Featured Post

OMBI LA ZANZIBAR KUJIUNGA CAF KUJADILIWA


Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limepitisha ombi la Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) la Zanzibar kuwa mwanachama kamili wa CAF. Katika kikao chake cha Kamati ya Utendaji kilichoketi Januari 12, mwaka huu kiliamua kupitisha ombi hilo kuwa moja ya ajenda za Mkutano Mkuu wa CAF utakaofanyika Machi 16, 2017 huko Addis Ababa, Ethiopia.
Hivyo sasa Mkutano Mkuu huo utapiga kura na kama Zanzibar itapata idadi ya kura theluthi mbili yaani 2/3 ya wanachama wote, itatangazwa kuwa mwanachama mpya kamili wa CAF ambako atakuwa na haki mbalimbali za kama mwanachama.
Haki hizo ni pamoja na kushiriki michuano yote inayoandaliwa na kusimamiwa na CAF na hii ni pamoja na Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), fainali za Afrika Wanawake (AWCON), fainali za vijana (AFCON U17 na AFCON 20)na pia kuhudhuria mikutano mbalimbali ya CAF kama mwanachama kamili, kupokea na kusimamia kozi mbalimbali za CAF nakadhalika.
Pia itakuwa na fursa ya kupiga kura katika masuala muhimu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) tofauti na sasa ambako inapata fursa ya klabu zake zinazoshika nafasi ya juu katika Ligi Kuu ya Zanzibar kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho.
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa shukrani kwa Mheshimiwa Nape Nnauye – Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Jamhuri ya Muungano Tanzania pamoja na Mheshimiwa Rashid Ali Juma - Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi Zanizbar (SMZ) kwa kufanikisha hatua hiyo.
Pia, TFF inatoa shukrani kwa Rais wa Chama cha Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFA), Ravia Idarus Faina pamoja na Rais wa Heshima wa TFF Leodegar Chilla Tenga ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji wa CAF na Marais wa Heshima wa TFF Said Hamad El Maamry ambaye ni Mjumbe wa kudumu wa CAF na Mzee Muhiddin Ndolanga na wadau wote wa familia ya mpira wa miguu kwa mafanikio ya hatua hii.
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa sasa linajikita kwenye kampeni nzito ya kuomba kura za kutosha kuhakikisha kwamba Zanzibar inapata nafasi hiyo ya uanachama kamili.
Kadhalika Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia viongozi wake wako kwenye mchakato wa kumfanyia kampeni Rais wa Heshima wa TFF, Bw. Leodegar Chilla Tenga kuhakikisha anashinda nafasi ya Ujumbe wa Kamati ya Utendaji (Council) ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
Leodegar Tenga anawania nafasi hiyo kutoka nchi za Afrika zinazozungumza lugha ya Kiingereza akishindana na Rais wa zamani wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Zambia, Kalusha Bwalya na Kwesi Nyantakyi wa Ghana.
TFF inaomba Watanzania wote na wadau wote wa mpira wa miguu nchini kutuunga mkono katika juhudi na jitihada zetu za kuona Zanzibar inapata nafasi hiyo kadhalika Tenga anakuwa mjumbe kwenye baraza la ushauri huko FIFA.

Comments