Featured Post

SALAMU ZA MKURUGENZI MKUU WA UNESCO SIKU YA KIMATAIFA YA AMANI



Pamoja kwa ajili ya Amani: Heshima, Usalama na Utu kwa Wote
Hii Siku ya Kimataifa ya Amani huadhimisha nguvu ya ushirikiano wa kimataifa katika kujenga ulimwengu wa amani na endelevu.
Jambo hili linazidi kuwa ni la muhimu sana hasa wakati huu tunapokumbana na changamoto zisizo za kawaida. Nguvu mpya za mgawanyiko zimeibuka, zikieneza chuki na kuondoa kuvumiliana. Ugaidi unachochea vurugu, wakati misimamo mikali inapandikiza sumu ndani ya fikra dhaifu za vijana. Katika maeneo maskini zaidi ya dunia na yasiyo na maendeleo, majanga ya asili yanayohusiana na hali ya hewa yanazidisha hali ya kukosa utulivu, yakiongeza idadi ya watu wanaolazimika kuhama makazi yao na kuongeza zaidi hatari ya kutokea kwa vurugu.
Vikwazo vya kuifikia amani vina utata mwingi na ni vigumu sana - hakuna nchi moja peke yake inayoweza kuviondoa vikwazo hivyo. Jambo hili linahitaji aina mpya ya mshikamano na hatua za pamoja, na kuanza kuchukua hatua hizo mapema iwezekanavyo.
Hiki ndicho kilichoko katika moyo wa wito wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, kuongeza jitihada zinazolenga kuendeleza amani, kuzishirikisha Serikali na mashirika ya kiraia, pamoja na jumuia za kimataifa na za kikanda.
Mabadiliko yanaenea duniani kote kwa kasi kubwa – ni lazima lengo letu liwe kuyapokea mabadiliko hao katika misingi ya haki za binadamu, kuyapa mwelekeo chanya utakaotupeleka kwenye dunia iliyo ya haki zaidi, jumuishi zaidi na endelevu zaidi.
Utamaduni wa amani ni utamaduni wa mazungumzo na kuzuia uvunjifu wa amani, na katika muktadha huu, jukumu la Umoja wa Mataifa halijawahi kuwa la muhimu sana kama wakati huu. Agenda ya 2030 ya Maendeleo Endelevu inathibitisha kwamba "hawezi kuwa na maendeleo endelevu bila amani na hakuna amani bila maendeleo endelevu". Moyo huo huo unaungwa mkono na maazimio ya Umoja wa Mataifa kupitia Baraza la Usalama na Mkutano Mkuu ya mwaka 2016 yanayohusu “amani endelevu”.
Tunahitaji namna mpya yenye kina zaidi, itakayoshughulikia sababu za msingi, na kuimarisha utawala wa sheria na kukuza maendeleo endelevu, yote haya katika misingi ya majadiliano na kuheshimiana. Hii ndiyo dira ya hatua zote za UNESCO za kujenga amani kupitia elimu, uhuru wa kujieleza, majadiliano kati ya tamaduni mbalimbali, heshima kwa haki za binadamu na kutambua uwepo wa tamaduni mbalimbali na ushirikiano wa kisayansi.
Katika hii Siku ya Kimataifa ya Amani, imetupasa wote tuweke upya ahadi na nia zetu za kujenga umoja wa kimataifa. Ili kuendeleza amani, ni lazima tuijenge amani kila siku, katika kila jamii, na kila mwanamke na mwanaume, kwa kufanya kazi pamoja ili kufikia wakati ujao ulio bora zaidi kwa wote.

Comments