Featured Post

MBEGU BORA ZA MIGOMBA, VIAZI LISHE NA MIHOGO KUWAKOMBOA WAKULIMA MKOANI KAGERA

Kaimu Ofisa Kilimo Wilaya ya Muleba,  Kokushubila Pesha akipanda mbegu ya muhogo katika shamba darasa la kikundi cha Ujamaa  lililopo Kata ya Magata Karutanga wilayani humo. 


Ofisa Mtendaji wa kata ya Magata Karutanga Joyce Rassia akizungumza na wakulima wakati wa uzinduzi wa upandaji wa shamba darasa la kikundi hicho.










Mjumbe wa kikundi cha Ujamaa,  Liberatha Lespicius akisoma risala wakati wa uzinduzi huo mbele ya mgeni rasmi.


Mtafiti wa mazao ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo Maruku,  Jojianas Kibula akitoa maelekezo kwa wakulima jinsi ya kupanda mbegu hizo bora za mihogo kwa wakulima wa kata ya Magata Karutanga wilayani Muleba.


Baadhi ya wana kikundi cha Ujamaa wakishirikiana kwenye kupanda mbegu hizo bora baada ya uzinduzi rasmi wa shamba darasa hilo.


Kaimu afisa ugani wa wilaya ya Muleba  Kokushubila Pesha akizungumza na wakulima wakati akizungua shamba darasa hilo kwa niaba ya Mkurugenzi mtendaji wa wilaya hiyo.


Afisa mtendaji wa kijiji cha Omurunazi Edga Rumanyika akitoa neno kwa wageni na wanakikundi cha Mendeleo wakati wa uzindizi wa shamba darasa la Migomba.


Muwakilishi wa mk urugenzi mtendaji wa wilaya ya Muleba Kokushubila Pesha akitoa neno kwa wageni na wanakikundi cha Mendeleo wakati wa uzindizi wa shamba darasa la Migomba.


Wanakikundi cha Maendeleo kwenye kijiji cha Omurunazi wilayani Muleba  wakisikiliza maelekezo na maneno ya viongozi na wataalamu kabla ya kuzindua upandaji wa shamba darasa lao la Migomba kijijini hapo.


Afisa kilimo Mkoa wa Kagera Luois Baraka akizungumza na wakulima wa kijiji cha Omurunazi na kutoa salama za ofisi ya mkuu wa mkoa kwa wakulima hao.


Picha ikionyesha shamba darasa lililoandaliwa na wanakikundi cha Omurunazi kikundi cha Maendeleo kwaajili ya kupanda mbegu safi za migomba iliyozalishwa kwa njia ya chupa.


Mtafiti kutoka COSTECH,  Bestina Daniel akizungumza na wakulima na kuwapa salamu za mkurugenzi mkuu wa COSTECH.


Msaidizi wa katibu wa kikundi cha Maendeleo Sekunda Peter akisoma Risala ya kikundi chao


Mtafiti kutoka COSTECH Beatrice Lyimo akizungumza na wakulima wa kikundi cha maendeleo na kuwaeleza malengo na faida za mbegu hizo wilayani humo.






Muwakilishi wa Mkurugenzi mtendaji wa wilaya ya Muleba Kokushubila Pesha akizungua shamba la kikundi cha Maendeleo kwa kupanda mche wa kwanza wa Mgomba kwenye shamba darasa hilo.
Na Dotto Mwaibale, Muleba, Kagera

Imeelezwa kuwa Usambazaji wa mbegu za mazao ya mizizi na Migomba kwa vikundi vya wakulima kwenye Mkoa wa Kagera utasaidia kuwahakikishia wananchi wa mkoa huo usalama wa chakula na mazao mbadala baada ya zao lao kuu la chakula la mgomba kuathiriwa na ugonjwa wa  mnyauko.

Kauli hiyo imetolewa na Afisa Kilimo Mkoa wa Kagera,  Louis  Baraka wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukamilika kwa zoezi la ugawaji wa mbegu bora za mazao hayo kwenye wilaya tano za mkoa huo ambazo ni Missenyi, Karagwe, Kyerwa, Biharamulo na Muleba.

Alisema kuwa wakazi wa mkoa huo wamekuwa na njaa kali kwa misimu miwili iliyopita  kutokana na zao lao kuu la chakula la migomba kushambuliwa na ugonjwa hatari wa mnyauko na hivyo kuwafanya wananchi kuhangaika kutafuta chakula na kuomba chakula cha msaada kutoka Serikalini.

Baraka alisema kuwa upatikanaji wa mbegu bora za migomba safi iliyozalishwa kwa njia ya chupa itafufua zao hilo ambalo wakulima wengi walishalitelekeza kabisa baada ya kuona zao hilo likikauka na kushindwa kuwapatia chakula walichokizoea kwa miaka mingi.

Aidha Baraka  ameishukuru  Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) na Jukwaa la Bioteknolojia kwa Maendeleo ya Kilimo OFAB kwa kuwapelekea pia mbegu bora za Mihogo aina ya Mkombozi na Mbegu bora za viazi lishe ili kuwapatia wananchi wa mkoa huo mazao mbadala baada ya kutegemea zao la mgomba pekee.

