- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA MWANDISHI WETU, ZANZIBAR
CHAMA cha Alliance for Democratic Change (ADC) kimepongeza
uamuzi wa Serikali wa kununua ndege mpya, ikiwemo ya Boeing 787-8 Dreamliner,
na kuwataka wale wote wanaombeza Rais Magufuli wajitafakari upya.
Mwenyekiti wa ADC, Hamad Rashid Mohamed, amesema hakuna nchi
duniani inayoweza kutangaza utalii wake bila kuwa na shirika la ndege imara
linaloendeshwa kwa ufanisi ili kukuza uchumi wake, biashara na mawasiliano.
Jumapili, Julai 8, 2018, Rais John Magufuli aliwaongoza
Watanzania kuipokea ndege ya abiria aina ya Boeing 787-8 Dreamliner kutoka
Seattle, Marekani ambayo imenunuliwa na Serikali kwa fedha taslimu, ikiwa
miongoni mwa ndege saba zilizopangwa kununuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
Mpaka sasa tayari ndege nne zimekwishawasili nchini na
nyingine zinafanya safari katika miji takriban 12 pamoja na Visiwa vya Comoro,
wakati ndege nyingine mbili zinatarajiwa kuwasili Novemba mwaka huu na
Dreamliner nyingine itawasili mwaka 2020.
Hamad amesema, jitihada za Rais Magufuli kulifufua Shirika
la Ndege la Tanzania (ATCL) zinahitaji kuungwa mkono kwani kuimarika kwake kutafungua
milango na kutanua wigo wa uchumi, utalii, kuvutia
wawekezaji na kukuza biashara za ndani na nje.
Alisema utalii ni moja kati ya sekta inayoongoza duniani na
alama mojawapo ya nchi kujitangaza kimatiafa ni kuwa na shirika lake la ndege
kama anavyotaka Rais Magufuli.
Hamad alisema, ni jambo la ajabu nchi ndogo kama Rwanda na Shelisheli
zina mashirika imara ya ndege huku nchi kubwa kama Tanzania ikiwa haina ndege
hata moja kama ilivyokuwa kabla ya ujio wa ndege mpya.
"Nchi inapokuwa na shirika lake la ndege ni kukuza
teknolojia na kuzalisha ajira mpya za ndani na nje, kwa wahandisi, marubani, wahudumu
pia biashara zitapanuka," alisema Hamad.
Alisema, wanasiasa wanaobeza hatua hiyo ya Rais wanahitaji
kutafakari maradufu kwani mpango wa kuwa na shirika ulikuwepo toka awamu ya
kwanza na anachokifanya Rais Magufuli sasa ni uthubutu wake wa kulifufua na
kuitakia mema nchi yake.
"Ipo haja ya kuwa makini katika kuwekeza mtaji wa
kutosha, umakini wa menejimenti, matengenezo ya huduma za ndege, tuna nafasi ya
kufanya vizuri, mfano mzuri wa mashirika madogo ya ndege za ndani yalivyoanza
na sasa yanavyotoa huduma bora," alieleza.
Alisema, Tanzania ina nafasi kubwa ya kutumia viwanja vyake
vyenye idadi ya wakazi wanaofikia
milioni 3 hadi 6 na iwapo vitatumika kwa
kujali soko la ndani na nchi jirani kama kongo, Rwanda, Uganda, Kenya na
Burundi na wanaobeza pengine hawatambui
umuhimu wa usafiri wa anga na reli.
"Anayebeza hajui misingi ya uendeshaji wa kibiashara, miundombinu
ni msingi mkubwa wa kukuza biashara zikiwemo barabara, reli, usafiri wa majini
na anga ni mambo yanayohitaji kutazamwa kwa muhimu wake," alieleza.
Mwenyekiti huyo wa
ADC alisisitiza kuwa, maeneo hayo ni lazima yapewe kipaumbele kwani hata wakati
wa utawala wa Mwalimu Julius Nyerere kulikuwa na mashirika mengi kama Tacoshil,
Nasaco, Dahaco, TRC, ATC, Kamata na UDA.
