Featured Post

MAUAJI YA ALBINO – 3: ‘MGANGA AKIKUAGIZA, HATA KABURI LA NYERERE UTAVUNJA KUTAFUTA MIFUPA’

Daniel Mbega na mauaji ya albino
Mwandishi wa makala haya, Bwana Daniel Mbega, akiwa na mganga wa jadi huko Kachwamba, wilayani Chato. (Picha zote na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini)

Daniel Mbega na mauaji ya albino
Mwandishi wa makala haya, Daniel Mbega, akiwa na mtoto Margreth Hamisi (6) mkazi wa Kona Nne, Kijiji cha Mwakashanhala wilayani Nzega, baada ya kuokolewa na wanausalama wakati akitaka kuuzwa mzima mzima na mjomba wake.


Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini
Kahama: SHABAN Kapulwa (siyo jina lake halisi) ni mganga wa jadi ambaye anajivunia ‘nguvu’ za tiba zake asilia zilizomwezesha kukutana na watu wengi – wanasiasa kwa wafanyabiashara – na ‘kuwasaidia’ kwenye mambo yao.
Anaishi katika eneo la Nyihogo kwenye Halmashauri ya Mji wa Kahama, na siku zote anategemea uganga kuendesha maisha yake.

Zaidi anaheshimika na wakazi wa eneo hili kwa sababu ni ‘mfumu’ (mganga) na kila unapofika kwake utashangaa kukuta watu wengi wakisubiri huduma.
Shaban anaishi kwenye nyumba nzuri ya kisasa na nje ameegesha gari dogo aina ya Toyota Verossa, ambalo anasema alipewa zawadi na mwanasiasa mmoja (hamtaji jina) baada ya ‘kumsaidia kupata ubunge’ katika mojawapo ya majimbo ya Kanda ya Ziwa.
“Wanakuja, wengi tu – wanasiasa, wafanyabiashara, maofisa wakubwa wa serikali na wengine – wanataka dawa ili ama wapate madaraka makubwa au mafanikio katika biashara zao, wengine ukiwatazama tu unaona wamevurugwa na maisha, wamejikati tamaa wenyewe, ninawasikiliza na kuwasaidia kwa kadili ya utashi wao,” Shaban anamweleza mwandishi wa MaendeleoVijijini.
Japokuwa anaishi kwenye nyumba nzuri, lakini mazungumzo na mwandishi wa makala haya yanafanyika kwenye kibanda maalum cha msonge kilichosilibwa kwa udongo na kuezekwa nyasi (Wasukuma wanasema ‘Kizimba’), ambacho ndicho hutumika kwa tiba zake.
Sakafu ya udongo imetandikwa mkeka mzuri ambao nao anasema aliletewa na mfanyabiashara mmoja kutoka Arabuni.
Kizimba hiki kimejaa harufu nzito inayotokana na kuchomwa kwa udi na ubani inayomfanya mwandishi apige chafya mara kadhaa.
Kizimba kimejaa pembe na tunguli nyingi pamoja na mikoba ya ngozi za wanyama wa kila aina.
“Wateja wengi wanakuja na matatizo mengine nje ya tiba kama kutaka madaraka, mafanikio katika kazi na biashara, ninawatibu kwa saikolojia tu kwa sababu hakuna dawa inayoweza kukupatia utajiri na madaraka, labda kwa njia za kichawi, ambao mimi siyo muumini wake,” anasema.
Shaban ameiambia MaendeleoVijijini kuwa, kutokana na ujinga na imani za kishirikina zilizotanda kwa jamii na kuamini kila linalosemwa na waganga, ndiyo maana wamekuwa wakifanya mambo magumu yanayokwenda kinyume hata katika jamii.
“Waganga tumaaminika sana, na ninakuhakikisha, mganga akikwambia kalete mfupa wa Mwalimu Nyerere ili ufanikiwe maishani, hata kama kaburi lile linalindwa, unaweza kwenda kulivunja bila kujali athari utakazozipata, kwa kuwa tu umeaminishwa ujinga,” anasema.
Anaongeza: “Ukisikia mganga anakwambia kaleta ‘mweso wa kanyerere’ – yaani moyo wa sisimizi – basi ogopa sana. Maana yake unatakiwa kwenye kuleta moyo wa mtu, na ili uupate ni lazima umuue… tangu lini moyo wa sisimizi ukaonekana?”
mweso wa kanyerere
 Karatasi hii ilikutwa kwa mganga mmoja akiwa amemwandalia mteja wake maelekezo (Chiranduzi) ya vitu vinavyohitaji, ikiwemo kumtaka akalete 'moyo wa sisimizi' akiwa na maana ya kuua mtu.

