- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na
Mwandishi Wetu, Kilolo
ZAIDI ya
wakazi 40,000 wa kata tano wilayani Kilolo wanalazimika kutembea umbali mrefu
huku wengine wakiwabeba wagonjwa kwa kutumia machela ili kuwafikisha kwenye
vituo vya afya.
Uchunguzi
uliofanywa umeonyesha kwamba, wananchi wa Kijiji cha Makungu
kilichopo Kata ya Ukwega, yenye wakazi 12,195, wilayani humo wanalazimika
kuwabeba wagonjwa kwa kutumia machela kwa zaidi ya kilometa 15 kuwafikisha kwenye zahanati iliyopo
Kijiji cha Ipalamwa.
“Changamoto
hii imegharimu uhai wa wenzetu waliopoteza maisha kabla ya kufika zahanati au
vituo vya afya huku wajawazito wakilazimika kuhama makazi yao kwa mwezi mzima
ili kusogea jirani na huduma za afya hasa Hospitali Teule ya Ilula iliyopo
umbali wa kilometa 60,” alisema Brown Kikoti, mkazi wa kijiji hicho.
Kikoti
alisema, wananchi wasio na uwezo hutumia zahanati ya Isagwa iliyopo umbali wa kilometa
10 kutoka kijijini hapo, ambako hata hivyo, hakuna huduma za uhakika.
Fredy
Nyaulingo alisema wenye magari wamekuwa wakiwatoza Shs. 280,000 ili kuwapeleka
wagonjwa katika Hospitali Teule ya Ilula, kiwango ambacho wananchi wengi
wanashindwa kukimudu.
Alisema
hali hiyo inasababisha wananchi wengi kutumia miti shamba katika kujitibu, huku
wajawazito wakijifungulia njiani baada ya kuanza kuumwa uchungu kabla ya siku
walizokadiriwa kujifungua kufika.
“Tatizo
hili la kukosekana kwa usafiri na umbali wa huduma ya afya linasababisha
wajawazito kujifungulia njiani, wengine wamekuwa wakipoteza watoto,” alisema
Nyaulingo.
Japhet
Mlwale, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Makungu, alisema ubovu wa barabara ni
sababu kubwa ya magari kushindwa kufika kijijini hapo hasa kutokana na
jiografia ya eneo hilo kuwa lenye milima mikali na mabonde, huku msimu wa mvua
kukiwa na utelezi.
“Barabara
zetu kama mlivyoziona ni hatari, hazina matengenezo yoyote, kwani zingekuwa
zinapitika wenye magari wangeweza kuleta usafiri, lakini wanahofia hali ya
usalama hasa msimu wa mvua,” alisema Mlwale.
Wakati
hali ikiwa hivyo katika kijiji hicho, wananchi wa kata za Kimala, Idete na
Masisiwe nao wanakabiliwa na changamoto za aina hiyo kutokana na kukosekana kwa
usafiri kunakosababishwa na ubovu wa barabara.
Eliya
Nyamoga, mkazi wa Kimala wilayani humo, alisema ili kumfikisha mgonjwa kwenye
Kituo cha Afya cha Kidabaga ni lazima mwananchi achangie Shs. 70,000 ‘za
mafuta’ kwa gari la kituo hicho, ambazo hata hivyo hazikatiwi stakabadhi.
“Usipotoa
fedha hizi hawawezi kumbeba mgonjwa, sasa kwa wananchi wa kawaida wanaotegemea
zaidi kilimo watapata wapi fedha hizo?” alihoji.
Herieth
Paschal Mponzi, mkazi wa Masisiwe, alisema ukosefu wa barabara unawanyima fursa
muhimu ya usafiri ambapo inapotokea mgonjwa amezidiwa, hulazimika kukodi gari
kutoka Kituo cha Afya Kidabaga kwa kiasi cha Shs. 80,000.
Kwa
mujibu wa Sensa ya Mwaka 2012, Kata ya Ukwega ina
wakazi 12,195, Kata ya Idete ina wakazi 8,059, Kata ya Masisiwe ina wakazi
10,053 na Kimala ina wakazi 7,649, ambapo maeneo yote yanakabiliwa na
changamoto hizo za usafiri na huduma za afya.
Taarifa kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Wilaya ya Kilolo zinasema, wilaya hiyo ina jumla
ya zahanati 50 tu kati ya vijiji 106 vilivyopo, huku vituo vya afya vikiwa
viwili na hospitali teule moja ambayo ipo chini ya shirika la dini.
Inaelezwa kwamba vijiji vingi wilayani humo vinaonja adha ya upatikanaji wa huduma hiyo muhimu
ya afya na akasema wilaya ina magari mawili tu ya kubebea wagonjwa (Ambulance)
ambapo moja ni la Kituo cha Afya Kidabaga na lingine la Hospitali Teule ya
Ilula.
“Kweli
wilaya yetu ina upungufu mkubwa wa vituo vya tiba, mfano katika tarafa nzima ya
Kilolo hakuna kituo hata kimoja cha afya, tatizo hili linasababisha wananchi
kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo, lakini hata upande wa usafiri pia
tuna changamoto, kwani tuna magari mawili pekee ya kubeba wagonjwa,” zimesema taarifa hizo.
Imetayarishwa
na www.maendeleovijijini.blogspot.com.
Simu: +255 656 331974.
Comments
Post a Comment