Featured Post

NMB KUISAIDIA SIMIYU KATIKA MAPINDUZI YA KILIMO CHA UMWAGILIAJI




Dar Es Salaam 20 Jan 2017
BENKI ya NMB imekubali kutoa fedha kwa ajili ya kujenga 'skimu' kubwa ya mfano ya umwagiliaji katika Wilaya ya Busega mkoani Simiyu.
"Maji ni raslimali muhimu sana inayotoa uhakika wa kuvuna pamoja mbali ya pembejeo na uhifadhi', alisema Seif Ahmed, afisa mkuu upande wa biashara ya kilimo (Agribusiness).

"Mkuu wa Mkoa ninakupongeza wewe na timu yako kwa nia ya kuwaletea wananchi wa Simiyu maendeleo, " alisema na kuongeza, "Ninawahakikishia kuwa tutawapatia mkopo huo."
Ahmed aliahidi kufanya kazi pamoja na Mkoa wa Simiyu kuhakikisha mradi unaleta mabadiliko ndani ya jamii.
Afisa Mwakilishi wa Serikali katika NMB,  Domina Feruz, alisema kilimo cha umwagiliaji kitatoa uhakika wa mavuno na kuwapo uhakika wa marejesho ya mkopo na chakula muda wote wa mwaka", alisema Afisa huyo.

NMB KUUNGANISHA NGUVU
Alisema kuwa NMB iko tayari kuwaunganisha na mfadhili wa kimataifa ambaye atawapatia ufadhili mkubwa zaidi wa kifedha alimradi wanunue zana za kilimo kutoka kwenye kampuni hiyo.
Ahmed alisema MMB iko tayari kushirikiana na washirika wengine kama PASS, katika uandaaji wa mpango wa mradi pamoja na Serikali ya Mkoa wa Simiyu ili mradi uanze mara moja.
"Ukweli ni kwamba tukiendelea kusubiri mvua ili tuvune, ni vigumu kupiga hatua kubwa ya maendeleo na mabenki yanatoa fedha zao kwa woga wa kuzipoteza endapo mvua haitanyesha," alisema.
Ahmed aliongeza kuwa skimu ya umwagiliaji itawaunganisha wakulima sio tu kuwapa sauti moja bali pia kusafirisha mazao yao katika masoko ya nje ya nchi (export markets).
Tanzania, katika utawapa wa Mwalimu Nyerere, iliwahi kuwa na kampuni ya uuzaji wa mazao ya kilimo katika masoko ya kimataifa, GAPEX, ambayo ililiwezesha Taifa kupata fedha nyingi za kigeni.

KUSHIRIKI UCHIMBAJI MITARO
"Mimi pamoja na Kamati yangu ya Ulinzi na Usalama mtupangie Kata za kwenda kushiriki uchimbaji wa mitaro ya umwagiliaji, " alisema RC Mtaka.
RC Mtaka alisema Mh Rais Magufuli atawashangaa endapo wataomba chakula wakati wana maji tee pale Busega.
Mh Rais atatushangaa. Tumeikataa hii aibu Simiyu kuomba chakula wakati tuna maji tele Busega, nitashirikiana na wananchi mimi na Kamati yangu ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa ikiwa sehemu ya mchango wetu," alisema.

ENEO LA MRADI
Mradi wa kujenga miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji maji utafanyika katika Kata sita za Wilaya ya Busega zenye ukubwa wa hekta 1,500.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Busega, ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kiloleli, Vumi Magoti, ameshauri kuangalia uwezekano wa kupanua mradi kufikia hekta 6,000.
"Inawezekana kupata impact kubwa zaidi endapo tutaweza kuongeza eneo la mradi,"alisema.
Alisema wananchi wa Busega huwa wanachanga fedha kumlipa mtu awaletee mvua bila kuwa na uhakika, "huu mradi una uhakika wa kuleta maji, watahamasika kushiriki kuchimba mitaro," alisema Bw Magoti.

SKIMU KUONGEZA UZALISHAJI WA MPUNGA
Katika hotuba yake ya ufunguaji wa mkutano huo wa kazi,  RC Mtaka alisema, pamoja na mazao mengine, mradi unalenga kuzalisha zao la mpunga.

AWATAKA NMB KUFUNGUA TAWI BUSEGA
Aliwataka NMB kuharakisha kufungua tawi lao Wilayani Busega kabla mradi haujaanza ili kukabiliana na ongezeko la uhitaji wa huduma za kibenki wilayani humo hasa baada ya mradi kuanza.
Katika ziara yake, Mkuu huyo wa Mkoa wa Simiyu mapema jana asubuhi (19 Jan 2017) alikubaliwa kupata mkopo mkubwa kutoka Benki ya Maendeleo ya TIB.
Mkopo huo utasaidia miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kuongeza uzalishaji katika kiwanda cha chaki.
Miradi mwingine ni ujenzi wa Kiwanda cha uzalishaji wa vifaa vya hospitali vinavyotokana na mazao ya pamba na upimaji wa viwanja vya makazi, biashara na taasisi katika eneo la Mperani katika Halmashauri ya Bariadi.
RC Mtaka na ujumbe wake wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Simiyu wanaendelea na ziara iliyodhamiria kuujenga mkoa wao.
Kamati hiyo leo asubuhi itatembelea SUMA-JKT na wanategemea kufanya makubaliano kadhaa.

Comments