Featured Post

MSUKUMO KIMAADILI NYENZO YA KUPAMBANA NA RUSHWA



NA ALOYCE NDELEIO
Wizi wa fedha za umma pamoja na rushwa ni matendo yaliyosambaa katika taasisi nyingi za umma nchini licha ya serikali kuwa na mikakati kadhaa ya kupambana na rushwa.
Katika kudhihirisha hilo Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali katika moja ya ripoti zake ilisema kwamba maofisa watatu waandamizi wa serikali katika Shirika la Ndege la Air Tanzania (ATCL) wafunguliwe mashtaka kutokana na kuingia mkataba wenye utata wa kukodi ndege ambao uliizamisha nchi kwenye deni la dola milioni 41. 

Hali hiyo ilimaanisha kuwa furaha ambayo jamii imekuwa nayo hususani baada ya kuwasili kwa ndege mpya iliyonunuliwa na serikali aina ya  Boeing Dreamliner  787-8 haikuwa ni bure bali  ni ishara ya kuona majeraha yalisababishwa na baadhi ya watu yameanza kupata tiba.
Kukithiri kwa rushwa kumesababisha kuwepo kwa mikakati si tu kwa Tanzania bali kwa Afrika  ambapo Jumatano iliyopita Julai 11 ilikuwa ni siku maalum iliyotengwa na Umoja wa Afrika kuadhimisha mapambano dhidi ya rushwa.
Sikui hiyo inatokana na maamuzi ya ya Mkutano wa Wakuu wa Nnchi za Umoja wa Afrika  uliofanyika Addis Ababa Ethiopia Julai3 hadi 7, 2017, kwa kutambua uzito wa tatizo la rushwa  na hivyo kuamua mwaka 2018 kuwa mwaka wa mapambano  dhidi ya rushwa
Tanzania iliungana na nchi nyingine za Afrika  kuiadhimisha siku hiyo maalum ya mapambano  dhidi ya rushwa kwa kutafakari athari za rushwa kwa maendeleo ya taifa  na kujipanga zaidi kupambana na kadhia hiyo.
Mikataba na makubliano ya kimtaifa ya kuzuia na kupambana na rushwa ni mambo yanayotambuliwa na Tanzania kuwa ni tatizo linalohitaji nguvu ya pamoja kulikabili.
Kwa kipindi kirefu sasa rushwa imechukuliwa kama utamaduni  ndani ya jamii na wamekuwepo watu ambao wamekuwa wakiendesha maisha yao kupitia ulaji  rushwa licha ya kuainishwa kuwa ni miongoni mwa maadui wakubwa wa maendeleo, na wakiwa wanalitambua hilo.
Hata hivyo wamekuwepo watu walio na ushauri kuhusu mienendo inayotakiwa ili kupambana na mambo kama rushwa kwa kuwa madhila yake yanaeleweka kuwa si kwa mtu mmoja bali ni kwa umma kwa ujumla.
Michelle Obama ambaye ni mke wa Rais wa 44 wa Marekani, Barrack Obama aliwahi kuainisha baadhi ya mambo ambayo Afrika inatakiwa  kuwa nayo aliposema kwamba  inahitaji  viongozi  wanaofanya mambo sahihi  hata wakati wanapokuwa hawaonekani mbele ya macho ya  wananchi, na kuongeza kuwa  inahitaji viongozi ambao watakataa kuvumilia mabaya wanayofanyiwa wengine.
Hata hivyo ili kufanikiwa katika hilo alisema kwamba  kunahitaji kuwa na msukumo wa kimaadili na huo hauwezi kupandikizwa  ndani ya mtu bali unastawishwa  kupitia uaminifu wa kuyatambua maadili.
Alisema, “Kujadili mifano halisi ya maisha moja kwa moja kunaleta uwazi katika kuonesha madhara ya rushwa. Miongoni mwa mambo  ambayo yanamgusa moja kwa moja  binadamu kwa mfano ni masuala ya tiba. Hoja ni kwamba nani atakayependa mama yake atibiwe na daktari ambaye alikuwa  anafanya mambo kwa kuhadaa alipokuwa akisoma?
“Hali hiyo inamaanisha kuwa  ili kupata huduma kwake ni lazima  atakuhadaa mpaka umpatie rushwa. Kwa hiyo ni gharama kiasi gani inatumika katika kuitafuta rushwa pamoja na udanganyifu ndani ya jamii?
“Kama tukiuvumilia  udanganyifu hivi sasa miongoni mwa vijana je, ni kwa namna gani tutaweza kusimama  na kupambana na rushwa  hapo baadaye?
