Featured Post

UNAIKUMBUKA HII? MBASHA ASEMA, “GWAJIMA NIACHIE MKE WANGU”!




GAZETI LA UWAZI: JUNI 10, 2014
MUME wa mwimba Injili Bongo, Flora Mbasha anayedaiwa kumbaka binti wa miaka 17 ( jina lipo), Emmanuel Mbasha ameibuka mzimamzima na kumtaka Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Uzima na Ufufuo la jijini Dar, Josephat Gwajima amuachie mke wake, yaani Flora.

Flora Mbasha akiwa na mumewe Emmanuel Mbasha kwenye pozi la kimahaba. Akizungumza kwa machungu kwa njia ya simu kutokea alikojihifadhi huku akionesha waziwazi hasira juu ya hisia zake, Mbasha alisema: "Nimesika mke wangu baada ya matatizo yetu amehamia nyumbani kwa Gwajima. Nataka mumwambie Gwajima aniachie mke wangu, mbona ananifanyia hivyo?"

KINACHOMSHANGAZA
Mbasha ambaye mpaka sasa hajulikani alipo, aliendelea kudai kwamba kinachomshangaza zaidi ni kwamba, Flora amekiuka utamaduni wa Kiafrika, kwamba kama mke na mume wamegombana kiasi cha kushindwa kuishi nyumba moja, mke anakwenda kwao lakini hilo la Flora kukimbilia kwa Gwajima ndilo la ajabu zaidi kwake.
"Kama kweli Flora ameshindwa kuishi nyumbani kwetu (Tabata -Kimanga) kwa nini asiende Morogoro kwa mama yake. Au kwa nini asirudi Mwanza kwenye chimbuko la familia ya mzee Moses Kulola?
"Yeye badala yake amechukuliwa na Gwajima na kwenda kuishi naye nyumbani kwake. Mimi sijapenda, sijapenda na sitapenda kamwe," alisema Mbasha. Mwimba Injili Bongo, Flora Mbasha, wakati akiongea na Uwazi mafichoni hotelini.

ATUHUMU MTOTO KULIPIWA ADA YA SHULE
Akiendelea kutoa la moyoni, Mbasha alituhumu kuwa mke wake kwa sasa ana pesa nyingi licha ya kwamba wakati matatizo ya yeye kutuhumiwa kubaka yanatokea na kuingia mitini alimwacha hana kitu.
Anasema: "Wakati matatizo yanatokea Flora nilimwacha mweupe. Mtoto wetu (Elizabeth) alitakiwa kupelekwa shule, kwa hiyo ina maana hakwenda.
"Sasa nasikia mtoto amelipiwa ada na anakwenda shule. Nani kamlipia ada mwanangu kama si Gwajima? Mimi naumia sana, kwa nini iwe hivyo? Kama Gwajima ameamua mke wangu kukaa kwake kwa ajili ya kumsaidia kipindi hiki cha matatizio ajue mimi sijapenda.
"Yeye Gwajima ana mke wake, najua hawezikusema kitu kwa sababu Gwajima ni kila kitu lakini sijapenda."

GWAJIMA SASA
Jumamosi iliyopita, Uwazi lilimtafuta Mchungaji Gwajima kwa njia ya simu ambapo alisema hataweza kuzungumza kwa sababu yupo Mikumi akielekea Dar.
Uwazi: "Sawa, lakini inadaiwa Flora yupo kwako. Hata jijini Dar habari zimeenea kwamba yupo kwako. Mbasha mwenyewe pia amesema mke wake yupo kwako. Unasemaje kuhusu hili?"
Gwajima: "Flora hakai kwangu na wala sijui alipo. Hao wanaosema anaishi kwangu si wa kweli. Hata mkija kwangu hamtamkuta Flora."

UWAZI LAMSAKA FLORA
Uwazi lilianza kuingia mitaani kumsaka mwimbaji huyo kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya kiintelejensia. Ilikuwa kazi kubwa sana iliyoanza saa mbili na nusu asubuhi ya Jumapili na ilipofika saa tano, Flora alipatikana kwenye hoteli moja (jina tunalo) iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam. Alikuwa akijiandaa kwenda kanisani ikabidi hekima zitumike ili aweze kutoa dakika ishirini tu za mahojiano ambapo alikubali.

KUMBE ULIANZA UGOMVI
Akizungumzia kuhusu ugomvi katika ndoa na tuhuma ambazo mumewe anadai kuhusika nazo, Flora alikuwa na haya ya kusema: "Mimi sina ugomvi na mume wangu Mbasha ninampenda sana ila ninamshangaa kutoa taarifa yetu ya ndani katika vyombo vya habari.
Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Uzima na Ufufuo la jijini Dar, Josephat Gwajima.
"Nimeshtushwa sana na kitendo hicho kwani kama ingekuwa ni ugomvi baina yake na mimi tungekaa chini na kuyamaliza kama wanandoa. Siamini kama njia hii anayoitumia italeta suluhu, bali itaendeleza matatizo."

