- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Unknown
on
- Get link
- Other Apps
John Bosco, nyanda wa
Simba.
Na Daniel Mbega
SIMBA, siyo tu kwamba
iliokoka na kuteremka daraja msimu huo ukiwa ni msimu wa pili mfululizo
kunusurika, bali ushindi wao wa magoli 2-1 dhidi ya mahasimu wao wakubwa, Yanga
Jumamosi Julai 23, 1988 mwaka huo kwenye Uwanja wa Taifa uliifanya ilinde hadhi
yake. Mchezo huo ulikuwa ni wa marudiano wa Ligi Daraja la Kwanza Tanzania
Bara, ambapo katika mchezo wa kwanza timu hizo zilifungana 1-1.
Kwa Coastal Union
kuchapwa magoli 2-0 na African Sports siku hiyo, Yanga ilihitaji sare tu ili
iweze kutetea ubingwa wake, lakini timu ya Tanga pamoja na kipigo hicho
ilifanikiwa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara kwa tofauti ya idadi ya magoli ya
kufunga. Yanga na Coastal zilikuwa na pointi 26 kila moja, lakini Coastal
ilikuwa na magoli 27 na Yanga ilikuwa na magoli 24.
African Sports
ilishika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 26 pia lakini ilikuwa na magoli 23 ya
kufunga. Timu hii, hata hivyo, iliingia kwenye Ligi Kuu ya Muungano na
kufanikiwa kutwaa ubingwa wa Tanzania nzima mwaka huo. Simba ilikuwa ya tatu
kutoka mwisho ikiwa na pointi 20.
Baada ya John
Makelele kufunga goli la ushindi mapema katika kipindi cha pili, Yanga
ilishindwa kuuvunja ukuta wa Simba. Mashabiki wa Simba walikuwa na furaha kubwa
jioni hiyo, kwani kwa msimu wote hawakuwa na imani kama timu yao ingeweza kunusurika
isishuke daraja.
Siku hiyo vijana hao
wa Msimbazi walionyesha mpira mzuri na ari ya ushindi ilikuwepo tangu mwanzo.
Yanga ilichanganyikiwa sana siku hiyo baada ya kutamba kwamba wangeifunga Simba
kwa kuwa timu hiyo msimu huo ilikuwa dhoofulhali, lakini wakajikuta wakiwa
katika wakati mgumu sana.
Hadi mapumziko timu
hizo zilikuwa zimefungana 1-1, kama walivyofanya katika mchezo wa kwanza Aprili
30, mwaka huo. Kama ilivyokuwa katika mchezo wa kwanza, Edward Chumila tena
ndiye aliyeanza kufunga goli la Simba katika dakika ya 21. Malota Soma
alimhadaa mlinzi wa Yanga kwenye wingi ya kulia na krosi yake ilisogezwa kidogo
tu na walinzi wa Yanga na hivyo kumwezesha Chumila kufunga kirahisi baada ya
kufumua shuti kali mara mpira ulipodunda.
Dakika tisa baadaye
mwamuzi Msafiri Mkeremi aliinyima Simba penati ya wazi baada ya Godwin Aswile
wa Yanga kuunawa mpira huo ndani ya eneo la hatari. Badala yake Mkeremi
akaamuru ipigwe ‘free - kick’ kuelekea goli la Simba, huku mashabiki wa Simba
wakiwa hawaamini.
Mpaka wakati huo
Yanga haikuonyesha kama ilikuwa inajiamini na mara nyingi ilikuwa ikitumia
mbinu za kuotea kuwavunja nguvu washambuliaji wa Simba. Katika dakika ya 36
Yanga ilifanikiwa kusawazisha goli hilo kupitia kwa nahodha Issa Athumani
aliyemzidi ujanja Mkandawire kabla ya kuunganisha wavuni kwa kichwa krosi ya
Athumani China. Mkandawire akabaki chini amelala asiamini yanayotokea langoni
mwake.
Bao hilo liliwapa
imani Yanga na mchezo ungeweza kuwa hivyo kama siyo makosa ya kipa Sahau Kambi
wa Yanga yaliyowapa ushindi Simba katika dakika ya 58. Kambi aliuona mpira wa
kichwa wa Malota Soma hauna madhara sana, akaudharau, lakini ghafla akatokea
Makelele aliyeukwamisha wavuni kabla haujamfikia kipa huyo.
Pamoja na jitihada
zote, ngome ya Simba ikawa makini zaidi kulinda bao lake. Mwamuzi Msafiri
Mkeremi kutoka Tabora hakuweza kutoa hata kadi moja katika mechi hiyo.
Mgeni rasmi katika
pambano hilo alikuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga
Taifa, Dk. Salim Ahmed Salim. Viongozi wengine waliohudhuria ni pamoja na Spika
wa Bunge, Chifu Adam Sapi Mkwawa, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii,
Utamaduni na Michezo, Zahra Nuru na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo (BMT),
Hamza Kasongo. Jumla ya watazamaji 30,000 walihudhuria pambano hilo.
YANGA: Sahau Said Kambi, Fred Felix/Yusuf Bana, Kenneth Mkapa,
Godwin Aswile, Lawrence Mwalusako, Athumani China/Abdallah Burhani, Justin
Mtekele, Said Mwamba ‘Kizota’, Issa Athumani, Dennis Mdoe na Celestine Mbunga.
SIMBA: John Bosco, Raphael Paul, Twaha Hamidu, Deo Njohole ‘OCD’,
Pazi Ally, Daniel Muhoja, John Makelele, Adolf Kondo/Francis Mwikalo, Edward
Chumila na Augustine Haule.
NB: Makala haya ni kutoka kwenye
miswada ya vitabu vya 'VUTA-NIKUVUTE: SIMBA NA YANGA' na ‘UBINGWA WA SOKA
TANZANIA’ vya mwandishi Daniel Mbega, ambavyo viko katika hatua za mwisho
kuchapishwa. Ukirejea ni lazima eleze chanzo ambacho ni www.maendeleovijijini.blogspot.com.
Comments
Post a Comment