Featured Post

KUKOSEKANA UZIO SHULE YA MSINGI MCHANGANYIKO PONGWE KUNA WEZA KUSABABISHA HATARI KWA WANAFUNZI

Diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi akiangalia namna wanavyoandika wanafunzi wanaosoma shule ya Msingi ya Mchanganyika Kata ya Pongwe Jijini Tanga wakati wa ziara yake
 Diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi wa kwanza kushoto akisikiliza kero za wanafunzi hao.
 Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule ya Msingi Mchanganyiko ya Pongwe ya wanafuzi wasiosikia na wenye matatizo ya ngozi (Albino),Waziri Mfaume kulia akimuonyesha diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi maeneo yenye mapori yaliyozunguka shule hiyo ambayo ni hatari kwa usalama wa wanafunzi hao wakati wa ziara ya diwani huyo
WATOTO wenye ulemavu wa ngozi na wasioona wanaosoma shule ya msingi ya mchanganyiko ya Pongwe iliyopo Jijini Tanga wapo hatarini kuvamiwa na watu waovu na kuwafanyia vitendo vya kikatili kutokana kukosa uzio na sehemu kubwa kuzungukwa na pori ambalo ni hatari kwa usalama wao.

Shule hiyo ambayo inapokea watoto wenye matatizo hayo kutokana mikoa mbalimbali Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa ya kukosekana uzio huku sehemu kubwa ikipakana na pori jambo ambalo linaweza kusababisha hatari kwa ustawi wao kielimu.

Hayo yalibainishwa na Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule hiyo, Waziri Mfaume wakati wa ziara ya Diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi aliyoifanya kuangalia changamoto ambazo zinaikabili na kuona namna ya kuzipatia ufumbuzi.

Waziri alisema licha ya kufanya jitihada kubwa za kuanza ujenzi wa
uzio huo eneo la mbele ya shule hiyo lakini mpaka sasa hakuna msaada wowote ambao wamekuwa wakiupata ili kukabiliana na tatizo hilo ambalo linatishia usalama wa watoto hao.

Alisema awali changamoto hiyo ilikuwa eneo la mbele ya shule hiyo na kuona namna ya kulipatia ufumbuzi haraka ikiwa ni mkakati wa kuendelea kuwavutia wadau kuweza kusaidia lakini suala hilo mpaka sasa limeshindwa kupatiwa tiba.

 “Awali tuliona tuanze kujenga ujenzi wa fensi mbele ya shule hii
lengo likiwa kuwavuta wadau wengine ili kutusaidia lakini tukashindwa kujenga eneo ambalo ni pori kubwa na hivyo ni hatari kwa usalama wa wanafunzi “Alisema.

Aidha alisema licha ya jambo hilo lakini lingine ambalo limekuwa
kikwazo kwao kwenye suala la usalama ni walinzi ambao wanalinda shule hiyo ambao ni mgambo wanaotumia virungu  na mapango ambazo ni silaha ndogo kuweza kuwakabili wahalifu.

 “Ukiangalia kwenye shule hii tuna wanafunzi 87 ikiwa ni mchanganyiko wa walemavu wenye ualibinisimu,wasiosikia na wengine hawaoni hivyo ni hatari sana iwapo kutakuwa hakuna uzio na hawa wanatoka mikoa mbalimbali hapa”Alisema .

Awali akizungumza wakati wa ziara hiyo, Diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi alisema shule hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa ya uzio kwa sababu ipo kwenye mazingira magumu kwani imezungukwa na pori ambalo ni hatari kwao.

 “Hii changamoto  ni kubwa sana na hatari kwa usalama wa wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo hivyo niwaombe wadau wa elimu,viongozi na serikali kuona namna ya kusaidia jambo hilo kwa maendeleo ya taalumu za watoto hao “Alisema.

Hata hivyo alisema pia suala la uhaba wa madarasa kwenye shule hiyo atalichukua na kulifikisha kwenye kikao cha baraza la madiwani ili waweze kuona namna ya kuyashughulikia.

Naye kwa upande wake,Mwenyekiti wa Mtaa wa Pongwe,Hemed Kileo alisema kukosekana kwa uzito kwenye shule hiyo ni jambo la hatari hivyo kuziomba mamlaka husika kuona namna ya kulishughulikia.

Alisema shule hiyo ambayo ilianzishwa mwaka 1948 ikiwa na darasa la kwanza mpaka la sita ambayo walikuwa wakisoma wakoloni kabla ya mwaka 1957 kubadilishwa matumizi na kuwa shule ya bweni  na baadae ikiwa ni ya mchanganyiko .
Habari kwa Hisani ya Blog ya Kijamii ya Tanga Raha.

Comments