- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA
NCHI
MHE. DKT. MWIGULU LAMECK NCHEMBA
(MB.), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI
KWA MWAKA 2018/19
A.
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja
kwamba Bunge lako Tukufu, baada ya kuzingatia taarifa iliyowasilishwa hapa
Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na
Usalama, likubali kupokea, kujadili na kupitisha Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka 2018/19.
2.
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kutujalia uzima na kuniwezesha kuwasilisha Hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani
ya Nchi ambayo itajadiliwa na Bunge hili.
3.
Mheshimiwa Spika, pia natumia fursa hii kumshukuru na kumpongeza Rais
wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Kwa
kuongoza vema Taifa letu Na kuendelea kusimamia amani, utulivu na usalama
nchini. Ni dhahiri kuwa hali ya usalama ni nguzo muhimu katika kuleta
maendeleo ya uchumi wa viwanda ambayo ni azma ya Serikali ya Awamu ya Tano.
4.
Mheshimiwa Spika, vilevile, napenda
kutumia nafasi hii kuwashukuru Viongozi Wote Wakuu wa Serikali na Bunge kwa
kuendelea kusimamia shughuli mbalimbali za Taifa. Aidha, nawashukuru wajumbe wote wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya
Mwenyekiti wake, Mhe. Mussa Azzan Zungu, Mbunge wa Jimbo la Ilala, kwa
kuyachambua Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
kwa mwaka 2018/19. Ushauri uliotolewa na Kamati utasaidia katika utekelezaji wa
majukumu ya Wizara hii.
5.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa pole kwa
familia, ndugu, jamaa na marafiki waliopoteza ndugu zao kutokana na maafa, majanga
na ajali mbalimbali zilizotokea katika kipindi cha mwezi Julai, 2017 mpaka
sasa.
B.
UTEKELEZAJI
WA SHUGHULI ZA WIZARA KWA MWAKA 2017/18 NA MALENGO YA MPANGO NA BAJETI KWA
MWAKA 2018/19
Mapato na Matumizi
6. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka 2017/18 Wizara iliendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia
vipaumbele vilivyopangwa. Wizara iliidhinishiwa bajeti ya jumla ya Shilingi
930,396,817,000 ambapo Shilingi 367,706,884,000 ni kwa ajili ya Matumizi
Mengineyo, Shilingi 522,681,568,000 ni Mishahara na Shilingi 40,008,365,000 ni
fedha za Miradi ya Maendeleo.
7. Mheshimiwa Spika, hadi
kufikia mwishoni mwa mwezi Machi, 2018 Wizara ilipokea jumla ya Shilingi
725,328,535,604 sawa na asilimia 78 ya bajeti yote. Kati ya fedha hizo,
Shilingi 21,800,000,000 zilikuwa ni kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo, sawa na asilimia 54 ya bajeti ya maendeleo, Shilingi
367,055,054,909 zilikuwa ni Mishahara na Shilingi 336,473,480,695 ni kwa ajili
ya Matumizi Mengineyo. Pia, Wizara ilikusanya mapato ya Shilingi 187,075,690,821
sawa na asilimia 63 ya lengo la kukusanya Shilingi 293,822,132,859. Katika
mwaka 2018/19 Wizara inatarajia kukusanya jumla ya Shilingi 297,014,614,300.
Mafanikio ya Wizara
8. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza majukumu na shughuli za Wizara kwa kipindi cha Julai,
2017 hadi Machi, 2018 mafanikio mbalimbali yamepatikana ikiwa ni pamoja na: kukamilika
kwa ujenzi wa nyumba za kuishi familia 32 za askari
wa Jeshi la Polisi Mkoani Arusha; kukamilika kwa ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Rungwe; kukamilika kwa asilimia 97 kwa ujenzi wa Vituo
vya Polisi Daraja A Mburahati na Daraja B Mbweni – Dar es Salaam;
kuhuishwa kwa mfumo wa ufuatiliaji wa mienendo ya kesi za jinai ili kuharakisha
upelelezi wa kesi; na kuanzishwa
kwa Mkoa Mpya wa Kipolisi Rufiji.
9. Mheshimiwa Spika, mafanikio
mengine ni pamoja na kuzinduliwa
kwa Mradi wa Uhamiaji Mtandao (e- immigration) mwezi Januari, 2018 kwa
kuanza na utoaji wa pasipoti za Tanzania za kielektroni za Afrika Mashariki;
kukamilika kwa Kituo cha Kutunzia Kumbukumbu (Data Centre) na Kituo cha Uokozi
wakati wa Majanga (Data Recovery Centre) kwa ajili ya utambuzi na
usajili wa watu; na kukamilika kwa ofisi 13 za usajili za wilaya Tanzania Bara
na Zanzibar.
10. Mheshimiwa Spika, Mpango na Bajeti ya Wizara kwa Mwaka 2018/19
umezingatia: Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano
2016/17 –2020/21; Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 - 2020; Mpango Mkakati
wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 2016/17 – 2020/21; Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kudhibiti na Kuzuia Ukatili dhidi ya
Wanawake na Watoto 2017/18 – 2021/22; Maagizo ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Viongozi wa
Juu wa Taifa yaliyotolewa kwa nyakati tofauti; na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti wa Mwaka 2018/19.
Utekelezaji wa shughuli za Wizara kwa mwaka 2017/18 na Malengo ya Mpango na
Bajeti kwa mwaka 2018/19 ni kama ifuatavyo:
JESHI LA POLISI
Hali ya Usalama Nchini
11. Mheshimiwa Spika,
amani na utulivu ni muhimu katika maendeleo ya nchi yetu kiuchumi, kijamii na
kisiasa. Jeshi la Polisi limeendelea kuchukua hatua stahiki za kubaini, kuzuia
na kudhibiti uhalifu wa aina zote ili kuendelea kuwa
na nchi yenye utulivu utakaowezesha shughuli za kiuchumi na kijamii kufanyika
kwa ufanisi.
12. Mheshimiwa Spika,
pamoja na kuwepo kwa hali ya amani na utulivu nchini yamejitokeza matukio kadhaa
ya uhalifu. Katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya makosa
makubwa ya jinai 47,236 yaliripotiwa ikilinganishwa na makosa 56,913
yaliyoripotiwa kipindi kama hicho mwaka 2016/17. Kwa jumla makosa hayo
yamepungua kwa asilimia 17. Kati ya makosa hayo, 44,866 yaliripotiwa Tanzania
Bara na 2,370 Tanzania Zanzibar ambapo makosa 9,252 yalikuwa dhidi ya binadamu,
23,278 ya kuwania mali na 14,706 ya maadili ya jamii. Kutokana na matukio hayo
ya uhalifu jumla ya watuhumiwa 42,702 walikamatwa na kufikishwa mahakamani.
Katika mwaka 2018/19 Wizara kupitia Jeshi la Polisi itaendelea kuimarisha mbinu
za kubaini, kuzuia na kupambana na uhalifu pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa
umma kuhusu umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Polisi kudhibiti vitendo vya uhalifu
nchini.
13. Mheshimiwa Spika,
kati ya mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018 Jeshi la Polisi limefanikiwa
kukamata silaha haramu 358 na risasi 1,970 kwa mchanganuo ufuatao: gobore 224
na risasi 127; shortgun 43 na risasi 654; bastola 36 na risasi 208; SMG
19 na risasi 423; SAR mbili (2); Mark iv mbili (2) na risasi 85, Riffle
23 na risasi 410; Uzi Gun tano (5) na risasi moja (1); AK 47 nne (4) na risasi
55; na risasi saba (7) za G3. Watuhumiwa 333 waliopatikana na silaha
hizo wamekamatwa na kufikishwa mahakamani ambapo kesi zipo katika hatua
mbalimbali. Katika mwaka 2018/19 Jeshi la Polisi litaendelea kutoa elimu ya
kuhamasisha umma kutoa taarifa za viashiria vya uhalifu pamoja na zile za watu
wanaomiliki silaha kinyume cha sheria.
Hali ya Usalama Barabarani
14. Mheshimiwa Spika, hali ya usalama barabarani
imeendelea kuimarika kutokana na hatua za kisheria zinazoendelea kuchukuliwa
kwa madereva na wamiliki wa vyombo vya moto. Katika kipindi cha mwezi Julai,
2017 hadi Machi, 2018 jumla ya ajali 4,180 za barabarani ziliripotiwa. Aidha, ajali 1,613
zilisababisha vifo vya watu 1,985 na watu 4,447 kujeruhiwa. Takwimu zinaonyesha
kupungua kwa ajali hizo kwa asilimia 35.7 ikilinganishwa na kipindi kama hicho
mwaka 2016/17. Ajali nyingi kati ya hizo zimesababishwa na madereva kutozingatia
Sheria za Usalama Barabarani na ubovu wa miundombinu katika baadhi ya maeneo. Aidha,
katika kipindi hicho jumla ya madereva 5,185
walikamatwa kwa makosa mbalimbali ya usalama barabarani kwa kukiuka Sheria na
kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria. Kati ya hao madereva wa magari walikuwa
4,102 na waendesha pikipiki 1,083.
