- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega
FREEMAN
Aikaeli Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)
alikuwa anahamaisha wanachama wake wafanye maandamano Septemba Mosi, 2016 (ambayo yameahirishwa) kwa kile
anachokiita ni ‘Operesheni ya Kupambana na Udikteta Tanzania (Ukuta)’.
Anasema
Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli inaendeshwa kidikteta
hasa baada ya majaribio yao ya kuitikisa kwa kususia vikao vya Bunge kushindwa
huku serikali ikipiga marufuku mikutano yote ya siasa na kuwahamasisha wananchi
wafanye kazi za maendeleo.
Mbowe
amekwenda mbali zaidi baada ya kuwatisha viongozi wa chama hicho kwamba yeyote
ambaye hatashiriki maandamano aliyoyapanga yeye na kuwashawishi viongozi wenzake
wayakubali, basi atakuwa amejitoa kwenye uongozi kwa sababu ni ‘msaliti’.
Niliandika
hivi karibuni kwamba, lingekuwa jambo la busara sana kama Chadema wangeanza
kwanza na Operesheni ya Kupambana na Udikteta ndani ya Chadema (Ukucha) kabla
ya kuanzisha Ukuta, lakini baadhi ya watu walinikosoa.
Leo
nataka kueleza kwamba, ingawa viongozi wa Chadema wamekuwa na kawaida ya
kukanusha kwa nguvu zote huku wafuasi wao wasiopenda kujiongeza kwa kutafakari
mara mbili wakiunga mkono, lakini udikteta umeshamiri ndani ya chama hicho na
zaidi kuna usultani uliotamalaki.
Udikteta
na usultani ndani ya Chadema uliingia rasmi Agosti 13, 2006 pale kwenye Ukumbi
wa PTA, kwenye Viwanja vya Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa (Saba Saba)
wakati wa Mkutano Mkuu Maalum wa kupitisha Katiba mpya ya chama hicho.
Japokuwa
wapo wanachama wa Chadema waliowahi kuthubutu kulisemea hilo lakini wakaitwa
‘wasaliti’, ‘wanatumiwa’ na majina mengine kama hayo, lakini ukweli bado ungali
pale pale kwamba kuna udikteta na usultani, ambao daima huwa hauna kikomo cha
madaraka.
Demokrasia
ya kweli huonyesha ukomo hata wa madaraka, lakini Chadema ambayo inajinasibu
kwamba ni chama cha kidemokrasia haina ukomo wa madaraka kwenye katiba yake ya
mwaka 2006, kipengele ambacho kiliondolewa makusudi ili kujenga himaya ya
udikteta, tofauti na waasisi wa chama hicho – akina Edwin Mtei, Bob Makani na
wenzao walivyokuwa wameazimia.
Katiba
ya mwaka 2006 inaeleza tu kwamba muda wa uongozi utakuwa wa miaka mitano
mitano, lakini haielezi ukomo wa uongozi, kwamba mtu anaweza kushika nafasi
hiyo kwa vipindi vingapi.
Ndiyo
maana Mbowe ameendelea kukaa madarakani kwa kipindi cha tatu sasa, na huenda
akaendelea mpaka atakapoamua mwenyewe kung’atuka, kwa sababu katiba inamruhusu
au iko kimya kuhusu ukomo wa kuongoza. Huu ni usultani!
Sasa
wanapata wapi ujasiri wa kuikosoa CCM kwamba ina udikteta wakati chaguzi zake,
pamoja na kuwepo kwa mapungufu ya hapa na pale yanayowahusu watu binafsi,
zimeendelea kufanyika kidemokrasia na ukomo wa uongozi unajulikana?
Ibara ya 6.3.2 ya Katiba ya
Chadema ya 2006 kuhusu Muda wa Uongozi inasomeka hivi: (a) Kila uongozi uliochaguliwa au kuteuliwa wakati wa uchaguzi mkuu wa
Chama utashika wadhifa wake kwa kipindi cha miaka mitano; (b) Kiongozi
aliyechaguliwa au kuteuliwa baada ya uchaguzi mkuu atashika wadhifa wake hadi
kipindi cha uchaguzi mkuu kinachofuata; (c) Kiongozi aliyemaliza muda wa
uongozi ana haki ya kugombea na kuchaguliwa tena mradi awe anatimiza masharti
ya kuchaguliwa kuwa kiongozi; (d) Muda wa uongozi unaweza kufupishwa kama mamlaka
iliyochagua au kuteua itaamua hivyo; (e) Ibara hii itahusu pia viongozi wa
Mabaraza ya Vijana, Wanawake na Wazee wa CHADEMA.
