- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega
MONICA Kiondo, mkazi wa Sinza jijini Dar es Salaam, yuko na
mfanyakazi wake akihangaika kumlazimisha sungura awanyonyeshe watoto huku jua la utosini
likiwaka.
“Mama yao hataki kuwanyonyesha, sasa naogopa wasije wakafa wote
kama wa kwanza ambao walikufa,” anasema.
Anaongeza: “Ni wiki sasa nawapigia watu walionifundisha na
kuniuzia sungura hawa ili wanipe msaada kama walivyoahidi, kila siku wanasema
wanakuja lakini hawaji, wakati mwingine wakiiona simu yangu wanaikata ama
hawapokei.”
Monica ni miongoni mwa wanajamii ambao wameamua kuingia kwenye
mradi wa ufugaji wa sungura ili kujiongezea kipato, ingawa hakuwa na uzoefu
wowote wa ufugaji wa wanyama hao wadogo wenye faida nyingi.
Anasema alishawishika kuingia kwenye ujasiriamali huo kwa vile ni
wanyama wasiogharimu muda wake mwingi lakini pia anahitaji kuongeza kipato
licha ya kuwa na ajira nyingine.
Pembeni ya banda la sungura lipo pia banda la kuku wa kienyeji wa
kila aina wanaokadiriwa kufikia 30 hivi.
“Ninapenda kufuga, nimeachana na ufugaji wa kuku wa nyama ambao
walikuwa wakinitia hasara sana nikaamua kufuga wa kienyeji na hawa sungura,”
anasema.
Anasema kwamba, licha ya kutafuta kipato cha ziada, kuingia kwake
kwenye ufugaji sungura kulitokana na matangazo ya kampuni moja ya uwakala (jina
linahifadhiwa) ambayo ilidai kwamba inatoa mafunzo, mbegu na mabanda kwa wakulima ikiwa ni pamoja na
kuwatafutia masoko, achilia mbali kusaidia kuwahudumia sungura hao.
Tofauti na alivyotegemea kwamba baada ya mafunzo angeweza
kuendelea mwenyewe na ufugaji huo, lakini kampuni hiyo licha ya kumuuzia
mabanda na sungura wa kuanzia 14 – majike 12 na madume wawili – kwa gharama ya
takriban Shs. 2 milioni, ilimsainisha mkataba wa miaka mitano kwa masharti
kwamba lazima chakula cha sungura anunue kwao pamoja na dawa za kuwatibu
wanyama hao.
Hata hivyo, kampuni hiyo hiyo kwa sasa imekwishapandisha bei
ambapo seti hizo mbili zinauzwa kwa Shs. 4 milioni, hii ikiwa inatokana na
mwamko wa wananchi katika ufugaji wa sungura.
“Walisema wangetoa wataalamu wao kuja kuwahudumia wanapokuwa na
matatizo, lakini lazima nilipe mimi gharama za wataalamu na dawa, huku
wakinizuia (kwa mujibu wa mkataba) kutafuta tiba za wanyama hawa sehemu yoyote.
“Lakini tayari nimeshapoteza sungura mkubwa mmoja na watoto nane
ambao walikufa kutokana na mama yao kugoma kuwanyonyesha, kwa vile sina uzoefu
na ufugaji huu, imekuwa ni hasara kubwa kwangu,” anasema.
Sharti jingine, kwa mujibu wa Monica, ni kwamba anawajibika
kuwauza sungura watoto wote kwenye kampuni hiyo ya uwakala pindi wanapofikisha
umri wa miezi minne na kwamba haruhusiwi kuwauza popote.
Sungura hao watoto, kwa mujibu wa Monica, wananunuliwa na kampuni
hiyo kwa uzito wakiwa hai (live weight) ambapo kilogramu moja wananunua kwa
Shs. 8,000.
Kwa mujibu wa mchanganuo wao ambao ndio kivutio cha wakulima wengi
kuingia kwenye biashara hiyo, wanasema katika umri wa miezi hiyo minne, sungura
anakuwa amefikisha uzito wa kilogramu 4, hivyo kwa bei ya Shs. 8,000 sungura
mmoja atanunuliwa kwa Shs. 32,000.
Kwamba ikiwa kila sungura atazaa watoto 6, na ikiwa utawazalisha
mara 6 pia kwa mwaka, maana yake kwa sungura 12 utakuwa na sungura watoto 432
ambao kwa Shs. 32,000 utapata Shs. 13,874,000 huku gharama zote zikiwemo za
matunzo zikiwa Shs. 3,456,000 na hivyo kukusanya faida ya Shs. 10,368,000.
“Faida inaonekana kubwa na inashawishi. Mwanzoni niliona kwamba
hiyo ni nafuu kwa sababu wanasema wao wana masoko na wanasafirisha kupeleka nje
ya nchi, hasa Uarabuni na China, ambako mahitaji ya nyama ni makubwa, lakini
kadiri ninavyoangalia naona nakula hasara,” anasema.
Hata hivyo, anasema uhalisi uko tofauti kwa vile katika umri wa
miezi minne sungura hao wanakuwa hawajafikisha uzito wa kilo 4, wengi wao
wakiwa na uzito wa kilo 1.5, tena waliotunzwa vizuri.