15. Mheshimiwa Spika, ili kupunguza ajali za barabarani, Wizara
kwa kushirikiana na wadau imeandaa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya
Usalama Barabarani Sura, 168, ambayo pamoja na mambo mengine inapendekeza kuzuia
matumizi mabaya ya simu wakati dereva anapoendesha gari, kuondoa nukta kwenye
leseni za madereva wanaokiuka Sheria za Usalama Barabarani na kufanya maboresho
ya Baraza la Taifa la Usalama Barabarani kulifanya kuwa tendaji na taasisi
kiongozi (Leading Agency) katika masuala ya usalama barabarani.
16. Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Jeshi la Polisi (Kikosi cha
Usalama Barabarani) itaendelea kudhibiti mwendokasi kwa kutumia vifaa
vya kudhibiti mwendo huo (Speed Radar)
na kufanya operesheni na doria za magari barabarani wakati wote. Aidha, Wizara
itaendelea kufuta leseni za madereva wanaofanya makosa hatarishi barabarani, kutoa
elimu ya Usalama Barabarani kwa umma na mashuleni, kufanya ukaguzi wa mabasi ya
abiria kabla hayajaanza safari, kusimamia mfumo wa kielektroniki wa udhibiti mwenendo wa mabasi barabarani (Vehicle Tracking System – VTS) kwa kushirikiana na SUMATRA na kupima kiwango cha
ulevi wa madereva.
17. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha
usimamizi wa usalama barabarani, masuala yote yanayohusu vyombo vya moto na
madereva, hususan katika mafunzo ya udereva na utoaji wa leseni yatafanywa na
Jeshi la Polisi kwa mujibu wa Sheria. Aidha, nasisitiza kuwa vifaa vyote
vinavyofungwa kwenye vyombo vya moto, vinavyohusu usalama barabarani (kama vile
ving’ora na taa za vimulimuli) wahusika wawasiliane na Jeshi la Polisi.
18. Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa
mamlaka zote zinazofanya operesheni na kazi mbalimbali zinazohusu shughuli zote
za usalama barabarani ikiwa ni pamoja na ukamataji wa vyombo vya moto, ufungaji
wa minyororo kwenye matairi hasa kwenye maeneo ya maegesho, kugeuza maeneo ya
pembezoni mwa barabara kuwa maegesho ya magari na kutoza fedha za maegesho,
kutoza fedha kwa magari yanayofika katika maeneo ya huduma za kijamii, hususan
hospitali ni vyema mamlaka husika ziwasiliane na Jeshi la Polisi ili kuondoa
kero na malalamiko yanayotokana na operesheni hizo.
Miradi ya Ujenzi wa Makazi na Vituo vya Polisi
19. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi kwa
kushirikiana na sekta binafsi limekamilisha ujenzi wa nyumba za
kuishi familia 31 za askari Mkoani Arusha. Mradi
wa nyumba hizo ulizinduliwa rasmi na
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli
tarehe 07 Aprili, 2018. Katika uzinduzi huo Mhe. Rais alitoa ahadi ya Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi
wa makazi ya askari wa ngazi za chini. Jeshi la Polisi linatarajia kutumia
fedha hizo kujenga nyumba 400 katika mikoa yote nchini. Nachukua nafasi hii kumshukuru kwa dhati Mhe. Rais kwa kusaidia
kuboresha makazi ya askari. Aidha, napenda kutoa rai kwa Wakuu wa Mikoa
wote nchini kutekeleza agizo la Mhe. Rais la kushirikiana na mashirika ya Umma
na sekta binafsi katika kufanikisha ujenzi wa makazi ya askari na vituo vya
Polisi katika mikoa yote nchini.
20. Mheshimiwa Spika, vilevile, Jeshi la Polisi limekamilisha ukarabati wa iliyokuwa Ofisi ya Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya Ofisi ya Makao Makuu ya muda ya Jeshi la
Polisi. Aidha, ujenzi wa ofisi mpya ya Jeshi la Polisi katika eneo hilo
umefikia asilimia 40. Vilevile, ujenzi wa nyumba za kuishi familia 48 za askari katika eneo la Mabatini – Mwanza na Musoma – Mara zenye uwezo
wa kuishi familia 24 kwa kila mkoa unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni,
2018.
21.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la
Polisi kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali limekamilisha ujenzi wa
Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Rungwe. Aidha, ujenzi wa Vituo vya Polisi Daraja A
Mburahati na Daraja B Mbweni – Dar es Salaam umefikia asilimia 97 na Kituo cha
Polisi Mbweni kimeanza kutumika.
22.
Mheshimiwa Spika, hatua za
ujenzi katika maeneo mengine ni kama ifuatavyo: ujenzi wa Vituo vya Polisi daraja C Mkoani Lindi
katika maeneo ya Mtama, Londo, Mchinga, Nanjilinji na Ikokoto vyote vimefikia
wastani wa asilimia 50; ujenzi wa nyumba nane (8) za makazi ya askari Mkoani
Kigoma umefikia asilimia 40; ujenzi wa Kituo cha Polisi daraja C Mkinga Madebe - Handeni pamoja na nyumba tatu
(3) za makazi ya askari zinazofadhiliwa na Kampuni ya Tanga Cement zote
zimefikia asilimia 55; ujenzi wa Vituo vya Polisi daraja C katika maeneo ya
Kombeni na Amani Zanzibar umefikia asilimia 40; ujenzi wa Kituo cha Polisi
daraja C Kinyasini Zanzibar umefikia asilimia 10; ujenzi wa nyumba mbili (2) za
makazi na Vituo vya Polisi daraja C katika maeneo ya Kamogi, Kakese na Karema
Mkoani Katavi umefikia asilimia 55. Kazi hizo za ujenzi
zitaendelea na kukamilika katika mwaka 2018/19.
23. Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii
kuwapongeza wananchi wote waliochangia katika miradi hiyo kwa lengo la
kuimarisha ulinzi katika maeneo yao.
Hiki ni kielelezo kuwa tukiamua tunaweza, hivyo natoa wito kwa wananchi
kuendeleza jitihada hizi katika maeneo mengine nchini.
24. Mheshimiwa Spika,
kazi ya upanuzi wa Chuo cha Polisi Moshi kwa ufadhili wa Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China inaendelea. Ujenzi wa mabweni yenye uwezo wa kuhudumia wanafunzi
662 na madarasa ya wanafunzi 320 umefikia asilimia 50. Kazi hiyo inatarajiwa
kukamilika katika mwaka 2018/19.
Udhibiti wa Dawa za Kulevya Nchini
25. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
Julai, 2017 hadi Machi, 2018 Jeshi la Polisi lilikamata jumla ya kilogramu 8.44
za dawa za viwandani. Watuhumiwa 833 wamefikishwa mahakamani, ambapo kesi zipo katika
hatua mbalimbali. Aidha, kilogramu 37,786.8 za bhangi na kilogramu 6,956.6 za
mirungi zilikamatwa na watuhumiwa 9,005 walifikishwa mahakamani. Vilevile,
mashamba ya bhangi 59 yenye takribani ekari 206.6 yaliteketezwa na watuhumiwa
39 walikamatwa na kufikishwa mahakamani.
Kuboresha Mfumo wa Upelelezi wa Kesi za
Jinai
26. Mheshimiwa Spika, mfumo wa ufuatiliaji
wa mienendo ya kesi za jinai umehuishwa ili kuhakikisha upelelezi wa kesi
unakamilika kwa wakati na hivyo kupunguza malalamiko kwa wananchi. Mfumo huo
unaofahamika kama Dossier Management Sytem unaimarisha ufuatiliaji wa
kesi kuanzia jalada linapofunguliwa Kituo cha Polisi hadi linapofikishwa
mahakamani. Mfumo huo pia hutumia
taarifa kutoka Maabara ya Uchunguzi wa Kisayansi ambayo imeimarishwa kwa
kukamilisha ufungaji wa mfumo wa uchunguzi wa vinasaba vya binadamu.
27. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi linaendelea
kuimarisha
ushirikiano na wadau wa Haki Jinai katika hatua mbalimbali za mashauri ya jinai
na kuimarisha vitengo vya ukaguzi kuanzia ngazi ya Makao Makuu ya Polisi,
Mikoa, Wilaya na Vituo ili kutatua mlundikano wa kesi.
Hatua za Utatuzi kwa Wananchi Kubambikiwa
Kesi
28. Mheshimiwa Spika, tatizo la kubambikiwa kesi kwa wananchi
limepungua baada ya Jeshi la Polisi kuchukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja
na: kuimarisha mfumo wa kusimamia mashauri ya jinai na kuyapitia kabla ya
kupelekwa kwa Mwanasheria wa Serikali; kuimarisha ushirikiano kati ya
wapelelezi na waendesha mashtaka kuanzia hatua za awali za upelelezi mpaka
hatua ya mwisho wa kesi mahakamani; na ukaguzi wa mahabusu/wafungwa unaofanywa
na wadau wa Haki Jinai katika Vituo vya Polisi na magerezani.
