- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
HOTUBA YA WAZIRI
WA NISHATI MHE. DKT. MEDARD MATOGOLO CHANANJA KALEMANI (MB.), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA
MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA NISHATI KWA MWAKA 2018/19
UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika,
kufuatia
taarifa iliyowasilishwa leo
hapa Bungeni na Mwenyekiti wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, naomba kutoa hoja kwamba Bunge
lako Tukufu likubali kupokea na kujadili Taarifa ya Utekelezaji ya Mwaka
2017/18 na kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na
Taasisi zilizo chini yake kwa Mwaka 2018/19.
2. Mheshimiwa Spika,
awali
ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na
kuniwezesha kutekeleza majukumu yangu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.
Vilevile, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha Waheshimiwa Wabunge
wenzangu kutekeleza kazi zao za Kibunge na kushiriki Mkutano huu wa 11 wa Bunge
lako Tukufu.
3. Mheshimiwa Spika,
kwa
namna ya pekee nitumie fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza Mhe. Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhe. Samia
Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miongozo
makini wanayonipatia ili kuhakikisha kuwa azma ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda
inafikiwa. Ni wazi kuwa viongozi wetu hawa wamekuwa mstari wa mbele katika
kutoa maelekezo yenye lengo la kuhakikisha kuwa umeme wa kutosha, wa uhakika,
unaotabirika na wa gharama nafuu unazalishwa ili kuchochea ukuaji wa viwanda
hapa nchini. Nampongeza Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuiongoza vyema
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
4.
Mheshimiwa Spika, nampongeza pia Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania kwa usimamizi thabiti wa shughuli za Serikali ndani na
nje ya Bunge lako Tukufu. Ni imani yangu kuwa kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu,
Viongozi wetu hawa wa Kitaifa wataendelea kuwa chachu ya uhamasishaji wa
shughuli za maendeleo nchini.
5.
Mheshimiwa Spika,
nitumie fursa hii pia kumshukuru Mhe. Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na
kuniteua kuiongoza Wizara ya Nishati. Uteuzi huo umenipa fursa ya kutoa mchango
wangu katika kuisimamia Sekta hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu. Napenda
kumhakikishia Mhe. Rais na Watanzania kuwa nitasimamia shughuli za Wizara hii
kwa nguvu zangu zote, akili zangu zote, ubunifu na weledi mkubwa ili
kuhakikisha kuwa Sekta ya Nishati inadhihirisha kuwa ndiyo injini kuu katika kujenga
uchumi wa viwanda wa Taifa letu. Vilevile, nampongeza Mhe. Subira Khamis Mgalu,
Mbunge wa Viti Maalum kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Nishati.
6.
Mheshimiwa Spika, napenda nikupongeze wewe binafsi, Naibu Spika, Wenyeviti
wa Bunge, Wenyeviti wote wa Kamati mbalimbali za Kudumu pamoja na watendaji
wote wa Ofisi ya Bunge lako Tukufu kwa uongozi wenu mahiri katika kuliongoza
Bunge hili na Kamati zake. Kwa namna ya pekee nampongeza Mhe. Dustan Luka
Kitandula (Mb.), kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini na Mhe. Mariam Ditopile Mzuzuri (Mb.), kwa kuteuliwa kuwa
Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo. Aidha, nawapongeza na kuwashukuru Wajumbe
wote wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa kupokea Taarifa ya
Utekelezaji wa Majukumu ya Wizara kwa Mwaka 2017/18 na Makadirio ya Mpango na
Bajeti kwa Mwaka 2018/19.
7.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na upya wa Kamati hiyo, imekuwa ikitoa michango
na ushauri unaolenga kuboresha utendaji wa Wizara kwa maslahi ya Taifa, hususan
katika kuhakikisha kuwa umeme wa uhakika unazalishwa na wananchi wengi zaidi
wanafikiwa na huduma hiyo hapa nchini. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu
kuwa Wizara ya Nishati itaendelea kupokea ushauri na mapendekezo ya Kamati hiyo
na Kamati nyingine za Bunge
katika kuhakikisha kuwa Wizara inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
8. Mheshimiwa Spika, naomba niungane
na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuwapongeza, Mhe. Dkt. Damas Daniel Ndumbaro,
Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini; Mhe. Justin Joseph Monko, Mbunge wa Jimbo
la Singida Kaskazini; Mhe. Dkt. Stephen Lemono Kisurwa, Mbunge wa Jimbo la
Longido; Mhe. Maulid Mtulia, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni; na Mhe. Dkt. Godwin
Mollel, Mbunge wa Jimbo la Siha kwa kuchaguliwa kwao kwa kishindo kuwa
Wawakilishi wa wananchi katika Majimbo yao. Hakika ni heshima kubwa waliyopewa
na wananchi na nawaombea kila la heri katika kutekeleza jukumu lao hilo la
uwakilishi katika Bunge letu Tukufu.
9.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kuungana na
Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pole kwako wewe binafsi, Naibu Spika, Bunge
lako Tukufu na kwa familia ya aliyekuwa Mbunge wa Songea Mjini, Mheshimiwa
Leonidas Gama kwa kuondokewa na mpendwa wetu huyo. Tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi, Amina.
10.
Mheshimiwa
Spika, baada ya utangulizi huo, naomba sasa kuwasilisha Taarifa
ya Utekelezaji wa Shughuli za Wizara ya Nishati kwa Mwaka 2017/18 na Makadirio
ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka 2018/19.
A.
TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA WIZARA YA NISHATI KWA MWAKA 2017/18
11.
Mheshimiwa
Spika, utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara kwa Mwaka
2017/18 ulijielekeza katika maeneo yafuatayo: kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na kuongeza
kasi ya usambazaji wa umeme nchini; kufanikisha utekelezaji wa Mradi mkubwa wa
Ujenzi wa Bomba la Mafuta ghafi kutoka Kabaale (Uganda) hadi Bandari ya Tanga
(Tanzania); kuendeleza miradi ya nishati jadidifu kama vile umeme-jua, maporomoko ya maji, jotoardhi na tungamotaka;
kuwezesha uwekaji wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia katika viwanda
mbalimbali na matumizi ya majumbani pamoja na kufanikisha utekelezaji wa Mradi
wa kusindika gesi asilia (Liquefied
Natural Gas - LNG); kuvutia uwekezaji katika Sekta ya Nishati, hususan katika
uzalishaji wa umeme kupitia vyanzo mbalimbali vilivyopo; utafutaji wa mafuta na
gesi asilia; na kuwezesha Taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Nishati
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
12.
Mheshimiwa Spika, maeneo mengine ni: kuendelea kutekeleza agizo la
Serikali la kuhamia Dodoma; kuwajengea
uwezo Watumishi wa Wizara katika fani za umeme, mafuta, gesi asilia na nishati
jadidifu; kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wananchi kunufaika na rasilimali za
mafuta na gesi asilia; kuelimisha umma na kuboresha
mawasiliano kati ya Wizara na wadau mbalimbali kuhusu masuala ya Nishati.
Wizara ilijielekeza pia katika kusimamia,
kufuatilia na kuboresha Sera, Sheria, Mikakati na Miongozo mbalimbali ili
kuboresha ufanisi na tija katika Sekta ya
Nishati.
13.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini (Fungu 58)
iliidhinishiwa na Bunge Jumla ya Shilingi bilioni 998.34. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 945.89 sawa na asilimia 94.7 ya bajeti
yote zilitengwa kwa ajili ya Sekta
ya Nishati. Kati ya fedha hizo, Shilingi
bilioni 916.84 sawa na asilimia 96.9
ni fedha za Maendeleo na Shilingi
bilioni 29.04 sawa na asilimia 3.1 ni
fedha za Matumizi ya Kawaida. Kati ya fedha za Maendeleo zilizotengwa, Shilingi bilioni 748.60 sawa na asilimia 81.7 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 168.24 sawa na asilimia 18.3 ni fedha za nje. Kwa upande wa Bajeti ya Matumizi ya
Kawaida, Shilingi bilioni 14.92 sawa
na asilimia 1.6 ni kwa ajili ya
Matumizi Mengineyo (O.C) na Shilingi
bilioni 14.12 sawa na asilimia 1.5
ya bajeti yote ni Mishahara ya Watumishi wa Wizara ya Nishati na Taasisi zake.
14.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwishoni mwa mwezi
Aprili, 2018 Wizara ya Nishati kupitia (Fungu 58) ilikuwa imepokea Jumla ya Shilingi bilioni 446.50 kwa ajili ya
utekelezaji wa shughuli za Sekta ya Nishati. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 424.91 sawa na asilimia 95.2 zilikuwa ni kwa ajili ya Miradi
ya Maendeleo ambapo fedha za ndani ni Shilingi
bilioni 413.09 sawa na asilimia 97.2
na Shilingi bilioni 11.82 sawa na asilimia 2.8 ni fedha za nje. Aidha,
kiasi kilichobaki cha Shilingi bilioni
21.58 sawa na asilimia 4.8
zilikuwa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida.
15.
Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2017/18 iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini
ilipanga kukusanya Jumla ya Shilingi
bilioni 532.83 kutokana na mapato yanayohusu Sekta ya Nishati. Mapato hayo yanatokana na
vyanzo mbalimbali vikiwemo: Shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asillia; Mauzo ya
gesi asilia; Mauzo ya Nyaraka za Zabuni; Tozo ya umeme na Stakabadhi
nyinginezo. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Aprili, 2018 Wizara ilikuwa
imekusanya Jumla ya Shilingi bilioni 280.27 sawa na asilimia 53. Wizara itaendelea na juhudi za kukusanya mapato ili kufikia lengo
lililowekwa kwa kipindi cha mwaka 2017/18.
Mafanikio yaliyopatikana kwa
Mwaka 2017/18
16.
Mheshimiwa Spika,
mafanikio yaliyopatikana katika
Sekta ya Nishati kwa kipindi cha mwaka 2017/18 ni pamoja na:
(i)
Kuendelea
na utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Kupeleka Umeme Vijijini kupitia REA Awamu ya
Tatu ambapo hadi mwezi Mei, 2018 kazi zilizokamilika ni pamoja na ujenzi wa
kilomita 985 za njia ya msongo wa kV 33, ujenzi wa kilomita 1,870.37 za njia ya
usambazaji umeme wa msongo wa kV 0.4 na ufungaji wa transfoma 751 zenye ukubwa
tofauti. Jumla ya vijiji 518 vimeunganishwa na kuwashwa umeme na wateja 14,817
wameunganishiwa umeme na Jumla ya vijiji 420 vimejengwa miundombinu ya umeme na
vinatarajiwa kuwashwa hivi karibuni;
(ii)
Kukamilika
kwa upelekaji umeme katika Makao Makuu ya Wilaya ya Tanganyika na Halmashauri
ya Wilaya ya Bumbuli na kufanya Makao Makuu ya Wilaya zote nchini kuwa
yamepelekewa umeme;
(iii)
Kukamilika kwa asilimia 100 kwa
Mradi wa ORIO katika Miji ya Ngara,
Biharamulo na Mpanda ambapo kwa sasa miji hiyo inapata umeme wa uhakika;
(iv)
Kusitisha matumizi ya mitambo ya kukodi ya binafsi ya kuzalisha umeme
kwa kutumia mafuta mazito katika kuzalisha umeme ikiwemo ya Aggreko na IPTL na
kuokoa wastani wa jumla ya Shilingi
bilioni 11.46 kwa mwezi;
(v)
Kukamilisha
ujenzi wa Mradi mpya wa Kinyerezi II na kuingiza katika Gridi ya Taifa umeme wa MW
168 mwezi Aprili, 2018;
(vi)
Kukamilika kwa Mradi mpya wa Kinyerezi II na ukarabati wa mitambo ya
kuzalisha umeme ya Kihansi, Kidatu, Mtera, New Pangani Falls na Ubungo II kumeongeza
uhakika wa upatikanaji umeme katika Gridi ya Taifa na kuwa na ziada ya umeme wa
wastani wa MW 280 kwa siku na
kuondokana na mgao wa umeme;
(vii)
Kukamilika kwa ukarabati wa mitambo ya kuzalisha umeme Mtwara pamoja na
kuongeza mitambo mipya miwili (2) yenye uwezo wa MW 4 na hivyo kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme katika Mikoa
ya Lindi na Mtwara;
(viii)
Kukamilika kwa asilimia 100 kwa
ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 132 yenye urefu wa kilomita
80 kutoka Mtwara hadi Mahumbika (Lindi) pamoja na vituo vya kupoza umeme vya
Mtwara na Mahumbika;
(ix)
Kukamilika kwa asilimia 95 kwa
ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 220 kutoka Makambako hadi Songea;
(x)
Kukamilika kwa ujenzi wa
vituo vipya vya kupoza umeme vya Mbagala, Kipawa, Gongolamboto na Mburahati
Mkoani Dar es Salaam;
(xi)
Kukamilika kwa ujenzi wa
vituo vya kupoza umeme vya Njiro B, Mount Meru, Sakina, Unga Ltd, Kiltex na
Themi Mkoani Arusha;
(xii)
Kukamilika kwa ujenzi wa
vituo vya kupoza umeme vya Bomambuzi na Trade School Mkoani Kilimanjaro;
(xiii)
Kukamilika kwa ukarabati wa
vituo vya kupoza umeme vya Mikocheni, Oysterbay, City Centre, Gongolamboto,
Kariakoo, Mbagala, Chang’ombe, Kipawa na Ubungo Mkoani Dar es Salaam;
(xiv)
Kuunganishwa kwa Mikoa ya
Lindi na Mtwara katika Gridi ya Taifa kutokana na kukamilisha ujenzi wa njia ya
msongo wa kV 33 kutoka Mbagala kupitia Mkuranga, Ikwiriri, Somanga Fungu, Lindi
hadi Mtwara yenye urefu wa kilomita 451;
(xv)
Kuunganishwa kwa Wilaya za
Ngara na Biharamulo katika Gridi ya Taifa kutokana na kukamilika kwa ujenzi wa
njia ya msongo wa kV 33 yenye urefu wa kilomita 70 na hivyo kupunguza gharama
za matumizi ya mafuta kwa wastani wa Shilingi bilioni 3.5 kwa mwaka. Kukamilika kwa ujenzi wa njia hizi kumewezesha kuunganisha nchi
yetu katika Gridi ya Taifa kutoka Mtwara mpakani mwa Msumbiji hadi Ngara
mpakani mwa Rwanda na Burundi;
(xvi)
Kusitisha uingizaji wa
vifaa vya ujenzi wa miundombinu ya umeme ikiwemo nguzo, transfoma, nyaya na
mita za LUKU ndani ya nchi na hivyo kulipunguzia gharama kubwa Shirika la Umeme
Nchini, TANESCO na kuokoa wastani wa Shilingi bilioni 162.57 kwa mwaka;
(xvii)
Kuanza maandalizi ya ujenzi
na utekelezaji wa Mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa maji wa maporomoko ya Mto
Rufiji MW 2100;
(xviii)
Kuunganishiwa umeme wateja
wapya 201,046 na kufanya jumla ya wateja waliounganishiwa umeme hadi mwezi Mei,
2018 kufikia 2,226,036;
(xix)
Kukamilika maandalizi
ya utekelezaji wa Mradi wa Kusafirisha Mafuta Ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi
Tanga (Tanzania);
(xx)
Kukamilika kwa ujenzi na kuanza kutumika kwa Bandari ya Mtwara kupokea
mafuta hivyo kufanya Tanzania kuwa na Bandari tatu (3) za kupokea mafuta zikiwemo
Dar es Salaam na Tanga;
(xxi)
Kuanza utekelezwaji wa Mpango wa Kusambaza Gesi Asilia Majumbani katika
Mikoa ya Dar es Salaam na Mtwara; na
(xxii)
Kuongezeka kwa gesi asilia
iliyogunduliwa kutoka Futi za Ujazo Trilioni
57.25 mwaka 2016/17 na kufikia Futi za Ujazo Trilioni 57.54 mwaka
2017/18 kutokana na ugunduzi wa kitalu cha Ruvuma cha Futi
za Ujazo Bilioni 466 kutoka Futi za Ujazo Bilioni 178.
17.
Mheshimiwa Spika,
mafanikio hayo yametokana na utekelezaji
thabiti wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 - 2020 chini ya Uongozi makini
wa Serikali ya Awamu ya Tano. Ilani hiyo imejielekeza katika kufikia uchumi wa
viwanda ifikapo mwaka 2020 ambao Sekta ya Nishati ndiyo injini.
