Featured Post

HII NDIYO ‘THRILLER IN NYAMAGANA’ ILIYOSABABISHA SHABIKI WA SIMBA AJITOSE KWENYE PIPA LA POMBE YA MOTO NA KUFA MWAKA 1974

Kipa wa Simba, Athumani Mambosasa, akiunyaka mpira huku akitazamwa na Kitwana Manara 'Popat' wa Yanga (kushoto).

Kikosi cha Yanga cha mwaka 1973 kabla Dk. Victor Stanculescu (wa pili kushoto) hajaondoka. Anayeongea na wachezaji na meneja wa timu, Shiraz Sharrif. Wengine ni Hassan Gobbos, Kitwana Manara, Maulid Dilunga, Sunday Manara, Elias Michael, Boi Idd 'Wickens', Selemani Said, Gibson Sembuli, Omar Kapera, Ally Yussuf, Abdulrahman Juma (nahodha).

Na Daniel Mbega
KWA wenye kumbukumbu nzuri bila shaka kipigo cha Nigeria cha magoli 2-1 toka kwa Italia katika raundi ya pili ya Kombe la Dunia huko Marekani mwaka 1994 kiliwarudisha mapema miaka ya 1970 pale Yanga ilipoichapa Simba magoli 2-1 kwenye fainali ya Ligi ya Taifa ya Soka kwenye Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.
Nasema huenda kumbukumbu hiyo ikawa imejitokeza kufuatia kufanana kwa kiasi kikubwa kwa matokeo hayo, hasa muda, yaani ‘timing’, magoli hayo yalipopatikana.
Katika mchezo wa Nigeria na Italia Alhamisi ya Julai 14, 1994, Nigeria ilikuwa ikiongoza kwa goli moja ililolipata mapema kunako dakika ya 26 hadi dakika ya 87 Roberto Baggio alipoisawazishia Italia na kuufanya mchezo huo uingie kwenye muda wa nyongeza.
Kisha kwenye dakika ya 11 ya muda wa nyongeza, Baggio tena alifunga goli la penati na kuiondoa Nigeria mashindanoni. Ndivyo ilivyokuwa kwenye mchezo wa Simba na Yanga wa mwaka 1974.
Pengine watu watajiuliza kwa nini Simba na Yanga zilipambana kwenye Uwanja wa Nyamagana, Mwanza badala ya Karume au Taifa mjini Dar es Salaam zinakotoka timu hizo. Kwa kweli hili lilikuwa pambano lao la kwanza la Ligi ya Taifa kufanyika nje ya Dar es Salaam.
Mashindano ya kutafuta klabu bingwa nchini mwaka 1974 yalifanyika kwenye Uwanja wa Nyamagana, Mwanza tangu Julai 18 hadi Agosti 10, 1974. Timu maarufu zilikuwepo pamoja na nyingine ngeni. Timu hizo maarufu zilikuwa Yanga na Simba za Dar es Salaam, Nyota ya Mtwara, Mwadui ya Shinyanga na Jumuiya ya Arusha. Halafu ikatokea timu mpya kabisa huko mkoani Dodoma iliyoitwa Ntomoko. Timu nyingine za mwaka huo zilikuwa ni za kazini. Hakukuwepo na timu kutoka Zanzibar msimu huu.
Hata hivyo, upinzani mkubwa kwenye ligi hiyo ulikuwa kati ya Simba na Yanga, watani wa jadi wa soka nchini. Wakati huo Simba walikuwa mabingwa baada ya kuwafunga Lake Stars ya Kigoma magoli 2-0 mwaka 1973 kama tulivyoona huko nyuma. Watu walikuwa wanajiuliza nani angeibuka bingwa mwaka 1974 hasa ikizingatiwa kwamba, Yanga ilifungwa na Simba goli 1-0 kwenye nusu fainali mwaka 1973.
Kwa matayarisho kabla ya mashindano hayo, Simba walikwenda kuzuru Poland nao Yanga walikwenda Brazil, ambako walikutana na Mfalme wa Soka Duniani, Edson Arantes do Nascimento ‘Pele’. Katika timu zote zilizokuwemo kwenye mashindano hayo hakuna hata moja iliyokuwa na matayarisho makubwa kama Yanga na Simba.
Simba na Yanga zilifanikiwa kuingia fainali baada ya kuzichabanga timu nyingine kwenye michuano ya awali ya mtoano. Pambano hilo la mwisho na la kihistoria lilifanyika Nyamagana Jumamosi Agosti 10, 1974.