Usalama wa Makundi Maalum
29. Mheshimiwa Spika,
katika kipindi cha kuanzia mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya watu 117
(wazee/vikongwe) waliuawa, kati ya hao wanawake 26 na wanaume 91. Matukio hayo
yalitokea katika Mikoa ya Arusha 6,
Dodoma 1, Geita 9, Iringa 1, Kagera 10, Katavi 3, Kigoma 1, Mara 2, Mbeya 7,
Morogoro 2, Mwanza 9, Njombe 5, Rukwa 10, Shinyanga 3, Simiyu 5, Singida 6,
Songwe 12 na Tabora 25. Aidha, katika kipindi hicho matukio mawili
(2) ya kujeruhiwa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi yaliripotiwa katika Mikoa ya
Morogoro na Tabora.
30. Mheshimiwa Spika,
kufuatia matukio hayo jumla ya watuhumiwa 100 walikamatwa na kufikishwa
mahakamani. Natoa
rai kwa wananchi kuacha kujihusisha na vitendo hivyo viovu vinavyokiuka haki za
binadamu.
Jeshi la Polisi litaendelea kudhibiti na kuzuia mauaji ikiwemo ya makundi
maalum na kuendelea kushirikiana na wadau katika kutoa elimu kwa umma ili
kuacha mila na imani potofu kama ilivyoelekezwa katika Ibara ya 146 (v) ya Ilani ya CCM ya
Mwaka 2015 – 2020.
Kuanzishwa kwa Mkoa
Mpya wa Kipolisi Rufiji
31. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 Serikali iliahidi
kuanzisha Mkoa Mpya wa Kipolisi wa Rufiji ili kusogeza huduma karibu zaidi na
wananchi. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa ahadi hiyo imetimizwa
na hatua hii imeleta utulivu na udhibiti wa viashiria vya uhalifu katika eneo
hilo. Nachukua nafasi hii kuvipongeza vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama
kwa juhudi na bidii kubwa waliyoifanya na wanayoendelea kuifanya ya kuhakikisha
eneo hilo na maeneo mengine nchini yanakuwa salama. Pia, naomba na kuwasisitiza
wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo hivi kwa ajili ya kutoa taarifa za
uhalifu na wahalifu. Aidha, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa
ujumla kuwa Serikali itaendelea kuwahifadhi na kuwalinda wanaotoa taarifa za
wahalifu na uhalifu.
Udhibiti wa Uhalifu Nchini
32. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi limefanya operesheni maalum na
za kawaida (misako na doria) kwa lengo la kuendelea kupambana na kudhibiti
uhalifu wa aina zote ikiwemo makosa ya ndani ya nchi (kama vile mauaji, ubakaji
na unyang’anyi) na makosa yanayovuka mipaka (kama vile uingizaji wa bidhaa
bandia nchini, uharamia, wizi wa vyombo vya moto na utakatishaji wa fedha).
Katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 operesheni maalumu saba (7) zilifanyika
katika maeneo ya Kibiti, Rufiji, Mkuranga – mkoani Pwani, mapango ya Amboni
mkoani Tanga, Mwanza, Morogoro, Mtwara na Lindi pamoja na operesheni za kawaida
ikiwa ni misako na doria zilikuwa 3,628. Kwa sasa hali ya usalama katika maeneo
hayo na kwingineko nchini ni tulivu.
Kushiriki katika Kuimarisha Amani na Usalama
katika Nchi Mbalimbali
33. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka 2017/18 jumla ya askari 74 wa Jeshi la Polisi walipelekwa
kushiriki kulinda amani na usalama katika nchi mbalimbali. Kati ya askari hao
48 walipelekwa katika jimbo la Darfur-Sudan (UNAMID), 10 Abyei - Sudan
(UNISFA), 15 Sudani Kusini (UNMISS) na mmoja nchini Marekani – New York (DPKO).
Lengo ni kuendelea kupata uzoefu na mbinu mpya za kiutendaji, kama ilivyoelekezwa
katika Ibara ya 146 (iv) ya Ilani ya CCM ya Mwaka 2015 – 2020.
Kushiriki katika Operesheni za Kimataifa na
Kikanda
34. Mheshimiwa Spika, kuanzia tarehe 4 hadi 5
Oktoba, 2017 Jeshi la Polisi kwa
kushirikiana na Ofisi za INTERPOL Kanda ya Kusini mwa Afrika limefanya
operesheni za pamoja katika Jumuiya ya SARPCCO na EAPCCO. Kufuatia operesheni hizo, magari 2
kutoka Uingereza na Malaysia yalikamatwa pamoja na dawa za kulevya kwa
mchanganuo ufuatao: Heroine gramu 51.41; Cocaine gramu 20.87; bhangi kilogramu
870.16 na mirungi kilogramu 13. Pia, silaha 8 (SMG 1 na Gobore 7) na risasi 31
zilikamatwa. Jumla ya watuhumiwa 265 walikamatwa kwa makosa hayo na kufikishwa
mahakamani. Vilevile, wahamiaji haramu 31 kutoka katika nchi za Burundi (12),
China watano (5), India mmoja (1), Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC)
watano (5), Kenya mmoja (1), Malawi wawili (2), Pakistan mmoja (1), Uganda
mmoja (1), Yemen mmoja (1) na Zambia wawili (2) walikamatwa na kufikishwa
mahakamani. Jeshi la Polisi litaendelea kufanya operesheni kwa
kuzingatia Ibara ya
146 (vi) ya Ilani ya CCM ya
Mwaka 2015 – 2020.
Kudhibiti Uvunjifu wa Amani unaotokana na
Migogoro ya Wakulima na Wafugaji
35. Mheshimiwa Spika,
katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya matukio ya migogoro ya
wakulima na wafugaji 86 yalitokea na kusababisha vifo vya watu 44 (wanaume 34
na wanawake 10) na majeruhi 75 (wanaume 71 na wanawake 4). Watuhumiwa 129
walikamatwa na kufikishwa mahakamani. Katika mwaka 2018/19, Jeshi la Polisi
litaendelea kudhibiti matukio hayo kwa kushirikisha mamlaka husika.
Upandishwaji Vyeo na Ajira Mpya kwa Askari
36. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 Jeshi la Polisi limeomba
kibali cha kupandisha vyeo maafisa 300 na askari 3,071 wa vyeo mbalimbali.
Aidha, katika kutekeleza agizo la Mhe. Rais, Jeshi la Polisi limepata kibali
cha kuajiri vijana 1,500 waliopo katika Jeshi la Kujenga Taifa
(JKT) na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU). Nafasi hizo zimeshatangazwa kupitia vyombo vya habari ikiwemo radio,
televisheni na magazeti.
Kuboresha Maslahi ya Askari
37. Mheshimiwa Spika, kati ya mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018
Serikali imelipa madeni ya askari na
watumishi jumla ya Shilingi bilioni 17.94 ikiwa ni utekelezaji wa
Ibara ya 146 (ii) ya Ilani ya CCM ya
Mwaka 2015 – 2020. Madeni hayo yalitokana na madai ya posho za likizo na stahili
mbalimbali kwa mwaka 2014/15 na 2015/16. Vilevile, Serikali imelipa madeni ya
wazabuni na watoa huduma ya jumla ya Shilingi bilioni 5.69. Aidha,
katika kipindi hicho askari 347 walioumia/kufariki wakiwa kazini wamelipwa
fidia ya jumla ya Shilingi bilioni 2.09.
Ununuzi wa Sare za Jeshi
la Polisi
38. Mheshimiwa Spika, taratibu
za ununuzi wa sare na vifaa vingine vya kijeshi kwa kutumia viwanda vya ndani
zinaendelea baada ya Kiwanda cha 21st Century kilichopo Mkoani Morogoro
kuthibithisha uwezo wa kutengeneza vitambaa bora vya kushona sare zinazotakiwa
na majeshi yetu. Aidha, Jeshi la Polisi linakamilisha mkataba wa ununuzi wa
jozi 15,000 za viatu (buti jozi 10,000, viatu vya kawaida (staff shoes) jozi
5,000) kutoka Kiwanda cha Viatu cha Jeshi la Magereza Karanga - Moshi.
Upatikanaji wa Vitendea Kazi
39. Mheshimiwa Spika, ili
kuendelea kuimarisha na kuboresha doria, misako na operesheni maalum na za
kawaida Jeshi la Polisi limepokea magari 172 aina ya Ashok Leyland yakiwa ni
sehemu ya ununuzi wa magari 777 kutoka Kampuni ya Ashok Leyland ya nchini
India. Magari hayo yatagawiwa katika Mikoa, Vikosi na Wilaya za Kipolisi.
Pia, Jeshi la Polisi limepokea pikipiki 10 aina ya Tongba kutoka kwa wadau wa
usalama wa mkoa wa Dar es Salaam. Pikipiki hizo zimesambazwa katika Vituo vya
Polisi katika kanda maalumu ya Dar es Salaam kwa kazi za doria za kuzuia makosa
ya usalama barabarani.
40. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Jeshi la Polisi la Polisi litaendeleza
juhudi za kupata vitendea muhimu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kwa lengo
la kuimarisha hali ya ulinzi na usalama nchini.
