- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Warangi ni warembo hasa.
Na Innocent Nganyagwa
NAWAKARIBISHENI tena kwenye safu yetu ya
mambo ya Asili na Fasili, kama ilivyo ada yetu kila leo ambapo huwa
tunapata fursa ya kutembelea makabila yetu mbalimbali na kujifunza asili na
fasili yao. Tunajifunza mengi juu ya Uafrika na Utanzania wetu halisi kwa
ujumla wake.
Basi kama nilivyowataarifu jana, bado tuko
kwenye eneo lile lile la kaskazini magharibi mwa nchi yetu, tunawatembelea
ndugu zetu Warangi, ambao tumewapigia hodi baada ya awali kuyatembelea makabila
mengine.
Basi kwa faida ya wale ambao hawakubahatika
kusoma sehemu ya kwanza ya simulizi hii ya Warangi juma lililopita, nifanye
muhtasari mfupi juu ya mambo tuliyoyaona halafu tutaendelea na mengine kwa leo.
Tulisema kuwa ndugu zetu hawa wanapatikana
kati ya Babati na Kondoa, lakini kiini chao hasa kikiwa huko Kondoa.
Tumezowea kuwaita Warangi sanjari na lugha
yao ya Kirangi, lakini kwa uhakika
wao kimatamshi halisi ya lugha yao ni ‘Valaangi’ na wanaongea ‘Kilaangi’.
Ndugu zetu hawa katika safari
iliyowafikisha mahali walipo, wamepata kutangamana na makundi kadhaa ya
makabila mengine yakiwemo yale ambayo kwa asili yanazurura muda mwingi wa
maisha yao.
Lakini wamefaulu kubaki kama walivyo, japo
kuna athari ndogo ndogo za lugha yao kimatamshi kama tutakavyoona hapo baadaye.
Baadhi ya makabila hayo wanayopakana nayo
tuliyoyataja jana ni pamoja na Wamaasai ambao wanatokea mbari ya Kinailotiki,
Wasandawe ambao ni Wakhoisan, Wairaqw, Waburunge, Wasi na Wagorowa ambayo ni
makabila ya Kikushi na Wambugwe ambao ni Wabantu.
Lakini, licha ya lugha ya Warangi
kuathiriwa kwa mbali na makabila hayo wanayotangamana nayo na yale mengine
waliyokutana nayo kwenye kipito chao, ndugu hasa wa Warangi si kwa lugha tu
bali hata kwa asili ni Wambugwe.
Jamii za awali za Warangi zinatokea
kaskazini na mashariki mwa bara letu la Afrika, walisafiri kupita eneo la bonde
la ufa wakaingilia Kenya wakitokea Ethiopia.
Ndiyo maana katika kuingia kwao hapa nchini
walifika Babati kwanza, kisha ndiyo wakajisogeza kwenye maeneo mengine hadi
wakafika huko Kondoa.
Safari yao haikuwa rahisi sana, kwanza
ukichukulia umbali waliotoka na pia mabadiliko ya hali ya hewa ukiwemo ukame,
waliokumbana nao kwenye maeneo mbalimbali.
Hali hiyo iliwasababisha wabuni mbinu
mbalimbali za kutafuta maji wakati wa kiangazi, walipofanikiwa kupata maji
katika eneo husika waliamini mahali hapo panafaa kuishi na walilowea.
Kwa hiyo, wenzetu hawa tunaweza kuwaita
kuwa wachimba visima hodari vya kutega maji, maana kwa kawaida walichimba visima
virefu na kutumbukiza vyombo ndani yake.
Kisha waliendelea na safari zao na siku
kadhaa baadaye walikuja kutazama kama vyombo hivyo vina maji, basi wakivikuta
vina maji hufurahi sana na kuamini kuwa sehemu hiyo ina neema na inafaa kuishi.
Kimsingi hawa Warangi walipofika Babati
waligawanyika makundi mawili wakati wakielekea mahali walipo hivi sasa.
Mgawanyiko huo ndiyo ulizaa sehemu mojawapo
ya Wambugwe, kutokana na kutelekezwa na wenzao mahali hapo baada ya kwenda
kuwinda kanga.
Siku moja, vijana hao wa jamii ya Kirangi
walikwenda kuwinda kanga kwenye maeneo ya pembezoni na hapo walipofika, yaani
Babati. Walikawia kurudi na waliporudi hawakuwakuta wenzao, walioendelea na
msafara wao na hivyo wao waliachwa.
