Featured Post

ELIMU YA URAIA KUHUSU ARDHI: MASWALI NA MAJIBU YANAYOHUSU MASUALA MBALIMBALI YA ARDHI


Swali 1: Ni taratibu zipi zinazotumika katika utoaji wa vyeti vya hakimiliki za kimila kwa wamiliki wa ardhi za kimila ndani ya maeneo ya vijiji?
Mfumo wa umiliki wa ardhi Tanzania ni wa aina mbili. Kwanza, ni kwa njia ya kimila; ambapo mmiliki wa ardhi aliyeipata kwa njia ya kurithi, kupewa zawadi, kugawiwa na kijiji, kununua ama kusafisha pori anakuwa na haki ya ardhi hiyo. Haki hiyo inalindwa kisheria hata bila ya kuwa na hati yoyote.

Njia ya pili ni kwa hati miliki ambapo mmiliki wa eneo hupewa cheti au hati inayothibitisha umiliki wake wa eneo husika. Mara nyingi ardhi ya jumla inamilikiwa na hatimiliki wakati ardhi ya kijiji inamilikiwa kimila.
Kwa mujibu wa sheria ya vijiji ya ardhi ya vijiji Na. 5 ya mwaka 1999, hakimiliki ya kimila inatolewa baada ya kutimiza taratibu za awali ambazo ni pamoja na kijiji husika kupata cheti cha ardhi ya kijiji (F.7 [7]), cheti ambacho hupatikana baada ya kutimiza masharti matatu ya msingi.
Kwanza, kijiji kisiwe na mgogoro wowote wa mipaka ya ardhi yake. Pili, kijiji kiwe kimejenga masijala ya ardhi kwa ajili ya kuhifadhia nyaraka muhimu, na tatu, kijiji kiwe kimeandaa mpango wa matumizi bora wa ardhi.
Baada ya taratibu hizo kukamilika, halmashauri ya kijiji kupitia kwa Afisa Mtendaji wake itatakiwa kutoa taarifa kwa halmashauri ya wilaya kwa ajili ya taratibu za kubainisha mipaka, kuchora ramani na kuendeleza mchakato wa upatikanaji wa cheti cha ardhi ya kijiji na baadaye vyeti vya hakimiliki za kimila ambavyo hutolewa kwa mmiliki mmojammoja wa ardhi kwa mujibu wa kifungu cha 22(3) na 25 cha Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na.5 ya 1999.
 Angalizo: Kwa kijiji ambacho kiliwahi kupata hatimiliki ya kijiji huko nyuma itabiti hatimiliki hiyo irejeshwe kwanza ndipo cheti cha ardhi ya kijiji kiandaliwe. Hii inamaanisha kuwa kijiji hakipaswi kuwa na hakimiliki ya kijiji pamoja na cheti cha ardhi ya kijiji kwa wakati mmoja.

Swali 2: Taratibu gani zinapaswa kufuatwa wakati eneo linapotangazwa kuwa la mipango miji?
Wakati eneo linapotangazwa kuwa la upimaji au mipangomiji, masharti ya sheria yaliyoko kwenye sheria ya utwaaji na sheria na sheria za ardhi yanapaswa kuzingatiwa. Kifungu cha 3 (1)(g) cha sheria ya ardhi Na. 4 na Na. 5 kimeeleza kwamba, umiliki wa mtu unapositishwa kwa namna yoyote ile, usitishwaji huo unapaswa kuambatana na malipo ya fidia kamili, ya haki na kwa wakati kwa mtu huyo.
Rachel Kilasi – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, akifafanua sheria ya Ardhi na. 4 ya mwaka 1999 sambamba na Umiliki wa Ardhi 
Hii ni pamoja na kumpa mtu notisi ya muda wa kutosha wa kujiandaa kuhama kuendana na mabadiliko hayo. Fidia hii inahusisha thamani ya mali iliyopo katika eneo hilo kwa kuzingatia gharama au thamani ya soko kwa wakati huo. Fidia inapaswa kutolewa kwa kuzingatia misingi ya haki na kwa wakati ingawa mara nyingi haya yamekuwa hayazingatiwi katika maeneo mbalimbali.

