Featured Post

MAPAMBANO DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA YATAPUNGUZA MAAMBUZI YA VVU TABORA

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akifungua warsha ya wanakamati wa Kamati ya kukomesha ukatili wa kijinsia Mkoani Tabora wakati wakijadiliana jinsi ya kutokemeza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa watoto, ndoa za utoto, na ukatili kwa wanawake na baadhi ya waume ikiwa ni njia ya kupunguza maambukizi mapya ya UKIMWI.


NA TIGANYA VINCENT
MKOA  wa Tabora ni miongoni mwa maeneo hapa nchini ambayo bado yakabiliwa na kiwango cha juu cha ukatili wa kijinsia ikiwemo ndoa na mimba za utotoni, pamoja na vipigo kwa wanawake kutoka kwa waume zao na baadhi ya wanaume wachache kupigwa na wake zao.

Hali hiyo imekuwa ikijidhihirisha katika maeneo mbalimbali kwa mfano mwaka jana kulitokea matukio makubwa na kusikitisha ikiwemo mauaji ya wanawake watano wilayani Nzega kwa kupigwa na kuchomwa moto na kule Wilayani Uyui wanawake wanne walinusurika kuwawa lakini wakiwa tayari wamepigwa na kudhalilishwa kijinsia.
Tukio jingine lilitokea hivi karibuni ambapo Jeshi la Polisi katika Wilaya ya Kaliua kwa kushirikiana na wananchi wenye huru lilifanikiwa kuwaokoa wananawake wane ambao walikuwa wachomwe moto kwa imani ya kishirikina
Matukio hayo hayaishi katika mauaji na vipigo kwa wakinamama bali pia kuna kiwango kikubwa cha mimba za utotoni kwa watoto walio chini ya miaka 18.
Mgamga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Gunini Kamba anasema jumla ya watoto 11,332 walio chini ya miaka 18 mkoani  hapa walipata  ujauzito katika kipindi cha  Januari hadi Juni mwaka huu.
Kufuatia matukio hayo na mengine ambayo yanahusu unyanyasaji wa kijinsia, Mradi wa Sauti unawakutanisha Wadau wa Kamati ya kukomesha ukatili wa kijinsia Mkoani Tabora ili kujadiliana jinsi ya kutokemeza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa watoto, ndoa za utoto, na ukatili kwa wanawake na baadhi ya waume ikiwa ni njia ya kupunguza maambukizi mapya ya UKIMWI.
Akifungua warsha hiyo ya siku moja Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri anasema njia ya kwanza ya kutokomeza ukatili kwa wanawake na watoto ni kuwaelimisha na kuwawezesha kiuchumi ili waweze kuwa na sauti ya kufanya maamuzi katika masuala mbalimbali yanayowahusu wao na jamii zao.
Anasema kuwa familia ambazo zimepiga hatua kiuchumi na kielimu hazina tena na mila potofu ya kuwaozesha watoto wao katika umri mdogo na kuwapiga wanawake.
Mwanri anasema kuwa hali duni ya kiuchumi na maisha duni kwa akinamama yamekuwa yakisababisha ongezeko la ukatili wanaofanyiwa wanawake na wenza wao pamoja na unyanyasaji na uyonyaji wa aina nyingine.
“Kipato duni ndio kinawafanya baadhi ya wanawake kupika chakula kwa kutumia kuni na hivyo kusababisha macho kuwa mekundu na hapo ndio tatizo linapoanzia kwa wanajamii ambao wana imani potofu ya kudhani kuwa na macho mekundi ni dalili za uchawi , kumbe yametokana maisha duni yanayosababisha matumizi ya kuni zaidi kama nishati ya kupikia…imi naona tukiweza kueleza tatizo hilo la umaskini na kuliondoa kwa akina mama na kuwasaidia kujikwamua kielimu na kiuchumi tutapunguza ukatili unaosababishwa na mila potofu zinazotokana na ujinga” anasema.
Anasema pia ni vema jamii ikawapa fursa ya ajira wanawake ili waweze kuwa na kipato ambacho kitawasaidia wao katika kupunguza utegemezi kwa wanaume.
Mwanri anasema kuwa  upande wa Serikali inajitahidi kutoa elimu na kutumia sheria zilizopo katika kuzuia ukatilii wa kijinsia na pia imeweka mazingira ya kuwawezesha kupitia vikundi watakavyojiunga pamoja katika kujiendeleza kwa kuziagiza Halmashauri zote hapa nchini kuhakikisha zinatenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya kuwapa mikopo wanawake, vijana na walemavu.