Alisema, katika nchi yoyote ikiwa watu hawazungushi biashara
kitaifa na kimataifa, uchumi hauwezi kukua.
"Kama huna usafiri wa ndege, barabara na reli utakwama.
Kuna Watu hawawezi kupanda treni, kwa muda mrefu wanapatanda ndege, lazima
fursa kama hizo ziwepo katika nchini," aliongeza.
Alitoa mfano wa China ambayo imeanzisha treni inayokimbia kwa
kasi kuliko zote duniani ili kuwafanya wafanyabiashara wake kuwafikia watu
wengi, lengo likiwa ni kuwapa nafasi kufanya biashara kwa uharaka na usahihi.
Katika hatua nyingine, chama hicho kimesema mradi wa
uzalishaji umeme wa maji wa Stigler's Gorge utamaliza matatizo ya nishati
nchini na kuchochea shughuli za maendeleo.
Chama hicho kimesema, ni aibu kwa Tanzania kutokuwa na
megawati 5,000 wakati vyanzo vya kuzalisha nishati hiyo vipo vya kutosha, hivyo
uamuzi wa sasa unastahili kuungwa mkono.
Mwenyekiti wa ADC Taifa, Hamad Rashid Mohamed, alisema jana
kwenye Makao Makuu ya chama hicho huko
Bububu, Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi kisiwani hapa kwamba,
suala la kujenga miradi kama huo wa Stigler's Gorge katika Bonde la Mto Rufiji
ni la muhimu kwa kuwa umeme ni nishati muhimu kwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.
"Tumeshuhudia wenyewe namna umeme kidogo ulopelekwa
vijijini ulivyosaidia kubadilisha hali za masiha ya watu kiuchumi na kijamii,
kwahiyo kukamilika kwa mradi huu wa Stigler's Gorge kutakuwa na manufaa makubwa
kwa Taifa zima," alisema.
Hamad alisema, licha ya kuwa umeme ni usalama wa nchi,
lakini pia ni fursa pekee ya kufikiwa kwa maendeleo ya kweli kwani ndoto ya
Tanzania ya Viwanda haiwezi kufikiwa ikiwa
hakuna umeme wa uhakika.
Alisema, kukamilika kwa mradi huo wa umeme wa maporomoko ya
maji huko Rufiji bila shaka kutakuwa na tija kubwa ya kupatikana umeme wa kutosha, jambo ambalo litatoa nafasi kwa
wananchi kujituma, kuzalisha mali na kufanya kazi kwa bidii.
"Huwezi kupata maendeleo ikiwa unatumia umeme usio na
uhakika, wataalam wanasema ili nchi ipate maendeleo ya kweli, lazima kuwe na
matumizi ya umeme na akiba ya megawati asilimia 35 kwa tahadhari," alisema
Hamad.
Alisema, kutengemaa kwa mradi huo kuna faida nyingi kuliko
kutokuwepo kwake, hivyo ni lazima kwanza tutazame manufaa ya mradi wenyewe na
tija yake kwani kunahitajika nchi iwe na vyanzo vingi kama vya umeme wa gesi, mawimbi
ya bahari, upepo na maji.
Akizungumzia uamuzi wa hivi karibuni wa Rais John Magufuli
kukutana na viongozi wastaafu ili kupata
maoni na ushauri, alisema ni jambo jema kwani viongozi hao wamebahatika kushika
nyadhifa za juu na sasa wamepanuka maarifa na kuwa na uzoefu kuliko mtu
mwingine ambaye hajashika nafasi hizo.
"Viongozi wastaafu wameongoza nchi na kushika nyadhifa
kadhaa za juu, sasa wako nje ya uwanja ni rahisi kutazama makosa na kumpa
ushauri, uzoefu waliopata unatosha wanajua makosa yao na mafanikio, hivyo
wamemshauri kwa nia njema," alisema.
CHANZO: FAHARI YETU
Comments
Post a Comment