Featured Post

SIKU DUNIA ILIPOMPOTEZA MTUNZI WA KIBAO CHA 'NZINZI' NA MCHAWI WA KIDEKUNE’ NA 'KIWANZENZA'

Mwandishi wa makala hii, Daniel Mbega (kushoto) akiwa na King Kester Emeneya katika iliyokuwa Hotel Embassy mwaka 2000.


Na Daniel Mbega
NAYAKUMBUKA maneno yake tukiwa katika Hotel 77 jijini Arusha, siku ya Ijumaa, Novemba 24, 2000, akiniambia kwa Kilingala: “Mdogo wangu Danny, nimemaliza fedha zote na sina cha kukupa kwa sababu nilikuja Tanzania kurekodi video ya albamu na nimeshakamilisha, sasa nataka niondoke na wewe twende Paris, halafu utatafuta chuo usome, ukimaliza utachagua mwenyewe urudi Tanzania ama utafute kazi huko!”
Namzungumzia mwanamuziki nyota wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Jean Baptiste Emeneya Mubiala Kwamambu ambaye alifahamika zaidi kama King Kester Emeneya, kiongozi wa bendi ya Victoria Eleyson.

Urafiki wetu ulivuka mipaka na kuwa udugu, ambapo kila wakati hakuniita ‘Mwandishi’, bali hata alipokuwa hanioni alipenda kuuliza: “Petit na ngai Danny eza wapi?” Akimaanisha “Mdogo wangu Danny yuko wapi?”
Siyo kwa sababu ya kuwa naye bega kwa bega kwenye kazi zake akiwa hapa nchini, ambako alikuja mara mbili, lakini pia alisema wazi kwamba nilifanana mno na mdogo wake wa damu.
Hakuwa na mzaha aliponiambia kuhusu suala la kwenda naye Paris, maana pale pale akamwita meneja wake, Guy Kimvula, na kumwelekeza kwamba afanye booking Nairobi, Kenya pamoja na jina langu, maana ndiko walikokuwa wanaondokea kurudi Paris, ingawa ilikuwa lazima warudi kwanza Dar es Salaam ilikokuwa mizigo yao na ndiko wangechukua ndege kuelekea Nairobi kabla ya kwenda Ufaransa.
“Una passport!” akaniuliza tena kwa Kilingala, nikamwambia: “Ninayo lakini iko nyumbani Dar es Salaam.”
“Hakuna shida, tunaondoka leo kwenda Dar es Salaam, keshokutwa itabidi twende Nairobi na mipango mingine yote tutakamilisha huko. Lakini tukifika Paris mimi nitakuacha pale nakwenda New York, Marekani nina shoo huko, nitarejea baada ya wiki mbili,” akaniambia.
Alikuja mara ya kwanza mwezi Julai 2000, kimya kimya, halafu naweza kusema ni mimi mwandishi peke yangu niligundua ujio wake kwa sababu hakupenda yeyote ajue. Nikafanya naye mahojiano pale Embassy Hotel – wakati huo ikiwa juu zaidi, na tangu hapo tukajenga urafiki uliokuwa kama udugu. Pengine ni kutokana na kuifahamu vyema historia yake na maswali niliyokuwa nikimuuliza, kwani mambo mengine, hasa yaliyomuumiza katika maisha yake ya muziki, ni wazi hakupenda kuyakumbuka na hakujua kama kulikuwa na mtu nchini Tanzania ambaye alikuwa anayafahamu.
Alifahamu kwamba watu walikuwa wanajua kuwa yeye alikuwa mmoja wa wanamuziki waliounda kundi la Les 7 Patrons de Langa Langa Stars (Wakali Saba wa Langa Langa Stars), lakini swali kwamba ilikuwaje yeye alifumu na kundi hilo kwa wiki mbili tu mara baada ya kuanzishwa, kamwe hakulitegemea.