Mafunzo kwa Askari/Watumishi wa Jeshi la Polisi
41. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
Julai, 2017 hadi Machi, 2018 mafunzo mbalimbali ya kuwajengea uwezo wa
kiutendaji maafisa 736, wakaguzi 395, askari wa vyeo mbalimbali 4,943 na
watumishi raia 10 yamefanyika. Katika mwaka 2018/19 Jeshi la Polisi litaendelea
kutoa mafunzo kwa maafisa, wakaguzi, askari wa vyeo mbalimbali pamoja na
watumishi raia ili kukabiliana na mbinu mpya za kiuhalifu pamoja na kuongeza
ufanisi.
JESHI LA MAGEREZA
Uhifadhi wa Wafungwa
na Program za Urekebishaji Magereza
42. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia
mwezi Machi, 2018 Jeshi la Magereza lilihifadhi jumla ya wafungwa na mahabusu 39,763 (wafungwa ni 20,312 na mahabusu ni 19,451)
ikilingwanishwa na uwezo wa kuhifadhi wafungwa na mahabusu 29,902. Hali hiyo
inaashiria kuendelea kuwepo msongamano magerezani kwa asilimia 33. Hatua
mbalimbali zimeendelea kuchukuliwa ili kukabiliana na hali hiyo zikiwemo:
kutumia utaratibu wa huduma kwa jamii; utaratibu wa Parole; kutumia Kamati za
Kusukuma Kesi; ujenzi wa magereza mapya; na ukarabati wa mabweni ya wafungwa.
Aidha, Jeshi
la Magereza liliendelea kutekeleza jukumu la kuwasindikiza mahabusu kwenda mahakamani
na kurudi Gerezani katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Wilaya ya Arusha mjini
na Wilaya ya Dodoma mjini.
Uboreshaji wa Makazi
ya Askari wa Jeshi la Magereza
43. Mheshimiwa Spika, ujenzi wa maghorofa 12 yenye uwezo wa kuishi familia 320 za maafisa
na askari eneo la Gereza Ukonga unaendelea kwa fedha Shilingi billion 10
zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli. Pia, ujenzi wa nyumba za askari zenye uwezo wa kuishi familia
24 unaendelea katika Gereza Chato. Nachukua nafasi hii kumshukuru Mhe. Rais
kwa nia yake ya dhati ya kuendelea kusaidia kuboresha makazi ya askari.
44. Mheshimiwa Spika, vilevile, ujenzi wa nyumba 323 za kuishi maafisa na askari kwa njia
ya kujitolea katika maeneo mbalimbali ya magereza nchini unaendelea. Ujenzi huo
upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Aidha, Shirika la Uzalishaji Mali
la Magereza limetoa Shilingi milioni 246 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi
wa nyumba za askari katika Magereza ya Bukoba, Muleba, Biharamulo, Kigongoni,
Mkuza, Kibiti, Arusha, Rombo, Karanga, Mwanga, Isanga na Gereza Mahabusu
Morogoro.
45. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19, Jeshi la Magereza litaendelea na ujenzi wa
nyumba za kuishi askari kwenye Magereza ya Ukonga na Chato pamoja na
kukamilisha ujenzi wa nyumba 323 zinazojengwa katika magereza mbalimbali
nchini.
Utekelezaji wa Sera
ya Uchumi wa Viwanda
46. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Uchumi wa
Viwanda, Jeshi la Magereza kwa ubia na Kampuni ya Mkulazi Holding Ltd
inayoundwa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii NSSF na PPF limewekeza katika kilimo
cha miwa na ufufuaji wa Kiwanda cha Sukari Gereza Mbigiri - Morogoro. Kiwanda
hicho kikikamilika kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 50,000 za sukari kwa
mwaka. Mpaka sasa hekta 800 zimeshalimwa na kupandwa miwa, sambamba na hilo ununuzi wa mitambo kwa ajili ya kiwanda unaendelea.
47. Mheshimiwa Spika,
vilevile, Jeshi la Magereza limeingia ubia na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa PPF
ili kuboresha Kiwanda cha Viatu Gereza Karanga na ujenzi wa kiwanda kipya
katika eneo hilo. Ubia huo umeunda kampuni inayoitwa Karanga Leather
Industries. Uboreshaji wa kiwanda unaendelea, ambapo mashine mpya
zinategemea kuwasili katika mwaka 2018. Hivyo, kiwanda kitakuwa na uwezo wa
kuzalisha jozi za viatu 400 kwa siku badala ya 150 zinazozalishwa sasa. Kiwanda
kipya kitakachojengwa kitakuwa na uwezo wa kuzalisha jozi 4,000 za viatu,
kuchakata ngozi sq. ft 12,500 na
kutengeneza soli jozi 3,000 kwa siku pamoja na kutengeneza bidhaa
mbalimbali za ngozi (mikanda, mikoba na pochi) 4,000 kwa mwaka. Katika mwaka 2018/19 Jeshi la Magereza litaimarisha viwanda vya kati
vya Useremala Mkoani Dodoma na Mtwara pamoja na mradi wa kuzalisha kokoto
Msalato.
Programu za
Urekebishaji wa Wafungwa
48. Mheshimiwa Spika, programu za urekebishaji wa wafungwa
zinaendelea kupitia shughuli za kilimo na mifugo. Jumla ya hekari 7,000 za
mazao kama vile mahindi, mpunga, maharage, alizeti, chai, pamba,
migazi/michikichi na mikorosho zimelimwa. Aidha, Jeshi la Magereza kwa kushirikiana
na Wakala wa Mbegu za Kilimo (Agricultural Seed Agency - ASA) limeendelea
kuzalisha mbegu bora katika Magereza ya: Wami Kuu, Mbigiri, Idete (Morogoro),
Isupilo (Iringa), Songwe (Mbeya), Mollo (Rukwa), Kitai (Ruvuma) na Karanga
(Kilimanjaro).
49. Mheshimiwa Spika, vilevile, Jeshi la Magereza linaendelea
kushirikiana na Wizara ya Kilimo katika uzalishaji wa vipando vya mihogo yenye
ukinzani dhidi ya ugonjwa wa batobato kali (cassava mosaic - Uganda
variant). Jumla ya hekta 170 zililimwa katika Magereza 23 yaliyopo
katika Mikoa ya Dodoma, Kagera, Lindi, Mara, Morogoro, Mtwara, Mwanza, Pwani,
Shinyanga, Singida, Tabora na Tanga.
50. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Jeshi la Magereza
linatarajia kulima jumla ya hekta 349 za mbegu bora za alizeti, mpunga, mahindi
na nyanya katika Magereza ya Wami, Mbigiri na Idete (Morogoro), Isupilo
(Iringa), Songwe (Mbeya), Mollo (Rukwa), Kitai (Ruvuma) na Karanga
(Kilimanjaro) na kuuzwa kwa wadau mbalimbali. Jeshi pia, litalima ekari 7,000 za mazao ya chakula ikiwemo mahindi,
maharage, mtama na mpunga.
51. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 urekebishaji wa
wafungwa kupitia ufugaji uliendelea, ambapo jumla ya mifugo 18,588 ya aina
mbalimbali ilihudumiwa kama ifuatavyo: ng’ombe wa maziwa (691), Ng’ombe wa
nyama (5,497) Mbuzi (2,405), Kondoo (134), Nguruwe (60), Sungura (175), Kuku na
Bata (9,626). Jeshi la Magereza litaendelea kuhudumia mifugo
26,632 ya aina mbalimbali katika mwaka 2018/19.
Shirika la
Uzalishaji Mali la Magereza
52. Mheshimiwa Spika, Shirika la Uzalishaji Mali la Magereza limefanya kazi mbalimbali za
ujenzi kwa Taasisi za Serikali na watu binafsi ikiwa ni pamoja na ukarabati wa
jengo la Utawala la Bunge ambalo limekamilika na kukabidhiwa mwezi Disemba, 2017. Katika mwaka 2018/19 Shirika
litaendelea na shughuli mbalimbali ikiwemo kupokea zabuni za ujenzi na kufanya
ukarabati wa majengo.
Upimaji wa Maeneo ya
Magereza
53. Mheshimiwa Spika, upimaji wa maeneo mbalimbali ya Magereza nchini unaendelea kwa lengo
la kupunguza migogoro iliyopo katika maeneo yanayomilikiwa na Jeshi la
Magereza. Hadi kufikia mwezi Machi, 2018 Jeshi limeweza kupima na kupata Hati
za umiliki wa maeneo ya Gereza Karanga, Hati tatu (3) za mashamba ya Mbigiri na
eneo la Gereza Isupilo.
Utunzaji na Hifadhi
ya Mazingira
54. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Magereza limeendelea na juhudi za
utunzaji wa mazingira kwa kupanda miti, kuendeleza misitu ya asili na ufugaji
wa nyuki kwenye eneo la hekta 14,698.5. Aidha,
kwa sasa miti ya aina mbalimbali inaendelea kutunzwa kwenye magereza kote
nchini kwa ufadhili wa Mfuko wa Misitu (Tanzania Forest Fund - TFF).
Aidha, Gereza Isupilo – Iringa limeanzisha kitalu cha miti kwa ajili ya
kuendeleza juhudi za utunzaji wa mazingira.
