Featured Post

CHIKU GALLAWA: LAMBALAMBA MARUFUKU MKOANI SONGWE

Mkuu wa Mkoa wa Chiku Gallawa akizungumza katika kikao cha wadua wa Afya kilichofanyika katika chuo cha Uuguzi Mwambani Mkwajuni-Songwe, Kulia kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Songwe Samwel Jeremia na Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Ileje Joseph Mkude.

Waganga wote wa jadi wanaopiga ramli chonganishi maarufu kama Lambalamba wamepigwa marufuku kufanya shughuli hizo mkoani Songwe huku wenyeviti wa vijiji ambavyo lambalamba watabainika kuendelea na shughuli hizo, hatua kali dhidi yao zitachukuliwa.
Marufuku hiyo imetolewa mapema leo na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Chiku Gallawa katika kikao cha wadau wa Afya mkoani hapa ambapo ameeleza kuwa changamoto mojawapo ya sekta ya afya ni uwepo wa waganga wa jadi ambao huwapotosha wananchi kwa imani zisizo za kweli.
Gallawa amesema, “Hatutaki kuona wala kusikia hivi vikundi vya vya lambalamba, kazi yao kubwa ni ulaghai na kuwaibia fedha wananchi, na ninaagiza, mwenyekiti yeyote wa kijiji atakayebainika kuwaendekeza hawa watu tunaanza naye kumchukulia hatua kali za kisheria”.
Ameongeza kwa kuwaagiza wakuu wa wilaya zote mkoani hapa wasimamie kuhakikisha wananchi hawatapeliwi na lambalamba hususani wilaya za Mbozi na Ileje ambako lambalamba wameonekana mara kwa mara.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Waganga wa Jadi na Machifu Mkoa wa Songwe Mwenenzunda Mteleshwa amesema kuwa yeye hawatambui lambalamba hivyo serikali iwachukulie hatua za kisheria kwakuwa wanaenda kinyume na taratibu za utoaji wa huduma za jadi.
Wakati huo huo Gallawa amezitaja changamoto nyingine katika sekta ya afya mkoani hapa ni uwepo wa ugonjwa wa ebola nchi jirani ya Congo, upungufu wa vituo vya kutolea huduma za afya pamoja na uwepo wa magonjwa yanayosababishwa na uchafu kama vile kipindupindu.
Gallawa amefafanua kuwa serikali imeweka mikakati ya kuboresha sekta ya Afya Mkoa wa Songwe kwa kutoa shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya uboreshaji wa vituo vya kutolea huduma za afya pamoja na Kuimarisha huduma za kitabibu kwa kuipandisha hadhi Hospitali ya Wilaya ya Mbozi ili itumike kama Hospitali Teule ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe.
Ameongeza kuwa mkoa unatarajia kuzindua mkakati wa usafi na mazingira ukiwa na kauli mbiu ya “Kataa uchafu Songwe” lengo likiwa ni kupambana na magonjwa yanayosababishwa na uchafu na kutunza mazingira.

Comments