Chifu wa sasa wa Wasangu, Salehe Alfeo Merere akiwa na mwandishi wa makala haya.
NA
INNOCENT NG'OKO, MBARALI
HISTORIA
ya kiongozi wa kabila la Wahehe, Mkwavinyika Munyigumba, maarufu kama Chifu
Mkwawa, haiwezi kukamilika bila kumtaja Chifu Merere wa kabila la Wasangu.
Hii ni kwa
sababu machifu hao wawili wa historia ya pekee, kwani licha ya wao wenyewe
kupigana, lakini kwa Chifu Merere ndiko mahali ambako kulitumika pia
kudhoofisha nguvu za Mkwawa hadi Wajerumani wakamshinda.
Chifu
Merere ni miongoni mwa machifu maarufu nchini Tanzania, hususan katika Nyanda
za Juu Kusini, pamoja na Mkwawa na Mbeyela wa Njombe.
Huyu
Merere alikuwa kiongozi wa kabila la Wasangu aliyetawala katika Bonde la Usangu,
Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya, bonde maarufu hivi sasa kwa kilimo cha mpunga pamoja
na kuwa ndiyo chanzo cha Mto Ruaha Mkuu wenye manufaa makubwa katika kilimo
pamoja na uzalishaji wa umeme katika mabwawa ya Mtera na Kidatu.
Ukifika Wilaya
ya Mbarali katika Kata ya Utengule-Usangu katika eneo la Mbalino utakuta Ngome
kubwa ya Chifu Merere, ambako ndiko chifu huyo alikotengeneza himaya kubwa.
Ngome ya Chifu
Merere ndiyo pekee inayouweka Mkoa wa Mbeya
kwenye ramani ya mmoja wa machifu madhubuti waliokuwa na himaya kubwa na
utawala imara ambao ulifanikiwa kuwaogopesha wakoloni wa Kijerumani kabla
hawajarejea tena kwa mbinu mpya za Umisionari.
Ukifika eneo
hilo la Mbalino kwenye Kata ya Utengule-Usangu utaona magofu ya ngome ya Chifu
Merere iliyojengwa tangu mwaka 1896 na Waarabu.
Hapa
utapata simulizi nyingi zikiwemo mbinu za Chifu Merere alizotumia kujiimarisha
kijeshi dhidi ya mahasimu wake wakiwemo Wahehe, Wasafwa na Wajerumani.
Kumbukumbu
zinaonyesha kuwa hadi kufikia mwaka 1830, Chifu Merere alikuwa amejiimarisha
kijeshi na kuwa moja ya machifu tishio wakati wa Ukoloni, hivyo kufanikiwa
kutanua himaya yake baada ya kuwapiga majirani zake, hasa Wasafwa.
Katika
eneo la Utengule, Mji wa Mbarizi Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Vijijini, kuna
ngome nyingine ndogo ambayo ilijengwa chifu huyo wa Wasangu baada ya kuwashinda
majirani zao Wasafwa. Ngome hiyo ndogo
aliitumia kujificha alipokuwa akizidiwa kivita.
Historia
inaonyesha, himaya ya Chifu Merere ilianzia katika eneo la Ngelyama lililopo
ndani ya Hifadhi ya Ruaha ambapo Chifu Merere aliyefahamika kwa jina la
Mwahavanga alikuwa amejiimarisha.
Baada ya
kifo cha Chifu Merere Mwahavanga hatimaye utawala ulichukuliwa na mwanaye
aliyefahamika kwa jina la Chifu Merere Mgandilwa, ambaye alijikita kuimarisha
ngome iliyopo eneo la Utengule-Usangu.
Ngome
ndogo katika eneo la Utengule katika Mji wa Mbarizi wilayani Mbeya Vijijini ilikuwa
inasimamiwa na ndugu yake Mgandilwa, Chifu Merere Tovela Mahamba, ambapo mpaka
sasa unaweza kuliona kaburi lake katika eneo hilo.
Chifu wa
sasa wa kabila la Wasangu, Salehe Merere, ambaye alitawazwa akiwa na miaka 20
tu mwaka 1988, anasema ngome ya machifu
karibu wote waliowahi kutawala katika Bonde la Usangu imekuwa kivutio kikubwa
kutokana na wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi wanaotembelea eneo
hilo.
Anasema,
mbali na kuwepo kwa ngome hiyo, wageni wanaofika hujionea makaburi ya baadhi ya
machifu wa Wasangu, akiwemo Chifu Alfeo Merere Nkahanga, na machifu wengine
waliopita katika tawala mbalimbali za kabila hilo.
Ukifika katika
Ngome ya Chifu Merere, utapata simulizi mbalimbali zenye kusisimua za nyumba maalum
zenye makaburi ndani yake, ambayo ni ya machifu waliowahi kutawala kwa nyakati
tofauti.
