Featured Post

FRIEDKIN CONSERVATION FUND YACHANGIA SARUJI MIFUKO 3000 NA MABATI 1000 SIMIYU

Mkurugenzi wa Friedkin Conservation Fund (FCF), Abdulkadir Mohamed (wa tatu kulia) akimkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (wa pili kulia) shehena ya mifuko 3000 ya saruji ikiwa ni jitihada za kampuni hiyo kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani Meatu. Kampuni hizo Mwiba Holdings na Tanzania Game Trackers pia zimekubali kusaidia mabati 1000 ikiwa ni msaada. Wengine ni viongozi mbalimbali walioshiriki katika tukio hilo.

Mkurugenzi wa Friedkin Conservation Fund (FCF), Pratik Patel akizungumza katika tukio la kampuni hiyo kukabidhi shehena ya mifuko 3000 ya saruji ikiwa ni jitihada za kampuni hiyo kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani Meatu. Kampuni hizo yaani Mwiba Holdings pamoja na Tanzania Game Trackers pia zimekubali kusaidia mabati 1000 kama msaada.

Mkurugenzi wa Friedkin Conservation Fund (FCF), Abdulkadir Mohamed (kulia) akimtamkia Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (kushoto) kuwa mbali na kampuni hiyo kutoa mifuko 3000 ya saruji kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani Meatu. Wataongeza msaada wa mabati 1000. Wengine ni Miss Universe Tanzania 2016/17, Jihan Dimack (wa pili kushoto) na Mkurugenzi wa FCF, Pratik Patel (wa pili kulia) wakishuhudia tukio hilo.

Na Mwandishi Wetu, Simiyu
KAMPUNI kitalii zilizo chini ya Friedkin Conservation Fund (FCF) Tanzania iliyowekeza katika pori la Makao wilayani Meatu na Maswa Mkoani Simiyu imechangia mifuko 3000 ya saruji na mabati na 1000 kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani humo.
Misaada hiyo yenye thamani ya zaidi ya sh milioni 70 imetolewa na kampuni hizo ikiwa ni kuunga mkono mkakati wa serikali ya awamu ya tano ya Rais Dk. John Magufuli kuendeleza elimu ya hasa katika maeneo ya wafugaji ambako kampuni hizo zinafanya shughuli za uwindaji wa kitalii.
Kampuni zilizokabidhi misaada hiyo juzi katika sherehe zilizofanyika mjini hapa ni pamoja na Mwiba Holdings na Tanzania Game Trackers ambazo kwa pamoja zimetoa saruji hiyo yenye thamani ya sh milioni 48 na mabati yakiwa na thamani ya sh milioni 25.
Vifaa hivyo vya ujenzi vitatumika kujenga vyumba vya madarasa na mabweni kwa ajili ya shule zitakazotumiwa na watoto wa jamii za wafugaji zinazoishi jirani na maeneo ya shughuli za uwindaji wa kitalii wilayani Meatu katika mkoa wa Simiyu.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (kushoto) akifurahia tamko la Mkurugenzi, Abdulkadir Mohamed (hayupo pichani) kuahidi kuongeza msaada wa mabati 1000 huku Miss Universe Tanzania 2016/17, Jihan Dimack akikabidhiwa kipaza sauti kurudia kauli ya neema za mabati 1000 toka FCF.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Meatu (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza katika hafla hiyo ya kukabidhi shehena ya mifuko 3000 ya saruji ikiwa ni jitihada za kampuni ya FCF kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani Meatu. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka pamoja na Miss Universe Tanzania 2016/17, Jihan Dimack.
Akizungumza kabla ya kumkabidhi mchango huo Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, wakati wa hafla iliyofanyikia katika viwanja vya stendi Mjini Mwanhnuzi, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo Abdulkadir Mohamed alisema kuwa mchango huo unatokana na kuanzishwa kwa mfuko uwekezaji katika pori hilo.
"Tunatoa msaada huo ikiwa ni kuunga mkono Serikali yetu ya awamu ya tano katika jitihada za kuimarisha sekta ya elimu nchini,na tumeanza kuwasaidia wananchi tunaoshirikiana nao katika shughuli za uhifadhi na huu ndio mwanzo wa kuendeleza ushirikiano huu ikiwa ni sehemu ya mchango wetu kwa jamii,” alisisitiza Mkurugenzi huyo
Alisema kuwa pamoja na kuchangia misaada hiyo,kampuni yake imekuwa ikitoa misaada katika vijiji tisa vinavyounda Jumuiya ya Hifadhi za Wanyama Pori Makao (WMA) na ranchi ya Mwiba hasa katika kusaidia uboreshaji wa huduma za jamii na hasa elimu.
“ Mpaka sasa Kampuni kupitia makampuni yake matatu tayari wamechangia kiasi cha sh Milioni 3000 kwa vijiji tisa pamoja na vingine 15 vinavyopakana pori hilo, ambapo shule, zahanati, pamoja na vituo vya maendeleo vimejsengwa katika vijiji hivyo kwa kushirikiana na halmashauri” Alisema Mohamed.
Aidha, aliongeza kuwa mchango huo umechangiwa na mafanikio mazuri ya shughuli za utalii zinazoendelea katika maeneo hayo na uwekezaji wa kampuni hiyo wilayani humo, huku akibainisha kuwa shughuli hizo zinazidi kupanda kila mwaka wilayani humo
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka akiongozana na wageni wake katika hafla hiyo.

