- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Unknown
on
- Get link
- Other Apps
Picha inayoonyesha mahali mafuta yanakochimbwa katika Ziwa Albert nchini Uganda.
Kisima cha Mafuta kinachomilikiwa na kampuni ya Tullow nchini Uganda.
AFRIKA Mashariki
inakadiriwa kuwa na kiasi cha mapipa bilioni 7.2 ya akiba ya mafuta
iliyothibitishwa na futi za ujazo trilioni 156 (trillion cubic feet – Tcf) za
akiba iliyothibitishwa ya gesi asilia, MaendeleoVijijini
inaripoti.
Kiwango cha mafuta kilichopo
ni kile ambacho tayari kimekwishagunduliwa nchini Uganda, ambako serikali ya
nchi hiyo imekwishaanza ujenzi wa bomba la mafuta hadi Bandari ya Tanga nchini
Tanzania, ambapo uzinduzi wake ulifanyika hivi karibuni.
MaendeleoVijijini inafahamu kwamba, katika upande wa gesi
asilia, kiwango cha futi za ujazo trilioni 156 kinachotajwa kinahusisha nchi za
Tanzania yenye akiba ya futi za ujazo trilioni 56 na Msumbiji ambayo ina akiba
iliyothibitishwa ya futi za ujazo trilioni 100, ambazo tayari zimekwishaanza
uzalishaji huku utafiti zaidi ukiendelea.
Uchunguzi unaonyesha
kwamba, mwaka 2015 Tanzania ilishika nafasi ya 10 barani Afrika na ya 66
duniani kwa uzalishaji wa gesi, wakati Msumbiji ilishika nafasi ya sita Afrika
na ya 54 duniani.
Msumbiji imehusishwa
ndani ya Afrika Mashariki kutokana na ukweli kwamba hata gesi iliyopatikana ipo
katika Bonde la Ruvuma, eneo ambalo ni la mpaka baina yake na Tanzania, ambayo
pia imefanya ugunduzi mkubwa kwenye bonde hilo.
Takwimu hizo
zinaonyesha kwamba, akiba ya mafuta iliyopo Afrika Mashariki ni sawa na
asilimia sita ya mafuta yaliyothibitishwa Afrika na wakati gesi asilia ni
asilimia 2.19 ya gesi iliyothibitishwa barani humo.
Taarifa ambazo MaendeleoVijijini inazo zinaonyesha kwamba,
ugunduzi wa mafuta nchini Uganda na gesi asilia katika Tanzania na Msumbiji umeendelea
kuvutia wawekezaji katika eneo hili tangu mwaka 2006 huku Msumbiji ikitajwa
kwamba inaweza kuwa nchi ya kwanza katika Afrika ya Mashariki kuanza
kusafirisha nje ya nchi gesi asilia iliyosindikwa katika mfumo wa kimiminika
(Liquefied Natural Gas – LNG).
Taasisi ya Habari za
Nishati duniani (EIA) inaripoti kwamba, historia ya uwekezaji katika gesi asili
nchini Kenya inalingana na ile ya Uganda, Tanzania, Madagascar na Msumbiji
ambako shughuli za utafiti katika eneo hilo zilianza zaidi ya miaka 100 iliyopita.
Ingawa utafiti wa
kwanza ulifanyika katika nchi za Uganda na Madagascar mwanzoni mwa karne ya 20,
lakini umesubiri kwa miaka mingi hadi hivi karibuni ambapo yameonekana
mafanikio madogo huku baadhi ya wawekezaji wakikatishwa tamaa na uwepo wa
mizozo ya ndani na kukosekana kwa uimara wa kiutawala kwenye eneo hilo.
Hata hivyo, hali hiyo
imebadilika kwa sasa, hasa baada ya kugundulika kwa kiasi kikubwa cha mafuta
nchini Uganda mwaka 2006 pamoja na ugunduzi na uchimbaji wa gesi asilia
unaoendelea Msumbiji na Tanzania.
Kwa mujibu wa maelezo
ya mkuu wa kampuni moja ya mafuta yaliyochapishwa katika Mwongozo wa Mafuta na
Gesi Afrika Mashariki wa Deloitte,
haidrokaboni zaidi zimegunduliwa ndani ya Afrika ya Mashariki katika kipindi
cha miaka mitatu iliyopita kuliko sehemu nyingine yoyote duniani.
