Featured Post

WATANZANIA WASIKITISHWA NA KIFO CHA MTOTO WA MUNA LOVE

Patrick Dickson


NA MWANDISHI WETU
MTOTO wa msanii wa Filamu za Bongo na Mjasiriamali, Rose Alphonce maarufu kama 'Muna Love', ameaga dunia.

Mtoto Patrick Dickson ambaye alikuwa na umaarufu sana katika mitandao ya kijamii amefariki jana Julai 3, 2018 nchini Kenya alikokuwa akipatiwa matibabu.
Patrick alianza kuugua tangu mwaka 2016, ambapo alisumbuliwa zaidi na maradhi ya mguu hali iliyompelekea kushindwa kutembea.
Kuanzia hapo Patrick alilazwa na kufanyiwa upasuaji mara kadhaa kwa lengo la kutafuta suluhu ya afya yake.
Mwaka 2017 Patrick alirejea tena na kuonekana akiwa na afya nzuri japo alikuwa akichechemea mguu mmoja.
Muna Love aliweka wazi kuwa ameokoka kwa kurusha video akihubiri Neno la Mungu, pia alionekana na wasanii mbali mbali wa muziki wa injili kama vile Joel Lwaga, Chris Shalom na Jimmy Psalmist.
Siku chache zilizopita taarifa zilizagaa mitandaoni kuwa Patrick amezidiwa na kulazwa katika hospitali iliyopo Nairobi nchini Kenya.
Taarifa za kuugua kwake zilisambaa katika kurasa mbali mbali za mitandao ya kijamii na wengi wakimuombea apone haraka.
Lakini jana wafuasi wake waligubikwa na simanzi baada ya taarifa za kifo chake kusambaa.
Wasanii na watu mbali mbali ndani na nje ya Tanzania wamerusha salamu za kumwombea Patrick apumzike kwa amani.
Mpaka sasa kupitia mitandao ya kijamii Watanzania mbali mbali waliopo ndani na nje ya nchi wanahamasishana kuchanga fedha ili kumsaidia mama yake aweze kuurejesha mwili wa Patrick Tanzania kwa ajili ya mazishi.
Patrick, maarufu kama Pat da Smart Boy, ni mtoto mwenye vipaji mbali mbali kama vile mwigizaji na mwana mitindo.
Miongoni mwa wanaouzungumzia msiba huu wanasema watamkumbuka Patrick kwa ujasiri wake, kuhubiri Neno la Mungu pia utanashati wake namna alivyokuwa akivaa na kupendeza.
Patrick alifahamika na wengi na kupata wafuasi zaidi ya 124,000 katika mtandao wa Instagram pekee.


Comments