Wakati ulipotokea mgogoro wa uongozi na mapinduzi ambayo hayakufanikiwa ndani ya Viva la Musica mwaka 1981 huku yeye akiwa kipenzi cha Papa Wemba katika safu ya uimbaji na Koffi Olomide akiwa kinara wa utungaji, Emeneya aliondoka pamoja na Esperant Djenga Ka, Djuna Djanana na Dindo Yogo kwenda kuungana na Evoloko Jocker, Djo Mali na Bozi Boziana (watatu hao kutoka Zaiko Langa Langa) na kuanzisha kundi hilo la 7 Patrons Langa Langa Stars.
Hata hivyo, yeye alidumu kwa wiki mbili tu, halafu akarejea Viva La Musica kabla hajaondoka kwa mara nyingine Desemba 24, 1984 na kuanzisha bendi yake ya Victoria Eleyson.
“Wewe umejuaje?” aliniuliza wakati huo. “Najua ulikuwa mdogo wakati huo!”
Nilimwambia kwamba, mimi nilikuwa mfuatiliaji mkubwa wa muziki wa Congo na zaidi nilikuwa shabiki namba moja wa nyimbo zake, kuanzia ‘Nzinzi’ na hata alipotoa albamu yake ya Polo Kina mwaka 1992 na mtindo wake wa Kidekune.
Naam. Namkumbuka kwa namna alivyoishi hata na wanamuziki wake kama familia moja, siyo mwajiri na mwajiriwa. Alikuwa kama baba kwa wanamuziki wake, wengine wakimfanya kama babu kutokana na kumtania.
Ungemuona wala usingejua kama ni mzungumzaji. Ndiyo, hakuwa mzungumzaji sana, bali mtu wa vitendo, lakini alipoamua kupiga stori, hasa kama ‘mnaiva’, basi ungependa. Siku zote alikuwa mtu wa mipango.
Wakati tunazungumza hapo 77 Hotel Arusha, tayari alikuwa amekamilisha kurekodi video ya albamu yake ya Longue Histoire (Hadithi Ndefu) iliyokuwa na Volume I na II ambayo ilirekodiwa na Calbass' Productions ya Paris, ambapo niliongozana naye kwenda Bagamoyo, Zanzibar na maeneo mengine ya Dar es Salaam kabla ya kwenda Moshi na Arusha.
Volume I ilikuwa na nyimbo za But Na Filet, Maousso, Washington, Lilas, Noni, Cigarette, Beatrice, Mimo na Mobeti Mbonda, wakati Volume II ilikuwa na nyimbo za Mademoiselle, Kimpiabi Bala, Didier Okito, Mamie, Mvula Mitano, Fololo, Basali Nteke, Pierroccini, Yo Ba Mbongo.
Ni wakati huo alipokuwa ameibuka na rap mbili mpya za Chakou Libondasi na Kiwanzenza kupitia kwa marapa wake Eric Masudi na Guy Moller.
Ni rap ambayo Ally Choki akiwa African Stars 'Twanga  Pepeta' aliamua kuichukua na kuweka maneno ya Kiswahili anaposema: "Tunatesa, Twanga Pepeta, hatutaki shari!" wakati Guy Moller alikuwa anasema: "Kiwanzenza, kiliba yaye eee kalika libonge!"
Ukiitazama DVD ya albamu hiyo utaona kwamba hata mwanadada aliyeigiza kwenye wimbo wa ‘Mousso’ ni Mtanzania, na wanamuziki wake walivalia mavazi ya Kimasai na kadhalika.
Picha iliyochukuliwa katika clip ya wimbo wa Mousso ambapo wanaonekana rapper Guy Moller, King Kester, Binti wa Kibongo na mwenye rasta na koti jeusi ni Zoe Bella, kaka wa Christian Bella.