Swali 3: Ni zipi haki za wakazi na wamiliki wa maeneo yanayotangazwa kuwa maeneo ya upimaji au mipango miji?
Mara nyingi, eneo linapotangazwa kuwa la mipangomiji au la upimaji huambatana na mabadiliko mbalimbali ya ukaaji na matumizi ya ardhi ya eneo hilo. Kuna uwezekano mkubwa wa mmiliki wa eneo hilo kuagizwa kuondoka kupisha shughuli husika, ama kutekeleza na kuendana na masharti mapya ya eneo lililotangazwa kuwa na mipango miji.
Hali hii inapojitokeza bado mmiliki anazo haki zinazoendana na uendelezaji uliofanyika mahali pale. Miongoni mwa haki hizo ni pamoja na kupewa fidia endapo mmiliki atalazimika kuhamishwa au sehemu ya umiliki wake katika ardhi hiyo inahamishiwa kwa mmiliki mwingine.
Fidia hii sharti iwe ya haki na itolewe kwa wakati kama ilivyofafanuliwa hapo awali. Sheria za ardhi zinakataza watu kuondolewa katika maeneo yao bila kulipwa fidia endapo ni wamiliki halali kwa mujibu wa sheria mbalimbali na taratibu zilizotumika kuwamilikisha maeneo hayo.

Swali 4: Kuna tofauti gani za kimsingi kati ya hatimiliki, cheti cha hakimiliki ya kimila na leseni ya makazi?

Hakimiliki ya kisheria
Ni cheti kinachompa mtu umiliki wa kisheria kwa maandishi. Cheti hiki kinatolewa kwa mujibu wa wa sehemu ya sita (6) ya sheria ya ardhi Na. 4 ya mwaka 1999kwa mmiliki wa ardhi ya jumla na sehemu ya ardhi ya hifadhi. Hati za namna hii hutolewa pia kwa wamiliki wa mashamba makubwa yanayomilikiwa kwa hati hata kama mashamba hayo yako ndani ya ardhi ya kijiji ilimradi tu yamepimwa na kukamilishwa kwa taratibu zinazotakiwa kisheria. Hati hizi hutolewa na kamishna wa ardhi kwa kipindi cha ama miaka 33 na 99 .

Cheti cha Hakimiliki ya Kimila
Ni cheti kinachompa mtu umilikiwa ardhi kwa taratibu za kimila. Kwa upande mwingine, cheti hiki hutolewa kama hati ya maandishi kwa mujibu wa kifungu cha 25 cha sheria ya ardhi Na.5 ya mwaka 1999 kwa wamiliki hasa katika ardhi ya kijiji. Cheti hiki hutolewa na halmashauri ya kijiji kwa mwanakijiji mmoja au kikundi cha wamiliki au taasisi.

Angalizo:Izingatiwe kuwa, kwa mujibu wa kifungu cha 18(1) cha Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na.5 ya mwaka 1999, hakimiliki ya kisheria kwa hali yoyote ina hadhi sawa na hakimiliki ya kimila. Hivyo, hakuna umiliki wenye hadhi ya juu kuliko mwingine.
Ufafanuzi huu unapaswa kuondoa mazoea ya watu kufikiri kuwa, hatimiliki ina hadhi ya juu kuliko milki ya kimila au cheti cha hakimiliki ya kimila, mazoea mabayo husababisha wamiliki wa kimila kujiona wanyonge na wakati fulani kupoteza haki zao kwa mazoea.
Leseni ya makazi

Swali 5: Je, lengo kubwa la hati/cheti cha hakimiliki ya kimila ni kuchukulia mikopo tu?
Watu wengi wamekuwa wakihusisha upatikanaji wa cheti cha hakimiliki ya kimila na mikopo ya kibenki. Hata hivyo, ukweli ni kwamba cheti cha hakimiliki ya kimila hakitolewi kwa lengo la kuchukulia mikopo tu.
Badala yake cheti hiki kinalenga kutimiza azma ya Sera ya Ardhi ya Taifa ya kuhakikisha kwamba haki zote zilizopo katika ardhi na imilikaji wa ardhi wa kwa muda mrefu unatambilika na kulindwa kisheria. Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 3 (b) cha sheria Na. 4 na 5 za 1999.
 Pamoja na faida nyingine, hati hii huboresha usalama wa kumiliki ardhi kijijini na kuondoa uvamizi holela. Vilevile, hati hii inamfanya umiliki wa ardhi wa kimila kuwa rasmi zaidi tofauti na ilivyo katika maeneo mengi ambayo hayana hati hizo kwani huonekana kama ni vigumu kuthibitisha umiliki wake.
Kadhalika, pale ambapo itaonekana kuwa mifumo ya taasisi za kifedha inakubaliana na matumizi ya hati hizo kama dhamana ya mikopo, hati zinaweza kutumika katika taasisi husika. Wapo pia wanaozitumia hati hizo kama dhamana mahakamani na hata katika taasisi za elimu ya juu kama dhamana ya mkopo.

