Featured Post

KOMBE LA DUNIA 2018: MO SALAH YUKO SAWA KUCHEZA DHIDI YA URUGUAY WALIO NA LUIS SUAREZ NA EDISON CAVANI



MOSCOW, RUSSIA
KOCHA wa timu ya taifa ya Misri Hector Cuper amesema kuna uwezekano wa "karibu 100%" kuwa mshambuliaji Mohamed Salah atacheza mechi yao ya kwanza Kombe la Dunia mwaka huu leo Ijumaa dhidi ya Uruguay.

Mechi hiyo itachezewa mjini Yekaterinburg na itaanza saa tisa alasiri saa za Afrika Mashariki.
Salah, 25, hajacheza tangu alipoumia begani wakati wa fainali ya Kombe la Klabu Bingwa Ulaya mnamo 26 ambapo timu yake ya Liverpool ilishindwa 3-1 na Real Madrid.
"Ninaweza kuwahakikishia karibu 100% kwamba atacheza, pengine kutokee mambo yasiyotarajiwa dakika za mwisho," amesema Cuper.
"Anaweza kuwa mfungaji mabao bora hapa na mmoja wa wachezaji nyota zaidi."
Cuper amesema Salah "anafanya vyema sana" na kwamba alipata nafuu "haraka sana, sana."
Aliongeza: "Tunajaribu kumfanya ajiamini zaidi. Madaktari wanampa fursa ya kuamua kama atacheza au hatacheza, lakini namfahamu Salah vyema sana na nina uhakika kwamba hana wasiwasi, hana woga."
Beki wao Ali Gabr pia anatarajiwa kuwa sawa kucheza baada ya kuumia usoni wakati wa mazoezi.
Uruguay upande wao wanatarajiwa kuchezesha kikosi cha wachezaji wachanga hasa safu ya kati, ambapo watakuwa pia na kiungo wa kati wa miaka 20 Rodrigo Bentancur na Nahitan Nandez, 22.
Lakini kwingineko, kikosi chao kina wachezaji wazoefu, na hata zaidi safu ya mashambulizi ambapo wana Luis Suarez na Edinson Cavani.
Mataifa hayo mawili yamo Kundi A pamoja na Urusi na Saudi Arabia.

Sababu ya wengi kuwapigia upatu Uruguay?
Maandalizi ya mechi hii ya leo jioni yamegubikwa na suala la Mo Salah na iwapo atacheza.
Alijiunga na kikosi cha Misri Jumatano kwa mazoezi ambapo alipasha misuli moto nao, lakini akamaliza sehemu iliyosalia ya mazoezi pekee.

Mechi za leo:
Misri v Uruguay (saa 9 alasiri Afrika Mashariki)
Morocco v Iran (saa 12 jioni Afrika Mashariki)
Ureno v Uhispania (saa 3 usiku Afrika Mashariki)

Madaktari wa timu walisema baadaye kwamba wanafuatilia hali yake siku baada ya siku.
Cuper alipuuzilia mbali umuhimu wa mchezaji huyo na kusema "mbinu zetu hazimzunguki mchezaji huyo pekee."
Kuangaziwa zaidi kwa nyota huyo wa Liverpool huenda kukawasaidia Uruguay, ambao wamekuwa hawaangaziwi sana licha ya kuwa wanapigiwa upatu kushinda Kundi A.
Wana kikosi chenye wachezaji wazoefu sana, ambapo wachezaji wanne wao wamecheza zaidi ya mechi 100 za kimataifa, na kipa wao Fernando Muslera (97) na mshambuliaji Luis Suarez (98) wanatarajiwa kucheza mechi mia wakifikia hatua ya kumaliza hatua ya makundi.
Washambuliaji wao wawili Suarez na Edinson Cavani wamefunga zaidi ya mabao 93 mechi ya kimataifa kwa pamoja.
Wengi wanatarajia Uruguay washinde.
Wanaelekea kwa mechi hiyo wakiwa wameshinda mechi tatu mtawalia.
Misri hawajashinda mechi hata moja 2018 na bado hawajashinda mechi yoyote Kombe la Dunia.
MAMBO MUHIMU
Uruguay waliwashinda Misri mechi yao pekee waliyowahi kukutana awali, waliwachapa 2-0 mjini Alexandria Agosti 2006.
Uruguay hawajawahi kushindwa na timu kutoka Afrika katika Kombe la Dunia (wameshinda mara moja na kutoka sare mara mbili). Hii aidha itakuwa mara ya kwanza kwa Misri kukutana na timu kutoka Amerika Kusini katika Kombe la Dunia.