KUHUSU MADAI YA UBAKAJI
"Nakumbuka ilikuwa asubuhi ya Ijumaa ya wiki mbili zilizopita, Ima (Emmanuel ) aliniambia nijiandae kwenda ofisini kwetu kuangalia shughuli, alinipitisha ofisini kisha yeye akarudi nyumbani.
"Baadaye alinipitia ofisini kurudi nyumbani. Nilimkuta binti mlalamikaji akiwa hana raha na hali siyo nzuri, nilimuuliza tatizo ni nini hakuniambia.
"Ilipofika Jumapili nilimwambia mume wangu twende kanisani lakini alikataa, nilimuomba ufunguo wa gari ili mimi niende na familia, akagoma. Ndipo ugomvi ulipoanzia, nilimuuliza umekuwaje? Mbona uko hivi? Au umechanganyikiwa? Alinijibu anataka aondoke aniache na familia. "Baadaye akabadilika, akasema hapana haiwezekani yeye akaondoka, bali mimi ndiyo niondoke."

ATISHIWA KUCHINJWA
"Nilimuomba tuwaite watu wazima ili waje kutupatanisha, akaniambia nikiondoka kwenda kutafuta watu atanichinja.
"Niliamua kuachana naye, nilimpigia simu rafiki yangu mmoja aje anipitie na gari kwenda kanisani, lakini huyo rafiki yangu alipita na kuniambia kuwa amepata dharura hivyo asingenipeleka kanisani.
"Nikamrudia mume wangu na kumwambia mbona kama umerogwa? Akasema ndiyo amerogwa, nikamwambia twende kanisani ukaombewe, akakataa. Matokeo yake akanikaba shingoni mpaka nikashindwa kuongea. Nikamwambia unaniua ndipo akaniachia.
"Nilichukua gari la watu na familia yangu tukaenda kanisani. Kufika kanisani nilimweleza Mchungaji Gwajima tatizo lililonipata, akaniambia nirudi tu nyumbani kama hali itakuwa mbaya ataangalia cha kufanya.
"Baada ya ibada nilimwambia mdogo wangu arudi nyumbani na watoto, mimi nikaenda kukaa mahali nikiwaza cha kufanya."

BINTI AMPIGIA SIMU
"Ilipofika kesho yake (Jumatatu) nikapigiwa simu na yule binti akidai anaondoka nyumbani kwa sababu shemeji yake amemdhalilisha sana. Nilimwambia asiondoke kuna mtu atakwenda kumchukua mchana kumleta nilipokuwa.
"Alipoletwa nilishangaa kumkuta katika hali ambayo hawezi kutembea sawasawa. Nikamuuliza vipi? Ndipo akanielezea jinsi mume wangu alivyomfanyia."

BINTI AENDA HOSPITALI
Flora aliendelea kusema kuwa, binti mwenyewe aliamua kwamba anakwenda hospitali kucheki afya. Akasindikizwa na mdogo wake Flora. Kule vipimo vilionesha kweli aliingiliwa kimwili. Madaktari walimshauri aende polisi.
"Ndipo akaenda polisi na kutoa maelezo na kuandikiwa faili ambapo mume wangu akawa anatafutwa.
"Mume wangu amekuwa akisambaza habari kwamba nina mwanaume sijui nani! Hicho kitu hakipo. Hata mwaka jana nilikwenda Uingereza lakini tulikuwa wote. "

KUHUSU KUWA NA PESA, MTOTO KULIPIWA ADA
Kuhusu madai kwamba mtoto amelipiwa ada, yeye hana pesa, Flora alisema: "Pale kanisani (Ufufuo na Uzima) waumini walipojua nina matatizo na mume wangu na sipo nyumbani, walipitisha harambee ambapo niliweza kupata shilingi milioni tisa ndiyo maana mtoto akaenda shule na mimi nikabaki na za matumizi maana kila kitu kuhusu akaunti ya benki anakijua mume wangu."

MBASHA AOMBA KESI IFUTWE
"Mume wangu aliniomba msamaha baada ya haya mambo kutokea, nimemsamehe. Aliniomba nifute kesi polisi, nikamwambia si mimi niliyepeleka kesi polisi. Mimi siwezi kumsaliti yeye, kwanza nampenda sana Mungu kisha yeye."

AKUTWA AMEVUA PETE YA NDOA
Uwazi lilimkuta Flora akiwa hana ile pete ya ndoa iliyozoeleka kuwepo kwenye kidole chake. Alipoulizwa alisema hakuna uhusiano wa pete kutokuwepo kidoleni na ugomvi.

FAMILIA YACHAFUKA
Mwimbaji huyo alikwenda mbele zaidi kwa kusema kwamba ugomvi kati yake na mume wake umesababisha familia kuchafuka maana umekuwa gumzo katika kila kona ya mtaa.

Comments