Featured Post

KUIGIZA TAMTHILIYA ZA MASOMO HUPANUA UPEO WA UCHAMBUZI



NA ALOYCE NDELEIO
Michezo ya kuigiza licha ya kwamba  haipo kwenye mihtasari ya masomo mara nyingi inatambuliwa kama sehemu muhimu inayowawezesha wanafunzi kuongeza uwezo wao wa kuelewa kutambua na hata kuwa na kiu ya kufikiri zaidi.
Ukweli  unabakia kwamba  maendeleo na  mbinu za kijamii zinaweza kufikishwa kwenye hadhira yoyote ile kupitia njia ya michezo ya kuigiza au tamthiliya.

Tamthilia zinawajumuisha wanafunzi kushiriki kwenye kuchunguza na kutafiti masuala kupitia ushirikiano na muingiliano na wengine na kushirki kwenye kuendeleza na kuwasilisha mawazo.
Aidha nyanja hiyo huwapa wanafunzi hususani walio kwenye ngazi ya sekondari utambuzi na uelewa wa namna ambavyo sanaa za maonesho kwenye ukumbi zinavyotumika kama njia ya mawasiliano na kujieleza.
Hali kadhalikaufanisi kwenye kufundisha kuigiza kunasaidia kuibua shauku ya kupenda michezo  na maonesho na hivyo kuongeza ubora kwenye uzoefu wa kiutambaduni na kijamii.
Mahitaji ya kuwa na ufanisi kwenye stadi za mawasiliano yamekuwepo kwa miongo mingi kutokana na kwamba kusoma na kuandika kulishathibitisha ufanisi. Aidha kwa upande mwingine ni kwamba  maendeleo ya taifa katika  kuzungumza na kusikiliza lugha ya taifa kumekuwa na msisitizo kwenye umuhimu wa malengo ya matumizi ya lugha yenyewe.
Kutokana na hali hiyo michezo ya kuiga  inakuwa na fursa ya kuwasilisha ujumbe na kuwafikia si tu wale wanaosoma  shuleni bali pia kwa wanajamii wengine kwenye ngazi zote za elimu na inatoa fursa ya kuendeleza stadi zote  hizo.