Misri
Misri hawajawahi kushinda hata mechi moja Kombe la Dunia, walitoka sare mechi mbili na kushindwa mechi mbili.
Ndiyo mara ya kwanza kwa Mafirauni kufika Kombe la Dunia tangu 1990 na mara yao ya tatu kwa jumla. Walishindwa 1-0 na England mechi yao ya mwisho waliyocheza Kombe la Dunia 1990.
Kocha wao Hector Cuper hii ndiyo mara yake ya kwanza kuongoza timu Kombe la Dunia. Michuano pekee mikubwa aliyowaongoza Misri ilikuwa wakati wa Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2017 ambapo walifika fanali lakini wakashindwa 2-1 na Cameroon.
Kipa wao ambaye pia ndiye nahodha wao Essam El Hadary huenda akaweka historia kwa kuwa mchezaji wa umri mkubwa zaidi kucheza Kombe la Dunia (akiwa na miaka 45 na siku 151).
Mohamed Salah alifunga mabao matano katika raundi ya tatu ya mechi za kufuzu Kombe la Dunia barani Afrika, zaidi kushinda mchezaji mwingine yeyote yule.
Salah anatimiza miaka 26 leo.

Uruguay
Mabingwa mara mbili wa dunia Uruguay wamefika hatua ya 16 bora mara moja pekee katika michuano sita waliyocheza Kombe la Dunia karibuni, walipomaliza nafasi ya nne mwaka 2010..
Uruguay wameshindwa mara moja pekee kati ya mechi nane walizocheza karibuni zaidi hatua ya makundi Kombe la Dunia (walishinda 4 na kutoka sare 3).
Hata hivyo, wameshindwa kushinda mechi yao ya kwanza katika michuano sita ya Kombe la Dunia waliyoshiriki karibuni, ambapo walitoka sare mara tatu na kushindwa mara tatu.
Hii ni mara ya nne kwa kocha wao Oscar Tabarez kuongoza timu Kombe la Dunia (1990, 2010, 2014 na 2018), zaidi ya kocha mwingine yeyote yule michuano ya mwaka huu.
Edinson Cavani alikuwa mfungaji bora katika mechi za kufuzu kwa Kombe la Dunia Amerika Kusini, ambapo alifunga mabao 10.
Luis Suarez amefunga mabao matano na kusaidia ufungaji wa mengine manane Kombe la Dunia.

Wachezaji

Misri
Walinda lango: Essam El Hadary (Al Taawoun), Mohamed El-Shennawy (Al Ahly), Sherif Ekramy (Al Ahly).
Mabeki: Ahmed Fathi, Saad Samir, Ayman Ashraf (all Al Ahly), Mahmoud Hamdy (Zamalek), Mohamed Abdel-Shafy (Al Fateh), Ahmed Hegazi (West Brom), Ali Gabr (Zamalek), Ahmed Elmohamady (Aston Villa), Omar Gaber (Los Angeles FC).
Viungo wa kati: Tarek Hamed, (Zamalek), Shikabala (Zamalek), Abdallah Said (Al Ahli), Sam Morsy (Wigan Athletic), Mohamed Elneny (Arsenal), Mahmoud Kahraba (Al Ittihad), Ramadan Sobhi (Stoke City), Mahmoud Hassan (Kasimpasa), Amr Warda (Atromitos Athens).
Washambuliaji: Marwan Mohsen (Al Ahly), Mohamed Salah (Liverpool).

Uruguay
Walinda lango: Fernando Muslera (Galatasaray), Martin Silva (Vasco da Gama), Martin Campana (Independiente).
Mabeki: Diego Godin, Jose Maria Gimenez (both Atletico Madrid), Sebastian Coates (Sporting Lisbon), Maximiliano Pereira (Porto), Gaston Silva (Independiente), Martin Caceres (Lazio), Guillermo Varela (Penarol).
Viungo wa kati: Nahitan Nandez (Boca Juniors), Lucas Torreira (Sampdoria), Matias Vecino (Inter Milan), Rodrigo Bentancur (Juventus), Carlos Sanchez (Monterrey), Giorgian De Arrascaeta (Cruzeiro), Diego Laxalt (Genoa), Cristian Rodriguez (Penarol), Jonathan Urretaviscaya (Monterrey).
Washambuliaji: Cristhian Stuani (Girona), Maximiliano Gomez (Celta Vigo), Edinson Cavani (Paris St-Germain), Luis Suarez (Barcelona).
BBC

Comments