa katika juhudi za kukabiliana na uhamishaji haramu wa bidhaa za maliasili, serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  imechukua hatua kadhaa  zikiwemo  kuongeza operesheni za kawaida na nyingine maalum pamoja na kampeni ya kujenga uelewa katika ngazi za ndani na jumuia ya kimataifa.
Hivi karibuni serikali ilijikita  kwenye uhifadhi wa wanyama pori na hususani tembo  ambapo  ilikuwa mwenyeji wa mkutano  uliobeba kauli mbiu ya “Acha uhalifu dhidi ya wanyama pori Ongeza uhifadhi wa wanyama pori” uliofanyika jijini Dar es Salaam.”
Ilibainishwa kuwa kwenye mkutano huo Serikali ya Tanzania na Mfuko wa Kimataifa wa Kuhifadhi  (ICCF) kwa kushirikiana na Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) na wadau wengine muhimu  walianzisha miundombinu sahihi na endelevu ya kupata fedha  kwa ajili ya kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa meno ya tembo.
Mfumo wa ikolojia wa msitu wa Tanzania na Zambia kwa kiwango kikubwa kinajumuisha mfumo wa Miombo/Mopane ambao ni eneo muhimu lililohifadhiwa kwa ajili ya rasilimali ya wanyama pori na misitu.
Kwa kuzingatia umuhimu huo ilibainika ni muhimu kujumuisha aina hii ya msitu  kwenye azimio la mkutano wa kikanda wa kutokomeza uhalifu dhidi ya wanyama pori na kukuza uhifadhi wa wanyama pori uliofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) kuanzia Novemba 7 hadi 8, 2014 ukiwa na mtazamo wa kuanzisha mtazamo shirikishi  wa kudhibiti uondoaji haramu wa bidhaa za maliasili.
Hatua ya kufikia maamuzi hayo serikali mbili za Zambia na Tanzania  zilikubaliana kuhakikisha kuwa watu wake kuwa wanajikita  kuhifadhina kusimamia ipasavyo  mfumo wa ikolojia wa Miombo/Mopane.
Japo sera za taifa za misitu na wanyamapori pamoja na sheria zinaunga mkono uhifadhi na usimamizi wa miombo aina hiyo ya misitu imeendelea kupunguzwa kwa kukata  miti hovyo. Hali hiyo kwa upande mmoja inaweza kuwa ni kwa sababu taasisi zinazoshughulikia mfumo huu wa ikolojia zinakuwa hazina uwezo wa kifedha na nguvu kazi.
Kutokana na Tanzania kutambua umuhimu wa kukuza usimamizi endelevu wa mfumo ikolojia wa Miombo  iliamua kuchukua nafasi hiyo kudokeza mambo kadhaa yanayohusiana na suala hilo.
Serikali ilisema, “Tumeshawishika na kuunga mkono usimamizi endelevu wa mfumo wa ikolojia wa Miombo kwa kuwa unasaidia uwezeshaji wa maisha ya idadi kubwa ya watu wake  kwa kuwapatia aina mbalimbali za bidhaa na huduma kama vile chakula, nishati ya kupikia (kuni), makazi, malighafi za ujenzi wa nyumba zao na dawa zikiwa ni baadhi tu miongoni mwa bidhaa na huduma nyingi.
“Kama nyongeza mfumo wa Miombo  unajumuisha fursa za kipekee  kwa jumuia za vijijini  nchini Tanzania  za kukuza  maendeleo ya kijamii na kiuchumi, ulinzi wa mazingira kwenye ukanda wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) na umekuwa ukizuia matokeo hasi ya  mabadiliko ya tabianchi. Ni muhimu kwamba kupunguza mabadiliko ya tabianchi na kuridhia hatua ambazo zitakuwa sehemu ya utekelezaji makubaliano yaliyosainiwa.”
Kwa kuzingatia masuala ya mabadiliko ya tabianchi na misitu, imekuwepo haja ya  kuweka kipaumbele katika kudhibiti vichocheo vya ukataji miti na kuteketeza misitu pamoja na uharibifu wa ardhi. Masuala mengine kama kilimo, nishati, ufugaji  na matumizi mengine ya ardhi yanahitaji kutupiwa macho pia.
Aidha serikali iliwataka wadau wote  kufanya kazi pamoja  ili kuhakikisha kwamba utekelezaji wa usimamizi endelevu wa misitu kupitia makubaliano juu ya mfumo wa ikolojia wa Miombo kwa manufaa ya watu wake ambapo kimsingi kutaharakishwa na kuungwa mkono kwa kutumia rasilimali za kutosha.
Serikali ya Zambia kwa upande wake ilisema kuwa changamoto kwenye usimamizi dhidi ya uhalifu unaofanywa kwenye misitu ikiwemo ukataji wa miti uchomaji haramu wa mkaa na kiwango kikubwa cha uvunaji haramu wa miti kwa ajili ya mbao kwa spishu adimu haziwezi kufanikiwa bila kuwepo juhudi za pamoja miongoni mwa nchi husika.
Ushirikiano kwenye shughuli mpakani utakuwa ni msingi wa kupata ufumbuzi kwenye usimamizi na uhifadhi wa mfumo ikolojia kwa ajili ya uendelevu wake ambapo Serikali ya Zambia iliamua kujikita kwenye makubaliano na kuhakikisha unakuwepo uhifadhi na usimamizi wa mfumo wa ikolojia.
Serikali ya Ujerumani  kupitia ubalozi wake nchini Tanzania, ilipongeza juhudi za Tanzania na Zambia  kwa hatua ilizochukua kuhifadhi mfumo huo  ili kuisaidia jamii katika mahitaji yake pamoja na maendeleo kupitia matumizi endelevu ya maliasili.
Hata hivyo ilibainishwa kuwa njia mbadala za kujipatia kipato kama ufugaji nyuki, ufugaji wa samaki na uwindaji kwenye mapori unahitaji kuungwa mkono.

Comments