Kwa mgeni
yeyote atakayetembelea eneo hilo atajionea kaburi la Binti wa Mkwawa wa kabila
la Wahehe, aliyefahamika kwa jina la Mapuga, ambapo Chifu Merere na Chifu Mkwawa
walibadilishana mabinti kwa lengo la kumaliza mapigano ya kivita baina yao.
Katika eneo la Ngelyama ndani ya Hifadhi ya Taifa ya
Ruaha ndiko kuna eneo la kufanya ibada za kimila (matambiko) ya kabila la Wasangu
ambayo yanatajwa kuwa na zaidi ya miaka 200. Machifu wote wa kabila hilo
wamekuwa wakienda kufanya matambiko katika eneo hilo.
Miongoni
mwa machifu wa Wasangu waliowahi kutawala katika himaya hiyo ni Mui'Gumbi
Merere I –(1834-1860), Tovelamahamba Merere II (1860-1893), Mugandilwa Merere
III (awamu ya kwanza 1893-1896 ), Mugandilwa Merere III (awamu ya pili
1896-1906), Mxabuwoga Merere IV (1906-1950).
Wengine ni
Myotishuma (1950-1953), Alfeo Mugandilwa Merere V (1953-1962), Yusuf Merere VI
(awamu ya kwanza 1962-1988), Ahmed Merere VII (1989 – 2002), Yusuf Merere VI (awamu
ya pili 2002 – 2003) na chifu wa sasa - Salehe Alfeo Merere VIII (2003-mpaka
sasa).
Ili
kuhakisha mazingira ya Ngome ya Chifu Merere yanaboreshwa na kuwa imara zaidi, Mbunge
wa Jimbo la Mbarali, Haroon Pirimohomed ameanza kuonyesha njia kwa kutoa fedha
ambazo zitasaidia ukarabati wa jengo la boma hilo ambalo lilianza kubomoka.
Mbunge
huyo anasema, sehemu hiyo ndiyo ya historia ya Wasangu ambayo inapaswa kulindwa
na kuhifadhiwa kwa ajili ya vizazi vijavyo na kuwa wageni mbalimbali wanaoembelea
eneo hilo wataweza kujifunza mambo
mbalimbali kuhusiana na historia
ya machifu wa kabila hilo.
Ofisa
Utalii katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Patrick Charles, anabainisha
kuwa, Ofisi ya Mkurugenzi imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha eneo la Himaya
ya Chifu Merere inaboreshwa kwa kuyafanyia ukarabati majengo yake.
"Ofisi
ya Mkurugenzi imejipanga kuhakikisha majengo katika himaya ya Chifu Merere
yanaboreshwa kwa kuyafanyia ukarabati
ili kuligeuza eneo hilo kuwa la kitalii kutokana na kuwa mpaka sasa kuna
wageni wengi ambao wanakwenda kutembelea," anasema Charles.
Aidha,
anasema, katika Shule ya Msingi Ibara katika Mji wa Rujewa, kuna eneo ambalo
halmashauri imetenga kwa ajili ya mambo ya kihistoria yakiwemo ya Chifu Merere
na vivutio mbalimbali vya kitalii vilivyopo katika Wilaya ya Mbarali.
Anasema, Ofisi
ya Utalii imejipanga kuhakikisha inavitangaza na kuviboresha vivutio vya utalii
vilivyomo katika wilaya hiyo kwa lengo la kuwawezesha wageni kutembelea kwa
wingi na kuongeza fursa za kiuchumi kwa wakazi wa Mbarali.
Ofisa Utalii
huyo anasema, mbali na kivutio cha utalii cha Ngome ya Chifu Merere, Wilaya ya
Mbarali imejaliwa kuwa na vivutio vingi na miongoni mwake ni Mlima Ngoni wenye
historia ya Wangoni uliopo katika Kijiji cha Chamoto, Kata ya Igurusi.
Anavitaja
vivutio vingine kuwa ni Mti mkubwa wenye historia ya kufanyika mapatano na
usuluhishi kati ya Chifu Mkwawa na Merere katika Kijiji cha Luwango, Kata ya
Ipwani na Masalia ya Kiwanda cha kutengenezea zana za Kale katika Kijiji cha
Mlungu, Kata ya Miyombweni.
Pia
anasema, kuna mabaki ya Ngome ya Wajeruman iliyopo katika Kiiji cha Ibelege,
Kata ya Ipwani.
Wilaya
hiyo imepakana na Hifadhi za Taifa za Ruaha na Kitulo na Pori la Akiba la
Mpanga Kipengere ambapo mgeni yeyote anayefika anaweza kutembelea hifadhi hizo
kwa urahisi zaidi.
CHANZO: TANZANITE
Comments
Post a Comment