Featured Post

WAHITIMU CHUO CHA MIPANGO WATAKIWA KUWA SEHEMU YA SULUHISHO YA CHANGAMOTO ZA JAMII

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akihutubia wahitimu na wageni waalikwa  katika mahafali ya 31 ya Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) mjini Dodoma.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) amewataka  Wahitimu 3108 wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP)   waliotunukiwa  tuzo zao  katika  Fani mbalimbali kwa mwaka 2016/2017 kuwa sehemu ya suluhisho katika changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi nchini pindi  watakapoanza kuwatumikia wananchi hao na siyo kuwa sehemu ya matatizo katika jamii.

Akizungumza katika mahafali hayo ya 31 ya Chuo hicho yaliyojumuisha Kampasi ya Dodoma na Mwanza yaliyofanyika katika ukumbi wa Mwalimu Nyerere 
Chuoni hapo Maeneo ya Miyuji mjini Dodoma Dkt. Kijaji amesema kuwa elimu waliyoipata wakaifanyie kazi kwa uhalisia wa maisha ya Wananchi waliopo maeneo mbalimbali ili kuliwezesha Taifa kufikia uchumi wa kati hata kabla ya 2025 kama Dira ya Taifa linavyotuelekeza.

‘Wahitimu wetu wana deni, deni hilo ni utumishi uliotukuka. Nendeni mkawatumikie Watanzania nendeni mkairejeshe imani ya Watanzania  iliyoanza kupotea kwa Wataalam wa fani ya Mipango ya Maendeleo Vijijini’. alisema Dkt. Kijaji.

Dkt. Kijaji aliongeza kwa kuwataka Wahitimu hao kwenda kuwafundisha Watanzania kwa vitendo mipango na mbinu thabiti ili waweze kuzalisha kwa tija kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu na ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja.

Aidha Dkt. Kijaji alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli haitokuwa tayari kuwavumilia Wataalamu wazembe makazini na kuwataka wakafanye kazi kwa weledi mkubwa kwa manufaa ya Taifa.

Dkt. Kijaji amefafanua kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha watoto wa kitanzania wanapata elimu bora itakayowaongezea maarifa ili kuwa chachu katika Maendeleo ya Taifa.

‘Serikali inatekeleza majukumu yake kwa vitendo, ndiyo maana mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu inapewa kipaumbele cha kwanza (first charge). Alisema Dkt. Kijaji.

Dkt. Kijaji ametoa wito kwa Taasisi za Elimu ya Juu zote Nchini kutoa mafunzo yatakayowawezesha Wahitimu mbalimbali kuweza kujiajiri pindi wamalizapo masomo yao ili kuongeza kasi ya uchumi nchini.

Katika hatua nyingine Dkt. Kijaji amekipongeza Chuo hicho kwa utoaji wa elimu bora katika fani mbalimbali kwa kuwa idadi ya wanachuo imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka na kwamba huo ni mfano tosha kuwa taaluma inayopatikana katika Chuo hicho ni nzuri na kutoa rai kwa wananchi wengine kuleta watoto wao kupata taaluma mbalimbali.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) Prof. Hozen Mayaya amesema kuwa wameendeleza, kuboresha na kudumisha mahusiano bora kati ya Chuo na wadau mbalimbali.

Prof. Mayaya aliongeza kuwa ushirikiano mzuri wa wadau wao umekuwa kichocheo kikubwa katika kutekeleza majukumu yao makuu ya kufundisha, kufanya utafiti na kutoa huduma za ushauri na uelekezi kwa wadau mbalimbali.

‘Chuo kinajivunia kuongeza udahili wa Wanafunzi 6,129 kwa mwaka 2016/17 kutoka wanafunzi 4,916 kwa mwaka 2015/16 ikiwa ni ongezeko la asilimia 24’. aliongeza Prof. Mayaya.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho Prof. Razack Lokina katika hotuba yake ya kumkaribisha Mgeni Rasmi amesema kuwa Uongozi wa Chuo umeendelea kutekeleza wajibu wake wa kuandaa wataalamu wa mipango ya maendeleo hasa vijijini ambako watanzania wengi wanaishi.

‘Utekelezaji wa wajibu huu umeendana sambamba na kuongeza uwezo wa Chuo katika kutoa mafunzo yanayozingatia umahiri, kufanya tafiti na kutoa huduma za uelekezi katika Nyanja zote za mipango ya maendeleo’. aliongeza Prof. Lokina.

Katika mahafali hayo ya 31 ya Chuo hicho jumla ya wahitimu 3,108, wanawake 1,631 wanaume 1,477 wamehitimu ngazi ya Astashahada, Stashahada, na Shahada za Uzamili.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akiwashudia  wahitimu wakiwa wanavaa  kofia (hawapo pichani) baada ya kuwatunuku tuzo  za fani mbalimbali kwenye mahafali ya 31 ya Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) mjini Dodoma.
Wahitimu wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) wakivaa kofia zao mara baada ya kutunukiwa tuzo  mbalimbali katika mahafali ya 31 ya Chuo hicho mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akimtunuku mhitimu Felista Mayunga Shahada ya Uzamili katika  Uchumi wa Maendeleo katika mahafali ya 31 ya Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (katikati) akiwa na  viongozi wa Chuo na  wageni waalikwa katika picha ya  pamoja na wahitimu wa  Stashahada za Uzamili  na Shahada za Uzamili katika  mahafali ya 31 ya Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) mjini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)

Imetolewa na:
Benny Mwaipaja
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Fedha na Mipango

Comments