Featured Post

JENEZA KUTOKA HONG KONG - (SEHEMU YA 10)


Niliingia ofisini asubuhi iliyofuata mara tu baada yam shale wa saa kugonga saa tatu kamili. Nilikuta waandishi kadhaa wa magazeti wakiwa nje ya mlango wa ofisi yangu. Walitaka kujua wapi lilikokuwa siku nzima ya jana. Walikuwa wamejaribu kunitafuta ili kusikia maelezo yangu kuhusiana na habari ya mauaji na wakafadhaika baada ya kushindwa kunipata.

Niliwakaribisha ofisini kwangu na kuwaeleza kwamba jana kutwa nzima nilikuwa kwenye makao makuu ya polisi. Niliwaambia sikujua chochote za zaidi katika suala la mauaji kama walivyokuwa wao wanajjua, pengine nilijua kidogo zaidi kuliko wao. Hapana, sikuwa naelewa kwa nini mwanamke wa KKichina alikuwa amekuja ofisini kwangu majira kama yale wala sijui aliingiaje kwenye jengo hilo. Walitumia nusu saa wakiniuliza maswali, lakini walikuwa wanapoteza bure muda wao. Hatimaye, wakiwa wamekata tamaa, wakaondoka.
Niliangalia kwenye boksi la barua zangu na kukung’uta kila kitu kwenye ndoo ya uchafu. Kulikuwa na barua kutoka kwa mwanamke aliyekuwa akkiishi huko Palma Mountain ambaye alinitaka nimtafute mtu aliyemlisha mbwa wake sumu.
Nilikuwa nachapa barua yenye maneno ya busara nikimwambia kwamba nisingeweza kumsaidia kwa wakati huo kwa kuwa nilikuwa nimetingwa, mara nikasikia mlango ukigongwa.
Nikaitikia kwamba aingie.
Jay Wayde, jirani yangu wa mlango wa pili, akaingia. Alionekana amefadhaika kidogo alipotulia futi chache kutoka mezani kwangu.
“Samahani kama nitakusumbua?” alisema. “Kwa hakika hainihusu, lakini nilikuwa nauliza tu kama wameweza kumpata muuaji.”
Udadisi wake haukuweza kunishangaza. Alikuwa miongoni mwa wale ambao huwa hawahofii kujiingiza kwenye matatizo.
“Hapana,” Nikamwambia.
“Sidhani kama inasaidia,” alisema kwa masikitiko, “lakini unapolifikiria hili, nakumbuka nilisikia simu yako ikiita majira ya saa moja usiku. Iliita kwa muda kidogo. Hii ilikuwa baada yaw ewe kuondoka.”
“Simu yangu kila wakati inaita,” nikamjibu, “lakini asante. Pengine inaweza kusaidia. Nitamwambia Luteni Retnick.” Akaanza kuzikuna nywele zake fupi zilizokatwa kwa ustadi.
“Nilidhani . . . Namaanisha katika upelelezi wowote wa mauaji kila jambo dogo linaweza kuwa muhimu hadi itakapothibitishwa vinginevyo.” Akakosa utulivu. “Ni jambo la ajabu namna alivyoingia ofisini kwako, au siyo? Nahisi umekuwa wakati mgumu kwako.”
“Aliingia ofisini kwangu kwa sababu muuaji alimfungulia,” nikamjibu, “na haujawa wakati mgumu kwangu.”
“Sawa, ni vizuri kusikia hivyo. Wameweza kumtambua alikuwa nani?”
“Anaitwa Jo-An Jefferson na anatoka Hong Kong.”
“Jefferson?” Akasema kwa mshangao. “Namfahamu rafiki yangu anaitwa Herman Jefferson ambaye alihamia Hong Kong: ni rafiki yangu wa tangu enzi za shule.”
Nilikirudisha nyuma kiti change ili niiweke miguu yangu mezani.
“Keti chini,” nikamwambia. “Niambie kuhusu Herman Jefferson. Mwanamke wa Kichina alikuwa mkewe.”
Hilo likamshtua sana. Aliketi chini na kunikodolea macho.
“Mke wa Herman? Alioa Mchina?”
“Ndivyo inavyoonekana.”
“Sawa, nimekuwa mjinga!”
Nikasubiri, nikimtazama.
Alitafakari kwa muda, kisha akasema, “Siyo kwamba imenishtua. Nimesikia wanawake wa Kichina ni wazuri, lakini sidhani kama baba yake angeweza kuafiki.” Akakunja uso, akkitikisa kichwa. “Alikuwa anafanya nini hapa?”
“Amerudisha maiti ya mumewe ili izikwe.”
Akaganda.
“Unamaanisha Herman amekufa?”
“Wiki iliyopita. . . ajali ya gari.”
Alionyesha kuchanganyikiwa zaidi. Akaketi akiwa amekodoa macho, kana kwamba hakuamini alichokisikia.
“Herman . . . amekufa! Masikitiko,” alisema hatimaye. “Huu utakuwa mshtuko kwa baba yake.”
“Ninadhani hivyo. Ulikuwa unamfahamu vizuri?”
“Hapana. Tulisoma wote shule moja. Jamaa alikuwa mkorofi sana. Kila wakati alikuwa matatani: akiruka na wasichana, akiendesha gari kama kichaa, lakini nilimpenda. Unajua watoto walivyo. Nilimchukulia kama shujaa. Halafu baadaye, baada ya mimi kwenda chuoni, nikabadili mtazamo wangu dhidi yake. Alionekana kama hakui. Kila wakati alikuwa akilewa na kupigana na kusababisha matatizo makubwa. Nikaachana naye. Hatimaye, baba yake akamchoka na kumpeleka Mashariki ya Mbali. Nadhani ni miaka mitano iliyopita. Baba yake ana miradi yake kule.” Akaukunja mguu wake mmoja juu ya mwingine. “Kwahiyo akaona mwanamke wa Kichina. Hilo linashangaza zaidi.”
“Inatokea,” nikamweleza.
“Alikufa kwenye ajali ya gari? Daima alikuwa akipata ajali za gari. Ninashangaa aliweza kunusurika mara zote.” Aakanitazama. “Unajua kwangu mimi naona mkanganyiko. Kwa nini mwanamke huyu ameuawa?”
“Hicho ndicho kitu ambacho polisi wanajaribu kukitafuta.”
“Ni tatizo, au siyo? Nina maana, kwa nini alikuja hapa kukuona? Ni jambo la kushangaza, au siyo?”
Nikaanza kuchoshwa na maswali yake.
“Yeah,” nikamwambia. Kupitia ukutani, nikasikia simu ikiita ofisini kwake. Akainuka.
“Nimetelekeza biashara yangu na kupoteza muda wako,” alisema. “kama nitakumbuka chochote kuhusu Herman ambacho nadhani kitasaidia, nitakueleza.”
Nilimwambia nitashukuru na kumtazama akiondoka, huku akifunga mlango nyuma yake.
Nikazama zaidi kwenye kiti changu na kuanza kutafakari yale aliyonieleza. Nilikuwa bado nimeketi pale, dakika ishirini baadaye, nikiendelea kutafakari na nikiwa sifiki mahali popote wakati simu yangu ilipoita na kunishtua. Niliudaka mkonga haraka.
Itaendelea kesho...
 
 

Comments