B. MPANGO NA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI KWA MWAKA 2018/19
18.
Mheshimiwa Spika, maeneo ya kipaumbele ya Wizara ya Nishati kwa kipindi cha mwaka 2018/19 ni
pamoja na: kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo:
Mradi wa kuzalisha umeme katika Mto Rufiji MW 2,100 uliopo wilayani Rufiji na
miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia ya Kinyerezi I - Extension MW 185; Kinyerezi II MW 240;
Somanga Fungu MW 330 Mkoani Lindi; pamoja na MW 300 Mkoani Mtwara; kuimarisha
mifumo ya usafirishaji wa umeme mkubwa nchini; kuendelea na utekelezaji wa
Awamu ya Tatu ya Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA III); kuendelea
na utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Bomba la kusafirisha Mafuta Ghafi kutoka Hoima
(Uganda) hadi Tanga (Tanzania); kuimarisha shughuli za utafutaji wa mafuta na
gesi asilia; na kuendeleza miradi ya nishati jadidifu (jotoardhi, upepo na
umeme-jua). Wizara imejielekeza katika kutekeleza maeneo mengine ya kipaumbele
yakiwemo: kuendelea kuwajengea uwezo watumishi wa Wizara
na Taasisi zilizo chini yake katika kusimamia Sekta ya Nishati; kuboresha
mazingira ya ofisi kwa watumishi wa Wizara na Taasisi zake ili kutoa huduma
bora zaidi; na kuendelea kuelimisha umma na kuboresha mawasiliano na wadau
mbalimbali kuhusu masuala ya nishati.
19.
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2018/19, Wizara
imepangiwa kukusanya Jumla ya Shilingi bilioni 394.45. Kati ya makusanyo hayo, Shilingi
bilioni 394.44 zitakusanywa kupitia shughuli za
mafuta na gesi asilia na Shilingi milioni 10.00
zitakusanywa
kupitia shughuli za utawala.
C.
SEKTA NDOGO YA UMEME
HALI YA UPATIKANAJI WA UMEME NCHINI
20.
Mheshimiwa Spika, katika kutimiza azma ya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa viwanda na kufikia
malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2025, Serikali kupitia Wizara ya
Nishati imelenga kuzalisha umeme MW
5,000 ifikapo mwaka 2020 na kufikisha MW
10,000 ifikapo mwaka 2025. Aidha, mahitaji ya umeme nchini yameendelea
kuongezeka kutokana na kukua na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi
zinazohitaji nishati ya umeme wa kutosha, wa uhakika, unaotabirika na wa gharama
nafuu katika uzalishaji.
21.
Mheshimiwa Spika, umeme uliozalishwa nchini uliongezeka kutoka GWh 7,092 mwaka 2016 na kufikia GWh 7,114 mwaka 2017 sawa na ongezeko la asilimia 0.3. Aidha, katika mwaka 2017/18 uwezo wa mitambo ya
kuzalisha umeme (installed capacity)
iliyopo nchini umeongezeka kutoka MW
1,450 mwaka 2016/17 na kufikia MW
1,517.47 mwezi Mei, 2018 sawa na ongezeko la asilimia 4.7. Ongezeko hilo limetokana na kukamilika kwa mitambo
sita (6) ya kuzalisha umeme ya Kinyerezi II ambayo hadi sasa inazalisha Jumla ya MW 168. Kati ya MW 1,517.47
zilizounganishwa katika Gridi ya Taifa ni MW
1,435.56 na zilizopo nje ya Gridi ya Taifa ni MW 81.91 (Kielelezo Na.1 na Na.2). Ongezeko hili limewezesha kuwa
na umeme wa ziada wa wastani wa MW 280
ambapo matumizi ya juu ya umeme yamefikia wastani wa MW 1,051 kwa siku.
MIRADI YA KUZALISHA UMEME
Ujenzi wa Mradi wa Rufiji (Rufiji
Hydro Power Project) – MW 2,100
22.
Mheshimiwa Spika, lengo la kutekeleza Mradi huu
ni kuzalisha umeme wa Jumla ya MW 2,100
kwa kutumia maji (Hydro Power Plant)
katika Bonde la Mto Rufiji. Utekelezwaji wa Mradi huu mkubwa nchini ni
kichocheo muhimu katika kuwezesha Tanzania kufikia azma yake ya kuwa nchi ya
uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 hatua iliyofikiwa ni pamoja na kufanya
uchambuzi wa zabuni (tender evaluation)
zilizowasilishwa na Wakandarasi walioonesha nia ya kutekeleza Mradi huu. Aidha,
ujenzi wa njia ya msongo wa kV 33
kutoka eneo la Dakawa kwa ajili ya kupeleka umeme utakaotumiwa na Mkandarasi
wakati wa ujenzi wa Mradi ulianza mwezi Novemba, 2017 na unatarajiwa kukamilika
ifikapo mwezi Julai, 2018.
23.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka
2018/19 Serikali itaendelea na utekelezaji wa Mradi huu ambapo kazi
zitakazofanyika ni pamoja na: ujenzi wa kambi na ofisi za wafanyakazi; ujenzi
wa bwawa (main dam and spillways); na
ujenzi wa njia kuu za kupitisha maji (tunnels).
Fedha za maendeleo za ndani Shilingi bilioni 700 zimetengwa katika mwaka 2018/19 kwa ajili ya kuanza kutekeleza kazi
hizo. Utekelezaji wa shughuli za ujenzi wa Mradi unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2018 kwa
Mkandarasi kuanza kazi za awali kwa miezi mitatu (3) na kufuatiwa na ujenzi wa
miundombinu ya Mradi unaotarajiwa
kukamilika katika kipindi cha miezi 36.
Mradi wa Kinyerezi I Extension - MW
185
24.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu upanuzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi I
kwa kuongeza mitambo itakayozalisha MW
185 na kufanya kituo hicho ambacho kwa sasa kinazalisha umeme wa MW 150 kuzalisha jumla ya MW 335. Mradi huu unagharamiwa na
Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 188 sawa na takriban Shilingi bilioni 434. Katika mwaka 2017/18 kazi zilizokamilika ni
pamoja na: ujenzi wa misingi ya kusimika mitambo ya kuzalisha umeme na
transfoma; ujenzi wa misingi ya kituo cha kupoza umeme; na ujenzi wa njia ya
msongo wa kV 220 inayounganisha
mtambo wa Kinyerezi I Extension na
Kinyerezi II na kuunganishwa katika Gridi ya Taifa.
25.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2018/19 kazi ya usimikaji wa mitambo pamoja
na ukamilishaji wa ujenzi wa kituo cha kupoza umeme zitafanyika kwa gharama ya Shilingi bilioni 164 zikiwa ni fedha za ndani. Ujenzi wa Mradi
ulianza mwezi Novemba, 2016 na unatarajiwa kukamilika mwezi Januari, 2019.
Mradi wa Kinyerezi II - MW
240
26. Mheshimiwa Spika, Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi
asilia wa Kinyerezi II unatarajiwa kuongeza Jumla ya MW 240 katika Gridi ya Taifa. Uzalishaji umeme katika Mradi huu
ulizinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli tarehe 03
Aprili, 2018. Hadi sasa mitambo sita (6) ya gas
turbines imefungwa na inazalisha umeme wa jumla ya MW 168 zilizoingizwa katika Gridi ya Taifa. Ufungaji wa mitambo
miwili (2) yenye uwezo wa kuzalisha Jumla ya MW 80.4 kwa kutumia mvuke (steam
turbines) unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018. Gharama za kutekeleza
Mradi huu ni Dola za Marekani milioni
344 sawa na takriban Shilingi
bilioni 794.12. Asilimia 15 ya
gharama za Mradi huu ni fedha za ndani na asilimia
85 ni mkopo wa masharti nafuu kutoka benki za Japan Bank for International Cooperation (JBIC) na Sumitomo Mitsui
Banking Corporation (SMBC) za Japan.
Mradi wa Somanga Fungu - MW 330
27.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa mitambo ya kuzalisha umeme wa MW 330 kwa kutumia gesi asilia. Aidha,
Mradi unahusu ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa kV 400 umbali wa kilomita 198.2 kutoka Somanga Fungu hadi
Kinyerezi. Mradi huu utamilikiwa na Serikali kupitia TANESCO kwa asilimia 100.
Gharama za Mradi zinakadiriwa kuwa Dola
za Marekani milioni 396 sawa na takriban Shilingi bilioni 914.16. Upembuzi
Yakinifu wa Mradi umekamilika na taratibu za kumpata Mkandarasi mwenye uwezo wa
kitaalam na fedha kwa kushindanishwa chini ya utaratibu wa EPC plus Financing zinaendelea.
28.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2018/19 kazi zilizopangwa kufanyika ni pamoja
na: kukamilisha taratibu za kumpata Mkandarasi na fedha za kutekeleza Mradi;
kumpata Mshauri Mwelekezi wa usimamizi wa Mradi; na kuanza utekelezaji wa
Mradi. Shilingi bilioni 4.5 fedha za
nje zimetengwa ili kutekeleza kazi hizo. Ujenzi wa Mradi huu unatarajiwa kuanza
mwezi Septemba, 2018 na kukamilika ifikapo mwezi Septemba, 2021.
Mradi wa Mtwara MW 300
29.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Mtwara unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa MW 300 kwa kutumia gesi asilia na
ujenzi wa kituo cha kupoza umeme. Mradi utahusu pia ujenzi wa njia ya
kusafirisha umeme wa kV 400 umbali wa kilomita 253 kutoka Mtwara hadi Somanga
Fungu. Utekelezaji wa Mradi huu utaimarisha upatikanaji wa umeme katika mikoa
ya Lindi na Mtwara. Mradi huu unatarajiwa kugharimu Dola za Marekani milioni 360 sawa na takriban Shilingi bilioni 831 na utamilikiwa
na Serikali kupitia TANESCO kwa asilimia 100. Katika mwaka 2017/18 kazi
zilizotekelezwa ni pamoja na kuanza Upembuzi Yakinifu chini ya ufadhili wa JICA
mwezi Julai, 2017 ambao unatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2018.
30.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 kazi zilizopangwa kufanyika ni pamoja na:
kukamilisha Upembuzi Yakinifu wa Mradi; kumtafuta Mshauri Mwelekezi; na kuandaa
nyaraka za zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi. Jumla ya Shilingi bilioni 3.7 zinakadiriwa kutumika
kuwalipa fidia wananchi watakaopisha Mradi. Katika mwaka 2018/19 fedha za nje Shilingi bilioni 4 zimetengwa ili
kutekeleza shughuli za Mradi huu. Ujenzi wa Mradi unatarajiwa kuanza mwezi
Novemba, 2018 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
Mradi wa Kakono – MW 87
31.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa MW 87 kwa kutumia maji ya Mto Kagera na
ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 132 yenye urefu wa kilomita 38.8 kutoka Kakono hadi Kyaka.
Gharama za ujenzi wa Mradi ni Dola za
Marekani milioni 379.4 sawa na takriban Shilingi bilioni 875.84. Kazi iliyofanyika katika mwaka 2017/18 ni kupima
na kutathmini eneo la Mradi ambapo taarifa kuhusu alama za mipaka na tathmini
ya eneo la ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme pamoja na njia ya kusafirisha
umeme imekamilika. Aidha, Mshauri Mwelekezi (Kampuni ya Studio Pietrangeli kutoka Italia) kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa Mradi
ameshapatikana.
32.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/19, kazi zitakazofanyika ni pamoja na: kuwalipa fidia
wananchi watakaopisha Mradi; kumpata Mtaalam Mshauri kwa ajili ya kufanya
utafiti zaidi wa kijiolojia na haidrolojia; na kutayarisha zabuni kwa ajili ya
Mkandarasi wa ujenzi wa kituo na miundombinu ya kusafirisha umeme. Jumla ya Shilingi bilioni 4.05 zimetengwa kwa
ajili ya shughuli hizo. Kati ya fedha hizo Shilingi
bilioni 2 ni fedha za ndani na Shilingi
bilioni 2.05 ni fedha za nje. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Machi,
2019 na kukamilika ifikapo mwezi Novemba, 2021.
Mradi wa Rusumo - MW 80
33.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme
wa MW 80 kwa kutumia maporomoko ya
maji ya Mto Kagera ambapo umeme huo utagawanywa kwa usawa kati ya nchi za
Tanzania, Rwanda na Burundi. Mradi unahusisha pia ujenzi wa njia za kusafirisha
umeme wa msongo wa kV 220 kutoka
Rusumo hadi kituo cha kusafirishia umeme kwa kila nchi. Kwa upande wa Tanzania
umeme utasafirishwa hadi Nyakanazi. Katika kipindi cha mwaka 2017/18, kazi zilizofanyika ni kuanza ujenzi wa: bwawa la
kuhifadhia maji; njia za kupitisha maji (intake
tunnel); eneo la kusimika mitambo (power
house); barabara za kuingia eneo la Mradi; pamoja na ofisi na nyumba za
wafanyakazi.
34.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kufanyika
mwaka 2018/19 ni: kukamilisha ujenzi wa kambi ya kudumu ya wafanyakazi;
kukamilisha miundombinu ya barabara za kuingia eneo la Mradi; na kuendelea na
ujenzi wa bwawa la kuhifadhia maji;
njia za kupitisha maji (intake tunnel);
na eneo la kusimika mitambo (power house). Fedha za nje Shilingi
bilioni 3 zimetengwa katika mwaka
2018/19 kwa ajili ya Mradi huu. Utekelezaji wa Mradi ulianza mwezi
Machi, 2017 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Februari, 2021.
Mradi wa Murongo/Kikagati - MW 14
35.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa MW
14 kwa
kutumia maji ya Mto Kagera zitakazogawanywa kwa usawa kati ya nchi ya Tanzania
na Uganda. Mradi pia utahusisha ujenzi wa njia za kusafirisha umeme wa msongo
wa kV 33 yenye urefu wa kilomita 0.7
kutoka Kikagati (Uganda) hadi Murongo (Tanzania). Mradi huu unatekelezwa na
mwekezaji binafsi, Kampuni ya Kikagati Power Company Ltd (KPCL) iliyosajiliwa
nchini Uganda ambapo umeme utakaozalishwa utauzwa kwa Kampuni za Uganda
Electricity Transmission Company Ltd (UETCL) na Tanzania Electricity Supply
Company Ltd (TANESCO). Mradi utagharimu Dola
za Marekani milioni 58 sawa na takriban Shilingi bilioni 133.89.
36.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na:
kusainiwa kwa Mkataba wa Ugawanaji wa Umeme kwa Usawa (Power Sharing and Sales Agreement) kati ya UETCL na TANESCO;
kusainiwa kwa Mkataba wa Kuuziana Umeme (Power
Purchase Agreement) kati ya kampuni ya KPCL na UETCL; kukamilika kwa malipo
ya fidia kwa wananchi wanaopisha Mradi; na kuanza kutekelezwa kwa kazi za awali
za ujenzi ikiwemo kambi ya wafanyakazi na barabara za kuingia kwenye eneo la
Mradi (access road). Kazi zitakazotekelezwa kwa mwaka 2018/19 ni pamoja na: kukamilisha ujenzi wa
kambi ya kudumu ya wafanyakazi na miundombinu ya barabara za kuingia eneo la
Mradi; na kuanza ujenzi wa bwawa (main dam and spillways) na njia kuu za
kupitisha maji (tunnels). Mradi huu ulianza mwezi
Novemba, 2017 na unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2020.
Mradi wa Malagarasi – MW 45
37.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa MW 45 kwa kutumia maporomoko ya maji ya
Mto Malagarasi Mkoani Kigoma na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo
wa kV 132 yenye urefu wa kilomita 53
kutoka Malagarasi hadi Kidahwe-Kigoma. Gharama za utekelezaji wa Mradi ni Dola za Marekani milioni 149.5 sawa na
takriban Shilingi bilioni 345.12. Katika mwaka 2017/18 kazi
zilizofanyika ni pamoja na: uboreshaji wa tathmini ya athari za jamii na
mazingira (ESIA) na tathmini ya fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi; upimaji
na uthamini wa eneo la Mradi wa njia ya kusafirisha umeme umeanza; na Mshauri
Mwelekezi (Kampuni ya Studio Pietrangeli
kutoka Italia) kwa ajili ya kusimamia
utekelezaji wa Mradi amepatikana.
38.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19, kazi zilizopangwa kufanyika ni pamoja na: kukamilisha
Upembuzi Yakinifu wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 132; kumpata Mkandarasi; na
kukamilisha upimaji na uthamini wa eneo la Mradi na njia ya kusafirisha umeme.