Ajira na Maslahi kwa Askari Magereza
55. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Magereza litaajiri askari wapya 2,750 kati ya hao askari 750 wataajiriwa katika mwaka
2017/18 na askari 2,000 katika mwaka 2018/19. Aidha, katika kuimarisha uongozi
wa ngazi za juu wa Jeshi la Magereza jumla ya maafisa 29 wamepandishwa vyeo
katika ngazi mbalimbali.
56. Mheshimiwa Spika, vilevile, Serikali imeendelea kuboresha maslahi ya Watumishi kwa
kuwalipa posho ya chakula kwa wakati na fedha za msamaha wa kodi ya bidhaa kwa
maafisa na askari nchini. Serikali pia imelipa baadhi ya madeni ya askari na
watumishi ya Shilingi bilioni 5.55 katika kipindi cha mwezi Oktoba hadi
Desemba, 2017.
Mafunzo kwa Askari
wa Jeshi la Magereza
57. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 Jeshi la Magereza limeendelea kuwawezesha
watumishi kupata mafunzo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Jumla ya watumishi
306 wanaendelea na mafunzo ya kitaaluma katika vyuo mbalimbali kwa mchanganuo
ufuatao: Astashahada 98, Stashahada 86, shahada 85, Stashahada ya Uzamili 08,
Shahada ya Uzamili 26 na Shahada za uzamivu 02. Jeshi pia limeendelea kutoa
mafunzo ndani ya Jeshi ambapo askari 37 walihitimu mafunzo ya Astashahada ya
ufundi bomba na useremala na askari 24 walipata cheti cha Sayansi ya
Urekebishaji wa Wafungwa. Aidha, askari 17 wanaendelea na mafunzo ya cheti cha
urekebishaji katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Ukonga.
58. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Jeshi la Magereza linatarajia kutoa mafunzo ya
ndani katika fani na ngazi mbalimbali kwa maafisa na askari 3,270. Vilevile,
litaendelea kutoa vibali kwa maafisa na askari kusoma vyuo vya nje ya Jeshi kwa
kuzingatia mahitaji kwa taaluma zenye upungufu Jeshini. Aidha, mafunzo ya
ufundi katika Chuo cha Ruanda kwa askari, pamoja na wafungwa kama sehemu ya
urekebishaji yataendelea kutolewa.
PROGARAMU YA ADHABU MBADALA YA KIFUNGO CHA
GEREZANI
59. Mheshimiwa Spika, Wizara inasimamia
utekelezaji wa Programu ya Adhabu Mbadala wa Kifungo Gerezani ili kupunguza
msongamano magerezani na gharama za kuhudumia wafungwa na mahabusu. Katika
kipindi cha mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya wafungwa 2,781
walinufaika na Programu hiyo. Uwepo wa wafungwa hao nje ya magereza umesaidia
Serikali kuokoa jumla ya Shilingi
bilioni 1.31 ambazo zingetumika kuwahudumia wafungwa hawa kama wangetumikia
adhabu zao magerezani ikizingatiwa kuwa gharama za kumhudumia mfungwa mmoja kwa
siku ni Shilingi 1,300. Serikali pia imeweza kuokoa jumla ya Shilingi billion 4.03 ambazo
zingetumika kuajiri vibarua kwenye Taasisi za Umma kwani kibarua mmoja hulipwa wastani
wa Shilingi 4,000 kwa siku.
60. Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2017/18 Wizara imefanikiwa kupanuwa wigo wa utekelezaji wa adhabu mbadala kwa
kuongeza Mikoa ya Kigoma na Simiyu na hivyo kufanya jumla ya mikoa 23 ya
Tanzania Bara inayotekeleza programu hiyo. Katika mwaka, 2018/19 Wizara
inatarajia kuongeza Mikoa ya Katavi, Rukwa na Lindi kwa ajili ya utekelezaji wa
programu hiyo.
JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI
Ukaguzi wa Tahadhari
na Kinga Dhidi ya Moto na Majanga
61. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi,
2018, Jeshi limekagua jumla ya maeneo 60,366 sawa na asilimia 74 ya lengo
la ukaguzi kwa kipindi husika. Katika mwaka 2018/19 Jeshi litaendelea na
ukaguzi wa tahadhari na kinga dhidi ya moto katika maeneo mbalimbali nchini ili
kuzuia na kupunguza matukio ya moto.
Matukio ya Moto na
Majanga Mengine
62. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeendelea kupambana na majanga ya moto
pamoja na kufanya maokozi katika maeneo mbalimbali nchini. Hadi kufikia mwezi Machi, 2018, Jeshi limefanikiwa kuzima moto katika
matukio 1,217 Tanzania Bara ikiwemo tukio la moto katika soko la SIDO,
mkoani Mbeya, moto katika nyumba za makazi ya Polisi mkoani Arusha, kuungua kwa
kiwanda cha Superdoll, kupasuka kwa bomba la gesi Buguruni – Mnyamani na moto
katika Kituo cha Utangazaji cha Clouds Media. Aidha, katika kukabiliana
na majanga mengine, jumla ya maokozi 335 yalifanyika katika matukio mbalimbali
ikiwemo mafuriko, kuangukiwa vifusi, ajali za barabarani, kutumbukia chooni na
kuzama kwa vyombo vya usafiri ziwani/baharini.
Hali ya Vituo vya
Zimamoto Nchini na Vitendea Kazi
63. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lina jumla ya vituo vya zimamoto 82
Tanzania Bara wakati mahitaji halisi ya vituo ni 162. Jeshi pia lina magari 72
ya kuzimia moto na maokozi, ikilinganishwa na mahitaji halisi ya magari 324.
Hata hivyo, Jeshi linaendelea na jitihada mbalimbali za kuimarisha hali ya
vitendea kazi ili kuendana na kasi ya ukuaji wa miji pamoja na maendeleo ya
viwanda nchini ikiwemo kukamilisha
taratibu husika ili kununua magari manne (4) ya kuzimia moto kupitia bajeti ya
mwaka 2017/18; kuimarisha uhusiano na nchi wahisani na wadau wa maendeleo ili
kuendelea kupata misaada mbalimbali ikiwemo vitendea kazi na mafunzo; na
kuendelea kutafuta mikopo yenye masharti nafuu kutoka kwa
wadau wa maendeleo. Katika mwaka wa 2018/19 Jeshi limepanga kununua magari
matano (5) ya kuzimia moto pamoja na vifaa vya kuzimia moto.
64. Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2017/18, Jeshi limepata msaada wa magari matano (5) ambapo matatu (3) ni ya
kuzimia moto na maokozi, moja la kubebea wagonjwa na moja la utawala kutoka
nchi za Ujerumani na Italia. Pia, Jeshi limepata msaada wa vifaa mbalimbali vya
kuzimia moto na maokozi zikiwemo mashine za kujazia mitungi ya kusaidia hewa ya
ziada wakati wa maokozi ambayo imepelekwa katika Mikoa ya Mbeya, Ruvuma na
Lindi.
Elimu kwa Umma kuhusu
namna ya Kukabiliana na Majanga ya Moto
65. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeendelea kutoa elimu kwa umma juu ya
namna ya kukabiliana na majanga mbalimbali ya moto kupitia vyombo vya habari
ikiwemo vipindi vya luninga 37, vipindi vya redio 754 na makala za magazeti 20
na katika maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu ikiwemo shule, masoko,
vivuko na vituo vya mabasi. Katika kukabiliana na matukio ya moto katika shule
za bweni nchini, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limetoa elimu ya namna ya kuzuia
na kukabiliana na matukio ya moto katika shule za bweni 256 katika mikoa
mbalimbali. Jeshi la Zimamoto
litaendelea kutoa elimu kwa umma kwa lengo la kupunguza majanga ya moto nchini.
Mafunzo kwa Askari
wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji
66. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeendelea
kuwapatia maafisa na askari wake mafunzo kwa lengo la kuboresha utendaji katika
majukumu yake. Katika mwaka 2017/18
askari 64 walipatiwa mafunzo mbalimbali ndani ya nchi ikiwemo mafunzo ya kuzima
moto na maokozi. Aidha, maafisa na askari 10 wamehitimu mafunzo ya kuzima moto
na maokozi nchini Morocco na maafisa 11 wamepatiwa mafunzo ya kukabiliana na
majanga mbalimbali nchini China. Katika mwaka 2018/19 Jeshi la Zimamoto na
Uokoaji litaendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa askari na watumishi ili
kuwaongezea ujuzi.
IDARA YA UHAMIAJI
Kuanzishwa kwa Mfumo wa Uhamiaji Mtandao
67. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mradi wa Uhamiaji Mtandao (e-immigration) ambao
ulizinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli tarehe 31 Januari, 2018 unaendelea. Mradi huo umeanza kwa
kutoa pasipoti za kielektroniki za Tanzania na Afrika Mashariki katika Makao
Makuu ya Idara ya Uhamiaji Dar es Salaam na Zanzibar. Pasipoti mpya za kielektroniki
zimetengenezwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa yenye uwezo wa kubeba taarifa
mbalimbali pamoja na alama nyingi za kiusalama. Aidha, pasipoti hiyo
inamwezesha mtumiaji kuwa na nakala yake ya pasipoti kwenye simu yake ya
kiganjani baada ya kupakua ‘app’ ya pasipoti yake kwenye simu.
68. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Idara ya Uhamiaji itaendelea kukamilisha ufungaji
wa mfumo wa pasipoti za kielektroniki katika mikoa yote hapa nchini. Vilevile,
itaendelea kufunga mifumo ya viza za kielektroniki (e-visa), Hati za
Ukaazi za kielektroniki (e-permit) na kufunga mifumo ya kudhibiti watu
wanaoingia na kutoka nchini (e-border management Control System) pamoja
na miundombinu ya uwekaji wa mtandao wa mawasiliano ya mifumo (wide area
network) katika ofisi na vituo vya uhamiaji vya mipakani. Kukamilika kwa
mradi huu kutasaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa mipaka yetu pamoja na
kuongeza udhibiti wa ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.
Hali ya Ulinzi na
Usalama Mipakani
69. Mheshimiwa Spika, jumla ya wageni 1,021,071 waliingia nchini kuanzia mwezi Julai 2017
hadi Machi, 2018 ikilinganishwa na wageni 1,032,978 waliongia katika kipindi
kama hicho kwa mwaka 2016/17. Aidha, jumla ya wageni 954,926 walitoka nchini
ikilinganishwa wageni 881,478 waliotoka kwa mwaka 2016/17. Katika mwaka 2018/19
Idara ya Uhamiaji itaendelea kutoa huduma kwa kufuata Sheria na Kanuni za
Uhamiaji kwenye mipaka kwa wageni wanaoingia na kutoka nchini.
Misako, Doria na
Ukaguzi
70. Mheshimiwa Spika, Idara ya Uhamiaji iliendelea kufanya misako, doria na ukaguzi katika
sehemu mbalimbali kama vile mipakani, migodini, viwandani, mahotelini na kwenye
mashamba makubwa kwa lengo la kudhibiti wahamiaji haramu pamoja na biashara
haramu ya usafirishaji binadamu nchini. Katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi,
2018 jumla ya watuhumiwa wa uhamiaji haramu 13,393 walikamatwa na kuchukuliwa
hatua mbalimbali za kisheria, ikiwa ni ongezeko la asilimia 40 ya wahamiaji
haramu 9,581 waliokamatwa katika kipindi kama hiki mwaka 2016/17. Vilevile,
jumla ya Watanzania 211 waliokwenda nje ya nchi kinyume na taratibu za uhamiaji
walirudishwa nchini. Wizara kupitia
Idara ya Uhamiaji itaendelea kufanya misako na doria ili kuwabaini na kuwaondoa
wahamiaji haramu nchini na kuhakikisha watu wote wanaoingia na kutoka nchini wanatumia
njia zilizo rasmi.
Vibali Vilivyotolewa
kwa Wageni Wakaazi
71. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018, jumla ya vibali vya
ukaazi 13,151 (daraja “A” 1,407; daraja “B” 8,551; na daraja “C” 3,193)
vilitolewa kwa wageni walioingia nchini kwa madhumuni mbalimbali kwa kuzingatia
sheria, kanuni na taratibu za kiuhamiaji
ikilinganishwa na vibali 11,259 (daraja A 2,474, daraja B 6,736, daraja
C 2,049) vilivyotolewa kwa mwaka 2016/17. Aidha, katika kipindi husika jumla ya
Hati za Mfuasi 1,335 zilitolewa ikilinganishwa na Hati 650 zilizotolewa katika
kipindi kama hiki mwaka 2016/17. Vilevile, Hati za Msamaha 2,393 zilitolewa
ikilinganishwa na Hati 1,427 zilizotolewa katika kipindi kama hiki mwaka
2016/17.
Pasipoti na Hati
Nyingine za Safari
72. Mheshimiwa Spika, jumla Pasipoti 45,965 zilitolewa kwa Watanzania waliotaka kusafiri nje
ya nchi kwa madhumuni mbalimbali katika kipindi cha
Julai, 2017 hadi Machi, 2018 kwa mchanganuo ufuatao: Pasipoti za Kawaida ni
45,697; Pasipoti za Kibalozi ni 220; Pasipoti za Kiutumishi ni 48. Katika
kipindi kama hicho kwa mwaka 2016/17 jumla ya Pasipoti 55,573 zilitolewa kama
ifuatavyo: Pasipoti za Kawaida ni 54,503, Pasipoti za Kibalozi 229, Pasipoti za
Kiutumishi 56, Pasipoti za Afrika Mashariki 785. Aidha, Idara ya Uhamiaji ilitoa Hati za
Dharura za safari 109,726 ikilinganishwa na Hati za Dharura za Safari 80, 445
zilizotolewa katika kipindi kama hiki mwaka 2016/17.
73. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Idara ya Uhamiaji itaendelea kuboresha na kukamilisha
huduma za kiuhamiaji kwa kutumia mfumo wa Uhamiaji Mtandao (e- passport,
e-visa, e-permit na e-border management control).
Wageni Walioomba na
Kupewa Uraia wa Tanzania
74. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya wageni 135
walipewa uraia, idadi hii ni ongezeko la asilimia 10 ikilinganishwa na kipindi
kama hiki mwaka 2016/17 ambapo wageni 110 walipewa uraia. Wageni waliopewa
uraia kwa kipindi hiki ni kutoka Burundi (4), Cameroon (2), China (1), Greece
(1), India (83), Jordan (1), Kenya (1), Korea (1), Lebanon (2), Rwanda (2),
Sierra Leone (1), Somalia (4), Uganda (2), Umoja wa nchi za Falme za Kiarabu
(6), Yemen (23) na Zambia (1).
Watanzania Waliopatiwa Uraia wa Mataifa
Mengine
75. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 Watanzania 60
waliukana uraia baada ya kujipatia Uraia wa mataifa mengine kama
ifuatavyo: Australia (2), Botswana (4), Canada (3), India (4), Kenya (4),
Lesotho (1), Norway (9), Sweden (1), Uganda (2), Uingereza (1), Ujerumani (19)
na Zimbabwe (3) hivyo kupoteza hadhi ya kuwa raia wa Tanzania kwa mujibu wa
Sheria ya Uraia Sura ya 357 Rejeo la 2002. Katika kipindi kama hiki kwa mwaka
2016/17 Watanzania 35 waliukana uraia wa Tanzania.
76. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa marekebisho ya Kanuni za Sheria ya Tanzania ya Uraia,
Tangazo la Serikali Na. 427/2017 imetoa punguzo la ada ya uraia kutoka Dola za
Marekani 5,000 hadi Shilingi 2,000,000. Punguzo hilo la ada linawahusu watu
waliozaliwa Tanganyika kabla na baada ya uhuru ambao wazazi wao hawakutambulika
kuwa raia wa Tanganyika kwa mujibu wa Sheria ya uraia ya Tanganyika Sura Na.
512 ya mwaka 1961. Vilevile, Kanuni imejumuisha watu waliongia nchini
Tanganyika kabla na baada ya uhuru na kuendelea kuishi nchini kwa kipindi chote
pamoja na watu waliozaliwa nje ya Tanzania kwa wazazi ambao ni raia kwa
Tanzania kwa kuridhi. Hivyo, natoa rai kwa watu hao kurekebisha hadhi yao ya
uraia ili kukidhi matakwa ya Sheria.
Mafunzo
katika Idara ya Uhamiaji
77. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 askari wapatao 23
wamehudhuria mafunzo ya muda mfupi nchini China na wawili (2) nchini Botswana
kwa ufadhili wa Serikali hizo. Aidha, askari 47 wamepatiwa mafunzo mbalimbali
ndani ya nchi.
Vitendea Kazi,
Majengo ya Ofisi na Makazi ya Askari wa Uhamiaji
78. Mheshimiwa Spika, Idara ya Uhamiaji imenunua nyumba 103 katika
eneo la Iyumbu mjini Dodoma kwa ajili ya makazi ya askari. Hadi sasa Idara
imekabidhiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jumla ya nyumba 63 na ujenzi wa nyumba 40 unaendelea.Aidha, ujenzi wa majengo ya ofisi
unaendelea katika Mikoa ya Geita (asilimia 50), Manyara (asilimia 40), Mtwara
(asilimia 11) na Lindi (asilimia 53). Ujenzi wa nyumba ya makazi ya Kamishna
Jenerali wa Uhamiaji umefikia asilimia 65. Namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kutoa ahadi ya Shilingi bilioni 10 kwa
ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Makao Makuu ya Idara ya
Uhamiaji Mjini Dodoma ambao utaanza mwaka 2018/19.
MAMLAKA YA VITAMBULISHO VYA TAIFA (NIDA)
Utambuzi, Usajili na Utoaji wa Vitambulisho
vya Taifa
79. Mheshimiwa Spika,
Wizara imeendelea kutekeleza lengo la Ibara 145 (f) ya Ilani ya CCM ya mwaka
2015 - 2020 kwa kuandikisha na kutoa Vitambulisho vya Taifa kwa Watanzania
kuanzia miaka 18 na zaidi, wageni wakaazi na wakimbizi. Hadi kufikia Machi, 2018 Mamlaka imesajili jumla ya wananchi 14,048,493,
wageni wakazi 13,254 na wakimbizi 6,289 katika mikoa yote ya Tanzania Bara na
Zanzibar. Zoezi la uchukuaji picha na alama za kibaiolojia linaendelea katika
mikoa yote ili kutengeneza vitambulisho na kuvigawa kwa walengwa.