Afisa Mradi wa Masuala ya kupinga Ukatilii wa Kijinsia kutoka Shirika la Jhpiego Shangwe Kimathi anasema warsha hiyo ililenga kuwajengea uwezo wa wadau mbalimbali ili wanaporudi katika maeneo yao wawe na mbinu mpya za  kupambana na ukatilii wa kijinsia kwa wanawake na watoto ikiwa ni sehemu ya kupunguza maambukizi mapya ya VVU.
Anasema baadhi ya watoto na wanawake wajikuta wakipata maambukizi ya VVU kwa sababu ya kubakwa, kulazimishwa kuolewa katika umri mdogo, kutumikishwa katika biashara ya ukahaba na katika kumbi za starehe.
Mrakibu wa Polisi kutoka Mkoa wa Tabora (SP)Ali Hamad anawataka watu wote wanaotendewa ukatili kuwa wazi kuwafichua waliowafanyia vitendo hivyo ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria.
Anasema mara nyingine familia ya wahanga wanapatama na upane wa familia ya mtuhumiwa na hivyo kupoteza ushahidi ambao ungesaidia kumtia hatiani mtuhumiwa wa kitendo cha ukatili wa kijinsia.
Naye Koplo Adelina Mgoha kutoka Dawati la Kijinsia Wilaya ya Tabora anatoa wito kwa wanaume ambao wanafanyiwa vitendo vya kikatili na wenza kutoona aibu kutoa taarifa ili waweze kusaidia badala ya kukaa nalo moyoni.
Anasema woga wa baadhi ya wanaume  ndio umekuwa ukisababisha baadhi ya wanaume ambao wanafanyiwa vitendo vya kikatili na wake zao kunywa sumu, kujiua na kufanya mauaji kwa watu ambao wanawadhani ni adui zao.
Adelina anasema hatua hizo zinaacha simanzi kubwa kwa wanafamilia na wakati mwingine kujenga uadui zaidi kati ya familia ya mwanamke na ya mwaume na hivyo kusababisha watoto kubaki njia panda.
Kwa upande wa suala la ushahidi anasema kuwa wakati mwingine inakuwa vigumu kupata ushahidi kutoka kwa wat waliofanyiwa vitendo vya kikatili kwa sababu wanakuta wameogeshwa na kupoteza ushahidi.
Aidha Mradi wa SAUTI kupitia Shirika la Jhpiego kusaidia katika ujenzi wa vyumba katika vituo vya Polisi ambavyo vitatoa usiri na kutoa uhuru kwa mtu aliyefanyiwa ukatili wa kijinsia kuweza kujieleza vizuri na kutokuwa na wasiwasi wa kusikilizwa na kila mtu hata ambaye hausiki  na Dawati.
Naye Mwanasheria kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora Richard Lugomela anasema ukatilii wa kijinsia unaweza kuwa kimwili, kisaikolojia, kingono, kiuchumi na unaotokana na mila potofu, mfumo dume, ndoa za utotoni, ulevi kupindukia, uasherati , matumizi mabaya ya fedha , umaskini, wivu na matumizi mabaya ya madaraka.
Mwanasheria huyo anasema ukatili wa kijinsia unasababisha kupotea kwa amani na upendo ndani ya familia, kujenga uhasama,kupoteza nguvu kazi ya jamii, ongezeko la watoto mitaani, maendeleo duni na kupoteza rasilimali na kuongezeka kwa umaskini.
Lugomela anasema ni vema yanapojitokeza matendo ya ukatili wa kijinsia taarifa zitolewe mapema katika vituo vya polisi kupitia dawati la jinsia, Afisa mtendaji wa Kata, Afisa maendeleo ya jamiii, Afisa ustawi wa Jamii na kwenye vyombo vya msaada wa kisheria (paralegal)
Anawataka wahanga wa vitengo ukatili wa kijinsia wanatakiwa kufuata taratibu zote zinazotakiwa wanaporipoti tukio hilo ili kutopoteza ushahidi ambao ndio utamtia hatiani mtuhumiwa.
Lugomela anasema wahanga wengine wamekuwa wakipelekea hati maalumu ya Polisi kwa ajili ya kupata matibabu(PF3 ) ikiwa haina mhuri na hivyo kuonekana kama sio nyaraka halali.
Anaongeza kuwa wengine wamekuwa wakiwacha kutoa taarifa kwa  viongozi walio karibu nao kama vile Mwenyekiti wa Mtaa au Kitongoji. Kijiji  na Mtendaji wa Kijiji.