Katika
umri wake wa miaka 24, Chadema imekwishakuwa na Katiba tatu – ile ya mwaka 1992
na ya 2004 pamoja na hii ya mwaka 2006, ambayo ilibadilishwa wakati wa
uenyekiti wa Mbowe mwenyewe kwa mara ya pili tangu alipoingia madarakani mwaka
2003 kuchukua nafasi ya Wakili Bob Makani, ambaye kama Mtei, aliongoza kwa
kipindi kimoja tu.
Katiba
za kwanza mbili – ya 1992 na 2004 – zilikuwa na kipengele cha ukomo wa madaraka
na hili lilizungumzwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson
Mwigamba, lakini akaitwa msaliti na kadhalika.
Mwigamba,
akitumia jina la Maskini Mkulima katika mtandao wa Jamii Forums hasa katika
kipindi cha mwaka 2013 wakati Zitto Kabwe akiwa anataka kuwania uenyekiti,
alisema: “Wakati tukifanya
mabadiliko ya katiba mwaka 2006 hatukugusa kipengele kinachomzuia kiongozi
kuongoza kwenye nafasi moja kwa zaidi ya vipindi viwili vya miaka mitano mitano.
Lakini wakati katiba inachapwa chini ya uongozi uliopo, kipengele hicho
kiliondolewa kinyemela. Mambo yanayotokea hivi leo yanaonyesha dhahiri
kipengele hicho kiliondolewa kwa makusudi kwa maslahi na kwa faida ya viongozi
waliopo madarakani kwa sasa. Hiki kinaweza kuchukuliwa kama kitendo kidogo
lakini kama viongozi wetu wanaweza kutokuwa waaminifu katika jambo kama hili,
ni dhahiri hawawezi kuaminika na wanaweza kufanya mambo mengine makubwa na yenye
athari zisizomithirika kwa chama.
“Ni muhimu wanachadema mkafahamu kwamba kitendo
cha kuondolewa kwa kipengele hicho ndicho kinacholeta mpasuko leo kwenye chama
unaotokana na Mbowe na Zitto kupigania uenyekiti. Kama kingekuwepo leo Mbowe
alikuwa anakatazwa na katiba kugombea kipindi cha tatu na hivyo vita iliyopo kati
yake na Zitto isingekuwepo na chama kingekuwa imara zaidi. Ni dhahiri Mbowe
aliondoa kipengele hicho kwa makusudi ili aweze kuendelea kugombea bila mwisho
na huu ni udikteta kama ule tu wa akina Lyatonga Mrema, John Cheyo na wengineo,
na wanachadema hatupaswi kuuruhusu si kwa Mbowe tu bali kwa yeyote atakayepata
nafasi ya kuwa mwenyekiti wa chama chetu.”
Mwigamba, ambaye alikuwa Katibu Mkuu mwanzilishi
wa Chama cha ACT-Wazalendo kabla ya kwenda masomoni Nairobi hivi karibuni,
alisema wakati huo kwamba, Katiba ya mwaka 2004 ipo wazi kabisa katika hoja ya
ukomo wa madaraka ambapo Ibara ya 6.3.2 kipengele cha (c) kinasema ifuatavyo; ''Leaders
who finish their term of office can be eligible for re-election provided he
qualifies but no leader can hold the
same post at the same level of the party structure for more than two terms.”
Licha ya ufafanuzi huo, bado viongozi wa chama hicho wakati huo
walisimama kidete kukanusha, huku aliyekuwa Katibu Mkuu, Dk. Wilbrod Slaa,
akinukuliwa ndani ya mtandao huo akisema: “WanaJF, Nataka kuwahakikishia
wanachadema wote, kuwa nilikuwepo nimekuwa ndani ya Chadema kuanzia 1998 ambapo
nilikuwa Makamu Mwenyekiti Bara, na baadaye 2003 Kaimu Katibu Mkuu, na hatimaye
Katibu Mkuu. Hivyo nimeshiriki kikamilifu kuandaa Katiba ya 2004 na pia Katiba
ya 2006 baada ya Rebranding ya Chama.
Nataka niwahakikishie wanachadema, hakuna toleo lolote la Katiba ndani ya
Chadema imeweka "muda wa Uongozi kuwa vipindi viwili tu", kuanzia
Katiba aliyoiasisi Mzee Mtei na kupitishwa na Mkutano Mkuu, wala si ya 2004 au
ya 2006. Kama kuna mtu anasema ilikuwepo na imeondolewa kinyemela, basi
aonyeshe kifungu hicho kwenye Katiba yeyote ile, au miniti za kikao chochote
kile.”