Migeka Mihagwa Masakilija (58) ni mganga wa jadi, mkazi wa Kachwamba, wilayani Chato katika Mkoa wa Geita, ambaye ameiambia MaendeleoVijijini kwamba, watu wametengenezwa ujinga wanaukubali na ndiyo maana matukio ya mauji ya vikongwe na albino yameongezeka nchini Tanzania na hata Afrika Mashariki na Kati.
www.maendeleovijijini.blogspot.com
Pichani inaonekana kipande cha ngozi ya na 'goroli' la Simba pamoja na simbi ambazo kwa mujibu wa mganga mmoja wa Kachwamba wilayani Chato, ikichanganywa na 'shingila' nyingine, inaweza kufanya mambo mengi. (Picha zote na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini)

Hata hivyo, anafafanua kuwa kuna makundi manne yanayohusiana na uganga ambayo ni wauaji (wakiwemo wakata mapanga), mawakala wa shingila (vichanganyio vya dawa), waganga walozi na waganga tiba.
Migeka anasema: “Kundi la wauaji, ambalo linahusisha waganga matapeli wanaomiliki mitandao ya wakata mapanga kazi yao kubwa ni kuua labda albino, kutafuta viungo vya vichaa, viungo vya uzazi vya binadamu, mafuta ya binadamu, mafuta ya nyoka au simba, mifupa ya watu maarufu – hata ya Mwalimu Nyerere – kama hakuna ulinzi wanavunja lile kaburi. Hawa wanaweza kuteka nyara, wakakunyonga, wakakubanika porini na kuchuja mafuta. Ndio wanaokwiba albino na kuchukua viungo. Wanaweza kuwa na mifupa ya bundi, mbwa na takataka zote,” anasema.
Kuhusu mawakala wa shingila, Migeka anasema, hilo ni kundi muhimu katika masuala ya uganga, kwani wakala huyo ndiye anayewasambazia waganga mahitaji yote. 
shingila 
Mifupa, pembe na vitu mbalimbali vinavyotumika kama 'shingila' baada ya kukamatwa nyumbani kwa mganga mmoja wa jadi huko Bariadi. 
nyoka wa uchawi 
Hawa ni nyoka waliokaushwa ambao wanausalama walimkamata mganga mmoja wa Kilyamatundu, Sumbawanga mkoani Rukwa akiwa nao.

“Kama mganga yeyote anahitaji kazi fulani ifanyike anamtafuta huyu wakala, ambaye naye anawasiliana na kundi la wauaji ambao ndio wanaomletea viungo hivyo,” anasema na kusisitiza kwamba kuna mtandao mkubwa kiasi kwamba kuuvunja ni shida.
MaendeleoVijijini imebaini kwamba, waganga walozi hawajishughulishi na tiba bali hutafuta shingila kwa ajili ya kufanya kafara, hata ya kuua mtu.
“Hawa kazi yao ni makafara na kuloga watu, unamwendea na kumwambia fulani amekutenda hivi na vile, yeye anakuuliza ‘unataka huyu tumfanye nini’, utakavyomwambia ndivyo atakavyofanya,” anasema Migeka.
Anaongeza; “Waganga wa tiba ni sisi ambao tunatibu watu waliologwa na waganga walozi.”