Hawakujihangaisha kuwafuata bali waliamua
kubakia mahali hapo, ndipo wakajulikana kwa jina la watu walioachwa kwa sababu
ya kuwinda kanga.
Kwa lugha ya Kirangi ndege huyo aina ya
kanga anayefanana na kuku, huitwa ‘mbuwe’.
Basi wale watu kutoka jamii za Kirangi
walioachwa kwa sababu ya kunogewa kuwinda mbuwe,
wakajulikana kama Wambugwe tangu wakati huo.
Ndiyo maana ukisikiliza lugha ya Kimbugwe
na Kirangi zina maingiliano ya karibu, kulikoni hata yale makabila mengine
niliyokutajia wanayotangamana nayo.
Waliowaacha wenzao ndiyo waliokwenda hadi
huko Haubi, mahali ambapo wakati wanafika walipakuta pana maji ya kutosha
kutokana na vijito vingi vilivyokuwa hapo.
Na kwa kuwa maji ndicho kilichowahangaisha
na kuwafanya wazurure tangu awali, kiasi cha kuchimba visima vya kutega, basi
kwao hapo waliikuta neema waliyoitaka. Ndiyo sababu inayowafanya Warangi wengi
waamini kuwa wanatokea hapo Haubi.
Lakini kwa uhakika kama nilivyokueleza, ni
kwamba jamii zao zimetokea mbali sana kwenye eneo la Wahamitiki.
Nitawafafanulia baadaye juu ya Uhamitiki
huo uliochanganyika na Ubantu wa hawa Warangi.
Basi hapo walipofika kwenye maji ya
kutosha, ndipo walipoweza sasa kuanza shughuli za kilimo cha mahindi na mtama
huko kusini magharibi mwa Kondoa.
Eneo hilo la kiini cha nchi ya Irangi
lilikuwa na vijito vingi vidogo vidogo, lakini baadaye waligundua kuwa kukiwa
na ukame mkali vijito hivyo hukauka.
Lakini hilo halikuwatatiza sana, maana kama
vilijaa tena wakati wa misimu mingine basi wakati ule vijito hivyo vilipokauka,
walitumia ile mbinu yao ya kale kwa kuchimba mashimo marefu kutafuta maji.
Kiini cha nchi yao kina maeneo ya vijiji
mbalimbali kama vile Hurui, Mwaikisabe, Kibaya, Mangoroma, Mafai, Mesanga,
Mnenya, Loo na Iyoli.
Tuliona pia kuwa hawa Warangi kutokana na
jiografia ya eneo lao ilivyo waliishi kwenye makundi bila kupoteza asili yao,
maana kutokana na vilima na miinuko ya uwanda wa nchi hawakuweza kutawanyikia
maeneo ya mbali.
Hata baadhi ya makabila majirani nao
yalikuwa maeneo ya pembezoni, baada ya mwendo wa umbali kadhaa kupitia kwenye
misitu iliyowatenganisha nao.
Kwa mazingira hayo, Warangi ni jamii ya
watu wanaopenda kujiweka karibu mno kwenye mambo yao na hujivunia sana asili
yao na si rahisi kugubikwa na jamii nyingine.
Lakini namna yao ya kulinda hadhi yao ni
kwa upole na si ubabe, maana kati ya makabila yenye sifa ya upole na ukarimu wa
kiwango cha juu, hawa ni wamojawapo.
Mathalan, Mrangi akiongea na Mbugwe
wanasikilizana na kuelewana, lakini Mrangi hapendelei kuongea Kimbugwe, hata
kama anaelewa yanayotamkwa na Wambugwe atajibu kwa Kirangi.
Wenyewe Warangi katika kujivunia mambo yao
hupendela sana kusema kuwa, Kimbugwe ukikisikiliza kinavyoongewa ni sawa na
kumsikiliza mtoto mdogo wa Kirangi anavyojifunza kuongea.
Lakini hawa ni watu wa asili moja,
isingekuwa yale mambo ya kuwinda kanga kama tulivyoona hapo awali, basi pengine
wangeendelea kuwa wamoja.