Wakati tuko Arusha, siku hiyo asubuhi ilikuwa twende Mirerani kwa ‘Wazungu wa Mawe’ ambao walitaka kwenda kutumbuizwa, lakini alipiga hesabu na kuona kwamba ratiba yake ingembana, hasa kutokana na ziara ya New York na alikuwa pia aende Japan baada ya kutoka Marekani.
Nimepata kusafiri na wanamuziki wengi nyota wa kimataifa, lakini kusafiri na kundi la Victoria Eleyson kulikuwa tofauti sana. Wanamuziki wote walikuwa kama ndugu, tulizungumza na kucheka bila wasiwasi kwa sababu lugha ya Kilingala haikuwa kikwazo kwangu. Hili nalo liliwafanya wanamuziki wote wasiamini hata nilipowaambia kwamba mimi ni Mtanzania.
Zoe Bella, kaka yake Chritian Bella, yeye mpaka anaondoka ananimbia: “Wewe mutu ya Kisangani, siyo Mutanzania!”
Alikuja na wanamuziki wake wengi ambao alikuwa amedumu nao kwa muda mrefu ingawa wengine walikwishaondoka. Lakini miongoni mwa aliokuja nao, ukiacha mwimbaji Zoe Bella, Erick Masudi na Guy Moller, ni mpiga kinanda Djudjo Chet Music, waimbaji Anthony Sampayo, Sweet Elesse, Denison Lutula, Spino Nola, Dikando Bols, Guejo Star Gelena, wapiga magitaa Auguy Lutula, Willy Ebondaki, Ade Lokela na Zozo Malaba, pamoja na mpiga bass Yves Tshum Tshum, mpiga konga Signora Depatra Uomo na mpiga drums Baby Mbonda.
Mara kadhaa alipokuja Kinshasa, alikuwa akiniagiza niende kumtembelea.
Lakini, kama alivyosema Joseph Kabasele Yampanya ‘Pepe Kalle’, “Liwa ya Moyibi”, yaani “Kifo ni mwizi!” Hakika kifo si kitu kizuri kabisa hapa duniani japokuwa kila nafsi lazima ionje mauti. Kama kilivyofanya kwa  Pascal Emmanuel Sinayomi maarufu kama Tabu Ley Rochereau ndivyo kilivyofanya kwa Emeneya, mwanamuziki mkongwe, msomi na mahiri, pale kilipomchukua akiwa kitandani jijini Paris, Ufaransa Alhamisi ya Machi 26, 2014.
Jeneza lililokuwa na mwili wa King Kester Emeneya wakati wa kuagwa jjijini Kinshasa.

Mwanamuziki huyo aliiacha dunia ikiwa na amali zake nyingi ambazo zitakumbukwa milele na wapenda muziki tangu wa rhumba hadi ule wa kimataifa wenye mahadhi ya kizazi kipya (funky).
Nakumbuka nilipofanya naye mahojiano mwaka 2000, alitamka wazi kwamba wanamuziki wengi wa Congo alimtukana sana mwaka 1987 wakati alipoibuka na wimbo wa ‘Nzinzi’.
Maneno ya kwenye wimbo huo hayakuwa na nongwa, tatizo ni midundo hasa baada ya kuingiza vyombo vingi vya ‘kutengeneza’ vya kielektroniki badala ya kupiga vyombo mubashara kama ilivyokuwa ada kwa muziki wa Congo.
Lakini wimbo huo wa Nzinzi uliotengenezwa na studio kubwa ya Sonny Disc, ambao wakongwe walimtukana, ukaibuka wimbo bora wa Congo kwa karibu miaka miwili mfululizo huku ukishika pia chati za juu duniani.
Wimbo huo unaelezea mwanamume ambaye ameoa, lakini hataki kumpendezesha mkewe na badala yake anawanyatia wake za watu ambao wamependezeshwa na waume zao akiwamwagia fedha kede kede. Mwanamume huyu anafananishwa na Nzi (Nzinzi) na anaambiwa kwa nini usitumie fedha hizo kumpendezesha mkeo?
Nimeuweka hapa kwa maneno ya Kilingala:
1) Mwasi ya bato elengi mingi na ko lula ye
Yayo moko po nini obongisaka ye te
Moninga abongisi elengi mingi nako lula ye
Ya yo moko po nini o vivaka ye te