Imani kwa waganga
Mganga Maria Masweduki, mkazi wa Buzirayombo wilayani Chato akiwa 'amepandisha maruhani' kumpigia ramli mwandishi wa makala haya (hayupo pichani) baada ya kulipa Shs. 2,000 inayoonekana hapo. 
Kwanini wanaheshimika? Na tiba za kisaikolojia zikoje? Ni kweli zinasaidia kuwapatia watu madaraka na utajiri?
Kabla ya Shaaban Kapula kujibu maswali hayo, anatabasamu.
“Nilitegemea utaniuliza hivyo. Ngoja nikwambie, kwanza jamii za Wasukuma wanaamini sana masuala ya kishirikina. Hawawezi kufanya jambo lolote mpaka wakamuulize ‘mfumu’, na atakachowaeleza, hata kama ni uongo, ndicho watakachoamini.
“Ninaheshimika hapa kwa sababu mtandao wangu ni mkubwa kuliko waganga wenzangu, watu wanaona magari ya kifahari yanakuja kila wakati, wanaamini mimi ni kiboko ndiyo maana nina wateja wengi. Wakija na matatizo yao, ninawasikiliza na ninapoona yamesababishwa na mkanganyiko tu wa maisha, nawapa dawa za uongo na kweli, lakini kikubwa masharti ninayowapa ndiyo dawa.
“Ninawashauri tu kwamba ili dawa zangu zifanye kazi wakaongeze bidii kazini na lazima bosi wake atampandisha cheo, kama ni mfanyabiashara namwambia apunguze matumizi ili apate mafanikio, kama ni mwanasiasa namwambia akazungumze sera zinazolenga kutatua matatizo ya wananchi na atomize ahadi zake.
“Sasa niambie, katika masharti hayo ni yapi ambayo yanahitaji dawa kama siyo kubadilisha fikra za mtu afanye yaliyo sahihi?” anahoji Shaaban. “Ukiongeza bidii kiongozi wako ataona mabadiliko, wengine wanajichukia wenyewe tu na kudhani kuna watu wabaya wanawaloga, hata mtaani wanakoishi.”
Kwa upande wake, Lumisha Nhinde (46), mganga wa jadi wa Kijiji cha Buhekela wilayani Igunga mkoani Tabora, ameiambia MaendeleoVijijini kuwa, watu wametengenezewa ujinga tangu enzi na enzi ambao wanauamini.
“Kwa mfano, kuna msemo wa ‘mganga hajigangi’, maana yake unaijua? Maana yake ni ujinga tu, hata yeye anaweza kutegemea mganga mwingine. Eti ili aweze kupona ni lazima amtafute mwingine… ina maana dawa zake hazifanyi kazi. Wanatumia lugha hiyo kama kinga ili usimhoji. Kama mganga anaamini dawa zake zinaleta utajiri, kwa nini asitengeneze akapata utajiri? Kwani yeye hataki kuwa tajiri?” anaeleza.
Aidha, ameithibitishia MaendeleoVijijini kuwa, ujinga huo wa watu kuamini kuwa ufumbuzi wa matatizo yao utapatikana kwa waganga wa jadi umewakumba hata wasomi, ambao, anabainisha kwamba, kwa miaka ya karibuni ndio wengi wanaoingia kwenye vizimba.
“Wasomi ni wajinga sana, wanajifanya wamesoma na kutuona sisi si lolote, nasi hutumia nafasi hiyo kuwakomoa,” anasema huku akininong’oneza: “Tena tunawakomoa zaidi kwa kulala na wake zao wakati wao wanahangaika usiku kwenye njiapanda wakipiga manyanga.”
“Nikimuona mjanja kama wewe lakini aliyeingia kwangu kwa dharau, nitamwambia ili tiba ifanye kazi, basi amlete mkewe kwani ndiye atakayetengeneza dawa.
“Nikiona mkewe ‘analipa’, usiku wa manane nitawaambia twende njiapanda ambako yeye atakuwa anaoga dawa za uongo na kweli, halafu nitabaki na mkewe na kumwambia tulale kwa sababu ni sehemu ya tiba ya mumewe, hawezi kukataa na inakuwa ni siri kubwa, hawasemi,” anasema na kuongeza kuwa kama mteja ni mwanamke, atamweleza kwamba kulala naye ni sehemu ya tiba yake.