Ndiyo maana haishangazi kuwa maneno yao
yana muingiliano mkubwa, kama vile ‘ijova’
yaani jua kwa Kimbugwe lakini kwa Kirangi ni ‘ijuva’. Hicho ni Kirangi kilichotumika zamani, maana kwa sasa
unaweza kusikia wenyewe wakiliita jua ‘mwaasu’.
Isikushangaze ndugu Mjadi, maana kama
zilivyo lugha nyingine, istilahi za lugha za makabila hubadilika kutokana na
sababu mbalimbali yakiwemo mazingira na kuchanganyika kwa jamii kwenye eneo
moja.
Mathalan, mwenzenu kabila langu ni Mhehe,
ambapo lugha yetu tunayoongea sasa si ile ya asili hasa.
Tuseme ni kama tunaongea Kihehe cha awamu
ya tatu au ya nne hivi, ndiyo maana ukimsikiliza Mbena au Mzungwa akiongea
lugha yake, utasikia matamshi ya Kihehe chetu cha kale.
Kwa sasa sisi Mungu tunamuita ‘Inguluvi’ lakini kwa Kihehe cha kale ni
‘Kimenya’ sawa na mtu akikupa pole ya
kazi kwa Kihehe akisema ‘makasi’
unajibu ‘aale’. Lakini ukikutana na
baadhi ya wazee wa Kihehe wakikujibu ‘oongo’
neno ambalo bado linatumiwa na Wabena, isikushangaze.
Naam, huo ndiyo uhondo wa kujitambua na
kutambua mambo ya kwenu jinsi yalivyo, na pengine hata kuyajua makabila watani
zako.
Usije siku ukamtania mtu ambaye pengine
huna utani naye kwa asili, (nazungumzia utani wa kijadi), itakusababishia
matatizo!
Basi hawa Warangi kwenye kiini cha nchi yao
ya Irangi, hata kuoana awali ilikuwa baina ya jamii zao wenyewe.
Na kama ilitokea wakaoana na mtu wa jamii
nyingine za pembezoni, basi yule mtu wa jamii ya pembezoni ndiye atakayegubikwa
na silika zao na sio wao kubikwa na silika za ugeni.
Na hata sasa, si tu watakuvutia kwa namna
hiyo, lakini bila kutia chumvi tuseme wazi kuwa ndugu zetu hawa wana maumbile
ya kuvutia sana.
Tena wana rangi mchanganyiko sana, kama
nafsi yako haina ustahimilivu unapokutana na mabibie wambuji (warembo) kwa asili, basi jaribu kukutana na mabibie wa
Kirangi na utanielezea jinsi utakavyogubikwa na ulimbwende wao.
Tukizidi kusonga mbele na mambo ya Warangi,
ni kwamba ndugu zetu hawa kwa asili ni Wabantu wa Kihamitiki.
Ndiyo maana licha ya kuzungukwa na yale
makabila mengine, ambayo mengine walikutana nayo kwenye kipito chao,
hawakubadilika.
Nimeyataja hapo awali kwenye simulizi ya
leo, Wamaasai, Wabarbaig (Wanailotiki), Wasandawe (Wakhoisan), Wairaqw,
Waburunge, Wagorowa na Wasi (Wakushi).
Katika bara hili la Afrika, Wahamitiki
wengi wanatokea upande ambao jamii za awali za Warangi zinakotoka, yaani
kaskazini.
Kuhusiana na mashariki, eneo hilo ni kipito
cha jamii nyingi za upande wa kaskazini zilizokuja huku mashariki na kusini.
Hata baadhi ya Wakushi kama vile Warimi
(Wanyaturu), walipita upande huo pia.
Nimekuwa na kawaida ya kuwafahamisha mara
kwa mara maana ya mbari, ambazo ndizo huzaa makabila. Mbari ni fungu kubwa la
jamii ambalo huzalisha makabila mengi, makabila yanayotokana na mbari moja huwa
na maingiliano mno ya mambo yao ikiwemo lugha.
Afrika kuna takriban mbari zipatazo tano,
Wabantu (ambao kimsingi walitoka kaskazini kabla ya kwenda kusini zaidi na kuja
mashariki na kati kati). Kisha kuna Wanailotiki, Wahamitiki, Wakushi na
Wakhoisan, kwa hiyo sehemu kubwa ya makabila yetu barani hapa yanatokana na
mbari hizo.
Japokuwa pia kuna jamii zilizochanganyika
kutoka mbari tofauti, hivyo kuzaa aina ya watu mchanganyiko sana.