Jumla ya Shilingi bilioni 7.8
zinakadiriwa kutumika kuwalipa fidia wananchi watakaopisha Mradi. Katika mwaka
2018/19 Shilingi bilioni 4.3 zimetengwa
kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za Mradi. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 1.5 ni fedha za ndani
na Shilingi bilioni 2.8 ni fedha za
nje. Shughuli za ujenzi wa Mradi huu zinatarajiwa kuanza mwezi Machi, 2019 na
kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2021.
Mradi wa
Ruhudji - MW 358
39.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme
wa MW 358 kwa kutumia maporomoko ya
maji ya Mto Ruhudji. Mradi utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa
msongo wa kV 400 yenye urefu wa
kilomita 170 kutoka Ruhudji Mkoani Njombe hadi kituo cha kupoza umeme cha
Kisada Mkoani Iringa. Kazi zilizofanyika hadi sasa ni pamoja na Serikali kuwasilisha maombi
ya ufadhili wa Mradi kwa Benki ya Dunia na kufanyika kwa zoezi la uhakiki wa
kiwango cha maji katika Mto Ruhudji ili kujua kiwango
halisi cha umeme kinachoweza kuzalishwa. Utekelezaji wa Mradi huu unakadiriwa
kugharimu Dola za Marekani milioni 460.6
sawa na takriban Shilingi trilioni
1.06. Katika kipindi cha mwaka
2018/19 Serikali itaendelea na majadiliano na wafadhili ili
kuwezesha upatikanaji wa fedha za kutekeleza Mradi. Mradi huu unatarajiwa kuanza
kujengwa katika kipindi cha mwaka
2018/19 baada ya fedha kupatikana na unatarajiwa kukamilika mwaka 2020/21.
Miradi ya Kinyerezi III - MW 600
40.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu utahusisha ujenzi wa kituo
cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia MW 600 katika awamu mbili
(2) za MW 300 kwa kila awamu katika
eneo la Kinyerezi - Dar es salaam. Kazi zilizopangwa
kutekelezwa katika mwaka 2018/19 ni pamoja na: kukamilisha Upembuzi Yakinifu;
na kumpata Mkandarasi mwenye uwezo wa kitaalam na fedha kwa
kushindanishwa chini ya utaratibu wa EPC
plus Financing. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Novemba, 2018 na kukamilika mwezi Desemba, 2021.
Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa kutumia Makaa ya
Mawe Kiwira – MW 200
41. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha
kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe chenye uwezo wa MW 200 katika eneo la Kiwira na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme
wa msongo wa kV 220 yenye urefu wa
kilomita 100 kutoka Kiwira hadi Uyole-Mbeya. Gharama za kutekeleza Mradi zinakadiriwa
kuwa Dola za Marekani milioni 320 sawa
na takriban Shilingi bilioni 738.72.
Katika mwaka 2018/19 TANESCO na STAMICO watakamilisha Makubaliano ya Awali (Memorandum of Understanding - MoU) ya
kuuziana makaa ya mawe na taratibu za kumpata Mkandarasi mwenye teknolojia na
uwezo wa kutekeleza Mradi na kuanza shughuli za ujenzi baada ya kukamilisha
Upembuzi Yakinifu. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2019 na
kukamilika mwezi Aprili, 2022.
Ukarabati wa Mitambo katika Kituo cha Kufua Umeme cha Hale (Hale Hydro Power Plant)
42.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ukarabati wa mitambo na ujenzi wa miundombinu ya
kuzalisha umeme katika Kituo cha Hale ili kuwezesha kituo hicho kuzalisha umeme
kwa kiwango cha uwezo wake wa MW 21
kutoka MW 10.5 zinazozalishwa sasa.
Makadirio ya gharama za Mradi huu ni SEK
milioni 200 sawa na takriban Shilingi
bilioni 50.98 ambapo asilimia 60
ya gharama hizo ni msaada kutoka Serikali ya Sweden kupitia Shirika lake la
Maendeleo la Kimataifa (Sida) na asilimia
40 ni mchango wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi
zilizofanyika ni pamoja na kukamilika kwa: usanifu (design) wa Mradi; uandaaji wa Mpango Kazi; pre-qualification ya Wakandarasi. Zabuni zitafunguliwa mwezi Juni,
2018. Kwa mwaka 2018/19 Mkandarasi ataanza kazi ya ukarabati wa mitambo ambapo
jumla ya Shilingi bilioni 6.7 fedha
za nje zimetengwa. Mradi unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2018 na kukamilika
mwezi Novemba, 2021.
Mradi wa Umeme Unaotokana na Nishati ya Jua
katika Mkoa wa Shinyanga – MW 150
43.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kufua umeme-jua MW 150 katika eneo la Ibadakuli Wilayani
Kishapu Mkoani Shinyanga. Mradi huu unatarajiwa kutekelezwa na Serikali kupitia
TANESCO kwa ufadhili wa Taasisi ya Maendeleo ya Ufaransa (AFD). Katika
kuendeleza Mradi huu AFD imetoa msaada wa Euro
520,130 sawa na takriban Shilingi
bilioni 1.3 kwa ajili ya kuwezesha na kukamilisha zoezi la Upembuzi
Yakinifu utakaojumuisha tathmini ya kitaalam, kiuchumi na mazingira. Kazi
zilizofanyika katika mwaka 2017/18 ni pamoja na: kukamilisha tathmini ya fidia
kwa wananchi watakaopisha Mradi pamoja na kupatikana kwa Mshauri Mwelekezi
ambaye ameanza kazi ya Upembuzi Yakinifu unaotarajiwa kukamilika mwezi
Septemba, 2018. Jumla ya Shilingi
bilioni 1.3 zinakadiriwa kutumika kuwalipa fidia wananchi watakaopisha
Mradi. Katika mwaka 2018/19 kazi zilizopangwa kufanyika ni pamoja na: kulipa
fidia wananchi watakaopisha Mradi;
kukamilisha taratibu za ufadhili wa Mradi; na kuanza utekelezaji wa
Mradi. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Januari, 2019 na kukamilika mwezi
Desemba, 2020.
Mradi wa Umeme wa Upepo Singida – Wind East Africa (WEA) MW 100
44.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu ni wa kuzalisha umeme wa MW
100 unaotokana na nishati ya upepo katika eneo la Kisaki na Utaho Mkoani Singida. Mradi utatekelezwa kwa ubia
kati ya Kampuni ya Six Telecoms
(Tanzania), International Finance
Corporation - IFC (Marekani) na Aldwych
International (Uingereza). Gharama za Mradi huu zinakadiriwa kuwa Dola
za Marekani milioni 285 sawa na takriban Shilingi bilioni 657.92. Kwa mwaka 2017/18 majadiliano ya Mkataba wa Kibiashara (PPA) kati ya
TANESCO na Kampuni ya Wind East Africa (WEA) yako katika hatua za mwisho. Katika mwaka 2018/19 kazi zilizopangwa
kufanyika ni pamoja na kukamilisha majadiliano ya PPA na kuanza utekelezaji wa
Mradi. Ujenzi wa Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2018 na kukamilika
mwezi Desemba, 2020.
UJENZI WA NJIA ZA KUSAFIRISHA UMEME
Mradi wa njia ya Umeme wa Msongo wa kV 220
kutoka Makambako hadi Songea na Usambazaji wa Umeme Vijijini kwa Mikoa ya
Njombe na Ruvuma
45.
Mheshimiwa Spika, lengo la Mradi ni kujenga njia ya umeme wa msongo wa kV 220 yenye urefu wa kilomita 250
kutoka Makambako hadi Songea kupitia Madaba. Kazi nyingine zinazohusu Mradi ni:
ujenzi wa vituo vipya viwili (2) vya kupoza umeme vya Madaba na Songea mjini;
upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha Makambako; utandazaji wa nyaya za
mawasiliano; ujenzi wa njia za
kusambaza umeme wa msongo wa kV 33
wenye urefu wa kilomita 900; na kuunganisha wateja wa awali 22,700 katika Vijiji 120 vya Wilaya za Makambako, Njombe na
Ludewa katika Mkoa wa Njombe; na Songea Vijijini, Songea Mjini, Namtumbo na
Mbinga katika Mkoa wa Ruvuma.
46.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizotekelezwa kwa mwaka 2017/18 kwa upande wa njia ya kusafirisha umeme kV 220 Makambako hadi Songea ni
kukamilika kwa usanifu, utengenezaji, usafirishaji wa vifaa na ujenzi wa misingi ya nguzo. Kwa upande wa ujenzi wa vituo vya
kupoza umeme vyenye uwezo wa kV 220/33 vya Makambako, Madaba na Songea,
usafirishaji wa vifaa na ujenzi wa misingi umekamilika. Hadi kufikia mwezi Mei,
2018 ujenzi wa miundombinu ya usambazaji umeme kwenye vijiji 32 kati ya 120
umekamilika na jumla ya wateja 1,500 kati ya 22,000 wameunganishiwa umeme.
47.
Mheshimiwa Spika, kwa ujumla hadi kufikia mwezi Mei, 2018 ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kV
220 kutoka Makambako – Songea umefikia asilimia
95; Ujenzi wa vituo viwili (2) vipya vya kupoza umeme vya Madaba na Songea
umefikia asilimia 76; na usambazaji
umeme umefika asilimia 68.5 kwa
Mikoa ya Ruvuma na Njombe. Kazi
zilizopangwa kufanyika mwaka 2018/19 ni kukamilisha: ujenzi wa vituo vya kupoza
umeme; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kV 220; na uunganishaji wa wateja. Jumla ya Shilingi bilioni 13 zimetengwa katika mwaka
2018/19 ili kutekeleza kazi hizo. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 7 ni fedha za ndani na
Shilingi bilioni 6 ni fedha za nje.
Mradi huu ulianza mwezi Desemba, 2016 na unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba,
2018.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha
Umeme wa Msongo wa kV 400 kutoka Iringa - Shinyanga (Backbone – Awamu ya Pili)
48.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu kuongeza uwezo (upgrade)
wa vituo vya kupoza umeme kutoka kV 220
hadi kV 400 katika miji ya Iringa,
Dodoma, Singida na Shinyanga. Gharama ya Mradi ni Dola za Marekani Milioni 120 sawa na takriban Shilingi bilioni 277.02 zinazotokana na mikopo kutoka Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AfDB), Benki ya Jumuiya ya Ulaya (EIB) na Serikali ya
Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa (JICA). Katika kipindi cha
mwaka 2017/18 Mkandarasi atakayefanya kazi katika vituo vya kupoza umeme vya
Dodoma na Singida amepatikana na tayari ameanza kazi. Katika mwaka 2018/19 kazi
zilizopangwa kufanyika ni: kumpata Mkandarasi kwa ajili ya vituo vya Iringa na Shinyanga na
kuendelea na utekelezaji wa Mradi. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Septemba,
2018 na kukamilika mwezi Juni, 2020.
Mradi wa Njia ya
Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 kutoka Masaka - Mwanza
49.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Masaka nchini Uganda hadi
Mwanza - Tanzania na upanuzi wa vituo vya kupoza umeme wa kV 400/220 katika
maeneo ya Kyaka na Rusumo/Nyakanazi. Kazi zilizofanyika kwa mwaka 2017/18 ni
kukamilika kwa majadiliano ya Mkataba kati ya TANESCO na Mshauri Mwelekezi
Kampuni ya Norconsult kutoka Norway atakayedurusu Upembuzi Yakinifu wa Mradi. Upembuzi
Yakinifu huo unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2018 na kukamilika mwezi Novemba,
2019. Katika mwaka 2018/19 Shilingi bilioni 2.5 fedha za nje zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha
Umeme wa Msongo wa kV 400, Iringa - Mbeya – Tunduma - Sumbawanga – Mpanda -
Kigoma – Nyakanazi (North West Grid)
50.
Mheshimiwa Spika, Mradi unahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400
kutoka Iringa - Mbeya – Tunduma - Sumbawanga – Mpanda - Kigoma – Nyakanazi
yenye urefu wa kilomita 1,372. Mradi huu utawezesha kuunganisha umeme maeneo ya
Magharibi na Kaskazini-Magharibi mwa Tanzania katika Gridi ya Taifa na kuondoa
matumizi ya mitambo ya mafuta (diesel)
katika maeneo hayo na kuwafikishia umeme wananchi wengi.
51.
Mheshimiwa Spika, Benki ya Dunia imeonesha nia ya kufadhili ujenzi wa vituo vya kupoza
umeme na njia ya kusafirisha umeme kutoka Iringa – Mbeya – Tunduma – Sumbawanga
– Kigoma yenye urefu wa kilomita 612 inayounganisha Zambia na Tanzania. Mradi
utagharimu Dola za Marekani milioni 455
sawa na takriban Shilingi trilioni 1.05.
Sehemu hii ya Mradi itaunganisha Mradi wa North-West grid kV 400 unaoanzia Sumbawanga – Mpanda – Kigoma –
Nyakanazi yenye urefu wa kilomita 760. Serikali ya Korea Kusini kupitia Mfuko
wake wa Maendeleo (EDCF) imeonesha nia ya kufadhili ujenzi wa vituo vya kupoza
umeme katika maeneo ya Kigoma na Nyakanazi kwa Dola za Marekani milioni 40.5 sawa
na takriban Shilingi bilioni 93.49 na
AfDB imeonesha nia ya kufadhili ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka
Nyakanazi hadi Kigoma yenye urefu wa kilomita 280 kwa Dola za Marekani milioni 93.5 sawa na takriban Shilingi bilioni 215.84.
52.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizofanyika katika kipindi cha mwaka 2017/18 ni
pamoja na: kupima na kufanya tathmini ya maeneo kwa ajili ya kujenga vituo vya
kupoza umeme vya Kigoma, Mpanda, Sumbawanga na Tunduma; kukamilisha uandaaji wa
taarifa za fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi kutoka Kigoma hadi
Nyakanazi; na kuendelea na majadiliano na wafadhili wa Mradi ambao ni Benki ya
Dunia, AfDB na EDCF. Jumla ya Shilingi
bilioni 25.5 zinakadiriwa kuwa zitatumika kulipa fidia wananchi
watakaopisha Mradi katika maeneo ya Iringa - Mbeya; Mbeya – Tunduma -
Sumbawanga; na Kigoma - Nyakanazi.
53. Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kufanyika mwaka 2018/19 ni:
ulipaji wa fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi; kukamilisha majadiliano na
wafadhili wa Mradi; kuwapata wakandarasi wa ujenzi; na kuanza utekelezaji wa
Mradi. Jumla ya Shilingi bilioni 33.2 zimetengwa
kwa ajili ya kazi hizo. Kati ya fedha hizo Shilingi
bilioni 31 ni fedha za ndani na Shilingi
bilioni 2.2 ni fedha za nje. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Desemba,
2018 na kukamilika mwezi Agosti, 2021.
Mradi wa Njia za
Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 na kV 220, North – East Grid
54.
Mheshimiwa Spika, lengo la Mradi huu ni kusafirisha umeme utakaozalishwa katika kituo cha
Kinyerezi, Dar es Salaam kwenda katika Mikoa ya Arusha na Tanga ambapo njia
zilizopo kwa sasa zimezidiwa na mahitaji makubwa ya umeme. Mradi huu utagharimu Dola
za Marekani milioni 692.7 sawa na takriban Shilingi trilioni 1.59. Kati ya gharama hiyo, asilimia 85 ni mkopo kutoka Benki ya Exim ya China na asilimia 15 ni mchango wa Serikali ya
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi
zilizofanyika ni pamoja na: kukamilisha upimaji na tathmini ya mali za wananchi
watakaopisha Mradi kwa kipande cha kutoka Kinyerezi - Kiluvya - Chalinze hadi
Segera. Fidia kwa kipande cha Kinyerezi – Chalinze inatarajiwa kulipwa wakati
wowote kuanzia sasa na maandalizi ya ulipaji fidia kwa kipande cha kuanzia
Chalinze hadi Segera yanaendelea. Kwa mwaka 2018/19 jumla ya Shilingi bilioni 47.8 zimetengwa kwa
ajili ya utekelezaji wa Mradi. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni
34.8 ni fedha za ndani na Shilingi
bilioni 13 fedha za nje.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha
Umeme wa Msongo wa kV 400 kutoka Somanga Fungu - Kinyerezi
55.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Somanga Fungu Mkoani
Lindi hadi Kinyerezi, Dar es Salaam wenye urefu wa kilomita 198 na kujenga
kituo cha kupoza umeme cha Somanga Fungu. Mradi huu utaunganisha na kusafirisha
umeme unaotarajiwa kuzalishwa katika maeneo ya Somanga Fungu na Mtwara hadi
Kinyerezi Dar es Salaam. Gharama za Mradi ni Dola za Marekani milioni 150 sawa na takriban Shilingi bilioni 346.27.