Utajiri wa kishirikina ukoje?
Baraka
 Bi. Prisca Mpesya akiwa na watoto wake wawili wenye albinism, Lucia aliyembeba na Baraka ambaye alikatwa kiganja cha mkono. Hapa alikuwa akimuuguza Baraka katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya.

Lakini Shaaban Kapulwa anasema, katika uhalisia, hakuna utajiri wa kishirikina bali ni imani potofu zilizopandikizwa katika fikra za jamii kuwa wakitumia dawa wanaweza kufanikiwa.
“Huu ni utapeli wa wazi wazi, lakini ukimwambia mteja ukweli kuwa hakuna dawa ya utajiri haamini na atakuona wewe ni mbabaishaji, kwa sababu yeye amefunga safari kutoka huko mpaka kwako akiamini wewe unaweza kumpa ‘zari’, hivyo tunalazimika kukubaliana na matakwa yao na kutengeneza dawa za uongo na kweli na kuwapa masharti magumu,” anasema.
MaendeleoVijijini ilitaka kujua kama kuna ukweli kwamba albino ni dili? Lakini Shaaban anajibu haraka kuwa hakuna kitu kama hicho.
“Ni utapeli tu kwamba kalete kiungo hiki cha albino ili wapate kupiga hela. Ninachokuthibitishia ni kwamba, albino siyo biashara ila watu wameaminishwa tu. Watu ni wepesi kuamini uongo kuliko ukweli,” anasema.
Shaaban anasema, siku za nyuma waliwahi kufanya kikao cha waganga na wananchi ili kuwahamasisha watu waondokane na dhana hiyo kwa sababu wanafahamu wanaosababisha mauaji ya vikongwe na albino ni waganga.
“Kwa sababu mganga anakuwa tayari amemtapeli sana mteja hivyo anamtengenezea mazingira ili akamatwe na kufungwa kwa sababu hakuna dawa yoyote ya utajiri ambayo unaweza kumpatia,” anasema.
Hata hivyo, anakanusha kuwepo kwa utajiri wa ‘manyoka’ ambao kwa muda mrefu umevuma katika jamii, akisema hizo ni fikra potofu na utapeli ambao waganga wa jadi wanaufanya kuwapumbaza watu.
“Hata wewe unaweza kufuga nyoka ilimradi tu mtu akukamatie. Ukishamchukua kwanza inabidi umtoe meno yote kwa kumsugua kwa gunzi la mahindi, halafu na wewe unatakiwa kukata kucha zako zote za mikono na miguu,” anaelezea.
Ameieleza MaendeleoVijijini kwamba, kwa kawaida, nyoka anapouma sumu yake inapitia kwenye meno, hivyo ukiyasugua maana yake hatakuwa na uwezo wa kuuma, ingawa meno ya baadhi ya nyoka huota tena.
“Kila kucha zako zinavyokua ndivyo na meno yake yanakua, kwa hiyo unatakiwa kumsugua meno yake kila mara ili uwe salama. Wale ambao unasikia wameumwa ama kuuawa na nyoka wao huwa wanakosea masharti hayo.
“Ukishamfuga nyoka, mganga atakupa masharti kwamba, fedha zote unazozipata kwenye biashara yako ni lazima uzitumbukize kwenye chumba alimo nyoka na usizitumie ovyo isipokuwa tu unapochukua kiasi cha kufungia bidhaa. Kwa kukuangalia tu ataona udhaifu wako uko wapi – kama siyo mlevi wa pombe basi utakuwa mzinifu na vinginevyo – kwahiyo nitakwambia achana na starehe na anasa zote, na usitoe fedha ovyo kwa watu. Hebu niambie, baada ya mwaka mmoja, fedha hizi zitakuwa kiasi gani?” anahoji.

