Featured Post

AFDB YAIPATIA TANZANIA MKOPO WA BILIONI 360 KWA AJILI YA KUIMARISHA TANESCO NA BENKI YA KILIMO NCHINI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw.  Doto James (kushoto) na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero wakisaini mikataba miwili ya mikopo yenye masharti nafuu yenye thamani ya shilingi Bilioni 360 kwa ajili ya kuongeza Ufanisi wa Tanesco na kuiongezea mtaji Benki ya Maendeleo ya Wakulima nchini-TADB, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw.  Doto James (kushoto) na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero(kulia), wakibadilishana mikataba ya Mkopo wa Sh. Bilioni 360, zitakazo kwenda katika Sekta ya Nishati ya Umeme na Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini-TADB, tukio lililofanyika makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dare salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James (wa tatu kulia) na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero(wa pili kulia), wakisaini mikataba miwili yenye thamani ya Sh. Bilioni 360 kwa ajili ya kutunisha mfuko wa bajeti Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/17 na kuendeleza kilimo kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo-AFDB, huku wakishuhudiwa na Mafisa wa pande zote mbili. Kushoto ni Kaimu Kamishna wa Fedha za Nje Mamelta Mutagwaba na wa pili kushoto ni  Naibu Kaibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Hamis Shaban, Makao Makuu ya Wizara hiyo Jijini Dar es salaam.
Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero (kulia), akizungumza baada ya kusaini Mikataba miwili ya Mikopo yenye masharti nafuu yenye thamani ya shilingi Bilioni 360, ambapo ameshauri fedha hizo zitumike kikamilifu katika maeneo husika ambayo ni Bajeti na kuendeleza kilimo. kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, jijini Dar es salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James (kushoto) akipiga makofi baada ya Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero (kulia), kuipongeza Serikali ya Tanzania kwa juhudi zake za maendeleo ya Uchumi hasa katika viwanda, baada ya kusaini mikataba miwili ya Sh. Bilioni 360, Makao Makuu ya Wizara hiyo Jijini Dar es salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (kushoto) akipeana mkono na aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero (kulia), baada ya kuagwa rasmi, katika Makao Makuu ya Wizara hiyo jijini Dar es salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (kushoto) akimkabidhi zawadi ya shukrani aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero (kulia) wakati akiagwa rasmi baada ya kupewa majukumu mengine ya Ukurugenzi Mkuu wa Benki ya AfDB kusini mwa Afrika, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) akizungumza na baadhi ya viongozi wa Serikali wakati wa kumuaga aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero, ambapo alimshukuru kwa jitihada zake katika kusaidia upatokanaji wa mikopo kwa ajili ya kutekeleza miradi ya Barabara, nishati, kilimo na elimu, Makao Makuu ya Wizara, Jijini Dar es salaam.
Baadhi ya Wakuu wa Idara na Taasisi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango wakiwa tayari kumuaga aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero baada ya kufanya kazi nchini kwa takribani miaka sita, Makao makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (kushoto) na aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero wakifurahia uhusiano mzuri uliopo kati ya Benki ya AfDB na Tanzania ambapo mpaka sasa miradi inayofadhiliwa na Benki hiyo inafikia thamani ya Dola za Marekani Bilioni 2, wakati wa kuagwa kwa Dkt. Kandiero, Makao Makuu ya Wizara, Jijini Dar es salaam.
Aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero akitoa maneno ya shukrani mbele ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (hayupo pichani), wakati akiagwa na Waziri huyo, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, jijini Dar es salaam.
(Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WFM)


