Featured Post

MADAKTARI BINGWA WABAINI ZAIDI YA WAGONJWA 460 WA MOYO SONGWE

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, George Lyego Longopa, kutoka Taasisi ya Magonjwa ya Moyo ya Jakaya Kikwete akichukua maelezo ya mgonjwa wa moyo katika hospitali ya Vwawa-Mbozi.

Na Mwandishi Wetu, Songwe
WAGONJWA 467 wenye matatizo ya moyo wamebainishwa na kupatiwa huduma ya ushauri na matibabu kutoka kwa madaktari bingwa waliotoa huduma kwenye kambi maalum ya siku 4 katika Hospitali ya Vwawa-Mbozi Mkoani Songwe.

Timu ya Madaktari Bingwa na wauguzi 5 wameeleza kuwa wagonjwa 18 kati ya hao waliowahudumia wamepewa rufaa ya kufika hospitali za Rufaa kwa ajili ya matibabu zaidi.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, George Lyego Longopa, kutoka Taasisi ya Magonjwa ya Moyo ya Jakaya Kikwete amesema wameanza matibabu siku ya Jumanne na kila Daktari amekuwa akiona zaidi ya wagonjwa 60 kutokana na hamasa ya wagonjwa waliojitokeza kupata matibabu ya magonjwa ya moyo.
 “Tumeona wagonjwa wengi na tumeamini kuwa Songwe tatizo la magonjwa ya moyo bado ni kubwa, wagonjwa wengi wamekutwa na matatizo ya shinikizo la damu, moyo kushindwa kufanya kazi vizuri pamoja na matatizo ya mishipa ya damu kuziba,” amesema Dkt. Longopa.
Afisa Muuguzi Kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Flora Kasembe, ameeleza kuwa mtindo wa maisha ya wananchi wa Songwe unaweza kuwa ni chanzo cha magonjwa ya moyo hasa kutokana na uwepo vyakula vingi lakini wananchi hawali mlo kamili.
Kasembe amefafanua kuwa, “Tumekuwa tukitoa elimu ya kuzingatia mlo kamili ili hivi vyakula vingi vilivyopo huku visaidie kuimarisha afya na sio waishie kuuza tu bila wao kutumia, pia wananchi wajenge mazoea ya kufanya mazoezi na endapo watabainika na matatizo na wakaanzishiwa dawa wazitumie kwa usahihi waiache.”
Baadhi ya wagonjwa waliohudhuria kupata matibabu ya moyo wameishukuru serikali kwa kusogeza huduma karibu na utaratibu huo ufanyike mara kwa mara ili wananchi wengi wapate huduma ya madaktari bingwa.
Brigita Haule ambaye amepata matibabu ya moyo ameeleza kunufaika na huduma hiyo kwani hakuwa akifahamu kama ana tatizo la moyo mpaka alipofika katika huduma hiyo.
“Wengi tunajiamini ni wazima kwakuwa hatusikii kuumwa sana ila tunatembea na magonjwa mbalimbali ambayo tunakuja kuyafahamu yakiwa katika hali mbaya, mimi pia sikufahamu kama nina tatizo hivyo nawashauri wote tuwe na utaratibu wa kupima afya zetu,” amefafanua Bi. Haule.
Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa, Dkt. Kheri Kagya, amesema utaratibu wa kuwaalika madaktari bingwa wa moyo kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete uliangaliwa na uongozi wa Mkoa baada ya kubaini kuwa kuna wagonjwa 210 wa moyo.
Dkt. Kagya ameongeza kuwa wagonjwa waliojitokeza wamekuwa wengi kuliko matarajio ya awali huku akieleza kuwa hayo ni mafanikio kwakuwa wameweza kuwabaini wagonjwa ambao hawakutambulika hapo awali.

Afisa Muuguzi Kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Flora Kasembe akimpima shiniko la damu mwandishi wa habari Manuel Kaminyoge katika hospitali ya Vwawa-Mbozi, 


Baadhi ya wagonjwa wakisoma kipeperushi kinachoeleza masuala ya lishe wakati wakisubiri kupata huduma ya madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete katika hospitali ya Vwawa-Mbozi.

Comments