56.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na: kuendelea
na ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha Mradi ambapo hadi kufikia mwezi
Aprili, 2018 jumla ya Shilingi bilioni
49.5 zimelipwa kwa wananchi 2,487 kati ya 3,901. Aidha, Mshauri Mwelekezi
(Kampuni ya Byucksan Power Limited ya
Korea Kusini) kwa ajili ya kudurusu Upembuzi Yakinifu ameanza kazi mwezi
Desemba, 2017 na anatarajia kukamilisha mwezi Julai, 2018. Kazi zilizopangwa kufanyika kwa mwaka 2018/19 ni:
kukamilisha malipo ya fidia kwa wananchi waliobaki na kudurusu Upembuzi
Yakinifu. Jumla ya Shilingi bilioni 23.5
zimetengwa kutekeleza kazi hizo. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 22 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 1.5 ni fedha za nje. Shughuli za ujenzi
zinatarajiwa kuanza mwezi Agosti, 2019 na kukamilika mwezi Machi, 2020.
Mradi wa Njia ya
Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 kutoka Rufiji – Chalinze – Dodoma
57.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kV 400 yenye urefu wa kilomita 512
kutoka Rufiji kupitia Chalinze Mkoani Pwani hadi Dodoma na upanuzi wa vituo vya
kupoza umeme wa kV 400/220 katika Mji wa Chalinze na Jiji la Dodoma. Gharama za
Mradi zinakadiriwa kuwa Dola za Marekani
milioni 276.36 sawa na takriban Shilingi
bilioni 637.97.
58.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni: Upembuzi Yakinifu kwa
kipande cha kutoka Chalinze hadi Dodoma; na Upembuzi Yakinifu wa Awali (Pre-feasibility Study) kutoka Rufiji
hadi Chalinze. Pia, maandalizi ya kumpata Mshauri Mwelekezi kwa ajili ya
kufanya mapitio ya Upembuzi Yakinifu kwa eneo la Rufiji hadi Chalinze yameanza.
Kazi zilizopangwa kufanyika kwa mwaka 2018/19 ni:
kufanya Upembuzi Yakinifu; kuweka mipaka na kufanya tathmini ya njia ya
kusafirishia umeme kutoka Rufiji hadi Chalinze; na kukamilisha malipo ya fidia
kwa wananchi watakaopisha Mradi. Fedha za ndani Shilingi bilioni
39 zimetengwa kwa ajili ya kazi hizo. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2018 na kukamilika mwezi
Desemba, 2020.
Mradi wa Njia ya Umeme wa
Msongo wa kV 220 kutoka Bulyanhulu – Geita
59.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kV 220 yenye urefu wa kilomita 55
kutoka Bulyanhulu hadi Geita; ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Geita;
upanuzi wa Kituo cha kupoza umeme cha Bulyanhulu; usambazaji wa umeme katika
vijiji nane (8) vitakavyopitiwa na Mradi (kilomita 115) ambapo wateja wapya
1,500 wataunganishiwa umeme. Gharama za Mradi huu ni Dola za Marekani milioni 23 sawa na takriban Shilingi bilioni 53.09.
60.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na:
kukamilika uhakiki wa fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi pamoja na kuwapata
Wakandarasi watakaotekeleza Mradi. Jumla ya Shilingi bilioni 2
zinakadiriwa kutumika kuwalipa fidia wananchi watakaopisha Mradi. Kwa mwaka
2018/19 Shilingi bilioni 5 fedha za nje zimetengwa kwa ajili ya kuanza
utekelezaji wa Mradi. Mradi unatarajiwa kuanza mwezi Agosti, 2018 na kukamilika
mwezi Aprili, 2020.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha
Umeme wa Msongo wa kV 220 ya Geita – Nyakanazi na Usambazaji wa Umeme katika
Vijiji vitakavyopitiwa na Mradi
61. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya kV 220 (km 133), kituo cha kupoza umeme
Nyakanazi na kusambaza umeme katika vijiji 32 vinavyopitiwa na Mradi. Gharama za utekelezaji wa Mradi huu ni EURO milioni 45 sawa na takriban Shilingi bilioni 113.31. Mradi huu
unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW), Taasisi ya Maendeleo ya
Ufaransa (AFD), Umoja wa Ulaya (EU) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
62. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi
zilizofanyika ni: kufanya tathmini na uhakiki wa mali zitakazoathiriwa na
Mradi; kumpata Mkandarasi atakayejenga njia ya kusafirisha umeme; kujenga vituo vya kupoza umeme; na
usambazaji wa umeme vijijini. Jumla ya Shilingi
bilioni 5.79 zinakadiriwa kutumika kuwalipa fidia wananchi watakaopisha
Mradi. Kazi zilizopangwa kufanyika katika kipindi cha mwaka 2018/19 ni kuwalipa
fidia wananchi na kuanza utekelezaji wa Mradi. Fedha za nje Shilingi bilioni 1.6 zimetengwa kwa
ajili ya shughuli za Mradi. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2018 na
kukamilika mwezi Desemba, 2019.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 kutoka
Singida - Arusha – Namanga
63.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Singida hadi Namanga
kupitia Arusha yenye urefu wa kilomita 414. Mradi umegawanyika katika maeneo
matano (5) ya utekelezaji ambayo ni: Singida - Babati (km150); Babati - Arusha
(km150); Arusha – Namanga (km114); ujenzi na upanuzi wa vituo vya kupoza umeme (Substations) na usambazaji wa umeme
katika vijiji 21 vitakavyopitiwa na Mradi. Gharama za Mradi huu ni Dola za Marekani milioni 258.82 sawa na
takriban Shilingi bilioni 597.48
ambapo asilimia 83 ya fedha hizo
zitatolewa na wafadhili (AfDB na JICA). Aidha, Serikali ya Tanzania itachangia Dola za Marekani milioni 43.89 sawa na
takriban Shilingi bilioni 101.32 ambazo
ni asilimia 17 ya gharama za Mradi.
64.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na:
Mkandarasi kufanya detailed survey ya njia ya umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Singida hadi Namanga;
kusanifu na kufanya majaribio ya nguzo na vifaa vingine vitakavyotumika katika
ujenzi; kufanya utafiti wa udongo katika njia ya umeme; na Serikali kukamilisha
uhakiki wa malipo ya fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi. Jumla ya Shilingi bilioni 68.31 zinakadiriwa
kutumika kuwalipa fidia wananchi. Kazi nyingine zilizotekelezwa ni kufanya
malipo ya awali (advance payment) kwa
Wakandarasi wote wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme na kumpata Mkandarasi
wa kujenga kituo kipya cha kupoza umeme cha Kisongo Mkoani Arusha. Vilevile,
taratibu za kumpata Mkandarasi atakayesambaza umeme katika vijiji 21
vinavyopitiwa na Mradi zinaendelea.
65.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kufanyika mwaka 2018/19 ni Serikali kuwalipa fidia
wananchi watakaopisha ujenzi wa Mradi na Wakandarasi kuendelea na shughuli za
ujenzi wa Mradi. Shilingi bilioni 15
fedha za nje zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza kazi hizo. Utekelezaji wa Mradi
huu ulianza mwezi Machi, 2017 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2019.
Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400
kutoka Mtwara - Somanga Fungu
66.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 yenye urefu wa kilomita 253
kutoka Mtwara hadi Somanga Fungu na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katika
Manispaa ya Mtwara. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizotekelezwa ni kufanya Upembuzi Yakinifu ulioanza mwezi Julai, 2017 na unatarajiwa
kukamilika mwezi Julai, 2018 pamoja na tathmini ya athari za mazingira.
67.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kutekelezwa kwa mwaka 2018/19 ni kukamilisha: Upembuzi
Yakinifu; Taarifa ya Athari za Mazingira; taratibu za ufadhili wa Mradi; uwekaji wa alama za mipaka na kutathmini mali za wananchi
watakaopisha eneo la Mradi; utafutaji wa Mshauri Mwelekezi kwa ajili ya
kusimamia utekelezaji wa Mradi; na upatikanaji wa Mkandarasi wa ujenzi. Mradi huu utafadhiliwa
na Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la JICA na unakadiriwa kugharimu Dola za Marekani milioni 231.1 sawa na takriban Shilingi bilioni 533.49. Fedha za nje Shilingi bilioni 2 zimetengwa
katika mwaka 2018/19 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi. Mradi
huu unatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2018 na kukamilika mwezi Machi, 2021.
Mradi wa Rusumo
– Nyakanazi kV 220
68. Mheshimiwa Spika, Mradi unahusu ujenzi wa
njia ya umeme ya msongo wa kV 220
yenye urefu wa kilomita
98.2 kutoka Rusumo hadi
Nyakanazi. Gharama za
Mradi ni Dola za Marekani milioni 35 sawa
na takriban Shilingi bilioni 80.79. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi
zilizotekelezwa ni pamoja na kukamilisha: usanifu wa Mradi; uandaaji wa taarifa ya mpango
wa mazingira; utangazaji wa zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi; na uhakiki
wa fidia kwa wananchi watakaopisha Mradi. Jumla ya Shilingi
bilioni 5.19 zinakadiriwa kutumika kuwalipa fidia wananchi watakaopisha
Mradi. Kwa mwaka 2018/19 kazi zilizopangwa
kufanyika ni: kukamilisha maandalizi ya mkataba wa ujenzi na kumpata Mkandarasi
wa Mradi; kuwalipa fidia wananchi; na kuanza ujenzi wa Mradi. Fedha za nje Shilingi
bilioni 5 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi. Mradi huu
unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2018 na kukamilika mwezi Julai, 2019.
MIRADI YA KUBORESHA NJIA
ZA KUSAMBAZA UMEME
Mradi wa Kuboresha Vituo 10 vya Kupoza Umeme
69.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu ujenzi na
uboreshaji wa vituo 10 vya kupoza umeme ambavyo ni Mlandizi, Chalinze, Mufindi,
Mwakibete, Zuzu, Tabora, Nyakato, Musoma, Kibeta na Same. Vilevile, Mradi
unalenga kuboresha Mfumo wa Usimamizi na Upatikanaji wa Data (Supervisory Control and
Data Acquisition - SCADA/Energy Management System –EMS) pamoja na kuunga waya
wa mawasiliano (optic fiber) wenye
urefu wa jumla ya kilomita 1,345 kwa vituo vya Kanda ya Kusini Magharibi, Kanda
ya Ziwa na maeneo ya Kondoa, Babati, Mbulu na Karatu ambayo hayana optic fiber. Gharama za Mradi zinakadiriwa kuwa Euro milioni 53 sawa na takriban Shilingi bilioni 133.45 na unafadhiliwa
na Taasisi ya Maendeleo ya Ufaransa (AFD). Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi iliyofanyika
ni kumpata Mshauri Mwelekezi kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa
Mradi na anatarajiwa kuanza kazi mwezi Julai, 2018.
70.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kufanyika mwaka 2018/19 ni pamoja na: kukamilisha
durusu ya wigo wa kazi (Scope of Work); kufanya tathmini ya athari kwa jamii na
mazingira (ESIA); kuandaa michoro (Conceptual Design); kuwapata Wakandarasi; na
kuanza utekelezaji wa Mradi. Mradi unatarajiwa
kukamilika mwezi Desemba, 2020.
Mradi wa TEDAP wa
kuboresha njia za usambazaji umeme (Distribution)
katika mikoa ya Dar es Salaam, Arusha na Kilimanjaro
71.
Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2017/18 ufungaji wa vifaa vya kuongozea na
kulinda mitambo (control and protection)
pamoja na transfoma umekamilika katika vituo vyote 19 na vituo 18 vimewashwa na
vinatumika. Aidha, ujenzi wa njia za msongo wa kV 33 na 11 katika Mikoa ya Dar
es Salaam, Arusha na Kilimanjaro umekamilika kwa asilimia 100. Kazi zilizopangwa kutekelezwa kwa mwaka 2018/19 ni:
kukamilisha kazi zilizobaki katika njia ya msongo wa kV 132 ya Mbagala kwenda
Kurasini pamoja na kituo cha kupoza umeme cha Kurasini. Fedha za nje Shilingi bilioni 6.4 zimetengwa katika
mwaka 2018/19 kwa ajili ya malipo ya Mkandarasi. Kazi hizo zinatarajiwa
kukamilika mwezi Julai, 2018.
Mradi wa Kuboresha Mfumo wa
Usambazaji Umeme katika Jiji la Dodoma chini ya Ufadhili wa JICA
72.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme
ya msongo wa kV 132 kutoka Zuzu kwenda Msalato na kutoka Zuzu kwenda Kikombo
pamoja na ujenzi wa vituo viwili (2) vipya vya kupoza umeme katika maeneo ya
Msalato na Kikombo Mkoani Dodoma. Kazi nyingine ni ujenzi wa njia za kusambaza
umeme wa msongo wa kV 33 katika Jiji la Dodoma. Lengo la mradi huu ni kujiandaa
na ongezeko la mahitaji ya umeme yanayokadiriwa kufikia MW 2OO ifikapo mwaka 2020 kutoka mahitaji ya juu ya sasa ya MW 28 kutokana na Serikali kuhamishia shughuli
zake Makao Makuu Jijini Dodoma. Katika kipindi cha mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na
Serikali kuwasilisha maombi ya ufadhili wa Mradi kwa
Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la JICA. Kazi zilizopangwa
kwa mwaka 2018/19 ni kukamilisha taratibu za ufadhili wa Mradi na kuanza
utekelezaji. Mradi unatarajiwa kukamilika mwaka 2020/21.
Mradi wa Usambazaji Umeme kwa Maeneo ya Mijini (Urban Electrification Program)
73.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusu kuongeza kasi ya kuunganisha
wateja mijini na kupanua miundombinu ya usambazaji umeme ili kuhamasisha ujenzi
wa viwanda na kufikisha umeme katika makazi na maeneo ya huduma za jamii. Kwa mwaka 2017/18 Serikali iliwasilisha
maombi katika Benki ya AfDB kwa ajili ya
ufadhili wa Mradi ambapo Benki hiyo imempata Mshauri
Mwelekezi kwa ajili ya kuandaa Mpango Kabambe wa Usambazaji Umeme (Distribution Master Plan) katika mikoa
minne (4) ya Dodoma, Mbeya, Arusha na Mwanza. Kazi hiyo
itakapokamilika itaiwezesha AfDB kupata makadirio ya fedha zinazohitajika kwa
ajili ya utekelezaji wa Mradi katika mikoa husika. Kazi ya kuandaa Mpango
huo inatarajiwa kufanyika katika mwaka 2018/19.
74.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imewasilisha maombi Benki ya Dunia
kwa ajili ya ufadhili wa Mradi katika mikoa mingine iliyobaki ya Tanzania. Bara
Katika mwaka 2018/19 Benki ya Dunia itamtafuta Mshauri Mwelekezi atakayefanya
Upembuzi Yakinifu ili kuainisha maeneo ya mijini yanayohitaji umeme katika
mikoa hiyo. Upembuzi Yakinifu unatarajiwa kuanza mwezi Septemba, 2018 na
kukamilika mwezi Septemba, 2019 ambapo fedha za nje Shilingi bilioni 7 zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.
MIRADI YA KUSAMBAZA UMEME VIJIJINI
Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Pili (Turnkey Phase II)
75.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu ulihusisha ujenzi wa vituo sita (6) vya kuongeza msongo wa umeme
(kV 11/33) katika miji ya Kigoma, Kasulu, Kibondo, Ngara, Mbinga na Tunduru;
ujenzi wa kilomita 17,740 za njia ya msongo wa kV 33; ujenzi wa kilomita 10,970
za njia za usambazaji umeme wa msongo wa kV 0.4/0.23; ufungaji wa transfoma
4,100 za ukubwa tofauti; na uunganishaji wa wateja wa awali 250,000.