MaendeleoVijijini inafahamu kwamba, hadi Januari 2013,
kampuni za kigeni zinazoongoza kwa uwekezaji Afrika Mashariki ni pamoja na
Anadarko na Eni zilizoko nchini Msumbiji upande wa kaskazini katika Bonde la
Ruvuma, Oil Madagascar iko nchini Madascar, Tullow inafanya tafiti mbalimbali
nchini Kenya lakini pia kampuni hiyo iko Uganda pamoja na kampuni za Total na
CNOOC.
Maeneo yaliyogundulika kuwa na akiba ya mafuta.
Nchini Tanzania,
japokuwa kuna kampuni nyingi, lakini ambazo tayari zimekwishaanza na uchimbaji
katika maeneo ya kusini mwa nchi hiyo upande wa Pwani na kwenye Bahari ya Kina
Kirefu ni BG Group, Statoil, Ophir Energy, ExxonMobil na Aminex.
Kutokana na
kugundulika kwa rasilimali za mafuta na gesi asilia Afrika Mashariki, kampuni
zinazomilikiwa na serikali za nchi za Asia nazo zimejipenyeza katika ushindani
kwenye akiba za nishati katika eneo hilo huku zikipata nguvu katika miradi ya
kusafirisha nje, shughuli ambazo zamani zilikuwa zikishikiliwa zaidi na kampuni
za Ulaya Magharibi kama Shell na nyinginezo.
Uchunguzi wa MaendeleoVijijini
unaonyesha kwamba, hivi sasa wawekezaji kutoka Asia wanaokuja juu katika sekta
ya mafuta na gesi ndani ya Afrika Mashariki ni CNOOC ya China, ambayo
inaendesha utafiti na maendeleo ya mafuta nchini Uganda, wakati kampuni
nyingine kutoka China, CNPC, iliyonunua hisa za dola za Marekani bilioni 4.2
kutoka kampuni ya Eni kuendesha shughuli za uchimbaji katika pwani ya Ruvuma
nchini Msumbiji, sasa iko katika hatua za mwisho za kujenga mtambo wa kusindika
gesia ya asilia katika hali ya kimiminika (LNG plant), shughuli ambazo zilianza
Machi 2013.
Wawekezaji wengine
wakuu wa Asia ni pamoja na Shirika la Mafuta Ghafi la Bharat la India, na
kitengo cha Viwanda vya Videocon vya India, ambao kwa pamoja wanamiliki asilimia
10 ya eneo la Msumbiji (1 Block).
Aidha, Kampuni ya Gesi
ya Osaka na Kampuni ya Nguvu za Umeme ya Tokyo (TEPCO) zimekuwa na mazungumzo
na Anadarko na washirika wake tangu mwaka 2012 kuhusu mauzo ya baadaye ya gesi
ya asilia iliyoweka katika hali ya kiminika nchini Msumbiji.
Lakini pia nchi za
Afrika Mashariki zenyewe zinatafuta wawekezaji kutoka Asia. Mnamo Agosi 2013,
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alipanga safari ya siku nane Urusi na China
kuvutia uwekezaji katika sekta ya mafuta na gesi nchini Kenya.
Wataalamu wa masuala
ya uchimbaji wanasema ukaribu wa masoko ya Asia, usalama wake kisiasa
ikilinganishwa na wasafirishaji nje wakubwa kutoka Mashariki ya Kati, pamoja na
kukua kwa mahitaji ya nishati, ndizo sababu za kukua kwa mvuto huo wa uwekezaji
Afrika Mashariki.
Ripoti
ya Dunia kuhusu Gesi Asilia ya Kimiminika (World LNG Report) ya mwaka 2011
inasema kwamba, Japani na Korea ya Kusini zinaingiza kutoka nje karibu asilimia
50 ya gesi asilia ya kimiminika katika mahitaji ya gesi hiyo tu duniani, na
kwamba India ni muagizaji mkuu wa sita duniani wa gesi hiyo, nyuma kidogo ya
China.