Alisema kuwa kwenye wilaya zote tano za mkoa wa Kagera COSTECH imeweza kuwapatia mbegu za marando ya viazi lishe  30,000, Mihogo mbegu 27,000 na Migomba 1,000, ingawa wameongea na wafadhili hao na kuwaahidi kuwaongeza mingine zaidi ya 500.

Kwa upande wake Mtafiti kutoka COSTECH, Bestina Daniel alisema kuwa mpango huo ni mkakati wa utekelezaji wa majukumu ya tume ya kufikisha matunda ya tafiti mbalimbali zinazofanywa hapa nchini kwa walengwa ili ziweze kuzaa matunda yaliyokusudiwa.

Alisema kuwa baada ya watafiti kumaliza kufanya tafiti zao huziacha kwenye vituo vyao vya utafiti lakini COSTECH inasaidia kuhakikisha tafiti hizo zinatoka kwenye vituo hivyo na kwenda kwa wakulima kama ambavyo wameamua kufanya kwenye zao la 
Muhogo,Migomba na viazi lishe ambavyo vinasaidia kuongeza lishe,usalama wa chakula na kipato.

Bestina pia alibainisha kuwa ili kufikia uchumi wa viwanda ni lazima maandalizi ya upatikanaji wa malighafi kwaajili ya viwanda hivyo yafanyike ili wawekezaji wanapokuja wakute tayari malighafi zipo na hivyo kumhakikishia upatikanaji wa 
malighafi hizo zitokananzo na mazao ya kilimo.

Mtafiti huyo kutoka COSTECH alisema mara viwanda vinapoanzishwa vitasaidia wakulima wengi wa mazao hayo kupata soko la uhakika na kuongeza chachu ya uzalishaji kwakuwa wakulima wengi nchini kilio chao kikubwa ni soko la mazao yao.

Hata hivyo amewataka kuendelea kuzalisha mazao hayo kwa wingi hususani mihogo na viazi lishe kwakuwa soko la kwanza ni wao wenyewe na hata sasa mahitaji ya mazao 

kama vile viazi lishe ni makubwa kwenye kaya na maeneo mengi nchini hivyo wasiwe na shaka na soko kwa sasa.

Akizungumzaia umeuhimu wa vikundi,mashamba darasa hayo ya mbegu Mtafiti kutoka  COSTECH Dkt. Beatrice Lyimo alisema kuwa COSTECH haiwezi kuwafikia wakulima wote kwenye mkoa mzima na kuwagawia mbegu hizo bora lakini kupitia vikundi wakulima  wanaweza kuzizalisha na kasha kugawana kwenda kwenye mashamba yao na baadae kuwapatia na wakulima wengine nje ya vikundi hivyo.

Aliwataka kuzitunza na kuhakikisha zinalindwa maana ni lulu na zimenunuliwa kwa gharama kubwa na endapo watazitunza vizuri baadae wataweza kuwauzia wakulima wengine kwenye maeneo mbalimbali na hivyo kuzifanya zienee kwenye maeneo yote ya 
mkoa huo.

Mtafiti wa Mazao ya Miziz kutoka Kituo cha Utafiti wa kilimo ARI-Maruku cha mkoani Kagera Jojianas Kabula aliwaambia wakulima kuwa hekta moja ya muhogo tani 25 hadi 
32 wakati viazi tani 7 hadi 9 kwa Hekta moja.

Alisema kuwa endapo watafuata kanuni bora za kilimo cha mazao hayo kwa kuzingatia nafasi kati ya mche na mche na mstari kwa mstari na matumizi ya mbolea wataweza kuongeza uzalishaji zaidi tofauti na sasa ambapo kwenye hekta moja ya muhogo tani
nane hadi kumi wakati kwenye viazi wanapata tani moja hadi 3.

Mtafiti huyo alisisitiza kuwa mbegu hiyo ya Muhogo ya Mkombozi imefanyiwa utafiti  na kuonekana kustahimili magonjwa hatari ya mihogo ya batobato kali na michirizi ya kahawia ambayo imekuwa ikiwapatia hasara kubwa wakulima wengini kwa kupoteza hadi asilimia 90 za mazao.

Akizungumzia zao la Migomba Mtafiti wa zao hilo kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo Maruku,  Jasmeck Kirangi alisema mbegu hizo zilizozalishwa kwa njia ya chupa ni safi na hazina magonjwa kabisa na endapo wakulima watazipanda kwenye maeneo safi wataweza kupata mavuno bora kulimo matumizi ya mbegu hizo zao za kawaida.

Aliwaondoa hofu kuwa mbegu hizo walizowaletea ni zilezile za asili zinazopendwa na wakulima wengi kama vile Nshakala hivyo wasiwe na shaka kuwa mbegu hizo zilizozalishwa kwa njia ya chupa sio zile walizozizoea.

Kilangi amesema kuwa mbegu hiyo aina ya Nshakala kama mkulima ataipanda vizuri na kuweka mbolea na kwa kuzingatia nafasi zinazoelekezwa na wataalamu mkulima anaweza 
kupata tani kumi na mbili hadi  ishirini na nne kwa ekari mavuno ambayo kwa sasa wakulima wengi hawafikii.

(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com simu namba 0712727062)



Comments