Na Benny Mwaipaja-WFM, Dar es Salaam
BENKI ya Maendeleo ya Afrika-AfDB, imeipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu wa dola Milioni 164, karibu Shilingi Bilioni 360, kwaajili ya kuchangia Bajeti kuu ya Serikali katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2016/2017 pamoja na kuongeza mtaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini-TADB.
Mikataba miwili imesainiwa leo Jijini Dar es salaam kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James kwa niaba ya Serikali na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika anayeondoka Dkt. Tonia Kandielo.
Mkataba wa kwanza uliosainiwa ni kwa ajili ya kutunisha Mfuko Mkuu wa Serikali ambapo Benki hiyo imetoa dola za kimarekani milioni 70 sawa na tsh 154 bilioni ambazo zitaelekezwa kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa Shirika la Ugavi wa Umeme nchini-TANESCO.
Mkataba wa pili ni kwaajili ya kuongezea mtaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini-TADB wenye thamani ya dola Milioni 94 sawa na shilingi Bilioni 204 kwa ajili ya kuiongezea uwezo Benki hiyo kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa wakulima ili kuongeza mnyonyoro wa thamani kuanzia uzalishaji, uongezaji thamani na upatikanaji wa masoko ya uhakika ya mazao ya wakulima.
Uhai wa mikopo yote miwili utakuwa ni miaka 40 ambapo serikali itaanza kuilipa baada ya miaka kumi tangu kutolewa kwake, huku riba yake ikiwa chini ya asilimia 1.
Akizungumza baada ya kusainiwa kwa mkopo huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James, amesema mkopo huo umekuja wakati muafaka na utasaidia kukuza na kuimarisha TANESCO na kuendeleza kilimo nchini.
“Tanzania ni nchi iliyonufaika zaidi na mikopo yenye masharti nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika-AFDB ikilinganishwa na nchi nyingine yoyote iliyoko katika  Ukanda wa Kusini mwa Afrika” Alisema Bw. James.
Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa AFDB anayeondoka Dkt. Tonia Kandielo amesema kuwa hadi sasa Benki yake imeipatia Tanzania mkopo wenye thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 2, ambazo zimewekezwa kwenye miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya barabara, maji, nishati ya umeme, elimu na kilimo.
“Ninaamini kuwa hatua ya kuongeza mtaji katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo-TADB itachochea maendeleo ya kilimo nchini, na tunaahidi kuwa tutaendelea kuiwezesha zaidi siku zijazo” Alisema Dkt. Kandielo.
Kuhusu Sekta ya Nishati, Dkt. Kandielo amesema kuwa Benki yake imeona umuhimu wa kuliwezesha shirika hilo ili liweze kutoa huduma kwa ufanisi zaidi ili kuchochea uchumi wa Taifa.
“Mikopo hii inahusiana na vipaumbele tulivyoviweka kama Benki ambavyo viko katika malengo matano ambapo tunataka kuwekeza katika sekta ya nishati, uzalishaji wa chakula, kuendeleza viwanda, kuiunganisha Afrika na kuboresha maisha ya waafrika kwa ujumla" aliongeza Dkt. Kandielo
Wakati huo huo, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, amemuaga rasmi Dkt. Tonio Kandielo ambaye amehamishiwa nchini Afrika Kusini kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo atakaye simamia Kanda ya Kusini mwa Afrika.
Dkt. Mpango, amesifu jitihada kubwa zilizofanywa na mwana mama huyo katika kipindi cha miaka 6 aliyokuwepo hapa nchini ambapo ameweza kusimamia vizuri maslahi ya Tanzania katika Benki hiyo.
Amesema kuwa katika kipindi hicho Tanzania imeshuhudia maendeleo makubwa katika sekta za ujenzi wa miundombinu ya barabara, kilimo, maji na umeme, ambapo benki hiyo ilihakikisha kuwa miradi inatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa.
Amemwomba Mkurugenzi Mkuu huyo kuwezesha upatikanaji wa fedha kwaajili ya ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha kimataifa (Standard gauge) inayohitaji fedha nyingi,  kusimamia utekelezaji wa mradi wa umeme wa kikanda unaoanzia nchini Zambia, uboreshaji wa Bandari ya Itungi na Mbambabay.
Akijibu hoja za Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Dkt. Tonia Kandielo amesema kuwa anaamini mrithi wake ataendeleza mazuri aliyoyafanya na kwamba yeye binafsi atahakikisha anafuatilia kwa karibu miradi ambayo mikataba yake imesainiwa katika nyanja za maboresho ya sekta ya umeme na kilimo.

Comments