Featured Post

BENKI YA DUNIA YAONESHA NIA KUSHIRIKI UJENZI RELI YA ISAKA-KIGALI

Ujumbe wa Tanzania (kulia) na ujumbe wa Benki ya Dunia (kushoto) wakiwa katika majadiliano ya miradi ya maendelea inayotarajiwa kuanza kutekelezwa mwaka ujao wa fedha.

Na WFM- Washington DC
Benki ya Dunia imeonesha dhamira ya kuisaidia Tanzania katika ujenzi wa Reli ya Kiwango cha Kimataifa (SGR) kutoka Isaka kwenda Rusumo na baadae Kigali pamoja na miundombinu mingine ya usafirishaji  kama barabara ili kusaidia kuendeleza biashara na ustawi wa jamii kwa ujumla.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) wakati wa majadiliano na wataalamu wa Benki ya Dunia yaliyoongozwa na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anayeshughulikia kanda ya Afrika Bw. Makhtar Diop, kwenye mikutano ya mwaka ya kipupwe inayoendelea mjini Washington DC Marekani.
Dkt. Mpango amesema kuwa miradi ya Kikanda ambayo Benki hiyo imeonesha nia ya kuitekeleza ni ile ya uboreshaji wa mazingira na bandari katika ziwa Victoria zikiwemo za mikoa ya Mwanza, Musoma na Kigoma na Bandari zilizoko katika Ziwa Tanganyika ambazo zitarahisisha usafiri wa kwenda Burundi na Congo.
"Miradi hii ya Kikanda na Kitaifa ambayo Benki ya Dunia imepanga kuitekeleza kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kwa mwaka ujao wa fedha itahakikisha kunakuwa na mazingira endelevu na tija kwa kuwa inagusa nchi zote zinazozunguka maziwa hayo mawili," alieleza Dkt. Mpango.
Amesema kuwa ni lazima kuhakikisha kunakuwa na udhibiti wa uchafuzi wa mazingira kadri iwezekanavyo ili kuendelea kufaidi rasilimali za maziwa hayo makubwa  kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na nchi jirani zinazozunguka maziwa hayo.
Aidha amebainisha kuwa mwakani, Benki ya Dunia imeonesha nia ya kutoa fedha kwa ajili ya tekeleza mradi wa kuzalisha umeme katika mto Rufiji eneo la Ruhuji ambapo utakapokamilika unatarajiwa kuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 300.
"Eneo hili la sekta ya umeme ni muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya viwanda kwa kuwa uchumi wa viwanda hauwezi kukua bila kuwepo umeme wa uhakika," alifafanua Waziri Mpango.
Vilevile Benki ya Dunia (WB) imekubali kuisaidia Tanzania kutoa mafunzo katika uchambuzi wa miradi mbalimbali ili kusaidia Serikali ya Tanzania kutokuingia kwenye madeni makubwa zaidi ambayo hayawezi kulipika.
Waziri Mpango alieleza kuwa kutokuwa na ufanisi wa kutosha katika kuchambua miradi ambayo inagharamiwa na fedha za mikopo inasababisha nchi kubeba mzigo mkubwa wa madeni hivyo ni vyema Tanzania ikahakikisha kuwa miradi hasa ile inayogharamiwa kwa fedha za mikopo inachambuliwa vizuri ili mradi husika unapokamilika uweze kulipa deni.
Amesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali itakua na miradi mingi ya kutekeleza, miongoni mwa miradi hiyo ni kupambana na tatizo la utapiamlo hivyo ni vema kama nchi ikaangalia namna bora ambayo Benki ya Dunia inaweza kusaidia katika utekelezaji wake.
“Kitaalamu mpaka mwanadamu anapofikisha siku 1000 ni kipindi muhimu sana kinachoamua maisha ya mwanadamu atakapokuwa mtu mzima atakuwa na uwezo gani wa kufikiri, kutokana na hali hiyo mtu ambaye atakua na utapiamlo uwezo wake utakua ni mdogo zaidi kulinganisha na mtoto aliyepata lishe bora’” alifafanua Dkt. Mpango.
Katika kutekeleza mradi huo Serikali itafanya kazi na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Wizara ya Afya pamoja na Taasisi ya Chakula na Lishe ili kuhakikisha kwamba Taifa linapunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la utapiamlo.
Mikutano hiyo ya mwaka ya kipupwe kati ya ujumbe wa Serikali ya Tanzania na Wataalamu wa Benki ya Dunia imekuwa na mafanikio makubwa kwa kuwa Tanzania itanufaika kutokana programu mbalimbali ambazo zitagharamiwa na Benki ya Dunia kwa mikopo nafuu.
Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anayeshughulikia kanda ya Afrika Bw. Makhtar Diop akitoa ufafanuzi wa miradi ambayo itatekelezwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania. Kulia ni Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Somalia, Burundi na Malawi Bi. Bella Bird na Kushoto ni Mkurugenzi wa Mipango Benki ya Dunia ukanda wa Afrika Bi. Mamta Murthi .
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) akielezea miradi ambayo itatekelezwa kwa mwaka ujao wa fedha. Kulia ni Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania-BOT, Prof. Florens Luoga.
Picha na Kitengo cha Mawasilano Serikalini
Wizara ya Fedha na Mipango
Washington D.C

Comments