Wateja wao akina nani?
 Yohana Bahati
 Aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Geita, ACP Joseph Konyo, akiweka mchanga kwenye kaburi la marehemu Yohana Bahati (1) wa Kijiji cha Ilyamchele wilayani Chato aliyetekwa na kuuwa, kisha kuondolewa mikono na miguu na watu wasiojulikana.
 Kaburi la marehemu Yohana likijengewa.

“Mashehe na wachungaji, waimbaji wa injili, wasanii, wanamichezo, na wasomi kwa ujumla ni wateja wetu wakubwa. Kama kuna mtu mwelewa kwamba kuna utapeli kwenye uganga basi siyo wengi, vinginevyo tunawapata sana,” anasema.
Anasema, suala la kiimani katika ushirikina hata watu wa Mungu wapo, wanaamini na wanakwenda kwa waganga kutafuta ‘nguvu’ za kukubalika kwa waumini wao.
Ameithibitishia MaendeleoVijijini kwamba, wakati viongozi hao wa dini wanapohubiri kuhusu uchawi na kuwaita waumini watoe ushuhuda maana yake wanakiri nguvu kubwa ya ushirikina na wanawanadi waganga na wachawi na kuzidi kuwatengenezea waumini ujinga mwingine.
“Labda nikupe mfano hai, niliwahi kupata wachungaji, kuna mchungaji mmoja wa Mbeya na mwingine wa Dar es Salaam. Huyu wa Dar es Salaam, tena mtu maarufu sana anatokea Kanda ya Ziwa (jina linahifadhiwa), alikuja akiwa amepewa anuani yangu, kwamba nikimtengenezea dawa atakuwa na uwezo kila atakaloongea watu wamsikilize na atajaza waumini kanisani mwake.
“Nikamuendelezea ujinga kwamba kila utakachoongea kinakubalika. Sikumpa dawa ya maana, nilimjenga kisaikolojia tu kwamba azungumze vitu vinavyoilenga jamii, halafu akachinje kuku, achukua dawa aichanganye na damu aoge halafu, ile itakayobaki amwage damu barabarani.
“Hakuna dawa yoyote kubwa, nilimpa ya kawaida tu kwa kumwaminisha kwamba yale maneno atakayoyasema yawe na nguvu. Hakujua ni yale maneno tu ambayo anayazungumza kulenga jamii ndiyo yanayomfanya akubalike katika jamii. Sasa amejipatia umaarufu mkubwa Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla.”
Anasema, kwa kiongozi wa dini kuambiwa atoe Shs. 500,000 hadi milioni moja ni jambo la kawaida na wengi wanatapeliwa kila siku lakini hawawezi kusema hadharani.
Anawataja baadhi ya viongozi wakuu wa dini wanaoheshimika (majina yanahifadhiwa) ambao wanaendesha utapeli hadi makanisani kwa sababu ya ujinga wanaoaminishwa na waganga.
“Sisi waganga tunawafundisha mazingaombwe, kwa mfano, kubadilisha maji kuwa soda, ni akili tu. Zinachukuliwa Juice Cola za pakti. Zinatafutwa tissue za kawaida, zile pakti zinapasuliwa kama mbili na kuwekwa kwenye tissue.
“Halafu yanaletwa maji, anawaambia waumini fumbeni macho waombe. Wanapofumba macho yeye anaingiza mkono kwenye maji huku akiufikicha na kukoroga akiendelea kuomba. Wakifumbua tayari wanaona maji yamebadilika rangi, anawaambia ni kwa uwezo wa Mungu wakati ni utapeli,” anasema.
Aidha, anasema ingawa siyo vyema kupinga Neno la Mungu, lakini ni wajibu wake kuielimisha jamii kuhusu baadhi ya madhehebu ambayo yanawapotosha watu kiimani kwa kutumia miujiza ambayo ni viinimacho.
Shaaban anasema, kwa kuwa kizazi cha sasa watu wanataka kuona miujiza ndipo waamini, wametokea watu ambao wanazifanyia biashara dini kwa mazingaombwe.
“Nenda kwenye kanisa ambalo kiongozi wake anajitangaza kufanya miujiza utaona. Kuna matayarisho makubwa ambayo wanafanya wanapodai kuwaombea walemavu na watu kama hao, kama wewe si mmojawao huwezi kuanguka kwa mapepo kwa sababu hukuandaliwa,” anasema.
Anaongeza: “Mchungaji mmoja (jina linahifadhiwa) aliwahi kuja pale Kigoma akawaandaa watu ili kujifanya walemavu. Akawapanga kesho yake alipokwenda mkutanoni akasema leo anaomba kwa ajili ya vipofu na vilema. Wale watu walioandaliwa walijipanga mle ndani sehemu tofauti tofauti. Aliposema sasa naombea wasioweza kutembea, wale waliopangwa wakajitokeza haraka.
“Wanapofika idadi fulani anayoijua yeye kwamba ndio ‘watu wake’ anasema nitawaombea hawa tu leo. Anaanza kuomba pale na wale wanadondosha magongo na kuanza kuruka ruka, halafu mkutano wanashangaa kuona miujiza hiyo na kumwamini.”