76.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
imeendelea kukamilisha utekelezaji wa
Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Pili (REA II) kwa kumalizia
kazi za nyongeza (additional scope)
na kuunganisha wateja. Hadi kufikia mwezi Desemba, 2017 Mradi huo ulikuwa
umekamilika kwa asilimia 99 kwa
kufikisha miundombinu ya umeme katika vijiji 2,598 kati ya 2,697 sawa na asilimia
96.3 na hivyo kuwezesha kuwaunganishia umeme jumla ya wateja 178,641 ambao
ni sawa na asilimia 71.46 ya
matarajio ya awali ya wateja 250,000. Zoezi la kuunganisha wateja ni endelevu
kulingana na wateja wanavyolipia na kazi hiyo itaendelea kufanywa na Shirika la
Umeme Nchini (TANESCO). Uunganishwaji wa wateja hao umechangia ongezeko la
upatikanaji wa huduma za umeme vijijini (access)
kufikia asilimia 49.5.
77.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa
Mradi huu uliokuwa umesimama katika Mikoa ya Kilimanjaro na Singida kutokana na
Mkandarasi wa awali Kampuni ya Spencon Services Ltd kushindwa kuukamilisha kwa
sasa unaendelea. Mradi huo unatekelezwa na Kampuni za Kitanzania za Njarita
Contractors na Octopus Engineering kwa Mkoa wa Kilimanjaro na JV EMEC
Engineering Dynamic and Systems na East African Fossil Co & CMG
Construction Co Ltd JV kwa Mkoa wa Singida. Kazi zitakazofanyika katika mwaka
2018/19 ni: ukamilishaji wa Mradi katika Mikoa ya Kilimanjaro na Singida;
kumalizia marekebisho madogo-madogo (snags)
yaliyojitokeza katika miundombinu iliyojengwa; na TANESCO kuendelea kuwaunganisha
wateja wanaolipia. Mradi katika Mikoa hii ya Kilimanjaro na Singida unatarajiwa
kukamilika Mwezi Agosti 2018.
78.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III)
unalenga: kufikisha umeme katika vijiji 7,873 ambavyo hadi kufikia mwezi Juni,
2016 vilikuwa havijafikiwa na miundombinu ya umeme. Aidha, katika kipindi cha
kuanzia mwezi Februari hadi Mei, 2018
jumla ya vijiji 518
kati 7,873 vilivyobaki tayari vimeunganishiwa umeme na
hivyo kubaki vijiji 7,355 vinavyoendelea kuunganishiwa umeme. Kazi
zinazofanyika ni pamoja na: kujenga miundombinu ya kusambaza umeme na kufunga
transfoma katika maeneo mbalimbali ikiwemo Taasisi za Umma, miradi ya maji na
shughuli nyingine za kiuchumi, vitongoji na vijiji ambavyo havijafikiwa na
umeme (Turnkey III - Round One);
vijiji vilivyopitiwa na miundombinu ya usafirishaji wa umeme kupitia Mradi wa Densification; vijiji vilivyopo pembezoni mwa Mkuza wa njia kuu ya
kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga. Kazi nyingine
zinazofanyika ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya usambazaji na ufungaji wa
mifumo ya nishati jadidifu katika maeneo yaliyo mbali na Gridi ya Taifa ambayo
yanahusisha visiwa vilivyomo ndani ya Maziwa na Bahari (Off-Grid Renewable Energy Project).
79.
Mheshimiwa Spika; utekelezaji wa miradi iliyopo katika Mpango wa REA III ni kama
ifuatavyo:-
(i)
Mradi wa Usambazaji Umeme katika
Maeneo ambayo yameshafikiwa na Miundombinu ya Umeme (Densification)
80.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusisha kuongeza wigo wa usambazaji
umeme katika vijiji, vitongoji na maeneo ambayo tayari yana miundombinu ya
umeme katika vijiji 4,395 vilivyounganishwa umeme. Mradi utatekelezwa katika Mikoa yote ya Tanzania
Bara na utahusisha: ujenzi wa kilomita 18,625 za umeme wa msongo wa kV 33;
kilomita 35,614 za umeme wa msongo wa kV 0.4; ufungaji wa transfoma 13,622;
pamoja na uunganishaji wa wateja wa awali 992,373 kwa kipindi cha miaka mitano
(5) kuanzia mwaka 2016/17 hadi mwaka 2020/21 sawa na wateja 300,000 katika utekelezaji
wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza.
81.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unatekelezwa kwa awamu ambapo Awamu ya Kwanza (Densification – Round I) ilianza mwezi Aprili, 2017 katika mikoa
nane (8) ya Pwani, Tanga, Arusha, Iringa, Njombe, Mbeya, Songwe na Mara na hadi
kufikia mwezi Mei, 2018 imekamilika kwa asilimia
98. Katika Awamu hii jumla ya vijiji 300 kati ya 305 vimepatiwa umeme
pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 12,084 kati ya 53,000. Gharama
ya utekelezaji kwa awamu hii ni Shilingi
bilioni 62. Aidha, Mradi wa Densification
– Round II utahusisha vitongoji vilivyomo katika vijiji 4,090 vilivyosalia na unakadiriwa
kugharimu jumla ya Shilingi bilioni
1,938. Awamu hii itaanza kutekelezwa mwezi Julai, 2018.
(ii) Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (Grid Extension) – Mzunguko wa Kwanza
82.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unatekelezwa katika vijiji 3,559 vya Mikoa yote ya Tanzania Bara na unahusisha ujenzi wa
takriban kilomita 15,600 za njia ya
msongo wa kV 33; kilomita 16,420 za njia za usambazaji wa msongo
wa kV 0.4; ufungaji wa transfoma
zenye ukubwa tofauti zipatazo 6,740
na uunganishaji wa wateja wa awali 300,000.
Aidha, maombi ya vijiji 1,541 vilivyorukwa
yamepokelewa na yanafanyiwa tathmini kwa ajili ya utekelezaji baada ya kupitia
taratibu husika. Ongezeko hilo litafanya
jumla ya vijiji vitakavyopelekewa umeme katika Mzunguko huu wa Kwanza kufikia 5,100 na kubaki na vijiji 2,773 vitakavyofikishiwa umeme katika
Mzunguko wa Pili. Mradi huu wa REA utaanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika
mwaka 2020/21.
83.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Mei, 2018 katika kipindi cha miezi mitatu (3) ya ujenzi
baada ya kukamilika kwa kipindi cha miezi mitatu (3) cha uhakiki wa vijiji na
miezi mitatu (3) mingine ya uingizaji wa vifaa na maandalizi ya ujenzi, jumla
ya vijiji 502 vinajengwa miundombinu ya umeme ikiwa ni pamoja na kusimikwa
nguzo na kufungwa transfoma katika Mikoa yote Tanzania Bara isipokuwa Mikoa ya
Kigoma na Katavi. Vijiji hivi vinatarajiwa kuwashwa umeme hivi karibuni na
vingine vinaendelea kuwashwa umeme. Mbali
na vijiji hivyo vilivyojengwa miundombinu, hadi kufikia mwezi Mei, 2018 vijiji
vingine 545 vimewashwa umeme sawa na wastani wa vijiji 182 kwa mwezi ambayo ni asilimia 92 ya lengo la kuwasha wastani
wa vijiji 197 kwa mwezi. Pia, katika vijiji vilivyowashwa umeme wateja 15,073 wameunganishwa
sawa na asilimia 90 ya lengo la kuunganisha
umeme wateja 16,666. Utekelezaji wa Mradi huu kwa upande wa Mkoa wa Kigoma
Mkandarasi CCC – ETERN-HEI Consortium amepatikana na ataanza kazi mwezi Juni,
2018. Aidha, kwa upande wa Mkoa wa Katavi Mkandarasi atapatikana mwezi Juni,
2018 na kuanza kazi mara moja.
(iii)
Mradi wa Kusambaza Umeme katika Vijiji vilivyopo pembezoni mwa Mkuza wa
Njia ya Msongo wa kV 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga
84.
Mheshimiwa Spika; Mradi huu unahusisha usambazaji wa umeme katika vijiji 121 vilivyo
pembezoni mwa mkuza wa Mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga
ambapo jumla ya wateja 25,000 wa
awali wanatarajiwa kuunganishiwa umeme. Mradi pia unahusisha upanuzi wa kituo
cha kupoza umeme cha Mtera. Hadi kufikia mwezi Mei, 2018, jumla ya vijiji 25
vimefikiwa na umeme na kufanya jumla ya wateja waliounganishiwa umeme kufikia
861. Kwa upande wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha Mtera usanifu unatarajiwa
kukamilika mwezi Mei, 2018. Shughuli za ujenzi wa kituo zitaanza mwezi Julai,
2018 na kukamilika mwezi Machi, 2019. Mradi huu unagharimu Shilingi bilioni 57 ambazo ni
msaada kutoka Serikali za Sweden na Norway.
(iv)
Miradi ya Uendelezaji wa Nishati Jadidifu (Off-Grid
Renewable Projects)
85.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahusisha uwekaji wa mifumo midogo (mini grids, micro grids and stand-alone systems) katika maeneo
ambayo yana vyanzo vya nishati mbadala kwa ajili ya kuzalisha umeme. Vilevile,
Mradi unahusisha ufungaji wa mifumo ya umeme-jua katika Taasisi za Serikali na
maeneo ya huduma za jamii zilizoko vijijini pamoja na kuwezesha ujenzi wa
mitambo ya kuzalisha umeme kwa bayogesi katika Taasisi za Umma kwa ajili ya
kupikia na kuwashia taa ili kupunguza matumizi ya kuni na mkaa ambavyo vina
athari kubwa kwa mazingira.
86.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Uendelezaji wa Nishati Jadidifu umegawanyika katika makundi mawili
ambapo Kundi la Kwanza
linahusisha usambazaji wa umeme vijijini kwa maeneo yaliyopo nje ya gridi kwa
mfumo wa Malipo kwa Matokeo (Results Based
Financing - RBF). Katika Kundi la Kwanza,
Mikataba ya miradi 22 yenye uwezo wa kuzalisha
jumla ya MW 24.4 zitakazosambazwa
katika vijiji 139 na kuunganisha wateja 33,939 imesainiwa kati ya REA na
Waendelezaji wa Miradi na kazi zinaendelea katika maeneo ya Mikoa ya Iringa,
Njombe, Tanga, Dodoma, Singida, Lindi, Mtwara, Tabora, Mwanza, Geita na Kagera.
87.
Mheshimiwa Spika, Kundi la Pili la Mradi huu linahusu kufunga mifumo ya umeme-jua (solar PV systems) katika Taasisi za Umma zikiwemo shule za sekondari,
vituo vya afya na zahanati zilizopo mbali na gridi pamoja na masoko ili
kuboresha huduma zinazotolewa katika taasisi hizo. Mradi huu unatekelezwa
katika Wilaya nane (8) za Biharamulo, Bukombe, Chato, Sikonge, Kasulu, Kibondo,
Tunduru na Namtumbo. Hadi kufikia mwezi Mei, 2018 utekelezaji wa Mradi umefikia
asilimia
92 na unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2019.
(v)
Mradi wa Usambazaji
Umeme katika Vijiji vilivyopo Pembezoni mwa Miji (Peri-Urban Rural Electrification Program)
88. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unalenga kusambaza umeme katika vijiji vilivyopo pembezoni mwa
miji ili kuboresha huduma za kijamii na kuhamasisha ujenzi wa viwanda vidogo,
vya kati na vikubwa katika maeneo hayo. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umekamilisha
usanifu wa mradi wa majaribio utakaotekelezwa katika Mkoa wa Pwani na Wilaya ya
Kigamboni Mkoani Dar es Salaam. Mradi huu utavinufaisha vijiji/vitongoji zaidi
ya 250 na kuwaunga wateja wa awali wapatao 37,000. Mradi huu unafadhiliwa na
Serikali ya Norway kwa gharama ya Shilingi
bilioni 83. Mradi unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2019.
89. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Aprili,
2018 REA ilikuwa imepokea jumla ya Shilingi
bilioni 313.5 kati ya Shilingi
bilioni 469 zilizopangwa kwa mwaka 2017/18 sawa na asilimia 67 ya bajeti. Aidha, katika mwaka 2018/19 fedha
zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya Usambazaji Umeme Vijijini ni
jumla ya Shilingi bilioni 412.08, kati
ya hizo, Shilingi bilioni 375.38 ni
fedha za ndani na Shilingi bilioni 36.70
ni fedha za nje.
D.
SEKTA NDOGO YA NISHATI JADIDIFU
90.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhamasisha uwekezaji katika vyanzo vya kuzalisha
umeme nchini kwa miradi midogo ya nishati jadidifu isiyozidi MW 10. Katika mwaka 2017/18 EWURA
imekamilisha uandaaji wa Kanuni za Uendelezaji wa Miradi Midogo chini ya MW 10 (The Electricity (Development of Small Power
Projects) Rules, 2018, GN No. 77 of 2018). Kanuni hizi zinarahisisha
uwekezaji katika miradi hiyo ambapo hupunguza muda na gharama za majadiliano
ikilinganishwa na miradi mikubwa. Vilevile, EWURA imekamilisha uandaaji wa
Kanuni za Kuhamasisha Matumizi Bora ya Umeme Unaozalishwa na Wateja kwa Kutumia
Umeme-jua na Upepo chini ya MW 1 (Electricity (Net Metering) Rules, 2018, GN
No. 76 of 2018). Kanuni hizi zinatoa mwongozo kwa wateja wa umeme
wanaowekeza katika mitambo ya uzalishaji umeme-jua na upepo katika majengo yao
kwa dhumuni la kupunguza matumizi ya umeme kutoka katika gridi.
(i) Nishati inayotokana na
Nguvu ya Jua (Solar Energy)
91.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka 2017/18 Serikali iliwasilisha miradi mbalimbali ya umeme-jua katika
Fungamano la Kimataifa la Nishati ya Jua (International
Solar Alliance). Kupitia Fungamano hilo Serikali ya India imetenga jumla ya
Dola za Marekani milioni 385 sawa na
takriban Shilingi bilioni 888.77 kwa
ajili ya kuendeleza miradi ya kuzalisha umeme wa jua katika Mikoa ya Shinyanga,
Singida, Dodoma, na Kilimanjaro. Katika mwaka 2018/19, Serikali itakamilisha
taratibu za kuridhia makubaliano ya International
Solar Alliance na kuanza maandalizi ya utekelezaji wa Mradi ikiwa ni pamoja
na kufanya Upembuzi Yakinifu.
92.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inashirikiana na Serikali ya Morocco kupitia
taasisi yake ya nishati endelevu (Moroccan
Agency for Sustainable Energy –MASEN) kuendeleza miradi ya kuzalisha umeme-jua
nchini yenye jumla ya MW 300. Katika
mwaka 2017/18 Wizara ya Nishati, TANESCO na MASEN walifanya tathmini ya awali katika
maeneo ya Zuzu (Dodoma), Manyoni (Singida) na Same (Kilimanjaro) ili kufahamu
ukubwa wa maeneo na kiasi cha umeme unaoweza kuzalishwa. Katika mwaka 2018/19 kazi
zitakazofanyika ni kukamilisha Upembuzi Yakinifu, tathmini ya mazingira na
kukamilisha taratibu za upatikanaji wa fedha za kutekeleza Mradi.
93.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka 2017/18 Serikali iliendelea kushirikiana na Sekta Binafsi katika kukuza
uzalishaji na matumizi ya teknolojia ya nishati ya jua ambapo hadi sasa kupitia
mfumo wa umeme-jua katika kaya na taasisi za huduma za jamii (shule, vituo vya afya
n.k) yaani Solar Home System, umeme wa MW 16 unazalishwa. Aidha, usambazaji wa umeme kwa kutumia gridi
ndogo za umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa na Gridi ya Taifa na maeneo ya
visiwani uliongezeka kutoka MW 1 mwaka
2016/17 na kufikia hadi MW 2 kwa mwaka 2017/18.
94.
Mheshimiwa
Spika, kufuatia
mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa Mradi wa
awali wa majaribio wa Solar PV Generators
kutokana na fedha za mkopo nafuu kutoka Benki ya Serikali ya Austria, Serikali
itaendelea na Utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi katika maeneo mbalimbali
nchini. Kupitia Mradi huu jumla ya wateja 2,015 watanufaika. Kazi
zitakazotekelezwa katika Mwaka 2018/19 ni kuainisha vijiji na maeneo mengine
ambayo hayapo katika Gridi ya Taifa ikiwemo visiwa pamoja na kuanza ujenzi.
Jumla ya Shilingi bilioni 2 fedha za
nje zimetengwa Mwaka 2018/19 kwa ajili ya utekelezaji wa kazi hizo.
(ii)
Miradi ya Tungamotaka na
Bayogesi
95.