Swali 6: Umiliki  wa kimila bila cheti cha hakimiliki ya kimila una nguvu?
Kimsingi, umiliki wa kimila tangu zamani haukuambatana na cheti au hati yoyote ya kimaandishi kuthibitisha. Nguvu yake kubwa ipo katika mila na desturi za eneo husika na hivyo sheria kwa kutambua mfumo wa milki ya ardhi ya kimila, imeupa hadhi sawa na ule umiliki wa kutumia hati na unatambuliwa hivyo hata kama cheti cha hakimiliki hakijatolewa.
Hata hivyo, ni lazima pia kuweka bayana kuwa kumekuwepo shinikizo kubwa kubadili mfumo wa kumiliki ardhi kimila kwa vile unaonekana kama haumpi mmiliki uhakika wa milki ya ardhi yake pale ambapo hana uthibitisho wa cheti.
Mashinikizo haya yanatokana na mabadiliko katika mfumo wa ardhi kidunia ambao unaweka mkazo katika maslahi binafsi kuliko yale ya kiujumla ambayo ndiyo mhimili wa mfumo wa umiliki ardhi wa kimila.
Lakini katika mazizingira ya sasa, bado wamiliki wengi wa ardhi waishio vijijini na hata walio mijini (maeneo yasiyopimwa) hutegemea mfumo wa ardhi wa kimila kwani ndio unaoonekana kuwapa uhakika wa kumiliki maeneo yao kuliko hatimiliki ambazo wengi huchukulia kuwa ni njia ya kuwatenga wengine kutoka katika umiliki wa ardhi ya pamoja.

Swali 7:  Je, kuna mtu akiwa na ardhi maeneo tofauti tofauti katika ardhi ya kijiji, cheti cha hakimiliki ya kimila kitatolewaje? Na pale mwanakijiji anapokuwa na ardhi kwenye kijiji kingine umiliki wake unakuwaje?
Ni dhahiri kwamba wanavijiji walio wengi wanamiliki eneo zaidi ya moja katika sehemu tofauti katika ardhi ya vijiji. Utaratibu uliopo katika utoaji wav yeti umezingatia hali hii. Kila eneo linapaswa kuwa nacheti chake kwa kuzingatia matumizi ya eneo hilo nikiwa ni pamoja na mila, desturi na tamaduni za maeneo hayo. Vilevile mtu anapokuwa na ardhi katika ardhi ya kijiji kingine anakuwa na umiliki sawa na wakazi wa kijiji kile na cheti kitatolewa kama taratibu za kijiji hicho ardhi ilipo kwa kuzingatia mila na desturi za kijiji husika. Endapo inakuwa vigumu kwa kijiji kuruhusu umiliki wa aina hiyo kwasababu mbalimbali ikiwemo uhaba wa ardhi kwa wanakijiji, basi itabidi mmiliki achague kijiji atakachoishi na kujiandikisha kama mkazi wake japo pia haki yake ya kumiliki na kutumia ardhi kama asiye mwanakijiji iko pale pale.

8. Je, ardhi ya kijiji inaweza kugawiwa kwa mtu asiye mwanakijiji na kwa taratibu gani?
Katiba ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania ibara ya 17 (1) inatoa fursa kwa raia wa Tanzania kuishi popote nchini ili mradi anafuata taratibu zinazotakiwa na kwa kufanya hivyo hakiuki haki za raia wangine. Ibara ya 24 inatoa haki kwa raia kumiliki mali ikiwemo ardhi. Kwa wananchi wengi wanaoishi vijijini, ardhi ndio mali ambayo kila mmoja anamiliki.
Hivyo kutokana na msingi huo, hata raia asiye mwanakijiji ana haki ya kuomba na kugawiwa ardhi ya kijiji haki hiyo imefafanuliwa katika fungu la 22 la sheria ya ardhi ya vijiji namba 5 1999, ambayo inatoa haki kwa mtu au kundi la watu ambao kwa kawaida si wakazi wakijiji kuomba kugawiwa ardhi ya kijiji.
Hata hivyo katika kufanya hivyo muombaji huyo anapaswa kufuata taratibu  za kawaida za uombaji. Tarataibu hizo ni pamoja na: kwanza,muombaji anatakiwa