Miss Universe Tanzania 2016/17, Jihan Dimack akijitambulisha katika hafla ya FCF kukabidhi shehena ya mifuko 3000 ya saruji ikiwa ni jitihada za kusaidia ujenzi wa shule za sekondari wilayani Meatu.
Mkurugenzi huyo aliahidi kuwa kutokana na kuimarika kwa shughuli hizo na kuwepo kwa mazingira mazuri ya uwekezaji,hasa ushirikiano wanaoupata kutoka kwa wananchi, hasa wavijiji vinavyopakana na pori hilo, wamepanga kuongeza uwekezaji wao kwa dola za kimarekani milioni 100.
Kwa upande wake Mbunge wa Viti maalum Mkoa (CCM) Leah Komanya alipongeza mchango wa mwekezaji huyo, huku akiunga mkono kwa kuchangia mabati 50 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni shule ya sekondari Makao.
“ niwaombe hawa wawekezaji wetu wasichangie kwenye vijiji hivyo tisa peke yake, bali wachangie hata kwenye kata nyingine za wilaya yetu ambayo ipo chini sana kielimu ili kila mwananchi atambue mchango wao, na niwapongeze kwa kuunga mkono ujenzi wa shule hasa mabweni kwa watoto wa kike” Alisema Komanya
Mkuu wa mkoa wa Simiyu, akizungumza kabla ya kupokea msaada huo, alimtaka Mkurugenzi huyo ambao alidai kuwa wamekuwa chanzo cha migogoro ya kila mara kati ya wananchi na kampuni hiyo ili kurejesha imani ya kuendelea kushirikiana na wawekezaji hao.
Mbali na hilo Mtaka alipongeza Kampuni hiyo kwa mchango wake, huku akielelekeza saruji hiyo pamoja na mabati vitumike kwa ajili ya kujenga mabweni katika shule za sekondari zinazopakana na pori hilo.
Mtaka aliwataka wawekezaji hao kuwa karibu na wananchi kwa kushirikiana na watendaji wa halmashauri na alimwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuwapatia kiwanja cha kujenga ofisi ili iweze kuratibu kwa karibu ushirikiano huo na wananchi.
Kwa sasa mgogoro uliodaiwa kuwapo kati ya mwekezaji huyo na wanakijiji wa Makao, umemalizika baada ya msuluhishi aliyeteuliwa na pande zote mbili, Jaji Thomas Mihayo, kutoa uamuzi hivi karibuni baada ya walalamikaji kushindwa kuwasilisha utetezi wao kwa wakati.
Hata hivyo, taarifa zimeeleza kwamba hali hiyo imetokana na kurejea kwa mahusiano kati ya pande hizo mbili na kuonekana njia bora zaidi ya kusuluhisha migogoro ni mazungumzo yasiyo na gharama zinazoweza kuigharimu serikali ya kijiji na wilaya.

Comments