Siku hiyo Uwanja wa Nyamagana ulifurika watu isivyo kawaida. Mashabiki walitoka sehemu mbalimbali za nchi - Arusha, Moshi, Tanga, Dodoma, Dar es Salaam, Tabora, Shinyanga, Kigoma, Morogoro, Mara na Kagera. Hao ni licha ya wale waliotoka kwenye vitongoji vya Mwanza. Ilipofika saa 10.30 jioni hapakuwa na nafasi ya kukaa mtu hapo uwanjani, ingawa wengine walikuwa wanaendelea kumiminika.
Mchezo ulianza kwa nguvu ingawa Yanga walianza pole pole kidogo wakijaribu kuusoma mchezo wa Simba. Baada ya dakika tano tu matokeo ya nguvu hizo yalionekana. Saad Ally wa Simba aliumia baada ya kugongana na Gibson Sembuli wa Yanga na akatolewa nje. Adamu Sabu aliyeingia badala yake, aliwafurahisha wapenzi wa Simba, kwani aliifungia goli timu yake katika dakika ya 16.
Yanga walijaribu sana kukomboa goli hilo lakini walipata taabu kwani ukuta wa Simba ulikuwa imara sana. Kadiri mchezo ulivyoendelea watu walidhani Yanga isingepata hata goli moja na kwamba, siku hiyo ingefungwa tena, kwani hadi mapumziko matokeo yalikuwa ni yale yale ya goli moja kwa Simba na Yanga wakiwa na gurudumu.
Katika dakika ya 87 ya mchezo, yaani dakika tatu kabla ya mchezo kumalizika, mambo yalibadilika. Ilikuwa ni golikiki, ambapo mlinzi wa Yanga, Ally Yussuf, alipiga mpira kuelekea golini kwa Simba. Mpira huo ulipita juu ya vichwa vya wachezaji kadhaa wakiwemo Abdallah Kibadeni wa Simba na Gibson Sembuli na Sunday Manara.
Mpira huo uliambaa ambaa kuelekea goli la Simba ambako Kitwana Manara, aliyekuwa amebanwa mno na beki wa Simba ambaye hakutaka mchezo, Omari Chogo ‘Chemba’, licha ya kuwa ameupa mgongo mpira huo aliruka na kupiga kichwa kushoto kwake.
Moja kwa moja mpira huo uliingia kwenye ‘anga’ za nambari nane wa Yanga, Gibson Sembuli, aliyeujaza wavuni kwa shuti kali la ugoko, lililoingilia kwenye kona ya kushoto na kumuacha kipa Athumani Mambosasa, aliyekuwa ametoka kumkabili mchezaji huyo, akiwa hana la kufanya zaidi ya kuutumbulia macho mpira huo ukitinga wavuni kuandika goli la kusawazisha kwa Yanga. Hivyo, hadi mwisho wa dakika 90 za kawaida za mchezo matokeo yalikuwa 1-1.
Goli hilo likabadilisha kabisa sura ya mchezo. Watazamaji ambao walianza kuondoka uwanjani wakidhani Yanga wameshindwa walikimbilia uwanjani kuangalia mchezo tena. Dakika 90 zilipokwisha ubao wa matokeo ukasomeka Yanga 1 Simba 1 na ndipo dakika 30 zilipoongezwa ili kupata mshindi.
Katika dakika ya saba ya muda wa nyongeza, mlinzi Ally Yussuf wa Yanga aliipangua ngome ya Simba na kutoa pasi ya juu kwa mchezaji wa kiungo wa Yanga, Sunday Ramadhan Manara, aliyefunga goli la pili kwa kichwa. Goli hilo likawa la ushindi kwa Yanga baada ya Simba kushindwa kusawazisha kwa dakika 23 zilizokuwa zimesalia.
Hili ni pambano lao la kwanza la ligi kumalizika baada ya muda wa kawaida, yaani ndilo pambano pekee kwa wakati huo lililokuwa limechezwa kwa dakika 120. Mapambano mengine manne huko nyuma yalikuwa yamevunjika kabla ya muda wake na siyo zaidi ya muda wake.
Ikawa Yanga wamechukua ubingwa wa Tanzania kwa ushindi wa magoli 2-1 na kuinyang’anya Simba iliyoutwaa mwaka 1973 kutoka kwao. Kombe hilo lilikabidhiwa kwa nahodha wa Yanga wa wakati huo, Abdulrahman Juma na aliyekuwa mgeni rasmi Meja Jenerali Mrisho S.H. Sarakikya mbele ya mashabiki takriban 50,000 waliohudhuria.