(Bongisa mwasi nayo Nzinzi eh eh)
Ebele ya mbongo oh yo oko zuaka papa
Kaka ba kwiti na basi oyo ba hina mabala oh

2) (Bongisa mwasi nayo oh Nzinzi eh eh)
Ne la laisse pas tomber
Elle est si fragile

(Bongisa mwasi nayo oh Nzinzi eh eh)
Ebele ya mbongo oh yo oko zuaka papa
Kaka depense na basi oyo ba hina mabala oh

3) (Bongisa mwasi nayo oh Nzinzi eh eh)
Ne la laisse pas tomber
Elle est si fragile

Oh Nzinzi eh eh eh
Mobali mabe oh, Nzinzi eh eh eh
Yo mobali mabe oh

4) Oh Nzinzi eh eh eh
Yo type kolo, Nzinzi eh eh eh
Yo type Kolo

Oh Nzinzi eh eh eh
Kitoko ya pampa oh, Nzinzi eh eh eh
Tala ndenge o nzulusi nga

Oh Nzinzi eh eh eh
Ba fiere ya pamba oh, Nzinzi eh eh eh
Yo mobali mabe eh

5) Mbanda a lati jaune oh
Nga na lata rose oh yoh oh oh
Mbanda a lati vert oh nga na lata blue oh yoh oh oh
Mbanda a kumbi Benz oh
Nga na kumba Rolls oh, yoh oh oh
Mbanda na Ferrari
Nga na Lamborghini, yoh oh oh
Mbanda a kumbi BMV oh
Nga na kumba nini, yoh oh oh
Mbanda a lati rose oh
Motema nanga mpasi eh, yoh oh oh