Lakini kauli hiyo ilipingana na kauli ya Naibu
Katibu Mkuu Bara, John Mnyika, ambaye naye katika mjadala huo alijitokeza na
kusema kwamba kipengele cha ukomo wa uongozi kilikuwemo kwenye Katiba ya 2004
lakini hakikuingizwa kwenye katiba ya 2006.
Mnyika alinukuliwa akisema: “Kuhusu Katiba, nina
nakala mango (hard copy) tu ya katiba
ya 2004, ilikuwa na kipengele cha vipindi viwili vya nafasi ile ile.
Hata hivyo, katiba mpya iliyoandikwa mwaka 2006 haikuwa na kipengele hicho.
Hivyo, sio kwamba kimeondolewa kinyemela ila hakikuwepo kwenye katiba mpya. JJ”
Hii maana yake ni kwamba, hata Dk. Slaa kama
Katibu Mkuu, alisema uongo kwamba hakukuwa na kipengele cha ukomo wa
madarakani, hii inaonekana kwamba kuna jambo ambalo limefichikia kuanzia katika
uandaaji wa katiba ya 2006 mpaka jinsi walivyoipitisha.
Taarifa zinaeleza kwamba, Mkutano Mkuu Maalum wa
mwaka 2006 ulikuwa na agenda nne tu ambazo ni Mosi, Kufungua Mkutano; Mbili,
Maboresho ya Katiba; Tatu, Maazimio juu ya Katiba Mpya; na Nne, Kufunga Kikao.
Inaelezwa kwamba, mkutano huo ulijadili vifungu
10 ambavyo vilifanyiwa marekebisho kutoka kwenye katiba ya 2004, lakini kati ya
vipengele hivyo, kipengele cha ukomo wa madaraka hakikuwemo na hii ni kusema
kuwa hoja hiyo haikuwa na marekebisho.
Wapo wafuasi wa Chadema, hususan ambao daima ni
watiifu kwa uongozi na hutetea hata kama kuna uozo, wanaodai kwamba katiba ya
sasa ni ya wanachama, lakini pia wapo baadhi yao ambao wanasema katiba hiyo
inaakisi matamanio ya viongozi waliotangulia, jambo ambalo linaleta mshangao.
Hoja
hii, ambayo imewahi kujadiliwa kwa mapana huko nyuma katika mitandao ya kijamii,
bado ina mantiki katika kipindi hiki, kwani ni Dhahiri usultani na udikteta upo
ndai ya chama hicho na ndiyo sababu kabla Zitto hajaondoka, kila alipotaka
kugombea aliwekewa vizingiti kwa kuwa waliamini angeweza kumng’oa Mbowe
madarakani.
Kwamba,
hata sasa akitokea mpinzani wa kweli ndani ya Chadema ataonekana ni adui na
kupewa sifa mbaya mbele ya wanachama na wananchi kwa ujumla kwa kuwa kumruhusu
mtu wa aina hiyo itakuwa ni kuukomesha usultani.
Leo
hii, kwa sababu ya nguvu kubwa waliyopewa viongozi na upungufu wa kikatiba
uliopo, lolote litakalosemwa na Mwenyekiti na kuvikwa kofia ya ‘Uamuzi wa
Kamati ya Utendaji’ litapigiwa makofi na wafuasi wao hata kama lina walakini,
kama tunavyoshuhudia suala la Ukuta.
Mbowe
ndiye Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, lakini kwa kofia yake ya
uenyekiti wa Chadema, wakati alipoinuka Bungeni na kususia vikao, wabunge wote
wa chama hicho waliamua kutii hata kama wao binafsi waliona hakuna sababu.
Ndiyo.
Inawezekana mtu anasukumwa na hisia zake binafsi, lakini kwa demokrasia feki
iliyopo ndani ya Chadema, hata wabunge nao wamekuwa wakifuata mkumbo huo kwa
kuhofia ‘kuanzisha bifu na uongozi’ japokuwa waliowatuma waende Bungeni ni
Watanzania wote bila kujali itikadi za vyama vyao.
Katika
Kata au Majimbo waliyoshinda, Chadema hawana idadi kubwa ya wanachama kama
waliowachagua, bali wengine walitoka katika vyama vingine ikiwemo CCM yenyewe,
hilo hawawezi kulikanusha.
Kwa
hiyo basi, ni vyema Chadema wakakomesha udikteta na usultani kwa kuweka ukomo
wa uongozi ndani ya katiba yao ili waonekane wanafuata demokrasia, kinyume
chake hawana tofauti na viongozi wengine wanaong’ang’ania kukaa madarakani kwa
kuwa tu ‘wamezichezea’ katiba zao.
Comments
In politics, what is logical is not always practical; what is practical is not always right; what is right is not always ethical; what is ethical is not always desired; and what is desired is not always logical!
ReplyDelete