9. Ni nani mwenye haki ya kumiliki ardhi nchini Tanzania na nani harusiwi kumiliki ardhi?
Kisheria , raia wote wa Tanzania wana haki ya kumiliki ardhi. Haki hii inajumuisha pia taasisi zilizosajiliwa kisheria na kutambuliwa kama mtu mbele ya macho ya sheria. Kwa mujibu wa fungu la 20 la sheria ya ardhi na 4 ya mwaka 1999, mtu asiye raia wa Tanzania haruhusiwi kupata au kumiliki ardhi isipokuwa tu kwaajili ya shughuli za uwekezaji kwa kuzingatia sheria ya uwekezaji ya mwaka 1977.
Hata hivyo kwa mujibu wa sheria hii, mmiliki wa ardhi hiyo hawi mwekezaji bali kituo cha uwekezaji ambacho humpangisha mwekezaji huyo kama umiliki wa upangaji. Mmiliki wa aina hii anakuwa na haki hafifu inayojulikana kama derivative right tofauti na mmiliki wa kawaida ambaye anakuwa na haki kamili inayotolewa kwa njia ya hati kupitia kamishna wa ardhi.

10. Je, mwanamke ana haki gani katika ardhi ya familia? Ya mumewe? Ya jumla?Au ya kijiji?
Kabla ya ujio wa sheria mpya za ardhi wanawake walikuwa wakibaguliwa katika mifumo ya umilikaji ardhi kutokana na kuzoeleka kuwa wangemiliki kupitia waume zao au ndugu zao wa kiume kama wajomba na kaka zao. Ukiachilia mbali sheria ya kikoloni ya mwaka 1923, sheria nyingi za kimila pia ziliwabagua na baadhi yake bado zimeendelea kuwabagua wanawake katika umiliki wa ardhi na hata mirathi.
Sheria mpya za ardhi za mwaka 1999, zimeleta mapinduzi makubwa katika mfumo wa milki ya ardhi kwa wanawake. Kwa mujibu wa sheria ya ardhi na 4 fungu la 161(1) mwanamke ana haki juu ya ardhi ya familia nay a mumewe. Katika fungu hili, sheria imeweka wazi ardhi hiyo itahesabika kuwa chini ya umiliki wa wanandoa wote, isipokuwa pale hakimiliki ya ardhi itakapobainisha wazi kuwa ardhi hiyo ni mali ya mwanandoa huyo pekee.
Hata hivyo, kifungu kidogo cha pili cha fungu hilo, kimeweka bayana kuwa hali hii inapotokea, bado mchango wa uzalishaji, maendelezo na utunzaji wa ardhi hiyo unaofanywa na mwanandoa mwingine (mwanamke au mwanaume) utampatia haki sawa ya umiliki wa ardhi hiyo. Haki ya mwanamke katika ardhi ya jumla na ile ya mwanaume katika kupata, kumiliki, kutumia, na kuuza au kuigawa ardhi kwa viwango vilevile na masharti yaleyale, kwa mujibu wa fungu la 3(2) la sheria za ardhi, 1999

11. Pale ambapo sheria za kimila zinamnyima haki mwanamke au makundi mengine katika jamii kumiliki ardhi nini kinapaswa kufanyika?
Sheria za kimila zinapaswa kuwiana na misingi ya sera ya taifa ya ardhi na sheria nyingine yeyote inayohusiana na ardhi ikiwa ni pamoja na katiba ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania. Endapo mila, desturi, au mazoea ya jamii yanaonekana kumnyima haki mwanamke, yatahesabika kuwa batili na yasiyotambulika wala kutelekezwa na halmashauri yoyote ya kijiji, mkutano wa kijiji, mtu au kundi lolote. Hii ni kwa mujibu wa fungu la 20(2) la sheria ya ardhi ya vijiji na 5,1999

12. Ni taratibu zipi zinapaswa kutumika wakati wa kutwaa ardhi kutoka kwa mmiliki kwa ajili ya matumizi mengine au maslahi ya taifa?
Utwaaji ni uwezo wa rais kuchukuwa sehemu yoyote ya ardhi ya Tanzania kwa kile kinachodaiwa kuwa ni kwa manufaa ya umma, kwa mujibu wa sheria ya utwaaji na 47 ya mwaka 1967 na sheria ya ardhi na.4 ya mwaka 1999.
Hatua hii inapochukuliwa Rais anapaswa kuzingatia taratibu zifuatazo: mosi, lazima atoe notisi ya kusudio la utwaaji wa ardhi inayoainisha sababu za utwaaji. Pili, anapaswa kutoa muda wa pingamizi wa siku tisini kwa wale ambao ardhi yao inatwaliwa. Tatu, endapo hakuna pingamizi, mtwaaji anatakiwa kufanya uthaminishaji na thamani za mali zilizo katika ardhi husika. nne na mwisho, mtwaaji anapaswa kutoa fidia ya haki na kwa wakati kulingana na viwango vya soko vya mali husika.

