Featured Post

MAKABURI YENYE 'UJUMBE WA KUZIMU' YAGUNDULIWA MISRI



Makaburi ya zamani ambayo yana majeneza kadha yaliyotengenezwa kwa mawe, na mkufu ulio na "ujumbe kutoka kuzimuni" vimegunduliwa nchini Misri.
Ugunduzi huo umefanywa Minya, kusini mwa Cairo. Makaburi yaliyogunduliwa ni ya zaidi ya miaka 2,000 iliyopita na shughuli ya ufukuzi inatarajiwa kuchukua miaka takriban mitano.

Waziri wa mambo ya kale Misri Khaled al-Enany amesema makaburi hayo yana majeneza 40, vito, vyungu na barakoa ya dhahabu.
Amesema kuna mashimo ya kuwekwa majeneza chini ya ardhi ambayo ni ya enzi za Mafirauni hadi enzi za Wagiriki mnamo mwaka 300BC hivi.
"Huu ni mwanzo tu wa ugunduzi huu mpya," aliwaambia waandishi wa habari.
"Karibuni tutaanza kuongeza kivutio kingine cha mambo ya kale Misri."
Mostafa Waziri, mkuu wa ufukuzi huo, amesema makaburi manane yaligunduliwa katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita lakini anatarajia mengine zaidi yagunduliwe.
"Shughuli ya ufukuzi inapangiwa kuendelea kwa miaka mitano hivi katika jaribio la kufukua eneo lote la makaburi," amesema.
Waziri amesema mengi ya makaburi na vitu vya kale vilivyogunduliwa ni vya makasisi wa miungu wa zamani wa Misri kwa jina Thoth.
Magudulia manne yenye vifuniko ambayo yamehifadhiwa vyema yameundwa kuwa na muonekano wa wana wanne wa kiume wa miungu Horus pia yaligunduliwa.
"Bado magudulia hayo yana viungo vya ndani ya mwili vya marehemu vilivyohifadhiwa vyema ndani. Magudulia hayo yamepambwa kwa maandishi ya kale yanayoonesha majina na vyeo vya wahusika," amesema Waziri.
Ameeleza sifa ya kugunduliwa kwa mkufu huo Mkesha wa Mwaka Mpya ukiwa umeandikwa ujumbe "Kheri ya Mwaka Mpya" ni ya ajabu.
"Huu ni ujumbe uliotumwa kwetu kutoka kuzimuni," amesema.
Mapema mwezi huu, wanaakiolojia waligundua kaburi la kasisi wa kike ambaye alizikwa miaka 4,400 iliyopita.
Kaburi hilo lilikuwa limehifadhiwa vyema na lilikuwa na picha ya ukutani ya kasisi huyo, Hetpet, zikimuonesha akitekeleza shughuli mbalimbali.




Comments