Malengo la elimu  kwenye michezo ya kuigiza 
Michezo ya kuigiza  shuleni  huchangia  kwa njia tofauti  maendeleo ya kijamii  na mtu binafsi kwenye kujifunza. 
Katika hatua zote zile za mchezo  hutoa fursa kwa wanafunzi kuingia kifikra kwenye ulimwengu mwingine  kwa kuyachukua masuala mbalimbali  na kutafiti uhusiano kutokana na mitazamo ya watu.
Kwa upana zaidi ni kwamba  elimu inayotokana na michezo ya kuigiza  shuleni inawapa wanafunzi  fursa za kuendeleza uelewa wao kwa kutafiti mwenendo, thamani na tabia, kujenga uhusiano, ushirikiano kwenye kundi, kutafsiri na kuchambua, kuwasiliana na kuwasilisha.
Kwa upande mwingine  sanaa  hii ya kujieleza inamtaka mwanafunzi kujenga uelewa wao wenyewe na wengine  kupitia  kuigiza, kujijengea ubunifu, kujenga mawazo ya kuwasiliana na kushawishika kutumia lugha, kujieleza  na mwenendo wa mazingira halisi na ya ubunifu.
Aidha inalenga kwenye kujenga kujiamini  kwenye uhusiano wao na wengine na ungamuzi  kwa wengine na kujenga stadi na mbinu  mbalimbali  kupitia uigizaji.
Kama  inakuwepo kozi hali ambayo inawahusu zaidi wanachuo  kutokana na mitaala ya shule za msingi na sekondari hapa nchini kutokuwa na somo hilo kwenye mitaala yake  huwezesha  mwanachuo kuyafikia malengo yake mahsusi.
Miongoni mwa malengo hayo ni pamoja kwa kutumia zana, mbinu, stadi na vyombo vya habari na    humtaka mwanafunzi  kuchunguza na kufanya majaribio kwenye uhusiano, mwendendo wa kuajiri,  kucheza, lugha, matumizi ya zana za kujifunza, sauti na mwanga.
Katika kuelezea hisia, mawazo, fikra na suluhisho huwapa wanafunzi fursa ya  kutoa michango  na uhusiano katika kutafiti tabia za binadamu kwenye mipangilio mbalimbali. Katika mazingira ya ushirikiano ni lazima watashirikiana miongoni mwao wenyewe katika kukubaliana  na tafsiri na kuwasiliana na kuwasilisha.
Lengo jingine ni kutathmini na kutambua vema ambako kunawapa wanafunzi  fursa za kuangalia, kusikiliza na kutafakari. Hali hiyo inawajenga kutambua mchango wao  wenyewe na mchango wa wengine.
Hali hiyo pia inajenga kutambua ufanisi wa  kitaaluma na ridhaa na mchango wa vyombo vya habari. Wanafunzi huwa na msukumo wa kutumia kile ambacho wameshajifunza wakati wanapokabiliana na masuala mengine yanayotokana na uzoefu.
Katika hatua nyingine inaweza kuelezwa kuwa tamthilia zinapoigizwa hutoa mchango maalumu na muhimu kwa mtu binafsi, kukua kwa jamii pamoja na ukomavu wake.
Katika mazingira hayo ni kwamba tamthilia  hujenga uelewa wa mtu  binafsi na wengine  kupitia  ugunduzi wa uhusiano, kutumia lugha, mikakati na mbinu katika maonesho, ugunduzi wa hali na thamani, uzoefu wa ubunifu, kufanya kazi  pamoja na wengine, kujenga uelewa wa msingi na kutoa msukumo wa kupenda na kufurahia tamthilia.
Kimsingi kwenye ubunifu ushiriki wa wanafunzi huwezesha kuwa na mwitiko unaochochea uelewa na  kutumia lugha sahihi na mwenendo mzima wa tamthilia na kwa kufanya hivyo wanakuwa wamegundua uhusiano uliopo katika mazingira wanayoishi.
Katika kuwasilisha wanafunzi hujikuta wakishirikiana pamoja  mazao ya  kazi yao ya ubunifu pamoja na watazamaji ambao wanakuwa wameingizwa kwenye shughuli za maonesho. Uwasilishaji ni kazi ya kikundi  lakini mchango wa mwanafunzi mmoja mmoja unaweza kutambuliwa. 
Kwa upande wa suala la maarifa na kuelewa wanafunzi huweza kupata habari, uzoefu na kuzitambua  stadi  zinazotolewa kupitia tamthilia.
Mifano ya tamthilia ambazo zimewahi kutumiwa kwenye fasihi  kwenye mihtasari ya masomo ya lugha kwa shule za sekondari ni pamoja na Ngoswe; Penzi Kitovu cha Uzembe Kazini, iliyoandikwa na Eddi Ganzel na Mashetani iliyoandikwa na Ibrahim Hussein.
Mfano katika tamthilia ya Mashetani kwa mtazamo wa juu juu fikra inaweza kuwa ni kusoma mambo ya mashetani lakini undani wake unaonesha jinsi mfumo wa kinyonyaji unavyokandamizi jamii wakati wengine wakitumbua raha kutokana kwa kuzifaidi mali au rasilimali zinazostahili kuwa ni za wote.
Fasihi andishi mara nyingi huwa na na mafumbo ambayo yanahitaji upeo mpana wa kuelewa  na hata hivyo inapoingizwa katika maigizo katika tamthiliya huwezesha ujumbe unaowakilishwa kufika kwa urahisi.
Hapo ndipo mtazamaji au  aliyewahi kuisoma  na kubakia akiwa na mawazo yanayoelewa  hufumbuliwa upande mwingine wa fikra na kuiona taswira iliyo sahihi kuwa ujumbe wake ulikuwa unamaanisha au unalenga jambo fulani.
Kwa kusoma tu tamthiliya hizo inachukua muda kupata ujumbe unaowasilishwa lakini kwenye maigizo inakuwa ni  rahisi zaidi kupata  ujumbe  huo na taswira inayowasilishwa na mwandishi kwa jamii inaonekana wazi badala ya kuitafuta picha hiyo kwa kusoma tu.
Inaweza kuelezwa kwa lugha rahisi kuwa kuigiza tatmthilia ni kusoma kwa vitendo kama inayokuwa kwenye  masomo ya sayansi ambako hufanyika majaribio baada ya kupata uelewa kwa njia ya  nadharia  za  somo husika.

Comments