80. Mheshimiwa Spika, Mamlaka
imeunganisha (interface) mfumo wake wa utambuzi na taasisi nyingine 35
ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa jamii na kuboresha hali ya ulinzi na usalama nchini. Aidha, Mamlaka
imekamilisha ujenzi wa kituo cha kutunzia kumbukumbu (Data Centre) huko
Kibaha Mkoa wa Pwani na kituo cha uokozi wakati wa majanga (Data Recovery
Centre) Kihonda Mkoa wa Morogoro pamoja na ofisi 13 za usajili za Wilaya
Tanzania Bara na Zanzibar. Vilevile, NIDA imeweka mtandao wa mawasiliano (fibre
optic) kati ya Makao Makuu na ofisi 117 za usajili za wilaya ili kusaidia
kusafirisha taarifa kutoka wilayani kwenda kituo kikuu cha kutengeneza
vitambulisho na kutunza taarifa.
81. Mheshimiwa Spika, uelewa kuhusu umuhimu wa Kitambulisho cha Taifa umeongezeka miongoni
mwa wananchi na kusababisha ongezeko kubwa la wananchi wanaojitokeza kusajiliwa
kwa ajili ya Vitambulisho vya Taifa. Hali hii imetokana na juhudi za Serikali
kupitia vyombo mbalimbali vya habari kutoa elimu ya umuhimu wa Vitambulisho vya
Taifa kwa uchumi na maendeleo ya mwananchi na nchi yetu kwa ujumla. Mamlaka
inaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa Kitambulisho cha Taifa na
jinsi kinavyoweza kuwasaidia katika kupata huduma mbalimbali mfano huduma za kibenki,
pasi ya kusafiria, fidia wakati wa majanga na kubaini vitendo vya kihalifu.
82. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Wizara itaendelea na zoezi la utambuzi na usajili
wa watu nchi nzima pamoja na kuunganisha mtandao wa mawasiliano kati ya ofisi
za usajili za wilaya 33 na Makao Makuu. Aidha, Wizara kupitia mkopo wa masharti
nafuu kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa Korea inatarajia kuanza ujenzi wa
Makao Makuu ya Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa katika Mkoa wa Dodoma pamoja
na ujenzi wa ofisi katika wilaya 42 Tanzania Bara na Zanzibar. Mamlaka pia
itaendelea na ukarabati kwa baadhi ya ofisi za usajili za wilaya na kuungunisha
mfumo wa utambuzi na mifumo ya taasisi nyingine ili iweze kusomana na hatimaye
kubadilishana taarifa.
83. Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji
wa lengo la utambuzi na usajili imebainika kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuanza
kutekeleza jukumu la utambuzi na usajili mara tu mtoto anapozaliwa na kupewa
namba ya pekee ya utambuzi na usajili. Suala la utambuzi wa watoto ni muhimu
katika kuimarisha hali ya usalama katika nchi yetu. Mtakumbuka kuwa katika siku
za hivi karibuni kumeibuka makundi mbalimbali ya kihalifu yanayowahusisha
vijana chini ya miaka 18. Tumeshuhudia makundi kama Panya Road na Wakorea weusi wakijihusisha na vitendo vya kihalifu
katika Jiji la Dar es Salaam na Mbeya. Athari za kutokuwatambua vijana hawa
wanapozaliwa mpaka wafikie umri wa miaka 18 umeathiri upelelezi wa kupata
taarifa sahihi za kuwatambua uasili wao, wazazi au walezi na makazi ili
kuwadhibiti kutojihusisha katika vitendo vya uhalifu.
HUDUMA KWA WAKIMBIZI
84. Mheshimiwa Spika, nchi yetu imeendelea
kutekeleza jukumu lake la kimataifa la kuhifadhi wakimbizi na waomba hifadhi
kutoka nchi mbalimbali. Katika kipindi cha mwaka 2017/18, Tanzania imeshuhudia
kwa mara nyingine ongezeko la waomba hifadhi wanaopokelewa, hususan kutoka
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Hadi kufikia mwezi Machi, 2018 Tanzania
ilikuwa na jumla ya wakimbizi na waomba hifadhi 356,548. Kati ya hao 276,047
kutoka Burundi, 79,950 Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, 150 Somalia na 401
kutoka mataifa mengine.
85. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018 Kamati ndogo ya Kitaifa ya Kuhoji Waomba
Hifadhi (Ad hoc Committee), iliwahoji
waomba hifadhi 1,342 kutoka nchi ya Burundi ambapo waomba hifadhi 198
walipendekezwa kupewa hadhi ya ukimbizi nchini baada ya kukidhi vigezo kwa
mujibu wa Sheria ya Wakimbizi ya mwaka 1998 na waomba hifadhi 1,144 walikosa
sifa za kupewa hadhi ya ukimbizi.
86. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kati ya Julai, 2017 hadi Machi,
2018 jumla ya wakimbizi na waomba hifadhi 50,437
kutoka Burundi walijiandikisha ili wasaidiwe kurejea kwa hiari kwenye nchi yao
ya asili. Zoezi la kuwarejesha kwa hiari linaendelea na mpaka kufikia mwezi
Machi, 2018 jumla ya wakimbizi 21,008 wamerejea Burundi. Ili kuongeza kasi ya kuwarejesha wakimbizi katika nchi zao,
Serikali ya Tanzania ilishiriki katika Mkutano wa ishirini (20) wa Pande Tatu
uliofanyika nchini Burundi tarehe 28 Machi, 2018 ambapo iliazimiwa kuwa ifikapo
mwezi Desemba, 2018 zaidi ya wakimbizi 72,000 wawe wamerejeshwa katika nchi ya
asili. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2019, wakimbizi wote
wa Burundi waliopo kwenye makambi ya Kigoma wawe wamerejea nchini kwao.
87. Mheshimiwa Spika, Wizara kwa
kushirikiana na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) na Shirika la
Kimataifa la Uhamiaji (IOM) inatekeleza mpango wa kuwapeleka wakimbizi katika
nchi ya tatu ikiwa ni moja ya suluhisho la kudumu linalotolewa kwa
wakimbizi.Katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2018 jumla ya wakimbizi
926 walihamishiwa nchi ya tatu katika mataifa ya Australia 25, Canada 137,
Finland 4, Marekani 756 na Uingereza 4.
88. Mheshimiwa Spika, Wizara kwa
kushirikiana na Mikoa ya Katavi, Kigoma na Tabora ilifanya zoezi la uhakiki na
usajili wa wakimbizi wa Burundi walioingia nchini mwaka 1972. Katika zoezi hilo
kwenye Mikoa ya Tabora na Katavi wakimbizi 19,187 walihakikiwa katika kipindi
cha mwezi Julai hadi Oktoba, 2017. Katika Mkoa wa Kigoma, zoezi la uhakiki
lilifanyika mwezi Januari na Februari, 2018 ambapo jumla ya wakimbizi 15,791
walihakikiwa. Lengo la zoezi hili ni
kuiwezesha Serikali kuwa na takwimu sahihi za wakimbizi wote wa kundi hilo.
89. Mheshimiwa Spika, Wizara
kwa kushirikiana na UNHCR imeendelea kuhamasisha na kusimamia shughuli za
hifadhi ya mazingira kwenye kambi za wakimbizi na vijiji jirani. Katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi,
2018, shughuli za mazingira zilizotekelezwa ni pamoja na: Upandaji wa miti
1,988,028; ujenzi wa majiko banifu 84,590; na nyumba za tofali na bati
2,274. Aidha, mradi wa matumizi ya gesi
umeendelea kutekelezwa ambapo jumla ya mitungi 26,450 ya gesi imegawiwa kwa
wakimbizi. Vilevile, Wizara kwa kushirikiana na UNHCR inaendelea na zoezi la
kufanya tathmini ya athari za mazingira kutokana na shughuli za wakimbizi ndani
ya kambi na maeneo ya vijiji jirani ili kuwa na mikakati endelevu ya
kukabiliana na athari hizo.
90. Mheshimiwa Spika, kwa ujumla hali ya
ulinzi na usalama imeendelea kuwa shwari ndani na nje ya kambi za wakimbizi. Wizara
kwa kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama katika mikoa inayohifadhi
wakimbizi, imeendelea kuimarisha ulinzi na usalama kwa kufanya doria za mara
kwa mara. Aidha, wakimbizi wanaobainika kujihusisha na vitendo vya kihalifu
wamekuwa wakichukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi.
VITA DHIDI YA BIASHARA HARAMU YA
USAFIRISHAJI WA BINADAMU
91. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi,
2018 Wizara kupitia Sekretarieti ya Kupambana na Kuzuia Biashara Haramu ya
Usafirishaji Binadamu kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji
(IOM) imewaokoa wahanga 20 (Watanzania 18, Afrika Kusini (1) na Mrundi (1)) wa
biashara haramu ya usafirishaji wa binadamu waliokuwa wakitumikishwa katika
maeneo mbalimbali nchini na kuwaunganisha na familia zao. Katika kipindi hicho
jumla ya kesi 24 zimefunguliwa ambapo kesi 23 zinaendelea katika mahakama
mbalimbali nchini na kesi moja (1) watuhumiwa wawili (2) wote Wanawake
walihukumiwa kifungo cha miaka saba (7) gerezani.