Lugomela anatoa wito kwa ndugu wa wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia kufuata taratibu wakati wanapotoa taarifa za tukio la ukatili waliofanyiwa ili ziweze kumsaidia Hakimu kutoa maamuzi ambayo yanao ushahidi wa kutosha na usio kuwa na shaka.
Anasema kwenye Ibara ya 12-29 za Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977  inapinga ukatili wa kijinsia kwani inatoa kwa kuwa inatoa Haki ya kuishi , Haki ya kutokubaguliwa ,Haki ya kumiliki mali na Haki ya kupata ujira.
Lugomela anaongeza kuwa Sheria ya adhabu sura namba 16 ya mwaka 2002 kifungu cha 241 inatoa adhabu ya kifungo cha miaka mitano kutokana na Shambulio la kimwili  na kwa  mujibu wa kifungu cha 169 A kinalezea kuwa, ni kosa la jinai kwa mtu yeyote kumtesa au kumtekeleza mtoto na akipatikana na hatia atawajibika kwa adhabu ya miaka 5 na faini isiyozidi laki tatu.
Anasema kuwa Kifungu cha 131 cha Sheria ya adhabu kikisomwa pamoja na Sheria ya Makosa ya kujamiana, ubakaji adhabu yake ni miaka 30.
Kwa upande wa Sheria ya Ndoa sura ya 29 ya mwaka 1971 kifungu cha 66 kinakataza ukatili baina ya wanandoa na Sheria ya Ardhi Na. 4 na  5 za mwaka 1999 kifungu cha 3(2) kinatoa usawa wa kumiliki ardhi. Pia sheria ya usimamizi wa miradhi sura ya 352 ya mwaka 2002 ni haki ya mtoto(wakike/wakiume) kurithi mali za wazazi wake pale watakapokuwa wamefariki.
Pia Sheria ya Mtoto Na.21 ya 2009 kifungu cha 10 kinatamka kwamba ni haki ya mtoto kufurahi mali iliyoachwa na  wazazi wake.
Kwa mujibu wa kifungo cha 62 cha Sheria ya Watu wenye ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kinatoa adhabu ya faini isiyopungua milioni mbili na isiyozidi milioni 20 kwa kusababisha  uelemavu, kuweka mazingira ya  ubaguzi ama kukaidi matakwa ya watu wenye ulemavu.
Lugomela anafafanua kuwa katika Kifungu cha 21 cha Sheria ya UKIMWI, 2008 kinapiga marufuku ukatili wa kiafya kwa kushindwa kumfahamisha mwenza wako au yeyote ambae una mahusiano naye ya kimapenzi kuwa una Virusi vya UKIMWI.
Kifungu cha 22 cha Sheria ya Elimu  mwaka 1978  kwa marekebisho ya mwaka 2016kinatoa Adhabu ya miaka 30 kwa mtu atakaepatikana na kosa la kuoa mwananfunzi au kumpa mimba. Hata hivyo, kifungu hiki kimezungumzia mtu atakaesaidia kufanikisha kuolewa/kuoa kwa mwanafunzi adhabu yake ni kifungo cha  miaka mitano au faini isiyo pungua milioni tano au vyote kwa pamoja.
Anasema hakuna sheria ya moja kwa moja ya kukabiliana na suala la ukatili wa kijinsia Tanzania, kwa kuwa  ukatili wa kijinsia upo wa aina mbalimbali  na ni kutoakana na aina hizo, kumepelekea sheria hizi kuwa nyingi kulingana na aina ya unyanyasaji.
Aidha, Lugomela anasema zipo sheria ambazo bado zinamapungufu mbali mbali  yakiwemo kupitwa na wakati na kutokuendana na hali halisi ya maisha yetu ya sasa. Mfano, sheria ya ndoa Na. 29 ya mwaka 1971 bado inatoa wigo wa kwa watoto chini miaka 18 kuolewa kwa idhini ya wazazi.
Naye Meneja wa Mradi wa SAUTI kutoka Shirika la Jhpiego Flavian Ngeni anasema mradi huo unajitahidia kuhakikisha unashirikiana na wadau mbalimbali katika kukabiliana na ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto na pia kupunguza maambukizi ya VVU hapa nchini.
Anasema Mradi huo unaratibiwa na  Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za MItaa(TAMISEMI)  na kutekelezwa na Shirika la jhpiego kwa kushirikiana na  mashirika ya Engender  Heath, Pact Tanzania na NIMR tawi la  Mwanza chini ya ufadhili wa Mfuko wa dharula wa Rais wa Marekani wa kupamana na UKIMWIkupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Watu wa Marekani (USAID) .
Mradi huo ambao ni miaka mitano unatekelezwa katika mikoa 14 na Halmashauri 51 ya Tanzania Bara.

Comments