“Kinachoniumiza zaidi ni kwamba, tayari nimekwishaingia kwenye
mkataba ambao umenifunga, maana yake siwezi kuwazalisha hawa watoto hata kama
nataka waongezeke na kwa mujibu wa mkataba, nikitaka niongeze wengine, lazima
nikanunue seti nyingine mbili, achilia mbali kuzuiwa kuwauza mahali pengine
hata kama nitapata soko zuri zaidi,” anasema kwa masikitiko.
Kilio cha Monica kinaonekana kuwakumba wakulima wengi, siyo wa
jijini Dar es Salaam tu, bali katika mikoa mingi ambako wameamua kuingia kwenye
ufugaji wa sungura kupitia kwenye kampuni za uwakala.
Simon Marwa, mkazi wa Kivule jijini Dar es Salaam, ni miongoni mwa
wakulima ambao wamenaswa kwenye mitego ya mwakala hao wa ufugaji wa sungura,
ambapo anasema alishawishiwa kujiunga na kampuni moja (ambayo aligoma kuitaja
kwa sababu ya usalama wa kibiashara) baada ya kuambiwa kwamba wangepatiwa
sungura 10 kila mmoja pamoja na mabanda yake, chakula na utaalamu.
Anabainisha kwamba, kabla ya kupatiwa mafunzo, alilazimika kwenda
na barua ya mjumbe, vitambulisho mbalimbali pamoja na ada ya kiingilio ya Shs.
500,000 na kuaminishwa kwamba atapata fursa zote muhimu ikiwemo kuunganishwa
kwenye mifuko ya kijamii pamoja na kupatiwa bima ya afya.
Hata hivyo, licha ya kujiunga, aliambiwa kwamba ni lazima waunde
kikundi cha watu 50 ili wakidhi vigezo, jukumu ambalo aliambiwa ni lake
kuhakikisha anawashawishi watu mbalimbali wajiunge naye kwa vile wanachama
wengine tayari walikuwa kwenye vikundi.
“Hapa ndipo niliposhtuka, kwa sababu mwanzoni tuliambiwa tunapewa
mikopo ya sungura, sasa masharti ya kutafuta watu 49 yalikuwa mapya, na je,
kama sikuwapata itakuwaje?
“Halafu najaribu kuangalia, kampuni inasema inatupatia mkopo – au
inatudhamini mkopo kutoka benki ambao unalipwa kwa kuwauza sungura
watakaozaliwa – lakini hebu piga hesabu, kama tayari mpaka sasa wameshafikisha
wanachama milioni moja kama wanavyosema, kwa kukusanya kiingilio cha Shs.
500,000 kwa kila mwanachama maana yake wamekusanya jumla ya Shs. 500 milioni!
Sisi ndio tumewapatia mtaji… huu ni utapeli,” anasema.
Hofu nyingine anayodai kwamba ilimpata ni maelekezo kuwa hata kama
watapatiwa sungura hao, hawaruhusiwi kuwachukua kwenda kuwafuga majumbani mwao,
bali wanatakiwa kuwekwa mahali pamoja na mhusika atakuwa anakwenda tu
kuwaangalia baada ya kuonyeshwa banda lake.
“Inakuwaje huyo ni mtoto lakini unaambiwa huruhusiwi kumnyonyesha,
anakaa kwa jirani na wewe unakwenda kumwangalia tu? Halafu ninawezaje kuwa na
uhakika kama banda nitakaloonyeshwa ni langu mwenyewe na siyo kwamba linaweza
kuonyeshwa kwa mwingine? Nimepata mashaka makubwa na ninahisi biashara hii
imekwishaingiliwa na madalali na matapeli licha ya ukweli kwamba ufugaji huu ni
mzuri na wenye tija,” anafafanua.
Kwa upande wake, Michael Samia, mkulima na mkazi wa Mbezi jijini
Dar es Salaam, anasema yeye alishtuka mapema kuhusu masuala ya mikataba, lakini
kwa vile anafahamu kuwafuga wanyama hao, alilipia seti nne na kupewa mahitaji
yote huku akigoma kusaini mkataba.
“Mimi kazi yangu ya kwanza kunipatia fedha nilipokuwa mdogo ni
ufugaji wa sungura, hivi sasa ninajiandaa kustaafu nataka kazi yangu ya uzeeni
iwe sungura, kwa hiyo sikwenda pale kwa kubahatisha, nimedhamiria kufuga
kibiashara.
“Walinifuata hapa nyumbani mwezi uliopita wakaja na mikataba yao,
lakini nikawaambia sina haja ya mkataba na mtu yeyote kwa sababu ninaweza
kujiendesha mwenyewe na kutafuta masoko… mkataba gani unaoingia na watu ambao
hawajakupa bure kitu chochote? Huo ni wizi na utapeli,” alisema kwa kujiamini.
Mkulima huyo ambaye kwa sasa anao sungura takriban 80, anasema
lengo lake kubwa ni kuwafuga kwa wingi shambani kwake Bagamoyo na kuanzisha
biadhara ya ‘sungura choma’ kama ilivyo kwa ‘mbuzi choma’.