92. Mheshimiwa Spika, Sekretariati ilifanya ukaguzi katika maeneo
hatarishi ya utumikishwaji wa wahanga wa biashara haramu ya usafirishaji wa
binadamu katika wilaya zote Jijini Dar es Salaam. Maeneo yaliyokaguliwa ni
pamoja na viwanda, massage parlor, gereji za Wachina, kampuni kubwa na
klabu za usiku. Lengo la ukaguzi huo ni kujiridhisha kuwa watumishi wanajua
haki zao za msingi na kuwaelimisha juu ya biashara haramu ya usafirishaji wa
binadamu.
93. Mheshimiwa Spika, vilevile, Sekretarieti kwa
kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Lawyers Without Borders imetoa
elimu juu ya biashara haramu ya usafirishaji wa binadamu kwa wadau muhimu
katika mikoa saba ambayo ni Arusha, Geita, Kagera, Mara, Mwanza, Shinyanga na
Simiyu. Wadau hao ni pamoja na Mahakimu, Waendesha Mashtaka, Askari wa Jeshi la
Polisi, Maafisa Uhamiaji, Maafisa Ustawi wa Jamii, Viongozi wa Serikali za
Mitaa na wawakilishi kutoka mashirika mbalimbali yasiyo ya Serikali.Lengo la
mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wa namna ya kupeleleza, kuchunguza na
kuendesha mashtaka na kusikiliza kesi dhidi ya biashara haramu ya usafirishaji
binadamu. Sekretarieti pia imetoa elimu kwa Watanzania hususan wasichana
wanaoomba hati za kusafiria kwenda nje ya nchi kufanya kazi kufuatia taarifa
mbalimbali zinazohusu manyanyaso kwa wasichana wanaopelekwa kwenda kufanya kazi
nje ya nchi. Aidha, kutokana na taarifa hizo, mnamo mwezi Januari, 2018
nilitoa tamko la kuzuia utoaji wa pasipoti za mafungu kwa wasichana wanaoenda
kufanya kazi za ndani nchi za nje, hususan nchi za Uarabuni.
94. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Sekretarietiitaendelea
kupambana na biashara haramu ya usafirishaji binadamu ikiwemo kutoa elimu kwa
umma pamoja na kuratibu mafunzo kwa wadau/vyombo vinavyosimamia sheria ya
Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji Binadamu.
UTARATIBU WA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO
95. Mheshimiwa Spika, jumla
ya Malalamiko 175 kutoka kwa wananchi dhidi ya utendaji wa Wizara yalipokelewa
katika kipindi cha mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018. Kati ya malalamiko hayo
121 yalihusu Jeshi la Polisi, 26 Jeshi la Magereza, 19 Uhamiaji, matatu (3)
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, matatu (3) Idara ya Huduma kwa Wakimbizi, mawili
(2) Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa na moja (1) Idara ya Huduma ya Sheria.
Aidha, malalamiko 100 yalishughulikiwa na kukamilika na mengine 75 yanaendelea
kushughulikiwa yakiwa kwenye hatua mbalimbali. Wizara itaendelea kupokea na kushughulikia malalamiko ya
wananchi katika mwaka 2018/19 ili kuimarisha utoaji wa huduma.
USAJILI WA VYAMA VYA KIJAMII NA KIDINI
96. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi,
2018 jumla ya maombi 252 ya kusajili vyama yalipokelewa
ambapo maombi 178 ni vyama vya kijamii na 74 ni vyama vya kidini. Kati ya
maombi hayo vyama 136 vilisajiliwa na maombi 5 yalikataliwa kutokana na
kutotimiza matakwa ya kisheria na sababu nyingine za kiusalama na maombi 111 ya
usajili wa vyama yapo katika hatua mbalimbali za kushughulikiwa.Wizara
itaendelea na zoezi la usajili na uhakiki wa vyama vya kijamii na kidini katika
mwaka 2018/19.
97. Mheshimiwa Spika, hata hivyo kuna malimbikizo mengi ya maombi ya
usajili ya vyama vya kidini kutokana na maombi yote kutakiwa kufikia ofisi ya
Msajili Makao Makuu ya Wizara. Wakati Serikali inaelekea kuwa na ofisi za
msajili kwa kila kanda, naelekeza wote wenye Taasisi za Kidini mikoani wafike
ofisi za wilaya na kuwasilisha maombi yao kwa Katibu Tawala wa Wilaya. Na wote
waliofikisha maombi katika wilaya husika, wapate utambuzi wa awali ili taasisi
hizo zifanye kazi zikifahamika wakati taratibu za kupata usajili wa kudumu ukiendelea.
Narudia wapatiwe utambuzi wa awali wakati wanasubiri usajili wa kudumu.
Maendeleo ya Rasilimali Watu na Ajira Makao Makuu ya Wizara
98. Mheshimiwa Spika, Makao Makuu ya Wizara imepanga kuajiri watumishi 74 ili kuziba nafasi zilizoachwa wazi
kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufariki, kustaafu na kuacha
kazi. Wizara pia itawapandisha vyeo watumishi 106 wa kada mbalimbali na nafasi
11 za watumshi watabadilishwa vyeo.
Mapambano Dhidi ya Maambukizi ya
VVU/UKIMWI
99. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia miongozo husika Wizara iliendelea kuwapatia fedha za
kila mwezi watumishi wanaoishi na virusi vya UKIMWI na UKIMWI kwa ajili ya
kuimarisha afya zao dhidi ya magonjwa nyemelezi. Aidha, Wizara ilitoa elimu ya jinsi ya
kujikinga na magonjwa sugu yasiyoambukizwa kwa watumishi 200. Katika mwaka
2018/19 Wizara itaendelea kutoa elimu ili kuwahamasisha watumishi kufuata
taratibu za afya ili kujikinga na maambukizi dhidi ya virusi vya UKIMWI na
UKIMWI pamoja na magonjwa sugu yasiyoambukizwa.
C. SHUKRANI
100. Mheshimiwa Spika, natoa shukurani zangu za dhati
kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mhandisi Hamad
Masauni kwa msaada wake anaonipa katika kutekeleza majukumu ya Wizara. Pia,
nawashukuru kwa dhati Katibu Mkuu Meja Jenerali (Mstaafu) Projest A. Rwegasira
na Naibu Katibu Mkuu Balozi Hassan S. Yahya kwa juhudi zao kubwa za kusimamia
utendaji kazi wa Wizara.
101. Mheshimiwa Spika, vilevile, nawashukuru Inspekta
Jenerali wa Jeshi la Polisi, Bw. Simon N. Sirro; Kamishna Jenerali wa Jeshi la
Magereza, Dkt. Juma A. Malewa; Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na
Uokoaji, Bw. Thobias E. Andengenye; Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna P.
Makakala; na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Bw.
Andrew W. Massawe. Natoa shukurani zangu pia kwa Makamishna; Makamishna Wasaidizi; Wakuu wa
Idara, Vitengo na Sehemu; askari na watumishi wote kwa kuendelea kutekeleza
vema kazi na majukumu ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
102. Mheshimiwa Spika, vilevile, ninatoa
shukrani zangu kwa nchi wahisani
zikiwemo Austarlia, Botswana, Canada, China, Finland, India, Italia, Jamhuri ya
Watu wa Korea, Marekani, Morocco, Uingereza na Ujerumani pamoja na Taasisi na
Mashirika ya Kimataifa ya DFID, FSDT, IOM, UNDP, UNHCR, Vyombo vya Habari,
Taasisi za kijamii, kidini na zisizo za Serikali na wananchi kwa kuendelea
kutoa misaada na taarifa mbalimbali ambazo zimesaidia utendaji kazi wa Wizara.
103. Mheshimiwa Spika, kipekee naishukuru familia
yangu, ndugu, marafiki na wananchi, hususan wa Jimbo langu la Iramba Magharibi kwa
ushirikiano wao katika kuchangia maendeleo ya jimbo letu.
D. HITIMISHO
104. Mheshimiwa Spika, Wizara itaendelea kudhibiti matukio ya uhalifu ili kuhakikisha
amani na usalama unaendelea kuwepo nchini. Katika kutekeleza jukumu hilo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itashirikiana na vyombo
vingine vya dola nchini pamoja na wadau mbalimbali.
105. Mheshimiwa Spika, naomba sasa Bunge lako
Tukufu liidhinishe Bajeti ya jumla ya Shilingi
945,555,651,000 kwa ajili ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka
2018/19. Kati ya fedha hizo, Shilingi
907,269,969,000 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida, ambapo Shilingi 385,725,478,187 ni kwa
ajili ya Matumizi Mengineyo na Shilingi 521,544,490,813 ni Mishahara. Fedha za Miradi
ya Maendeleo ni Shilingi 38,285,682,000
kati ya fedha hizo Shilingi
37,500,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi
785,682,000 ni fedha za nje.
106. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa Hoja.
Comments
Post a Comment