Featured Post

KOREA KUSINI YAONESHA NIA YA KUWEKEZA TANZANIA

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza  na Wajumbe wa Baraza la Uwekezaji la Korea nchini Tanzania  (KICoT Corporation) leo, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo  na Wajumbe wa Baraza la Uwekezaji la Korea nchini Tanzania  (KICoT Corporation) leo, Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiimba wimbo wa Taifa pamoja na Mshauri Mkuu wa Baraza la Uwekezaji la Korea nchini Tanzania  (KICoT Corporation), Mhe. Balozi Mstaafu wa Korea Kusini hapa nchini Kim, Young-Hoon ambaye alimwambia Mhe. Makamu wa Rais kuwa bado anaukumbuka wimbo wa Taifa la Tanzania.

                                     ..................................................................... 


         Watanzania waliosoma Nchi Korea Kusini wameunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya Tano ya kujenga uchumi wa viwanda kwa kuleta wawekezaji ambao wanataka kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya nguo, vifaa tiba, uzalishaji wa nishati ya umeme wa jua, kilimo na katika sekta ya Sanaa,utamaduni na michezo.

Mwenyekiti wa Baraza la Uwekezaji kutoka Korea Kusini hapa nchini Kakono David ametoa kauli hiyo wakati anaongoza Ujumbe wa Baraza la Uwekezaji la Korea Kusini ambao wamekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Jamahuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti huyo amesema ujenzi wa viwanda hivyo utatoa fursa kubwa katika kukuza uchumi wa nchi na kutoa ajira nyingi kwa Watanzania na amesisitiza kuwa kwa kuanzia wawekezaji hao wataanza kuwekeza katika wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza.
Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan katika mazungumzo na ujumbe huo wa Baraza la Uwekezaji Kutoka Korea Kusini amesema amefurahishwa na ujio wa wawekezaji hao na amewahakikishia kuwa Serikali ya awamu ya Tano inaendelea kujenga mazingira bora ya uwekezaji ili kazi ya ujenzi wa viwanda nchini iweze kwenda kwa kasi inayotakiwa.

Makamu wa Rais amesema ujenzi wa viwanda unaoendelea kufanywa na wawekezaji nchini utasaidia kuongeza pato la taifa na kutoa ajira kwa Watanzania.
Amesema Tanzania ina maeneo mengi na mazuri kwa ajili ya uwekezaji Tanzania Bara na Zanzibar hivyo ni wakati muafaka kwa watendaji wa sekta husika kwa ushirikiano na serikali kujiimarisha katika kuondoa ukiritimba ili kuvutia wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali Duniani.

 Makamu wa Raia pia amefurahishwa na mpango wa wawekezaji hao kutoka Korea Kusini ambao wanataka kusaidia uimarishaji wa haki za wanawake hapa nchini na amekaribisha Jumuiya ya Wanawake kutoka Korea Kusini kuja Kufanya ziara ya kikazi hapa nchini.
 

Comments