Ilielezwa kuwa, sababu kubwa iliyoifanya Simba isalimu amri ni ukweli kwamba, haikuwa na stamina ya kumudu kucheza dakika 120 wakati ambapo watani wao, Yanga, walikuwa na uwezo huo na kufanikiwa kufunga magoli safi yaliyotinga wavuni katika staili ambayo ingemshinda golikipa yoyote kuzuia, ingawa baadhi ya wachezaji wa Simba walikaririwa baadaye wakimlaumu kipa wao Mambosasa kwamba, aliwafungisha kwa uzembe.
Kadiri mchezo ulivyokuwa ukisonga mbele ilijidhihirisha kuwa Yanga walistahili ushindi huo ukitilia maanani jinsi mashambulizi yalivyoielemea Simba. Mtu aliyeivunja nguvu kabisa ngome ya Simba alikuwa mshambuliaji hodari nambari tisa, Kitwana Manara, aliyekuwa na mazoea ya kutegea mbele anakobaki na beki mmoja tu, na ambaye kwenye mechi hiyo alikuwa Chogo. Haikuwa ajabu pale beki huyo alipotolewa nje baada ya mambo kumzidia uwanjani.
Katika pambano hilo, golikipa wa Yanga, Elias Michael aligongana na Willy Mwaijibe wa Simba katika dakika ya 70 na wote wawili wakakimbizwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Bugando. Nafasi zao zilichukuliwa na Muhidin Fadhil kwa upande wa Yanga na Kessy Manangu kwa upande wa Simba.
Simba walifanya faulo 17 dhidi ya wachezaji wa Yanga, nane zikiwa katika kipindi cha kwanza, wakati ambapo Yanga ilicheza faulo 18, 10 zikiwa katika kipindi cha kwanza, ambacho kwacho Simba ilitawala zaidi kiasi cha Yanga kulazimika kutumia, japo kwa kiasi kidogo, uamuzi wa ‘Aende mtu mpira ubaki, au uende mpira mtu abaki’.
Aidha, katika mchezo huo, Yanga ilitumia zaidi mchezo wa kuotea (offside trick) na kuwafanya wachezaji wa Simba waotee mara 15 wakati wale wa Yanga, kwa kutowekewa mtego kama huo, walijikuta wakiotea takribani mara mbili tu.
Udhaifu wa Simba kwenye kufunga magoli ulionekana kwenye upigaji mipira ya kona, ambapo ilipata kona sita bila hata moja kutinga wavuni. Yanga ilipata kona mbili zote katika kipindi cha kwanza, na kwa jinsi zilivyolikosakosa goli la Simba, huenda magoli zaidi yangetinga kama ingepata kona zaidi.
Shabiki mmoja wa Simba huko Nzega aliamua kujitumbukiza kwenye pipa la kirusu cha pombe kilichokuwa jikoni na kufa wakati Yanga iliposawazisha bao. Kiingilio cha juu siku hiyo kilikuwa shilingi 30.
Timu zilipangwa hivi:-
YANGA: Elias Michael/Muhidin Fadhil. Ally Yussuf, Selemani Saidi, Hassan Gobbos/Boi Iddi ‘Wickens’, Omari Kapera, Abdulrahman Juma (nahodha), Bona Max Mwangi, Sunday Manara, Kitwana Manara, Gibson Sembuli na Maulid Dilunga. Kocha: Tambwe Leya (Zaire)
SIMBA: Athumani Mambosasa, Shaaban Baraza, Mohammed Kajole, Athumani Juma, Omari Chogo, Omari Gumbo, Willy Mwaijibe/Kessy Manangu, Haidari Abeid ‘Muchacho’ (nahodha), Saad Ally/Adamu Sabu, Abdallah Kibadeni, Abbas Dilunga. Kocha: Paul West Gwivaha.
Mgeni rasmi, alikuwa Meja Jenerali Mrisho S.H. Sarakikya.

NB: Makala haya ni kutoka kwenye miswada ya vitabu vya 'VUTA-NIKUVUTE: SIMBA NA YANGA' na ‘UBINGWA WA SOKA TANZANIA’ vya mwandishi Daniel Mbega, ambavyo viko katika hatua za mwisho kuchapishwa. Ukirejea ni lazima eleze chanzo ambacho ni www.maendeleovijijini.blogspot.com.

Comments