Featured Post

UBALOZI WA MAREKANI WAWAPIGA MSASA MABLOGGER TANZANIA


Mmiliki wa blogu ya MaendeleoVijijini, Daniel Mbega, akipokea cheti cha ushiriki kutoka kwa Bi. Ricci Shryock, mwezeshaji wa mafunzo ya Multimedia Journalism yaliyofanyika leo hii kwenye Ofisi za Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania jijini Dar es Salaam. (Picha zote na MOHAMED MVUMBAGU/UBALOZI WA MAREKANI)


LEO hii Machi 21, 2017, mablogger wa Tanzania wamepata wasaa wa kukutana na mwandishi mzoefu wa Marekani Bi. Ricci Shryock ambaye ni mtaalam wa masuala ya Uandishi Mtanzuko (Multimedia Journalism) na kupigwa msasa kuhusu namna bora ya kuendesha blogu.

Bi. Ricci, ambaye maskani yake yako Dakar, Senegal, ni mwandishi wa kujitegemea ambaye pamoja na kuandikia magazeti mbalimbali kama New York Times pamoja na kuripoti Sauti ya Amerika (VOA), ni mtaalam katika uandishi wa mitandao hasa kwa kutumia mitandao ya kijamii kama tovuti, instagram na mingineyo.


Katika mafunzo hayo ya takriban saa tatu yaliyoandaliwa na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania na kufanyika kwenye ofisi za ubalozi huo jijini Dar es Salaam, pamoja na mambo mengine, Bi. Ricci amewataka mablogger kuwa wabunifu kwa kuandika habari, picha na video za kwao ili kuweza kupata watembeleaji wengi.
 Washiriki wa mafunzo ya Multimedia Journalism wakimsikiliza mwezeshaji Bi. Ricci Shryock (picha ya chini kulia) akielezea masuala mbalimbali ya uandishi wa habari za mtandaoni ikiwa ni pamoja na namna ya kupiga picha nzuri na kuandaa video bora.


Amewaelekeza namna bora ya kutengeneza video pamoja na upigaji mzuri wa picha, huku akiwapa mbinu mbalimbali za kusambaza taarifa zao.

Hata hivyo, amewaasa mablogger hao kwamba, hawapaswi kuchukua ‘bahasha za khaki’ kwani hizo zinaminya uhuru wako kwa vile watakuwa wanaripoti habari kwa ‘shinikizo la fedha’ wanazopewa na wahusika.

“Jitahidini sana kuziepuka bahasha za khaki, kama mnataka kuingiza kipato kupitia blogu ni lazima muwe wabunifu, muandike habari za kwenu hasa (original) badala ya kuchukua mahali pengine, lakini kwa kuandika habari nzuri kutawafanya mpate watembeleaji wengi na hatimaye mnaweza kuwashawishi watangazaji kutangaza nanyi,” alisema.

Alisisitiza kwamba, kupokea bahasha za khaki ni kinyume na maadili ya habari, hivyo hawapaswi kuzikimbilia.
Akizungumza kwa niaba ya mablogger hao, Josephat Lukaza, ameushukuru Ubalozi wa Marekani kwa kuandaa mafunzo hayo huku akieleza kwamba yamewapanua uelewa na kwamba mambo mengi waliyojifunza watayafanyia kazi.
Hata hivyo, kwa niaba ya washiriki wenzake, ameuomba uongozi wa ubalozi huo kuangalia fursa zozote za kuwapatia mafunzo kwani dunia inabadilika na mambo mengi yanabadilika.

Comments