Inaelezwa pia kwamba,
tangu mwaka 2012, nchi za Indonesia na Malaysia zinaagiza kutoka nje gesi ya
asilia ya kimiminika na Singapore na Israeli zinasemekana kujenga vifaa vya
kurudisha upya gesi na hivyo zinajiandaa kuagiza gesi asilia ya kimiminika.
Kutokana na ukaribu wa
masoko hayo, blog ya The Next
Oil Rush inakadiria kwamba inachukua siku 19 kusafirisha
mafuta kutoka Lamu nchini Kenya hadi Shanghai, China ikilinganishwa na siku 27
kutoka Soyo, Angola hadi Shanghai na karibu siku 17 kutoka Saudi Arabia au Iran
hadi Shanghai.
Kongamano na Maonesho
ya Sekta ya Mafuta na Gesi Tanzania
MaendeleoVijijini inafahamu kwamba, kugundulika kwa kiwango
kikubwa cha gesi asilia nchini Tanzania kulichochea kuanzishwa kwa Kongamano
na Maonyesho ya Sekta ya Mafuta na Gesi Tanzania (TOGaCE) ambalo
linawakusanya wadau wa sekta ya mafuta na gesi nchini humo.
Lengo kubwa la
kongamano hilo lililofanyika mwaka 2012 lilikuwa kukuza ufahamu na uelewa wa
umuhimu wa maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi nchini Tanzania, kutoa nafasi
kwa taasisi za ndani kujitangaza, kujadili sera, sheria na mwongozo mzima wa
sekta hiyo na kutoa nafasi kwa wadau mbalimbali wenye nia ya kuwekeza
nchini. Kongamano pia linatoa nafasi kwa kampuni na watu binafsi
kutangaza bidhaa na huduma zao.
Kongamano la kwanza
kabisa lilifanyika Dar es Salaam kuanzia Oktoba 18 mpaka 19, 2012 ambalo
liliandaliwa kwa pamoja na Wizara ya Nishati na
Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli
Tanzania (TPDC), Mamlaka ya Udhibiti wa
Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na
Taasisi ya Wahandisi Tanzania (IET).
Lengo kuu la kongamano
hilo la kwanza lilikuwa kujenga uelewa wa dhana nzima ya mafuta na gesi
miongoni mwa washiriki wa Tanzania lakini pia kuangalia mchango wa sekta ya
mafuta na gesi katika kuchochea viwanda na maendeleo ya kijamii na kiuchumi
huku washiriki walijadili njia mbalimbali za kukuza sekta husika.
Mambo matano
yaliwasilishwa kwenye kongamano hilo, ambayo ni: Sera na Sheria zinazohusika na
gesi asilia; Masuala ya teknolojia yanayohusiana na utafutaji, tathmini ya
visima, uchimbaji, usafirishaji, uchakataji na matumizi ya gesi asilia; Kujenga
uwezo kwa wazawa kushiriki katika sekta hii ikiwemo masuala ya maendeleo ya
miundombinu, mafunzo na tafiti; Masuala ya usalama, uharibifu wa mazingira na
namna ya kusimamia na kulinda mazingira; na Kukuza uelewa kuhusu sekta ya gesi,
umuhimu wake na fursa zilizopo.
Kumbukumbu ambazo MaendeleoVijijini
inazo zinaonyesha kwamba, changamoto za sekta hiyo zilibainishwa na washiriki
wa kongamano zikijumuisha, pamoja na masuala mengine, kuongeza idadi ya
wataalamu kwenye sekta ya mafuta na gesi, kuendeleza miundombinu na kuwekeza
kwenye nishati endelevu. Washiriki walikubaliana kuanzishwa kwa mfuko wa mafuta
na gesi kama ilivyo nchini Norway na kutafuta suluhisho za ndani katika kutatua
changamoto zinazoikabili sekta hii. Maazimio ya kongamano yalitengenezewa mpango
mkakati wake.
Kongamano la pili
lilifanyika pia Dar es Salaam kwa siku mbili kuanzia Oktoba 23 – 24, 2013 na
liliandaliwa kwa pamoja na Idara ya Uhandisi Kemikali na Madini ya Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam, Taasisi ya Wahandisi Tanzania (IET), Wizara ya Nishati na
Madini, TPDC na EWURA.