Mathalan, Wanyaturu katika kipito chao kwenda
Singida walichanganyika na Wanyantuzu (Wabantu).
Kwa hiyo, Mjadi usishangae ukikutana na
Mnyaturu anayefanana mno na Mhabeshi, huyo damu yake imeelemea zaidi upande wa
Ukushi.
Kuna Wanyaturu weusi wanene (wamechanganya
Ubantu na Ukushi, kutokana na kuzaliana na Wanyantuzu).
Pia kuna weupe kama Waarabu wa sasa,
(kutokana na maingiliano na Waarabu wa kale ambao nao wamo ndani ya Uhamitiki).
Naam, usichanganyikiwe sana, nilikuwa
nakumegea kidogo kina cha ujadi maana ni kirefu na kuna mambo mengi.
Ila huwa nawazamisha kina hicho mara chache
kutokana na fursa yenyewe, tukizama moja kwa moja naamini kuna baadhi yenu
mtapoteza mwelekeo wa fikra za ujadi.
Lakini ni changamoto nzuri ya utopevu wa
kijadi, basi turudi kwenye mambo ya ndugu zetu Warangi.
Hawa ndugu zetu licha ya kujitahidi
kujilinda dhidi ya kugubikwa na makabila wayanayotangamana nao, lakini
ukisikiliza lugha yao ina baadhi ya athari za makabila hayo.
Si katika ule msingi wa muundo, bali jinsi
Kirangi kinavyotamkwa kinasababisha aina nne za utamkaji wa lugha hiyo.
Hayo mafungu manne yanatokana na maeneo
yao, mathalan, matamshi ya Kirangi cha Kondoa (ambako ni magharibi mwa nchi ya
Irangi) na Haubi (mashariki), muundo wake unafanana kwa karibu sana.
Kwa upande wa pili, matamshi ya Kirangi cha
Kolo (kaskazini magharibi) na Mondo (kusini mashariki), nacho kinakaribiana
kwenye muundo wa matamshi.
Maneno ni yale yale, lakini tofauti ndogo
ndogo ni za namna ya utamkaji, kuna wanaovuta silabi za kimatamshi na wanaokata
silabi hizo.
Hiyo ni moja ya athari za mtangamano na
makabila mengine, kutokana na kuyaambukiza makabila hayo lugha yao.
Kuna makabila yanaongea Kirangi kama vile
ni lugha yao, mojawapo ni Waburunge au ndugu zetu Wasi (Waalagwa). Lakini hivyo
sivyo ilivyo, japo wanaweza kuwa na muingiliano na makabila hayo, lakini nao ni
kabila linalojitegemea.
Hawa ndugu zetu Warangi si wengi sana kwa
idadi japo pia si wachache. Lakini kinachokufanya uwatambue kuwa wapo, ni ile
hali ya kujivunia asili yao. Maana katika sifa yao mojawapo ni kukuza na kupenda
sana kuongea lugha yao.
Mrangi huzoeshwa kumudu kuongea kikwao
tangu akiwa mdogo, kwa wale ambao wazazi wao wanazingatia mambo ya kabila lao.
Hiyo huwajengea hulka ya kujivunia asili
yao, ndiyo maana ukibahatika kufika kwenye maeneo ya kiini cha nchi yao ya
Irangi kule Kondoa kwenye maeneo ya Bereko, Kikilo, Kisese, Masange, Mnenia,
Chandama, Chemba, Goima, Mrijo, Kolo, Soera, Changaa, Thawi, Kingale, Suruke na
Dalai. Au maeneo ya Jangalo, Mondo, Paranga, Bumbuta, Busi, Haubi, Kalamba,
Kwadelo na Pahi unaweza kushangazwa na baadhi ya mambo yao.
Huko tofauti na kwingineko, hata sehemu
wanazofanya biashara zao za mazao, maana wao kwa sasa kwa sehemu kubwa wao ni
wakulima, hutumia sana lugha yao ya Kirangi.
Hawa ndugu zetu hata barua zao hupenda
kuzianza kwa salamu za kikwao, hata maandishi ya mapambo kwenye vyombo vya
usafiri mengi huyaandika kwa Kirangi.
Tukutane kesho kwa simulizi ya kabila
jingine.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Machi 21, 2009.
Comments
Post a Comment