Mheshimiwa Spika, Serikali iliendelea na uhamasishaji wa Sekta
Binafsi ili kuongeza uzalishaji wa umeme unaotokana na Tungamotaka. Katika
kipindi cha mwaka 2017/18, Uzalishaji wa umeme kutokana na chanzo hicho
umefikia MW 42 kutoka MW 38 za mwaka 2016/17. Aidha, uhamasishaji
wa matumizi ya bayogesi katika mikoa yote ya Tanzania Bara ulifanyika ambapo
mitambo 2,000 ilijengwa. Kwa mwaka
2018/19 miradi hii itatekelezwa kupitia Programu ya Uendelezaji wa Nishati
Endelevu kwa wote.
(iii)
Maporomoko Madogo ya
Maji
96.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 kiwango
cha uzalishaji wa umeme kupitia maporomoko madogo ya maji kilifikia MW 42 kutoka MW 36.99 zilizokuwa zinazalishwa hadi mwaka 2016/17 sawa na
ongezeko la asilimia 13.5. Ongezeko hili lilitokana na miradi ya Kiliflora (Arusha), Darakuta
(Manyara) na Matembwe (Njombe). Aidha, matumizi ya nishati inayotokana na
maporomoko madogo ya maji kwa ajili ya kukuza shughuli nyingine za kiuchumi ikiwemo
umwagiliaji yaliongezeka kufutia uhamasishaji wa matumizi ya nishati hiyo.
(iv) Uendelezaji wa Jotoardhi (Geothermal)
97.
Mheshimiwa Spika, rasilimali ya jotoardhi hapa nchini inakadiriwa
kuwa na uwezo wa kuzalisha hadi MW 5,000 za umeme. Serikali kupitia Kampuni ya
Uendelezaji wa Rasilimali ya Jotoardhi Nchini (TGDC), imekamilisha tafiti nne
(4) za kina (detailed surface studies) za
uendelezaji wa rasilimali hiyo katika maeneo ya Ngozi na Kiejo-Mbaka Mkoani
Mbeya, Songwe Mkoani Songwe na Luhoi Mkoani Pwani. Ili kuharakisha uendelezaji
wa rasilimali ya jotoardhi, Serikali inatarajia kununua mitambo kwa ajili ya
uchorongaji wa visima vya utafiti na uvunaji wa jotoardhi. Jumla ya gharama za
ununuzi wa mitambo hiyo ni Shilingi
bilioni 80.50, kati ya fedha hizo
Shilingi bilioni 66.70 ni gharama za ununuzi wa mtambo mkubwa na Shilingi bilioni 13.80 ni gharama za
ununuzi wa mtambo mdogo.
98.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19
Serikali itaendelea na utekelezaji wa Mradi wa jotoardhi katika eneo la Ngozi.
Kazi zitakazofanyika ni pamoja na: kuajiri Mshauri Mwelekezi wa kuandaa Mpango
Kazi na kusimamia uchorongaji wa visima vya utafiti; kufanya tathimini ya ardhi
hitajika na kulipa fidia; kuajiri Mkandarasi wa uchorongaji; na ujenzi wa
miundombinu ya barabara na maji. Aidha, Serikali
itakamilisha Upembuzi Yakinifu katika eneo la Songwe kwa ajili ya uzalishaji wa
umeme na matumizi mbadala. Jumla ya Shilingi bilioni 40.20 zimetengwa katika mwaka 2018/19 ili
kutekeleza kazi zilizopangwa. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 32.50 ni fedha za
ndani na Shilingi bilioni 7. 70 ni
fedha za nje.
(v)
Matumizi
Bora ya Nishati (Energy Efficiency)
99.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2017/18 Serikali kupitia ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) iliandaa
Mkakati wa Kitaifa wa Matumizi Bora ya Nishati (Energy Efficiency Strategy) pamoja na kukamilisha maandalizi ya
Mpango Kazi wa Matumizi Bora ya Nishati (Energy
Efficiency Action Plan). Umoja wa Ulaya umetenga Euro milioni 8 sawa na takriban
Shilingi bilioni 20.14 kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango Kazi huo. Katika mwaka
2018/19 itachaguliwa Taasisi ya Umma ya Mafunzo ambayo itajengewa uwezo (Centre of Excellence) kwa ajili ya
kutoa mafunzo ya uangalizi wa matumizi ya nishati (energy management) na ukaguzi wa upotevu wa nishati (energy audit). Aidha, wananchi wataelimishwa ili waweze
kufahamu umuhimu na njia za kuepuka upotevu wa nishati kwa lengo la kuokoa
fedha na kuipunguzia Serikali gharama za uwekezaji katika miundombinu ya umeme.
Fedha za nje Shilingi bilioni 1.35
zimetengwa katika mwaka 2018/19 kwa ajili ya utekelezaji wa kazi hizo.
(vi) Programu ya Nishati Endelevu kwa Wote (Sustainable Energy for All - SE4ALL)
100.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18
Serikali iliingia makubaliano na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP)
kwa ajili ya ufadhili wa utekelezaji wa Programu ya miaka mitano (5) ya Nishati
Endelevu kwa Wote (SE4All) ambapo UNDP itachangia Dola za Marekani 350,000 sawa na takriban Shilingi milioni 807.97 na kusaidia upatikanaji wa fedha kutoka
vyanzo vingine. Katika kuendeleza vyanzo vya nishati jadidifu, Programu ya SE4All ilisaidia upatikanaji wa taarifa
za vyanzo vya nishati ya jua na uandaaji wa miradi katika maeneo ya Zuzu (Dodoma);
Manyoni (Singida); na Same (Kilimanjaro) ambapo maeneo haya kwa ujumla yana
uwezo wa kuzalisha MW 300. Taarifa
hizo zitasaidia Serikali kutafuta wawekezaji katika miradi hiyo.
101.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2018/19, kazi zitakazotekelezwa kupitia Programu hiyo ni pamoja na: kuendelea
na uboreshaji wa miongozo mbambali itakayosaidia upatikanaji wa nishati endelevu nchini; kuandaa Mkakati wa
Tungamotaka na utekelezaji wake; kujenga
uwezo kwa watendaji katika kusimamia utekelezaji wa mipango na miradi ya
nishati hapa nchini; kuandaa mazingira bora yatakayosaidia kukuza uwekezaji
katika miradi ya Nishati Jadidifu na Matumizi Bora ya Nishati; na kuandaa mfumo
wa ukusanyaji na utunzaji wa takwimu za Nishati Jadidifu. Jumla ya Shilingi bilioni 3 zimetengwa kwa ajili
ya utekelezaji wa Mradi huu katika Mwaka 2018/19, ambapo Shilingi bilioni 2.5 ni fedha za nje na Shilingi milioni 500 ni fedha za ndani.
E. SEKTA NDOGO YA MAFUTA NA
GESI ASILIA
Shughuli
za Utafutaji, Uzalishaji na Usambazaji wa Mafuta na Gesi Asilia Nchini
102.
Mheshimiwa Spika, Kazi za utafutaji wa mafuta na gesi asilia zinaendelea ambapo jumla ya
kampuni nane (8) zinafanya utafutaji wa mafuta na gesi asilia kupitia mikataba
kumi na moja (11) ya Uzalishaji na Ugawanaji Mapato (Production Sharing Agreement -PSA). Katika mwaka 2017/18 Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa kushirikiana na Kampuni
ya Statoil zimechoronga kisima kimoja (Pilipili-1) katika kitalu Na. 2
kilichopo Bahari ya Hindi na hivyo kufanya jumla ya visima vilivyochorongwa kufikia 96. Vilevile, TPDC ikishirikiana na
Kampuni ya Ndovu Resources ilifanya uhakiki wa mashapo ya gesi asilia katika
kitalu cha Ruvuma, uhakiki huo umeongeza kiasi cha gesi asilia kufikia futi za
ujazo bilioni 466 kutoka futi za ujazo bilioni 178 mwaka 2016/17. Hadi kufikia
sasa kiasi cha gesi asilia kilichogunduliwa nchini ni Futi za Ujazo Trilioni 57.54.
103.
Mheshimiwa Spika, Kampuni za Heritage Rukwa (TZ) Ltd na Swala Oil and Gas Tanzania
zimeendelea na maandalizi ya kuchoronga visima vya utafutaji mafuta katika
vitalu vya Rukwa Kusini na Kilosa-Kilombero sawia. Aidha, Kampuni ya Ndovu
Resources imeendelea na maandalizi ya Mpango wa Uendelezaji (Development Plan) wa gesi asilia
iliyogunduliwa katika eneo la Ntorya - Mtwara. Vilevile, Kampuni ya Dodsal
Hydrocarbons imeendelea na uchukuaji wa data za mitetemo (seismic) katika Kitalu cha Ruvu ili kuhakiki ukubwa wa mashapo ya
gesi asilia iliyogunduliwa katika kitalu hicho. Kwa upande mwingine, Kampuni za
PanAfrican Energy na Maurel et Prom zimeendelea na uzalishaji wa gesi asilia
katika Vitalu vya Songo Songo na Mnazi Bay kwa wastani wa futi za ujazo milioni
95 na milioni 80 kwa siku sawia. Gesi inayozalishwa inatumika kuzalisha umeme katika mitambo ya TANESCO.
MIRADI YA UTAFITI KATIKA
VITALU VYA KIMKAKATI VYA SHIRIKA LA MAENDELEO YA PETROLI NCHINI (TPDC)
(i)
Vitalu Namba 4/1B na
4/1C
104.
Mheshimiwa Spika, TPDC imeendelea na
utafiti katika vitalu vyake namba 4/1B na 4/1C sambamba na taratibu za kuwapata
Wabia wa Kimkakati (Strategic Partners)
ili kushirikiana nao katika kuendeleza vitalu hivyo. Katika mwaka 2017/18 kazi
zilizotekelezwa ni pamoja na kufanya tathmini ya kifedha na kiuchumi na
kukamilisha tathmini ya awali kwa kutumia data
za mitetemo za 2D ambazo zinaonesha uwepo wa mashapo mazuri ya gesi asilia
katika vitalu hivyo. Kazi zitakazotekelezwa kwa mwaka 2018/19 ni
ukusanyaji, uchakataji na tathmini ya data
za mitetemo ya 3D zenye ukubwa wa kilomita za mraba 2,500. Fedha za ndani Shilingi bilioni 2 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji
wa Mradi.
(ii) Kitalu cha Eyasi – Wembere
105.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TPDC imekusanya data
za kijiolojia na kijiofizikia kupitia data
za mgandamizo (Airbone Gravity
Gradiometry-AGG) na sumaku (Magnetic)
katika Bonde la Eyasi-Wembere. Lengo la utafiti huu ni kubaini uwepo wa mashapo
yenye kuhifadhi mafuta au gesi asilia katika eneo hilo. Katika mwaka 2017/18 wataalam
wa Wizara ya Nishati na TPDC wameendelea kufanya mashauriano na wataalam kutoka
sekta ya mafuta nchini Uganda. Aidha, mwezi
Oktoba, 2017 wataalamu hao walitembelea eneo la utafiti pamoja na kuandaa
mpango kazi wa kufanya tafiti za kina za kijiolojia na kijiofizikia. Kwa mwaka 2018/19, TPDC imepanga: kutafuta Mbia na kuomba leseni ya utafiti;
kufanya Tathmini ya Athari za Mazingira (EIA) kwa ajili ya ukusanyaji wa data za mitetemo za 2D; pamoja na
kukusanya, kuchakata na kutafsiri data
za mitetemo zenye urefu wa kilomita 150
katika eneo la Manonga. Fedha za ndani Shilingi
bilioni 2 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji kwa shughuli za Mradi.
(iii) Kitalu cha Mnazi Bay
Kaskazini
106.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18,
shughuli zilizotekelezwa katika kitalu hiki ni: kufanya tathmini ya kifedha na
kiuchumi; kuomba leseni ya kitalu; kumpata Mshauri Mwelekezi wa kuchakata na kutafsri data za mitetemo za 3D; maandalizi ya kuchukua zaidi data za mitetemo za 3D; kuandaa Mkataba Kifani
wa Ushirikiano (Model Joint Operating Agreement)
utakaozingatia maboresho ya mikataba inayopitiwa na Serikali ili kuiboresha;
na kuanza mchakato wa kumpata Mbia wa Kimkakati wa Mradi. Kwa mwaka 2018/19,
shughuli zilizopangwa kufanyika ni pamoja na: kufanya maandalizi ya uchorongaji
kwa kushirikiana na Mshauri Mwelekezi; kuanza ununuzi wa vifaa vya awali
vitakavyotumika katika kuchoronga kisima; kutafuta mkandarasi wa kukusanya data zaidi za mitetemo za 3D; na kuandaa
na kutafsiri data zenye ukubwa wa
kilomita za mraba 141.63. Fedha za ndani za Shirika Shilingi bilioni
13.28 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hizo.
(iv)
Kitalu cha Songo Songo Magharibi
107.
Mheshimiwa Spika, Kitalu cha Songo Songo Magharibi kimeonesha kuwa na mategemeo chanya ya
uwepo wa gesi asilia. Katika kipindi cha mwaka 2017/18, TPDC imekamilisha
kutafsiri data za mitetemo za 2D na kubaini maeneo yatakayochorongwa visima.
Vilevile, TPDC imeanza taratibu za kumtafuta Mbia wa Kimkakati ambapo Mkataba
Kifani wa Ushirikiano (Model Joint Operating
Agreement) umeandaliwa utakaozingatia
maboresho ya mikataba inayoendelea kufanyiwa mapitio na Serikali kwa lengo la
kuiboresha. Kwa mwaka 2018/19 shughuli zilizopangwa kufanyika ni pamoja na
kumpata Mbia wa Kimkakati wa kukusanya, kuchakata na kutafsiri data
zaidi za mitetemo za 3D katika eneo la kilomita za mraba 306. Fedha za ndani za Shirika Shilingi bilioni 11.3 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hizo.
MIRADI YA USAMBAZAJI WA
GESI ASILIA NCHINI
108.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TPDC inatekeleza miradi ya
usambazaji wa gesi asilia kwa kuunganisha miundombinu ya usambazaji wa gesi
hiyo katika matoleo ya bomba linalotoka Madimba Mkoani Mtwara na Songo Songo
Mkoani Lindi hadi Dar es Salaam. Uunganishaji wa wateja umeongeza matumizi ya
gesi asilia hadi kufikia wastani wa futi za ujazo milioni 175 kwa siku (mwaka
2017/18) kutoka futi za ujazo milioni 145 kwa siku (mwaka 2016/17) sawa na
ongezeko la asilimia 17.
(i) Miradi ya Kusambaza Gesi Asilia Viwandani
109.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18, TPDC
imeendelea kutafuta wateja zaidi wa gesi asilia kwa matumizi ya viwanda pamoja
na ujenzi wa miundombinu ya kusambazia gesi hiyo kwa wateja. Shirika limepitia
na kuhakiki michoro (Design Drawings)
ya awali iliyowasilishwa na Mkandarasi kwa ajili ya kuunganisha gesi asilia
katika viwanda vya Lodhia Steel, Knauf Gypsum na Bakhressa Food Products
vilivyopo Mkuranga. Mkandarasi wa ujenzi
wa bomba la kusambaza gesi asilia katika viwanda vya Coca-Cola Kwanza Limited
na BIDCO Industry vilivyoko eneo la viwanda Mikocheni ameanza kazi mwezi
Aprili, 2018. Kiwanda cha Goodwill Ceramic Tanzania Limited kilichopo Mkuranga
kimeendelea kutumia gesi asilia kwa ajili ya shughuli za uzalishaji kiwandani
hapo. Aidha, awamu ya kwanza ya ujenzi wa miundombinu ya kupeleka gesi asilia
katika kiwanda cha Dangote Cement Tanzania Limited kilichopo Mtwara ulikamilika
mwezi Septemba, 2017. Hivi
sasa Kampuni ya Dangote inaendelea na maandalizi ya awali ya utumiaji wa gesi asilia
(Testing and Commissioning).
110.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/19, TPDC itakamilisha
majadiliano na kuingia mikataba ya kusambaza gesi asilia katika kiwanda cha
Knauf Gypsum kilichopo Mkuranga Mkoani Pwani. Vilevile, TPDC itafanya
majadiliano na wateja wapya wa viwanda walioonesha nia ya kuunganishiwa gesi
asilia wakiwemo LN Future Building Materials Co. Ltd na Kings Alluminium
vilivyopo Mkuranga-Pwani pamoja na MM-1 Intergrated Steel Mills Ltd kilichopo
Mikocheni.
