Featured Post

ASILIMIA 90 YA MAONI YA WADAU YAMEJUMUISHWA KWENYE MUSWADA WA HABARI


Na Georgina Misama-MAELEZO
Serikali imesema asilimia 90 ya maoni yaliyotolewa na wadau mbalimbali wa sekta ya habari nchini yanaohusu Muswada wa Huduma ya Habari wa mwaka 2016 yamechukuliwa na kujumuishwa kwenye muswada huo.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO ambaye pia ni msemaji wa serikali Bwn Hassan Abbas wakati wa kipindi cha TUONGEE ASUBUHI  kinachorushwa na kituo cha televisheni cha Star Tv kuhusu  Muswada wa Huduma ya Habari.
Bw. Abbas alisema kuwa moja kati ya jambo la msingi ambalo serikali iliyafanya wakati wa uandaaji wa muswada huo ni kuwakutanisha na kuwashirikisha wadau wa sekta ya habari kutoa maoni ili kuuboresha na kwa kuzingatia umuhimu ya maoni waliyoyatoa kwa kiasi kikubwa serikali imeyajumuisha kwenye muswada huo.
“Vitu ambavyo serikali isingeweza kuvipuuza ni maoni ya wadau wa sekta ya habari kuhusu muswada huu na nikuhakikishie kuwa asilimia 90 ya maoni yaliyotolewa na wadau yamejumuishwa na lengo ni moja tu kuja na sheria nzuri itakayoiongoza sekta ya habari na hatimaye kuiwezesha sekta hii iheshimike na iwe rasmi” alisema Bw Abbas
Aidha, Mkurugenzi Abbas alisema kuwa sekta ya habari ni sawa na sekta nyingine yeyote nchini, ina haki na wajibu wake na kuwashauri wadau kuangalia zaidi  upande wa haki zao zitakazopatikana kwenye mswada huo badala ya kulalamika ili kwa pamoja waweze kulivusha suala hili kwa ustawi wa sekta ya habari nchini.
Wakatihuo huo Bw. Abbas amewataka wadau wa sekta ya habari nchini kuendelea kujenga hoja hasa kwenye maeneo wanayotaka kuboreshwa kwenye muswada huu ili kuisaidia taaluma ya habari kukua na kuheshimika kama fani nyingine nchini.

Comments