- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Mwandishi Maalum
KAMA Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema) Godbless
Lema alidhani kwamba kesi za lugha za uchochezi dhidi ya Rais John Magufuli
ambazo zinamkabili zinamuongezea umaarufu, inabidi ajifikirie upya.
Inaelezwa kwamba, kitendo
cha kuendelea kusota rumande bila dhamana kimeuweka ubunge wake rehani wake, kwa
mujibu wa wachambuzi wa masuala ya siasa.
Na ikiwa atabaini hilo, naamini anaweza
asinyooshe vidole viwili kila anapokwenda mahakamani, badala yake anapaswa
kunyoosha mikono yote juu kumuomba Mungu walau ajalie heri apate dhamana.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wanasema
kwamba, kwa mujibu wa taratibu za Bunge, huenda Jimbo la Arusha Mjini likatangazwa kuwa wazi baada ya kupita siku 90 ikiwa Lema ataendelea kubaki mahabusu.
“Hii ni kwa sababu kisheria wananchi wa
Arusha Mjini watakuwa hawana uwakilishi kutokana na mwakilishi wao kuwa
mahabusu,” amedokeza mhadhiri mmoja wa Chuo Kikuu cha Iringa (zamani Tumaini).
Jumatano, Januari 4, 2017 Mahakama Kuu
Kanda ya Arusha, ilishindwa kusikiliza rufani ya Jamhuri kupinga dhamana ya Lema,
baada ya mawakili wa Serikali kuwasilisha notisi ya kukata rufaa katika
Mahakama ya Rufaa wakipinga kusikilizwa kwa rufani hiyo.
Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Salma
Maghimbi alitarajiwa kutoa uamuzi juu ya rufaa ya Jamhuri iliyopinga Lema
kupatiwa dhamana Novemba 11 na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Arusha,
Desderi Kamugisha katika kesi namba 440 na 441/2016 za kutoa lugha za uchochezi
dhidi ya Rais Magufuli, ambapo siku hiyo Jamhuri iliwasilisha notisi ya mdomo.
Kwahiyo, baada ya Lema kufikishwa
mahakamani Januari 4, 2017 saa 3.25 asubuhi akiwa chini ya ulinzi mkali, huku
pia polisi wakiwa wametanda viwanja vya Mahakama Kuu ndani na nje sanjari na
gari moja la maji ya kuwasha, na baada ya mawakili wa pande zote kujitambulisha,
Jaji Maghimbi alisoma notisi ya Jamhuri kupeleka shauri hilo Mahakama ya Rufaa
na kueleza kufungwa kisheria kutoa uamuzi wa rufani hiyo.
Hatua hii inamaanisha kwamba, shauri hilo
sasa linahitaji kupangiwa tarehe na Jaji katika Mahakama ya Rufaa kwa ajili ya
kutajwa kwanza kabla ya kuanza kusikilizwa, jambo ambalo linaweza kushuhudia
Lema akiendelea kubaki mahabusu hadi mwishoni mwa Januari au mwanzoni mwa
Februari, 2017.
Lema (40) alikamatwa na polisi Novemba 3,
2016 akiwa Bungeni Dodoma na kupelekwa Arusha ambako alifunguliwa mashtaka.
Ikumbukwe pia Lema na mkewe, Neema Lema (33),
wana kesi nyingine ya kumtukana Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, ambapo
ilielezwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi jijini Arusha Agosti 20, 2016 kwamba,
wakitumia simu na mkewe walimtumia ujumbe wenye lugha ya matusi mkuu huyo wa
mkoa huku wakijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Ujumbe huo ulisema: “Karibu, tutakuthibiti kama Uarabuni wanavyothibiti mashoga.”
Kuhusu kesi ya uchochezi dhidi ya Rais
Magufuli, Lema alipewa dhamana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, lakini kabla
hakimu hajatoa masharti ya dhamana, upande wa Jamhuri ulisimama na kuweka
pingamizi la mdomo na mahakama ikakubaliana nao bila kutekeleza uamuzi wa
dhamana.
Katika kesi hizo, Lema alifikishwa
mahakamani kwa mara ya kwanza Novemba 8, 2016 na kusomewa mashtaka ya uchochezi
kwa viongozi wa serikali kwa maana ya kumtishia Mkuu wa Mkoa Mrisho Gambo pamoja
na kauli dhidi ya Rais Magufuli kwamba asipojirekebisha atafariki.
Kauli kwamba Rais Magufuli asipojirekebisha
atakufa aliitoa wakati akiwa Bungeni mjini Dodoma akichangia mjadala, ambapo
alisema kwamba ‘ameoteshwa’ na Mungu.
“Mimi nimeoteshwa, kwamba Rais Magufuli
asipojirekebisha atakufa,” alikaririwa akisema.
Lakini hofu ya kuupoteza ubunge kutokana na
kuendelea kubaki mahabusu kwa kipindi kirefu siyo tu itamwathiri Lema na Chadema,
bali hata serikali ambayo – ikiwa kweli hali hiyo itatokea – basi italazimika
kutumia fedha nyingi kuandaa uchaguzi mdogo.
Comments
Post a Comment