Kufunga kipindi

mkono wa albino 
Kitanga cha mkono wa mtoto Baraka Cosmas kikiwa kimeoza na kutoa funza baada ya kupatikana.
Muuza albino 
Sajenti Kalinga Malonji, mkazi wa Kijiji cha Hanseketwa wilayani Mbozi akiwa chini ya ulinzi baada ya kukamatwa akiwa na kiganja cha mtoto Baraka Cosmas.

MaendeleoVijijini imegundua kuwa waganga wana lugha maarufu wanayoitumia pale wanapoona wamekwisha mtapeli mtu fedha nyingi na bado anawafuatilia.
“Huwa tunasema ‘tunafunga kipindi’, yaani inabidi utafute namna ya kumpoteza kabisa mtu huyo asikufuatilie kwa sababu ulichomwaminisha kuwa ni dawa ni uongo tu hazifanyi kazi yoyote,” anasema Shaaban.
Anasema baadhi ya viongozi wa dini wametapeliwa na waganga mpaka Shs. 50 milioni wanapohitaji dawa na mvuto wa waumini makanisani mwao, lakini katu hawawezi kulalamika hadharani kwa sababu jamii itawashangaa.
“Kama hawajafanikiwa watarudi tena kwa waganga, na kwa kuwa hakuna dawa yoyote ya maana, inabidi umuuzie kesi – wengine wanaambiwa wakafanye makafara kwa kutumia viungo vya binadamu au wakazini na watoto wadogo huku wakidanganywa kuwa hakuna atakayewaona baada ya kuogeshwa dawa, matokeo yake wanajikuta wamekamatwa na kufungwa jela,” anasema na kuongeza kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya kuepukana na mteja wa aina hiyo kwani tayari amemlia fedha na mwendelezo wa kumdanganya hana.

Jiandae kusoma kitabu maalum cha ‘MAUAJI YA ALBINO NJE-NDANI’ kinachotokana na uchunguzi wa kipelelezi wa mwandishi DANIEL MBEGA alioufanya kwa miezi nane katika mikoa 10 ya Tanzania iliyokumbwa na matukio hayo, huku nyakati nyingine akihatarisha maisha yake usiku na mchana. Kitabu hicho kina ripoti za ndani kabisa kuhusu namna mauaji hayo yanavyofanyika, wahusika wakuu, mtandao hatari uliopo na unawahusisha akina nani, jinsi polisi wanavyopeleleza kesi hizo, rushwa ndani ya mahakama za sheria ili kuwalinda wahalifu, mambo yanayotokea kwa waganga wa kienyeji na mengi kadha wa kadha ambayo hayakuwahi kuripotiwa hadharani.

0656331974

Comments