Kongamano
lilikutanisha wadau mbalimbali kutoka serikalini, sekta binafsi ikijumuisha
kampuni za mafuta na gesi na wanataaluma ambao walijadili masuala mbalimbali
yanayohusu sera, hali halisi ya sekta hususan masuala yanayohusu mkondo wa juu
(upper
stream), mkondo wa kati (midstream)
na mkondo wa chini (downstream).
Mkondo wa juu ndio
unaohusika na utafiti na uchimbaji, mkondo wa kati unahusika na uchakataji na
miundombinu ya usafirishaji, wakati mkondo wa chini unahusika na usambazaji
tayari kwa matumizi.
Masuala kadhaa
yalijadiliwa ambayo ni pamoja na Ufanyaji wa biashara, kodi na masuala ya
fedha; Uendelezaji na ufaidikaji wa rasilimali za mafuta na gesi; Utafutaji
endelevu na matumizi ya mafuta na gesi; Kujenga uwezo kwa wazawa; na Changamoto
na mustakbali wa sekta ya mafuta na gesi nchini Tanzania.
MaendeleoVijijini inafahamu kwamba, sehemu kubwa ya majadiliano
ilitazama namna gani Watanzania wanaweza kushiriki katika ngazi zote za
mlolongo wa thamani wa sekta hiyo na kupendekeza kuwepo kwa mwongozo wa
kuhakikisha sekta binafsi inasaidiwa kushiriki katika sekta hiyo, ukilenga hasa
uhamishaji wa maarifa na teknolojia kutoka nje ya nchi kwa manufaa ya wazawa.
Oktoba 21-22, 2014
kongamano la tatu lilifanyika Dar es Salaam ambalo liliandaliwa na taasisi zile
zile zilizoandaa kongamano la pili, ambapo kwa mara ya kwanza kongamano hilo
liliendeshwa kwa lugha ya Kiswahili, lengo likiwa kuwapatia nafasi Watanzania
wasioweza kutumia lugha ya Kiingereza kushiriki kwenye mijadala mbalimbali.
Katika kongamano hilo,
Naibu Waziri wa Nishati na Madini wa wakati huo, Stephen Masele, aliahidi
kutungwa kwa Sera ya Ushirikishaji na Uwezeshaji Wazawa Tanzania ambayo
itahakikisha Watanzania wanashiriki katika mlolongo mzima wa thamani na
kufaidika na sekta ya gesi na mafuta.
Lakini mwaka huo pia,
mnamo Novemba 14-15, lilifanyika kongamano jingine mjini Mtwara, maarufu kama
Kongamano la Mafuta na Gesi Mtwara (MOGBE), ambalo lilikuwa la kwanza na la
aina yake kuhusiana na sekta ya mafuta na gesi. Lengo kubwa lilikuwa kulifanya
liwe kiunganishi miongoni mwa wadau kwenye mlolongo wa thamani nchini humo kwa
kuwawezesha, kuwapatia fursa za ajira na kujenga uwezo miongoni mwa wanajamii
wa maeneo ya Kusini mwa Tanzania.
Kongamano
la Nne linalohusu sekta ndogo ya mafuta na gesi lilifanyika kuanzia tarehe
20 – 21 Oktoba, 2016 jijini Dar es Salaam na kukutanisha wadau mbalimbali zikiwemo
kampuni zinazojishughulisha na utafiti na uchimbaji wa mafuta na gesi, Vyuo
Vikuu, Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali.
Kutokana na uwekezaji katika shughuli
za gesi na mafuta, kumekuwepo na mabadiliko ya kiuchumi katika mikoa ya Lindi
na Mtwara kama vile kuongezeka kwa fursa za ajira, malazi na utoaji
wa huduma kwa wawekezaji.
Hali hiyo inawapa fursa wananchi kujiona kama nao ni sehemu ya
maamuzi lakini ni wanufaika wa rasilimali hizo asilia ambazo zinachimbwa katika
maeneo yao badala ya kujiona kana kwamba wametengwa.
Comments
Post a Comment