(ii) Miradi ya Kusambaza Gesi
Asilia Majumbani
111.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa jumla ya nyumba 70 zilizopo maeneo ya Mikocheni, Dar es Salaam
zimeunganishwa na miundombinu ya gesi asilia. Katika mwaka 2017/18, miundombinu
ya kuunganisha gesi asilia majumbani imeanza kutandazwa katika Jiji la Dar es
Salaam. Maeneo yanayoanza kupelekewa gesi kupitia Mradi huu ulioanza mwezi
Aprili, 2018 ni pamoja na Ubungo, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Makongo Juu,
Survey, Sinza, Shekilango, Mwenge, Viwanda vya Coca Cola na maeneo ya
Mikocheni. Mradi huu ni endelevu kutegemeana na mahitaji yatakavyokuwa
yanajitokeza katika maeneo husika. Zaidi ya wateja 1,000 wanatarajiwa kufikiwa
na miundombinu ya kuunganishia gesi katika awamu ya kwanza.
112.
Mheshimiwa Spika, Mradi mwingine unaofanyiwa maandalizi utakaotekelezwa pamoja na Mradi huu
ni usambazaji wa gesi asilia katika maeneo ya Magereza, Magomeni, Hospitali Kuu
ya Mkoa na Chuo cha Ualimu katika Manispaa ya Mtwara. Kazi inayofanyika sasa
hivi ni ukamilishaji wa taratibu za kuunganisha bomba lenye msukumo mdogo (low pressure) kwa ajili ya kupeleka
gesi asilia katika nyumba. Kazi hizi zitakamilika mwezi Juni, 2018 na kazi ya
usambazaji wa gesi asilia itaanza mwanzoni mwa mwezi Julai, 2018 ambapo wateja
wa awali wanatarajiwa kuwa zaidi ya 580. Kazi hii itakuwa endelevu ambapo maeneo
mengine yataendelea kusambaziwa gesi asilia baadae ikiwemo vijiji vinavyopitiwa
na bomba la gesi asilia kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam.
113.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19, TPDC inatarajia kuweka miundombinu itakayowezesha zaidi
ya nyumba 2,000 kuunganishiwa gesi asilia pamoja na kusambaza gesi asilia
katika Mgahawa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Soko la Feri la Jijini Dar es
Salaam na Kampuni ya Usimamizi wa Mabasi ya Mwendokasi Jijini Dar es Salaam
(UDART). Ili kuwezesha uunganishwaji wa wateja hao, uchambuzi wa kifedha pamoja
na Tathmini ya Athari za Mazingira na Jamii (Environmental
and Social Impact Assessment-ESIA) utaendelea kufanyika. Fedha za ndani za
TPDC Shilingi bilioni 20.9
zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi huu.
Ujenzi wa
Miundombinu ya Usambazaji Gesi Asilia katika Mikoa ya Dar es Salaam, Lindi,
Mtwara, Pwani, Morogoro, Tanga na
Dodoma
114.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu unajumuisha usambazaji wa gesi asilia kwa njia ya bomba (Piped Natural Gas-PNG), ujenzi wa vituo
vya gesi asilia iliyoshindiliwa (Compressed
Natural Gas (CNG) stations) na miradi midogo ya gesi kimiminika (Mini-LNG). Katika mwaka 2017/18, TPDC
imeandaa Mkataba wa Ushirikiano wa Ubia (Joint
Venture Agreement) pamoja na Hati ya Zabuni (Tender Document) ili kuwapata wawekezaji kwa njia ya ushindani.
Aidha, Mpango wa utekelezaji wa Mradi huu upo katika hatua za mwisho za mapitio
kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) pamoja na
kitengo cha PPP cha Wizara ya Fedha na Mipango. Awamu ya kwanza ya utekelezaji,
inahusisha utafutaji wa Mbia atakayeshirikiana na TPDC kutekeleza Mradi kwa
Mkoa wa Dar es Salaam. Mikoa mingine ya Lindi, Mtwara, Morogoro, Tanga na
Dodoma iliyoainishwa katika Mpango itafuata baada ya kukamilika kwa Upembuzi
Yakinifu. Katika mwaka 2018/19, fedha za ndani Shilingi bilioni 2 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi.
Mradi unatarajiwa kuanza mwezi Novemba, 2018 baada ya taratibu zote kukamilika na
utatekelezwa kwa muda wa miaka mitano (5).
Mradi wa Ujenzi wa Kiwanda
cha Mbolea Mkoani Lindi
115.
Mheshimiwa Spika,
Serikali kupitia TPDC imeendelea na majadiliano kuhusu Mradi wa kujenga kiwanda
kikubwa cha Mbolea katika eneo la Kilwa Masoko, Mkoani Lindi ambacho
kitazalisha mbolea ya Amonia tani 2,200 na Urea tani 3,850 kwa siku. Mradi
utatekelezwa na Kampuni ya Ubia ya Mradi Tanzania
Mbolea and Petrochemicals Company Limited (TAMPCO) (inayohusisha kampuni za
Ferostaal ya Ujerumani, Fauji ya Pakistani, Haldo Topsoe ya Denmark na TPDC),
ambayo imeundwa na kupata hati ya uwekezaji (Certificate
of Incentive). Mradi huu pamoja na mambo mengine utasaidia upatikanaji wa
mbolea kwa urahisi ili kukuza Sekta ya Kilimo na uchumi wa nchi kwa ujumla.
Mradi unakadiriwa kugharimu Dola za
Marekani bilioni 1.92 sawa na takriban Shilingi
trilioni 4.43 katika utekelezaji wake.
116.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19 Serikali itaendelea na majadiliano ya bei ya gesi asilia
kwa ajili ya matumizi ya uzalishaji wa mbolea nchini. Serikali kupitia TPDC
itasimamia tathmini ya utwaaji ardhi na usanifu wa kihandisi wa upelekaji wa
gesi asilia kwa njia ya bomba kuanzia Nangurukuru hadi Kiwandani. Kazi hizi zitatekelezwa kwa kutumia fedha za ndani
za Shirika ambapo kiasi cha Shilingi
milioni 266.4 kitatumika.
Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia (LNG Project)
117.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa LNG unalenga kusindika gesi asilia
iliyogunduliwa katika kina kirefu cha Bahari ili iweze kutumika ndani na kusafirishwa
na kuuzwa nje ya nchi. Jumla ya gharama za Mradi zinakadiriwa kuwa Dola za Marekani bilioni 30 sawa na
takriban Shilingi trilioni 69.25.
Katika mwaka 2017/18 kazi zilizofanyika ni pamoja na marudio na ukamilishaji wa
uthamini ya eneo la mradi, kukamilisha tafiti za kihandisi na uchaguzi wa
teknolojia (concept selection) ya
uzalishaji na usafirishaji wa gesi asilia kutoka baharini hadi nchi kavu na
kuendelea kwa majadiliano ya kimkataba (Host
Government Agreement - HGA) kati ya Serikali na wawekezaji. Katika mwaka
2018/19, kazi zinazotekelezwa ni pamoja na: kufanya Usanifu wa Awali wa
Kihandisi (Pre-FEED) kwa ajili ya
ujenzi wa kiwanda cha LNG; kuendelea na majadiliano ya HGA na ulipaji wa fidia
kwa wananchi watakaopisha Mradi.
118.
Mheshimiwa Spika, faida zinazotarajiwa
kutokana na Mradi huo ni pamoja na kuongezeka kwa mapato ya Serikali kupitia
mauzo ya gesi asilia katika soko la kimataifa, upatikanaji wa nishati ya
uhakika kwa ajili ya matumizi ya ndani, upatikanaji wa ajira kwa wazawa, ukuaji
wa Miji ya Lindi na Mtwara ikiwa ni pamoja na upanuzi wa bandari na uwanja wa
ndege, upatikanaji wa malighafi za viwanda kama vile mbolea, plastiki na kemikali
(Petrochemicals). Fedha za ndani Shilingi
bilioni 6.5 zimetengwa kwa mwaka 2018/19 kwa ajili ya kazi hizo na ujenzi
wa Mradi unatarajiwa kuanza mara baada ya kukamilika kwa majadiliano ya HGA.
Mradi wa Kusafirisha Gesi
Asilia kutoka Tanzania kwenda Uganda
119.
Mheshimiwa Spika, Mradi unahusu ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Dar es
Salaam (Tanzania) kwenda nchini Uganda kupitia Mikoa ya Pwani, Tanga, Manyara,
Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga, Geita na Kagera. Utekelezaji wa Mradi huu
utasaidia upatikanaji wa gesi asilia katika mikoa itakayopitiwa na bomba hilo
na mikoa mingine ya jirani. Katika mwaka 2018/19 fedha za ndani Shilingi bilioni 1.5 zimetengwa kwa
ajili ya Upembuzi Yakinifu utakaobainisha gharama za Mradi na namna bora ya
utekelezaji wake. Kulingana Mpango Kabambe wa Matumizi ya Gesi Asilia (NGUMP) kiasi
cha futi za ujazo trilioni 3.2 kinakadiriwa kusafirishwa kwa njia ya bomba
kwenda nchi za jirani ikiwemo Uganda. Serikali
za Tanzania na Uganda zinaendelea na majadiliano ili utekelezaji wa mradi huu
uende sambamba na ule wa EACOP.
MIRADI YA USAFIRISHAJI WA
MAFUTA
Mradi wa Bomba la
Kusafirisha Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) kutoka Kabaale (Uganda)
hadi Bandari ya Tanga (Tanzania)
120.
Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa Mradi huu utatekelezwa na Kampuni Maalum ya Mradi (Special Purpose Vehicle) itakayoundwa
na wabia wa Mradi ambao ni Kampuni za Total (Ufaransa), Tullow (Uingereza),
CNOOC (China) pamoja na Serikali za Tanzania na Uganda. Gharama za Mradi
zinakadiriwa kufikia Dola za Marekani
bilioni 3.5 sawa na takriban
Shilingi trilioni 8.07.
121.
Mheshimiwa Spika, Hatua za awali za utekelezaji wa Mradi huu zilianza mwezi Januari, 2018.
Kazi zilizotekelezwa ni pamoja na: Usanifu wa Kihandisi wa Mradi (Front End Engineering Design);
kuridhiwa kwa Mkataba wa Intergovernmental
Agreement (IGA) na Mabunge ya nchi za Tanzania na Uganda; kulipa fidia ya
utwaaji ardhi kwa eneo la Chongoleani, tathmini ya fidia kwa maeneo ya kambi za
wafanyakazi na hifadhi ya mabomba; utafiti wa Geological, Geotechnical
na Geophysical katika eneo la
Chongoleani; na utafiti wa Geological
na Geophysical kwenye njia ya bomba.
Katika kipindi hiki majadiliano ya HGA pamoja na maandalizi ya majadiliano ya
mkataba wa Ubia (Shareholding Agreement -
SHA) yameendelea kufanyika. Kazi zilizopangwa kutekelezwa kwa mwaka 2018/19
ni pamoja na: kukamilisha majadiliano ya HGA na SHA; kukamilisha Usanifu wa
Kina wa Kihandisi (Detailed Engineering
Design); na kuwalipa fidia wananchi watakaopisha utekelezaji wa Mradi.
Kiasi cha Shilingi bilioni 54.2 fedha
za ndani zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji. Ujenzi wa Mradi unatarajiwa
kuanza mwezi Juni, 2018 na kukamilika
mwaka 2020.
Mradi wa Ujenzi wa Bomba la
Kusafirisha Mafuta Safi (White Petroleum
Products) kutoka Dar es Salaam (Tanzania) hadi Ndola (Zambia)
122.
Mheshimiwa Spika, Mradi huu upo katika hatua za awali na unahusu ujenzi wa bomba lenye urefu
wa kilomita 1,710 litakalojengwa sambasamba na bomba la TAZAMA linalosafirisha
Mafuta Ghafi (Crude Oil) baada ya
kuridhiwa na Serikali za nchi za Tanzania na Zambia. Ili kuleta manufaa katika
maeneo yatakayopitiwa na bomba hili, Mradi utahusisha ujenzi wa matoleo ya
mafuta (take–off points) katika
maeneo ya Morogoro, Iringa, Njombe, Mbeya na Songwe. Katika mwaka 2017/18,
Andiko la Awali la Mradi (Project Concept
Paper) kuhusu namna Mradi utakavyotekelezwa na faida zake liliandaliwa.
Aidha, eneo kwa ajili ya ujenzi wa matenki ya hifadhi ya mafuta Morogoro
limepatikana na hatua za utwaaji ardhi zinaendelea. Katika mwaka 2018/19,
shughuli iliyopangwa kutekelezwa ni kufanya Upembuzi Yakinifu (Feasibility Study) utakaoonesha gharama
halisi za Mradi na namna bora ya kutekeleza Mradi. Jumla ya Shilingi bilioni 1.5 fedha za ndani
zimetengwa kwa ajili ya kugharamia shughuli hizo.
Mradi
wa Hifadhi ya Kimkakati ya Mafuta ya Akiba ya Dharura Nchini
123.
Mheshimiwa
Spika, uanzishaji na usimamizi wa Hifadhi ya Kimkakati ya
Mafuta ya Akiba ya Dharura (Strategic
Petroleum Reserve - SPR) ni muhimu kwa nchi ili kujilinda na mabadiliko hasi ya upatikanaji wa mafuta Duniani
yanayoweza kutokea. Katika utekelezaji wa Mradi huu, miongozo mbalimbali
ikiwemo kanuni (SPR regulations),
mwongozo wa usimamizi (SPR manual) na
mfumo wa bei (price template)
imekamilika. Katika mwaka 2017/18, kazi zilizotekelezwa ni pamoja na kumpata
Mshauri Mwelekezi na Mkandarasi wa kuondoa mabaki ya mafuta (sludge) katika Tenki Na.8 la TPDC
lililopo TIPER litakalotumika kutunzia mafuta ya dharura. TPDC
imeendelea na taratibu za kupata ardhi kwa ajili ya ujenzi wa matenki mengine ya kuhifadhia mafuta katika Manispaa za Kigamboni na Tanga. Kazi
zilizopangwa kutekelezwa kwa mwaka 2018/19 ni kukarabati Tenki Na. 8 ili kufanikisha uanzishwaji wa hifadhi hiyo nchini. Shilingi bilioni 14.5 fedha za ndani
zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa shuguli
za Mradi.
Mradi
wa Usimamizi wa Rasilimali za Mafuta na Gesi Asilia Nchini
124.
Mheshimiwa Spika, Mradi
huu unalenga kuchochea maendeleo ya tasnia ya uziduaji (extractive industry) katika sekta ya mafuta na gesi asilia nchini
na kuimarisha uendelezaji wa rasilimali hizo zinazotoa mchango mkubwa katika
ukuaji wa uchumi. Mradi huu utaiwezesha Serikali kuimarisha uwezo wa kukusanya
na kusimamia mapato yanayotokana na rasilimali za mafuta na gesi asilia hususan
katika maeneo ya utafutaji, uzalishaji na uendelezaji wa rasilimali hizo. Mradi
unatarajiwa kugharimu Dola za Marekani
milioni 29.53 sawa na takriban Shilingi
bilioni 68.17. Katika Mradi huu Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) itachangia
Dola za Marekani milioni 26.58 sawa na takriban Shilingi bilioni 61.35 zikiwa ni mkopo
wa masharti nafuu na Serikali itachangia Dola
za Marekani milioni 2.95 sawa na takriban Shilingi bilioni 6.8.
125.
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2018/19, Taasisi za Serikali zinazohusika
na Mradi huu zitajengewa uwezo katika maeneo ya usimamizi wa rasilimali za
mafuta na gesi asilia. Jumla ya Shilingi bilioni 14 zimetengwa ambapo Shilingi bilioni
2 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 12 ni
fedha za nje. Mradi unatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu (3) kuanzia mwezi
Juni, 2018.
Udhibiti wa Shughuli za Mkondo wa Juu wa Mafuta na
Gesi Asilia Nchini
126.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2017/18, Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (Petroleum Upstream Regulatory Authority
-PURA) imeendelea kusimamia shughuli
za utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa gesi asilia katika kampuni nane (8)
kupitia PSA 11 zinazofanya shughuli hizo nchini. Katika kutekeleza jukumu hilo
kazi zilizotekelezwa ni: kusimamia na kudhibiti uchorongaji wa kisima cha Pilipili-1 katika kitalu Na. 2 unaotekelezwa na Kampuni ya
Statoil ikishirikiana na TPDC; kufanya uhakiki na kuidhinisha Mpango Mkakati na Bajeti kwa PSA 10; na kuanza ukaguzi wa hesabu za PSA ambapo ukaguzi wa PSA ya
kitalu Na.2 umekamilika.