Hata hivyo, anawaasa wakulima wenzake kujihadhari na madalali na
matapeli akionya kwamba, biashara hiyo hivi sasa imekwishaingiliwa na wajanja
kama ilivyokuwa ufugaji wa kware.
Kauli ya Samia inaungwa mkono na Exaud Mkufya, ambaye licha ya
kuwa mhanga wa ufugaji wa kware, anasema madalali na matapeli wameuvamia
ufugaji huo wa sungura na muda si mrefu unaweza kuonekana hauna maana.
Anasema kwamba, kupanda ghafla kwa bei za mbegu za sungura pamoja
na vitisho vinavyotolewa na baadhi ya madalali kwamba bila kupitia kwenye
kampuni mkulima hawezi kufanikiwa ni ishara tosha kuwa wapo ‘wapiga dili’
wanaotaka kujinufaisha kupitia kwa wakulima.
“Kuna kijana namfahamu kabisa, aliwahi kuniulizia wapi anaweza
kununua sungura, hawa wa kienyeji, nikamwelekeza mahali huko kijijini ambako
alikwenda na kununua kwa Shs. 2,000 kila mmoja, hivi sasa namuona kwenye
mitandao ya kijamii akiwauza sungura wale wale – ambao amewapachika majina ya
sungura wa kigeni – kwa bei ya Shs. 35,000!” anasema Exaud.
Anaongeza kwamba, biashara ya ufugaji wa kware nayo ilianza hivyo
hivyo, ambapo yeye alihamasika katika uuzaji wa mayai kwa maelezo kwamba bei ya
tray moja ni Shs. 30,000, lakini baada ya kutumia Shs. 8 milioni, alishindwa
kupata soko na kupata hasara ya ajabu.
Hata hivyo, amebainisha kwamba, ufugaji wa sungura ni kama wanyama
wengine na kuwataka wakulima wafuge si kwa kupewa ndoto za mafanikio ya haraka,
bali watambue faida na umuhimu wake.
Meshack Maganga ni mwalimu wa ujasiriamali anayeishi Iringa,
ambaye anabainisha kwamba, ufugaji wa sungura ni muhimu katika kuongeza kipato
bila kutumia muda mwingi.
Anasema kwamba, kwa uzoefu wake, sungura wala nyama yake haijawahi
kusafirishwa kutoka Tanzania kwenda nje kama baadhi ya madalali wanavyowahadaa
wananchi, bali wanyama hao wanaweza kufugwa kutokana na faida nyingi
walizonazo.
“Ufugaji wa sungura ni kama wa kuku, na nyama ya sungura ni nyeupe
kama ya kuku, samaki na nguruwe ambayo haina lehemu kutokana na kutokuwa na
mafuta mengi, hivyo inafaa sana kwa matumizi ya binadamu,” anasema na kuongeza
kwamba, ikiwa jamii itawafuga kwa kutambua umuhimu wa kwanza wa matumizi ya
familia, hiyo itaondoa wimbi la matapeli ambao daima wanatafuta fursa za
kujinufaisha.
Wataalamu wengi wa mifugo wanaeleza kwamba, licha ya nyama yake
kuwa na viinilishe vingi, lakini mkojo wa sungura una faida kwa kuwa unatumika
kwenye viwanda kutengeneza dawa za kuulia wadudu na unatumika pia kama mbolea
hai ya majimaji (organic fertilizer) na unaweza kunyunyiziwa moja kwa moja
kwenye miche kama kahawa, michunywa, miembe na korosho badala ya kutumia
kemikali za kuulia wadudu.
Aidha, kinyesi cha sungura kinafaa kuzalishia minyoo kwa ajili ya
kulishia kuku wa kienyeji pamoja na samaki, hivyo kama wanyama hao wanafugwa
katika kilimo mchanganyiko wanakuwa na manufaa makubwa.
Serikali imekuwa ikihamasisha wananchi kujikita katika miradi
endelevu ya ufugaji wa wanyama mbalimbali, wakiwemo sungura, ikiwa ni jitihada
za kuongeza uhakika wa chakula na kipato na hivyo kutokomeza umaskini na
kukabiliana na baa la njaa, kama inavyoelekezwa kwenye Dira ya Taifa ya
Maendeleo kuelekea mwaka 2025, Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupambana na Umaskini
(Mkukuta II).
Aidha, ufugaji huo wa sungura na wanyama wengine upo katika
utekelezaji wa malengo namba 1 na 2 ya Malengo Endelevu ya Dunia (SDG) yaliyopitishwa
na Umoja wa Mataifa Septemba 22, 2015 ambayo yanasisitiza kutokomeza umaskini
pamoja na kuongeza uhakika wa chakula.
Katika kipindi hiki ambacho serikali inahimiza kilimo na ufugaji
endelevu wenye manufaa, taasisi za umma kama Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
imefungua milango kwa vijana wajasiriamali kujifunza ufugaji mbalimbali,
ukiwemo wa sungura.
CHANZO:
FIKRAPEVU
Comments
Post a Comment