6) Oh Nzinzi eh eh eh
Mobali mabe oh Nzinzi eh eh eh
Yo mobali mabe oh

Oh Toko eh eh eh
Yo type kolo oh Toko eh eh eh
Yo mobali mabe eh

7) Oh Christino eh
Yo type kolo oh Christino eh
Tala ndenge o nzulusi nga

Oh Nzinzi eh eh eh
Mobali mabe oh Nzinzi eh eh eh
Yo mobali mabe oh

Alikotokea…
Jean Baptiste Emeneya Mubiala Kwamambu alizaliwa Novemba 23, 1956 huko Kikwit katika Jamhuri ya Kiemokrasia ya Congo. Alikulia katika mazingira ya kidini na wakati nilipozungumza naye, alisema kwamba alitamani sana awe Padre kabla ya kubadilisha uamuzi na kusomea elimu dunia, ambapo alihitimu shahada ya Sayansi ya Siasa katika Chuo Kikuu cha Lubumbashi mwa 1977.
Alianza kujihusisha na muziki tangu akiwa chuo kikuu na mwaka 1977 alijiunga na Viva la Musica akitokea Isifi Lokole na kibao chake cha kwanza ndani ya Viva la Musica cha Milena kilichowaacha hoi-bin-taaban mashabiki wa muziki ndani na nje ya DRC.
Kama kawaida ya wanamuziki kuhitilafiana, mwaka 1982 ulikuwa mbaya kwa Papa Wemba kwani kulitaka kufanyika mapinduzi ya uongozi ndani ya bendi hiyo lakini yalishindikana.
Uasi huo ulisababisha wanamuziki kadhaa mahiri wa bendi hiyo kujitenga na kila mmoja kuanzisha kundi lake lililojipambanua kuwa ni mpinzani mkubwa wa  bendi ya Viva la Musica.
Wanamuziki hao ni pamoja na Dindo Yogo aliyejiunga na Zaico, Djuna Djanana, Debaba Star na Pepe Bi Polie walioanzisha bendi yao ya Chocky Star, Kisangani Esperent aliyeanzisha Langa Langa Star na Koffi Olomide aliyeamua kuwa mwanamuziki huru hadi alipoanzisha bendi yake ya Qarte Laten.
Katika vuguvugu hilo, Emeneya alianzisha bendi yake ya Victoria Eleyson ambapo miaka mitano baadaye alitoka na wimbo kabambe wa “Nzinzi” aliouimba akiwa na kundi maarufu la Kassav la Visiwa vya Carrebean.
Wachungizi wa masuala ya muziki wanasema kuwa Emeneya mpaka anarudi kwa Mungu Baba hakuweza kupiga kibao kilichoichengua dunia kama hicho.
Ukweli huo unatokana na jinsi ulivyoimbwa kiufundi kwa kurekodi na Studio ya kimataifa ya Sony Disc ambayo iliingiza madoido na vimbwanga kabambe na kuufanya uwe wa kimataifa zaidi.
Wimbo wa “Nzinzi” ulimpatia Emeneya mkataba wa miaka saba kufanya kazi nje ya DRC na kumfanya apae kimuziki na kupendwa na mashabiki wa kila rika wa dunia.
Ukichanganya na utanashati wake wa uvaaji nguo murua, Emeneya alikuwa mpenzi wa vijana wa iliyokuwa Zaire na kumfanya awe “pedeshee” wa kukata na shoka.
Pamoja na kuizunguuka dunia, lakini Emeneya hakukosa kufika Tanzania ambako alitumbuiza kwenye ukumbi maarufu wa wakati huo wa Silent Inn jijini Dar akiwa pamoja na akina Dodoo La Zeula Bouche na bendi yao ya MK Sound.
Wakati huo ndio alikuwa juu ya dunia na mtindo wake wa “Kide Kune” ambao ulisheheni vimbwanga vya uchezaji na upigaji Drums kwa umahiri  na kuwachanganya mashabiki wasikae vitini wakati akipiga nyimbo zake.
Emeneya alikuwa mwanamuziki pekee wa DRC ambaye alifanya onyesho lililoingiza watu zaidi ya 80,000 kwenye ukumbi wa Studio Manue Engebi jijini Kinshasa aliporejea akitokea duniani baada ya mkataba wake alioingia na Sony Disc kumalizika mwaka 1984.
Kadhalika mwaka 2002 mwanamuziki huyo alifanya onesho kabambe kwenye ukumbi wa Zenith jijini Paris Ufaransa, ukumbi ambao ulizinduliwa kwa mara ya kwanza mwaka 1973 na Tabu Ley na kuujaza kimakwelini.
Akiwa mzaliwa wa jimbo la Ikwiti huko Lubumbhashi, Emeneya alijikuta bila kutegemea akiwa tajiri wa kutupa kwa wimbo wake wa “Nzinzi”.
Kwani, pamoja na nyimbo zake kadhaa kati ya 1000 alizopiga katika uhai wake, wimbo huo ulimtofautisha na wanamuziki wengine wengi wa bara la Afrika.