13. Mmiliki wa ardhi ana haki gani pale ardhi yake inapotwaliwa kwa matumizi mengineyo?
Kifungu cha 3(1)(g) cha sheria ya ardhi na.4 na na.5 kinaeleza kwamba umiliki wa mtu unapositishwa kwa namna yoyote ile usitishwaji kwa namna yoyote ile usitishwaji huo utapaswa kuambatana na malipo ya fidia kamili, ya haki na kwa wakati kwa mtu huyo ikiwa ni pamoja na kumpa mtu huyo notisi na muda wa kutosha wa kujiandaa kwa ajili ya kuhama au kuendana na mabadiliko hayo.
Fidia hii inahusisha thamani ya mali iliyopo katika eneo hilo ikiwa ni pamoja na maendelezo yaliyofanyika katika eneo hilo ikiwa ni pamoja na maendelezo yaliyofanyika katika eneo hilo kwa kuzingatia gharama au thaman ya soko kwa wakati huo. Fidia inapasa kufanyika kwa haki na kwa wakati ingawa mara nyingi haya yamekuwa yakipuuzwa katika maeneo mbalimbali.

14. Je, unaweza kuzuia uporaji wa ardhi ya kijiji isichukuliwe kwa madai ya kuwa ardhi tupu?
Mkanganyiko uliopo katika tafsiri ya ardhi ya jumla katika sheria na.4 ya 1999 inayoingiza ardhi ya kijiji isiyokaliwa, kumilikiwa wala kutumiwa katika kundi hilo unarahisisha uporaji wa ardhi ya kijiji na pia kupunguza mamlaka ya usimamizi wa ardhi ya kijiji kutoka kwa wanavijiji na halmashauri zao.
Ili kuzuia uporaji huu, wanavijiji wanashauriwa kuweka mpango wa matumizi bora ya ardhi. Mpango huu unalenga kuhakikisha kuwa hakuna ardhi inayobakia kijijini bila kuwa na matumizi maalumu ama kwa wakati huo au wakati ujao.

15. Kwanini wamiliki wa nyumba na mali nyinginezo zilizo kando ya barabara hubomolewa kunapokuwa na upanuzi wa barabara hizo? Yapi ni makosa yao na kama wanahaki ni zipi kisheria?
Ni makosa kwa mtu kujenga ndani ya hifadhi ya barabara. Inapotokea mtu akajenga au kufanya shughuli yoyote ndani ya eneo hilo, mara nyingi hukutana na tatizo hili kwani anakuwa amelikalia kwa hasara yake.
Na ni vigumu kudai fidia hata hivyo,mamlaka husika zinawajibika kutoa taarifa kabla ya kuchukua hatua hiyo. Uzoefu unaonyesha kwamba wakati mwingine nyumba nyingi hubomolewa pale wakazi hao wanapokaidi wito wa kuondoka kwa kutoelewa kwamba hawana haki ya kumiliki maeneo hayo. Lakini pale inapotokea mamlaka za upanuzi wa barabara ukavuka mipaka ya hifadhi yake na akuingilia makazi au miliki za watu waishio maeneo hayo, basi mamlaka hizo zinawajibika kuzingatia sheria ikiwa ni pamoja na kutoa notisi, kusikiliza na kuzingatia pingamizi pamoja na kutoa fidia kwa wahusika.

Hitimisho
Ndugu msomaji, bila shaka umefurahia mfululizo wetu wa maswali na majibu. Matumaini yetu ni kwamba umeelimika na kutambua masuala mbalimbali yahusuyo ardhi, ikiwa pamoja na kujua maana, usimamizi, matumizi na utawala wa ardhi na rasilimali nyingine nchini Tanzania. Tunaamini pia kuwa umepata fursa ya kujua haki na wajibu wako katika kulinda na kutetea rasili mali hizo muhimu ikiwa una maoni, maswali au mchango mwingine wowote katika kuboresha kazi hii uandikie kupitia:

Taasisi ya Utafiti na Utetezi wa Haki za Ardhi (HakiArdhi)
P. O Box 75885
Dar-es-Salaam.
Barua pepe:info@hakiardhi.org
Tovuti: www.hakiardhi.org

Comments