“Kama unataka kuongoza lazima uwe na msukumo wa kimaadili ulioufanya  kumea na kustawi  ndani mwako, na hivyo kukuwezesha  kuwafanya wengine  kuutafuta msukumo huo.”
Katika vipindi tofauti vya uongozi wa hapa nchini kila awamu iliyoingia madarakani  imekuwa ikitangaza rushwa  kuwa ni adui namba moja na kwamba mapambano yataendeshwa  kwa kutumia kila  aina ya silaha kuitokomeza.
Hata hivyo kadri muda  unavyosogea  rushwa imeenea  na kuathiri kila sekta ya uchumi.  Rushwa imeongezeka kiasi kwamba  imekuwa ndio aina au mtindo wa maisha ya kila siku na kuwa jambo la kawaida katika jamii.
Mapambano dhidi ya rushwa kwa Tanzania hayakuanzwa na utawala uliopo  sasa licha ya kwamba awamu hii inaonesha kuendesha mapambano hayo kwa nguvu kubwa zaidi na kufikia hatua ya kulinganishwa na mapambano yaliyokuwa yakiendeshwa katika awamu ya kwanza.
Lakini awamu zote zilizotangulia  zimechangia kwa kiasi kikubwa  kupambana na rushwa  ambayo imekuwa ikisambaa kama saratani.
Miaka ya hivi karibuni Taasisi ya Kimataifa ya Tansparency (TI) iliiweka Tanzania kwenye kiwango cha asilimia 39.1 kwenye vidokezo vya rushwa  kwa  asilimia 100; lakini  wachambuzi wa masuala ya rushwa waliona kuwa vidokezo hivyo vilishindwa kutoa  taswira halisi ya madhara ya rushwa katika maisha ya kila siku kwa jamii.
Nafasi hiyo ya Tanzania kwa vigezo vya CPI ilionesha kuwa ina afadhali  kuliko Uganda na imefanya vizuri kuliko Kenya.
Katika kupambana na rushwa  Serikali iliunda Tume  ya Warioba  ambayo ilichapisha ripoti yake ambayo ilitathmini  hali ya rushwa Tanzania  mwaka 1996, viongozi waliofuta walichukua mikakati mbalimbali kupambana na rushwa ikiwa ni pamoja na kupitisha sheria ya kupambana na rushwa  na kuanzisha taasisi za kudhibiti hali hiyo.
Taasisi ya Kupambana na Kutokomeza Rushwa (Takukuru) ilianzishwa ikiwa ni matokeo ya mikakati hiyo.  Kila awamu  imekuwa ikifanya shughuli zake za kupambana na rushwa  na hata baadhi ya maofisa wa serikali wamefikishwa mahakamani na kufunguliwa mashtaka kutokana na tuhuma za rushwa.  
Umma kwa jumla unaweza kwa kiasi fulani ukawa uliridhishwa na mapambano dhidi ya rushwa lakini uhalisia ulionekana zaidi kwa watoa au wapokeaji rushwa ndogo kuliko  ilivyokuwa kwa wala rushwa kabambe.
Hata hivyo kwa hivi sasa kumekuwepo na viashiria kuwa mapambano hayo yameanza kujikita kwa wala rushwa kabambe na wakwapuaji mahiri.
Hali hiyo inatokana na kile kilichojengeka  kama utamaduni  uliojikita ndani ya jamii  kwamba katika maisha ya kila siku ni mara chache watu hukwepa hali hiyo kwani wanaona kuipokea rushwa ni kama  sehemu ya utamaduni.
Kutoka kwa wafanya biashara jijini Dar es Salaam hadi kwa hakimu Tabora, trafiki Kilimanjaro, dereva wa basi Mwanza na mwalimu wa shule ya msingi Arusha  rushwa imekuwa ni janga kwamba imeshaathiri kila mmoja.
Mkazi wa Dar es Salaam yuko radhi kutoa mlungula ili kupata  matibabu ya upendeleo anapotafuta  huduma ya tiba.  Analazimika kufanya hivyo  kwa sababu  anaona ni kupoteza muda  kufuata mlolongo wa kirasimu  uliopo katika hospitali za umma. Anapata dawa ambazo awali alielezwa hazipo. Hivyo mfano huu unatoa picha mbaya kwa nchi ambapo asilimia kubwa  wanaishi kwenye lindi la umaskini.
Kuna kila dalili kwamba mwanga upo hivi sasa kwamba maadili yakizingatiwa suluhisho la kuwa na jamii isiyosujudia rushwa na kuvikataa vitendo nuru ya ustawi katika jitihada zake za maendeleo itakuwa inang’aa.

Comments