Wachunguzi wa masuala ya muziki wanasema kuwa wimbo huo ulimfanya awe nje zaidi ya nchi yake na hivyo kufanya baadhi ya watu ndani ya DRC kutomfahamu zaidi ya kumuona kwenye mitandao kama Yu-Tube, TV na magazeti.
Sifa kubwa ya Emenea ni uwezo wake wa kila mwaka kuipua kibao kinachotingisha anga la muziki wa dunia kama kile cha “Okosi Ngai Mfumu” ambacho kilimfanya awe mwanamuziki bora wa Zaire mwaka 1983.
Akafunga kazi mwaka 1992 na wimbo wake wa “Polo kina mfundo” ambao ulikisindikizwa na kuhanikizwa na mirindimo mikali ya mtindo wake mpya uliomuongezea umaarufu wa “Kide kune”.
Hata hivyo, Emeneya alitengeneza “bifu” la sheria yake kati yake na Wenge Musica mwaka 1994 kiasi cha kuwa maadui kama Paka na chui.
Kisa kilitokana na kile kilichodaiwa na wanamuziki wa Wenge Musica kuwa Emeneya alikuwa amewatukana pale walipokutana kwenye jukwaa moja jijini Kinshasa.
Katika mchuano huo uliohudhuriwa na watu wengi na hasa vijana watanashati kutokana na bendi zote mbili kuwa na utitiri wa vijana, Emeneya alipiga wimbo maarufu wa bendi ya Wenge Musica wa “Kala yi Boinge” (Kama Ndege Boieng) kwa umahiri uliotopea.
Alipomaliza kutumbuiza wimbo huo akawataka Wenge Musica nao wapige wimbo wake wa “Nzinzi” ambapo vijana hao machachari walishindwa.
Ndipo alipowaambia, “Nyinyi kumbe ujanja wa bure lakini hamjui muziki. Mimi ndio baba lao kwenu. Nimepiga wimbo wenu pasipo mazoezi hata kidogo. Nyinyi bado makinda kwangu”.
Maneno hayo yaliwauma vijana wa Wenge Musica ambao waliapa kuwa wasingeshirikiana tena na Emeneya katika mambo yoyote yale.
Hata hivyo, mpiga solo wao mashuhuri, Allan Makaba, alikuja baadaye kufanya “kolabo” na Emeneya, kitendo ambacho kilisababisha asakamwe na wenzake.
Inaelezwa kuwa kitendo hicho cha kusakamwa ndiyo sababu kubwa ya Makaba “mchawi wa solo” kujitoa Wenge Musica na kuwa “Mwanamuziki wa Studio” (Recording Artist).
Mambo hayo ndugu zanguni. Basi ndiyo hivyo; Emeneya, aliyezaliwa Novemba 23 mwaka 1956  alitutoka kwa ugonjwa wa moyo na shinikizo la damu ambavyo baadhi ya watu wake wa karibu wanasema maradhi hayo yalisababishwa na mshtuko wa kifo cha Pascal Onema maarufu “Tabu Ley” mwishoni mwa mwaka 2013.
Inaelezwa kuwa kifo hicho kilimmaliza nguvu kwa huzuni iliyotopea na hivyo kumfanya akate tamaa ya maisha.
Yote kwa yote dunia haitasimama bali itaendelea kuwako huku mashabiki wa muziki wakimhani kwa masikitiko makubwa mwanamuziki huyu mtanashati “King Kester Emeneya”.
Baadhi ya nyimbo alizoziimba na mwaka katika mabano ni pamoja na Milena (1977), Teint de Bronze (1978), Ndako ya Ndele (1979), Musheni (1979), Kayole (1979), Fleur d'ete (1978), Ngonda (1979), Dikando (1980), La Runda (1980), Ata Nkale (1979), Dembela (1981), Naya (1982), Ngabelo (1982), Okosi ngai mfumu (1983), Surmenage (1984), Kimpiatu (1985), Willo mondo (1985), Wabelo (1986), Manhattan (1986), Deux Temps (1987) na Nzinzi (1987).
Nyingine ni Mokusa (1990), Dikando Remix (1991), Polo Kina (1992), Every Body (1993), Live in Japan (1991), Every Body (Remix) (1995), Pas de contact (1995), Succès Fous (1997), Mboka Mboka (1998), Never Again Plus jamais (1999), Longue Histoire (Volume 1 & 2) (2000), Live au Zénith de Paris (2001), Live à l'Olympia (Bruno COQUATRIX) de Paris (2002), Rendre à César ... ... ce qui est à César (2002), Nouvel ordre (2002) na Le Jour Le Plus Long (2007).

Katika miaka mingine yote hadi anakufa, Emeneya amekuwa akialikwa na kufanya maonesho kadhaa dunia nzima huku wengi wakidhani alikuwa amestaafu muziki.

Comments