Featured Post

YONDAN ‘AWAZODOA SIMBA’ AIBUKA JANGWANI NA KUTETA NA MKWASA, NYIKA



Kelvin Yondan (katikati) akiwa na Hussein Nyika (kushoto) na Kaisi (kulia) leo Jangwani 

Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM NAHODHA wa Yanga SC, Kevin Patrick Yondan ameonyesha dalili atabaki baada ya leo kufika makao makuu, Jangwani na kufanya mazungumzo na uongozi.
Yondan ambaye anahusishwa na mpango wa kurejea timu yake ya zamani, Simba SC asubuhi ya leo alifika makau ya klabu makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam na kuzungumza na Katibu, Charles Boniface Mkwasa pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Hussein Nyika.
Kabla ya kuondoka, Yondan akapiga picha ya pamoja na Nyika na mwanachama maarufu wa klabu hiyo, Kaisi – ingawa bado haijulikani mazungumzo yao yalihusu nini.
Yondan amemaliza mkataba wake Yanga SC na inasemekana na kusaini mkataba mpya kunacheleweshwa na fedha, kwa sababu klabu kwa sasa inakabiliwa na hali ngumu kiuchumi.
Yondan hayumo kwenye kikosi cha Yanga kilichoondoka mchana wa leo kwenda Kenya kwenye michuano ya SportPesa Super Cup kwa sababu ambazo hazijawekwa wazi.
Kikosi kilichokwenda Kenya kinaundwa na kipa Mcameroon Youthe Rostand, mzawa Ramadhani Kabwili, mabeki Hassan Kessy, Mwinyi Hajji Mngwali, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Pato Ngonyani.
Viungo ni Baruan Akilimali, Pius Buswita, Ajib, Maka Edward, Thabani Kamusoko, Juma Mahadhi, Said Juma ‘Makapu’, Said ‘Ronaldo’ Mussa, Papy Kabamba Tshishimbi, Yussuf Mhilu na Raphael Daudi, wakati washambuliaji ni Yohana Oscar Nkomola, Matheo Anthony na Mrundi Amissi Tambwe.
Yanga watafungua dimba na Kakamega Homeboys Jumatatu, siku moja baada ya mahasimu wao, Simba SC kumenyana na Kariobangi Sharks Jumapili, mechi zote zikichezwa Uwanja wa Afraha, Nakuru.
Mabingwa watetezi, Gor Mahia wao pia wataanza na JKU Jumapili, wakati Singida United itaanza na AFC Leopards Jumanne. 
Ikumbukwe bingwa wa michuano hiyo ataondoka kitita cha dola za Kimarekani, 30,000, mshindi wa pili dola 10,000, wa tatu dola 7,500 zitakazoishia Nusu Fainali dola 5,000 na za Robo Fainali dola 2,500.
Pamoja na dola 30,000, bingwa wa michuano hiyo kwa mwaka huu atapata fursa ya kwenda kumenyana na klabu ya Everton Uwanja wa Goodison Park mjini Walton, Liverpool nchini England.
Mwaka jana Gor Mahia ilikuwa bingwa wa kwanza wa michuano hiyo baada ya kuwafunga mahasimu wao, AFC Leopard 2-1 katika fainali kwenye michuano iliyofanyika Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
BIN ZUBEIRY

Comments