Featured Post

WABINIFU MAJENGO NA WAKADILIAJI MAJENZI NDANI YA JESHI LA POLISI WAHIMIZWA KUPATA MAFUNZO

Mwenyekiti wa Bodi DKT. Ambwene Mwakyusa, akizungumza na waandishi wa habari nje ya Mkutano wa Mashauriano baina ya Bodi ya  Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi, Jeshi la Polisi na Mkurugenzi wa Mashitaka nchini DPP, unafanyika kwa siku mbili kuanzia jana, Rock City Mall Jijini Mwanza.

Judith Ferdinand, BMG
Jeshi la Polisi nchini limehimizwa kuwaruhusu na kuwawezesha wataalamu katika fani ya ubunifu majengo na ukadiriaji majenzi waliosajiliwa, kuhudhuria mafunzo mbalimbali yanayoandaliwa na Bodi  ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi.

Wito huo ulitolewa leo na Mwenyekiti  wa Bodi ya Wabunifu Majengo Dkt.Ambwene Mwakyusa, katika ufunguzi wa mkutano wa mashauriano kati ya Bodi ya  Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi,Jeshi la Polisi na Mkurugenzi wa Mashitaka Biswalo Mganga, uliofanyika kwenye ukumbi wa Rocky City Mall.

Dkt.Mwakyusa alisema, mafunzo hayo endelevu yanayoandaliwa na Bodi hiyo mara mbili kwa mwaka yanalengo la kuwaelimisha wataalamu hao,ili waendane na kasi ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia sambamba na kukabiliana na changamoto.

"Tunatambua jeshi la polisi lina wataalamu katika fani za ubunifu majengo na ukadiriaji majenzi waliosajiliwa na ambao hawajasajiliwa na bodi, hivyo naomba liendelee kuwaruhusu na kuwahimiza  wataalamu hao, ili waweze kusajiliwa," alisema Mwakyusa.

Hata hivyo alisema, kwa mujibu wa Sheria namba 4 ya mwaka 2010, Bodi inamajukumu ya kusajili na kuratibu mienendo ya Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi na wataalamu wanaoshabiana ambopo mpaka mwaka 2016 imesajili wataalamu 1442 na makampuni 393 pamoja na kukagua miradi ya ujenzi kwa lengo la kuhakikisha imebuniwa na inasimamiwa na wataalamu waliosajiliwa na Bodi.

Aidha alisema, kwa mwaka 2016/ 2017 Bodi imepanga kukagua miradi 1800 nchi nzima,ambapo hadi kufikia mwaka jana jumla ya miradi 1227 imekaguliwa sawa na asilimia 68 ya lengo,huku hatua mbalimbali zilichukuliwa kwa miradi iliyokuika sheria ikiwa ni pamoja na kusimamisha shughuli za ujenzi na kufungua mashtaka mahakamani.

Pia aliliomba Jeshi la Polisi  kufuata taratibu za ujenzi katika ubunifu na usimamizi wa majengo ya jeshi hilo,ikiwa ni pamoja na kutumia makampuni ya ubunifu majengo  na ukadiriaji majenzi,kama sheria namba 4 ya mwaka 2010 inavyotaka,hivyo itasaidia kuhamasisha jamii kutii sheria za nchi.
Kamishna wa Polisi (Oparesheni na Mafunzo), Nsato Marijani akiongea na waandishi wa habari nje ya ukumbi Jijini Mwanza.

Kamishina wa Polisi na Oparesheni na Mafunzo, Nsato Marijani, alisema, wataendelea kuwatumia Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi ,ambao ni watumishi wa Jeshi la Polisi na kuwaendeleza wale ambao hawajasajiliwa na Bodi, ili wawe na sifa za kusajiliwa.

Alisema jeshi hilo litaendelea kuwatumia kuwatumia wahandisi na makandarasi waliosajiliwa katika ujenzi wa makazi na ofisi za askari, kwani kwa kufanya hivyo jamii haitaona ajabu pale watakapo wachukulia hatua za kisheria wale ambao wanajenga bila kutumia wataalamu.

Comments