127.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/19, Serikali kupitia PURA itasimamia shughuli za utafutaji
wa mafuta na gesi asilia zikiwemo uchorongaji wa kisima cha Hammerkop-1 katika
kitalu cha Rukwa kusini na kisima cha Kito-1 katika kitalu cha
Kilosa-Kilombero. Mamlaka itasimamia ukusanyaji, uchakataji na tathmini ya data za mitetemo za 2D yenye jumla ya
urefu wa kilomita za mstari 840 zitakazokusanywa katika vitalu vya Ruvuma na
Eyasi-Wembere. PURA itatathmini pia data
za mitetemo za 3D zenye jumla ya kilometa za mraba 1,357.63 katika vitalu vya
Kiliwani Kaskazini, Ruvuma, Songo Songo Magharibi, Mnazi Bay Kaskazini na 4/1B.
PURA itaendelea kusimamia uzalishaji wa gesi asilia katika Vitalu vya Songo
Songo na Mnazi Bay na kufanya
ukaguzi wa hesabu za PSA 10. Fedha za ndani Shilingi bilioni 1.69 zimetengwa kwa ajili ya kugharamia kazi hizo.
Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja
(Petroleum Bulk Procurement System) Nchini
128.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (Petroleum Bulk Procurement Agency- PBPA) imeendelea kusimamia
Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (Bulk
Procurement System – BPS). Kwa kipindi cha Mwezi Januari hadi Desemba, 2017 jumla ya lita bilioni 5.36
za mafuta ziliingizwa nchini. Lita bilioni 3.19 sawa na asilimia 60 za mafuta yaliyoingizwa zilikuwa kwa ajili ya matumizi
ya ndani na lita bilioni 2.17 sawa na asilimia
40 zilikuwa kwa ajili ya nchi jirani. Mafuta kwa ajili ya matumizi ya ndani
yalipungua kwa asilimia 3.3 kutoka
lita bilioni 3.302 mwaka 2016 hadi lita
bilioni 3.19 mwaka 2017. Kupungua huko kulitokana na mitambo ya kuzalisha umeme
pamoja na baadhi ya viwanda kutumia gesi asilia kuzalisha nishati badala ya
mafuta ya Dizeli na Mafuta mazito (HFO). Mafuta yaliyoagizwa kwa ajili ya nchi
jirani za Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Rwanda, Uganda na
Zambia yalipungua kwa asilimia 0.8 kutoka
lita bilioni 2.185 mwaka 2016 hadi lita bilioni 2.168 mwaka 2017. Upungufu huo
ulitokana na baadhi ya kampuni za mafuta kubadili matumizi ya mafuta
yaliyoagizwa kwa ajili ya nchi jirani na kutumika hapa nchini (localization of transit fuel) Kielelezo Na 10.
129.
Mheshimiwa Spika, katika kupunguza upotevu wa mafuta na gharama zinazotokana na muda unaotumika kwa meli kupakua mafuta bandarini
(Demurrage Charges), Serikali
inatarajia kuanza upokeaji mafuta sehemu moja (Single Receiving Terminal - SRT). Katika kipindi cha mpito utaratibu
wa SRT utaanza kwa kutumia miundombinu ya kuhifadhia mafuta ya TIPER ambayo
Serikali inamiliki hisa asilimia 50 hadi
hapo Serikali itakapojenga miundombinu yake. Utaratibu wa SRT utakuwa chini ya
usimamizi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA). Katika kufanikisha utaratibu huo,
kazi zinazotekelezwa kwa sasa ni pamoja na: uboreshaji wa Kanuni za Uagizaji wa
Mafuta kwa Pamoja za Mwaka 2017; uandaaji wa Kanuni za Usimamizi wa SRT;
uundaji wa Timu itakayofanya ufuatiliaji na tathmini ya utaratibu wa SRT; na
uandaaji wa mikataba itakayotumika katika kutekeleza utaratibu wa SRT.
Matumizi ya Bandari za Tanga na Mtwara katika
Upakuaji wa Mafuta
130.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mafanikio yaliyopatikana kwa kuanza kutumia Bandari ya Tanga
kupokea mafuta kwa ajili ya matumizi ya Mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na
Manyara, Serikali itaanza kutumia Bandari ya Mtwara kupokea mafuta kwa ajili ya
matumizi ya Mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Njombe, Mbeya, Songwe, Rukwa,
Katavi pamoja na nchi za jirani. Bandari ya Mtwara itaanza rasmi kupokea mafuta
kwa kutumika mfumo wa uagizaji kwa pamoja mwezi Juni, 2018. Utaratibu wa kupanga bei ya mafuta yatakayoingizwa kupitia Bandari hiyo
utazingatia taratibu zilizotumika katika Bandari ya Tanga. Miundombinu ya
kuhifadhia mafuta iliyopo katika Bandari hiyo ina uwezo wa kutunza lita milioni
26 zinazotosheleza mahitaji ya ukanda huo kwa sasa. Hata hivyo, kutokana na kuongezeka kwa shughuli
za kiuchumi katika maeneo hayo, Serikali inawakaribisha wawekezaji kuwekeza
zaidi katika ujenzi wa miundombinu ya kuhifadhia mafuta katika Bandari za Tanga
na Mtwara.
Matumizi ya Gesi inayotokana na Petroli (Liquified
Petroleum Gas – LPG)
131.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kukamilisha utaratibu wa uagizaji wa LPG kwa
mfumo wa pamoja
ambapo kwa mwaka 2017/18 Mshauri
Mwelekezi anakamilisha utafiti kuhusu viwango vya ubora wa LPG
unaohitajika kwa ajili ya matumizi nchini na ujenzi wa miundombinu ya kupokelea
na kuhifadhia gesi hiyo. Kwa mwaka 2018/19 EWURA itaandaa mwongozo wa uagizaji
wa LPG kwa mfumo wa pamoja baada ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia
na kuidhinisha viwango vitakavyopendekezwa na Mshauri Mwelekezi. Aidha,
Serikali imeendelea kutoa elimu kuhusu matumizi bora ya LPG katika maeneo
mbalimbali nchini ili kulinda afya, usalama na mazingira ya watumiaji.
Vilevile, Serikali kupitia EWURA imeendelea kusimamia biashara ya LPG ili
kubaini wafanyabiashara wasio waaminifu na kuwachukulia hatua stahiki. Kwa
mwaka 2017 kumekuwa na ongezeko la uagizaji wa LPG ikilinganishwa na mwaka 2016
ambapo kuanzia mwezi Januari hadi Desemba 2017, gesi iliyoagizwa nchini ilikuwa
tani 107,263 ikilinganishwa na tani 90,296 za mwaka 2016, sawa na ongezeko la asilimia 19.
F.
UIMARISHAJI WA MAWASILIANO KATI YA WIZARA NA JAMII
132.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18 Wizara ya Nishati
na Taasisi zake imeendelea kuelimisha umma kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu
Sekta ya Nishati ili kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu shughuli
zinazotekelezwa na Wizara. Njia mbalimbali zimetumika kutoa elimu hiyo zikiwemo
magari ya matangazo, redio, magazeti, televisheni, tovuti na mitandao ya
kijamii. Aidha, elimu imeendelea kutolewa kupitia Jarida la kila wiki la Wizara
(MEM News Bulletin) ambapo hadi
kufikia mwezi Aprili, 2018 jumla ya Matoleo 42 yamechapishwa na kusambazwa kwa
wadau mbalimbali zikiwemo Ofisi za Balozi za Tanzania. Taarifa zaidi kuhusu Wizara
zinapatikana kupitia Tovuti (www.nishati.go.tz), ukurasa wa Facebook (Wizara ya
Nishati), Twiter (Wizara ya Nishati);
na You Tube (Wizara ya Nishati
Tanzania).
133.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017/18 Wizara imeshiriki katika vipindi
mbalimbali vya Redio na Televisheni kwa lengo la kuwaelimisha wananchi kuhusu
mipango inayotekelezwa na Serikali mathalan kipindi maalum cha ‘TUNATEKELEZA’ kinachoratibiwa
na Idara ya Habari (MAELEZO) kwa kushirikiana na Shirika la Utangazaji Tanzania
(TBC).
G.
AJIRA NA MAENDELEO YA
RASILIMALIWATU
134. Mheshimiwa
Spika, katika kuongeza tija na motisha kwa watumishi
wa Wizara, kwa mwaka 2017/18 Wizara iliwapandisha madaraja jumla ya watumishi 10 katika kada mbalimbali. Katika
kipindi cha mwaka 2018/19 Wizara
inatarajia kuwapandisha madaraja watumishi 100
ambao wamepata sifa za kitaaluma na wenye utendaji mzuri wa kazi. Aidha, Wizara
pamoja na Taasisi zake inatarajia kuajiri jumla ya watumishi 207 katika kada mbalimbali. Kati ya
watumishi hao, 43 wataajiriwa na
Wizara, 116 TPDC na 48 PURA.
135. Mheshimiwa
Spika, ili kuhahakikisha kuwa Nchi inakuwa na
wataalamu wa Kitanzania wa kutosha katika Sekta ya Nishati, Wizara imeendelea
kushirikiana na Washirika wa Maendeleo kutoa ufadhili wa masomo kwa Watanzania
wanaokidhi vigezo kwenda kusoma nchi mbalimbali kwa ngazi za Shahada, Uzamili
na Uzamivu. Kwa mwaka 2017/18 watanzania 22
walipata ufadhili wa masomo kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China katika
masuala ya mafuta na gesi asilia. Aidha, kupitia Programu za Uendelezaji wa Rasilimaliwatu
(Capacity Building), Development in Oil and Gas Industry na Energy Sector
Capacity Building Program watumishi
16 walipata ufadhili katika fani mbalimbali zikiwemo: usimamizi katika masuala
ya mafuta na gesi asilia, sheria na
uhasibu na fedha. Kwa mwaka 2018/19, watanzania 22 watapatiwa ufadhili wa masomo kutoka Serikali ya Jamhuri
ya Watu wa China.
136. Mheshimiwa
Spika, katika kujali afya za watumishi, Wizara
imeendelea kutekeleza Waraka wa Utumishi wa Umma Na. 2 wa Mwaka 2006 kwa
kuwahudumia watumishi wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (VVU) na wenye UKIMWI
waliojitokeza kwa kuwapatia lishe na dawa maalum. Aidha, Wizara itaendelea kutoa elimu mahali
pa kazi ili kuzuia maambukizi mapya na kuwahudumia waathirika wa UKIMWI kadri
watakavyojitokeza. Sambamba na jitihada hizo, Wizara pia itaendelea kuhamasisha
watumishi kupima afya hususan kwenye Magonjwa Sugu Yasiyo ambukiza (MSY)
ikiwemo shinikizo la damu, kisukari na saratani. Aidha, Wizara
imeanzisha utaratibu wa kuwahamasisha Watumishi kufanya mazoezi baada ya saa za
kazi ili kuimarisha afya zao na kuwawezesha kufanya kazi kwa ufanisi.
137. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kutekeleza agizo la Serikali la
kuhamishia shughuli zake Makao Makuu Dodoma ambapo hadi sasa watumishi 50
kati ya 153 wamehamia Dodoma. Wizara inaendelea kukamilisha taratibu husika
ili watumishi wote waweze kuhamia Dodoma katika kipindi cha mwaka huu wa fedha.
H.USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
138.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Nishati imekuwa
ikishirikiana na Washirika wa Maendeleo katika utekelezaji wa Programu,
Mikakati na Miradi mbalimbali ya maendeleo. Kwa niaba ya Serikali, napenda
kutambua mchango wa: Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Benki ya Dunia (WB), Benki
ya Exim ya China, Benki ya Ushirikiano wa Kimataifa ya Japan (JBIC), Benki ya
Unicredit Austria, Economic Development
Cooperation Fund (EDCF- Korea), Mfuko wa Uendelezaji Jotoardhi (Geothermal Risk Mitigation Facility - GRMF),
pamoja na Taasisi na Mashirika ya: JICA (Japan), KfW (Germany), AFD (Ufaransa),
OfD (Norway), DFID (Uingereza) Sida (Sweden), Umoja wa Ulaya (EU), Shirika la
Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na
USAID (Marekani). Vilevile, natoa
shukrani kwa Serikali za China, Sweden, Ufaransa, Finland, Ujerumani, Iceland,
Norway, Korea ya Kusini, Uganda na Ethiopia. Kwa kipindi cha mwaka 2018/19 Serikali
kupitia Wizara ya Nishati itaendelea kushirikiana na Washirika hawa pamoja na
wengine katika uendelezaji wa Sekta hii muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa Nchi
yetu.
I.
SHUKRANI
139.
Mheshimiwa
Spika, kipekee namshukuru
kwa dhati Mhe. Subira Khamis Mgalu, Mbunge wa Viti Maalum, na Naibu Waziri wa
Nishati kwa namna anavyonisaidia katika kusimamia Sekta ya Nishati. Hakika tangu
ameteuliwa kuwa Naibu Waziri amekuwa na mchango mkubwa katika kusimamia Sekta
hii ambayo ina mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi na ujenzi wa viwanda
nchini.
140.
Mheshimiwa Spika, usimamizi bora wa Sekta ya Nishati
nchini unategemea ushirikiano unaotolewa na watendaji mbalimbali wa Wizara.
Hivyo, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru Katibu Mkuu wa Wizara Dkt. Hamisi
Hassan Mwinyimvua, Wakuu wa Idara na Vitengo pamoja na Watumishi wote wa Wizara
kwa ushirikiano wanaonipatia kuniwezesha kuzisimamia shughuli mbalimbali zilizo
ndani ya Sekta ya Nishati. Ni matumaini yangu kuwa ushirikiano huu utazidi
kuimarika.
141.
Mheshimiwa
Spika, naomba nitumie
nafasi hii kuwashukuru Wenyeviti na
Wajumbe wa Bodi, Wakuu wa Taasisi na Watumishi
wote wa Taasisi zinazosimamiwa na Wizara kwa ushirikiano wanaonipatia.
Ni wazi kuwa ushirikiano huo umekua chachu katika kufanikisha utekelezaji wa
majukumu yangu.
142.
Mheshimiwa Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu,
nawapongeza wananchi wa Jimbo la Chato kwa uvumilivu wao hasa wanaponikosa
Jimboni nikiwa natekeleza shughuli hizi muhimu. Naipongeza sana familia yangu
ikiongozwa na mpendwa wangu mama Kalemani kwa ustahimilivu wao hasa ninapokuwa
mbali nao kifamilia nikiwa katika majukumu haya ya kitaifa, nawaomba waendelee
kuwa wavumilivu kwa kuwa kazi hizi ni muhimu kifamilia na kitaifa.
J.
HITIMISHO
143.
Mheshimiwa Spika, Bajeti ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka
wa Fedha wa 2018/19 pamoja na matumizi mengine imeelekezwa katika kutekeleza
Miradi Mikubwa ya Nishati ya Kielelezo ambayo itakapokamilika itasaidia
upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.
144.
Mheshimiwa Spika, naomba Bunge lako Tukufu sasa likubali
kupitisha Makadirio ya Jumla ya Shilingi 1,692,286,014,000 kwa ajili ya matumizi ya
Wizara ya Nishati na Taasisi zake. Mchanganuo wa fedha hizo ni kama ifuatavyo:
(i)
Shilingi
1,665,141,000,000 ni kwa ajili ya miradi ya
maendeleo. Kati ya fedha
hizo, Shilingi 1,489,741,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi 175,400,000,000 ni fedha za nje; na
(ii)
Shilingi 27,145,014,000 ni kwa
ajili ya Matumizi ya Kawaida. Kati ya fedha hizo Shilingi 15,025,821,000 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo (OC). Shilingi 12,119,193,000 ni kwa ajili ya Mishahara (P.E) ya watumishi wa
Wizara na Taasisi zilizo chini yake.
145.
Mheshimiwa Spika,
naomba tena nitoe shukrani zangu za dhati kwako na kwa
Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunisikiliza. Hotuba hii pia inapatikana katika
Tovuti ya Wizara kwa anuani ya www.nishati.go.tz. Vilevile, Hotuba hii ina vielelezo mbalimbali kwa ajili ya ufafanuzi wa masuala
muhimu yanayohusu Sekta ya Nishati.
146.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa
hoja.
Comments
Post a Comment