Featured Post

SHIKAMOO MWANAMKE!

 Ndugu zangu,
Kweli ninaamini mwanamke ni sehemu ya mwanamume, yaani ametoka katika ubavu wa mwanamume ili awe msaidizi.
Hata hivyo, kazi ambazo mwanamke anazifanya ni nyingi na ngumu ingawa jamii imekuwa haioni ugumu wake na inachukulia kama ni za kawaida na lazima zifanywe na mwanamke.
Mwanamke ndiye ana majukumu yote ya kutunza familia - hata kama mwanamume ndiye anayetafuta riziki (japokuwa hivi sasa wote wanatafuta riziki). Mwanamke huyu ndiye anayejua watu wale nini, wanywe nini, walale wapi.


Pindi wanapojaliwa kupata watoto, mwanamke ndiye wa kwanza kujua kama mtoto mzima au anaumwa, hata kama mtoto huyo hajaanza kuongea.
Mwanamke ndiye anayejua mumewe avae nini anapokwenda mahali fulani - pamoja na kazi zake za kila siku, lazima afue nguo za mumewe pamoja na zile za ndani - hata kama naye anafanya kazi - lakini ni nadra sana kumkuta mwanamume akifua nguo za mkewe!
Mkienda wote shambani, mwanamke ndiye anayelima muda mrefu kuliko mwanamume. Mwanamume anaweza kuchelewa kufika shambani au mkiwa shambani anaweza kujifanya anashughulika na hili au lile au anakwenda kuongea na jirani wakati mwanamke anaendelea kulima.
Mkimaliza kulima, mwanamke atatafuta kuni na mboga huku akiwa na mtoto wake mgongoni, atajitwisha vitu hivyo wakati mwanamume anapuyanga. Akifika nyumbani mwanamke huyu atatafuta maji na kuanza kupika wakati mwanamume ameketi kivulini akiuliza "Yaani ugali bado tu?"
Na kwa asili mwanamke anaanza kuitunza familia tangu akiwa mdogo. Lazima ahakikishe wadogo zake hawasumbuliwi, wakiwa na kiu atawatafutia maji na kadhalika.

 
Hivi sasa mwanamke anafanya kazi ngumu ambazo zamani zilikuwa zikifanywa na mwanamume pekee. Tazama ndani ya majeshi yetu - yumo mwanamke! Angalia kwenye nafasi za uongozi - yupo mwanamke! Angalia shughuli za ujenzi - yupo mwanamke! Mwanamke huyu anabeba mizigo ambayo wanaume wengi hawawezi kuibeba.
Tena basi ukiona mwanamume ana mafanikio, basi ujue kuna mwanamke mwenye busara nyuma yake!
Tazama mwanamke alivyo mvumilivu kwa mumewe. Mwanamume hata kama ni mlevi, mwanamke atamsubiri mumewe, atamvua nguo na kumlaza kitandani huku yeye hajitambui. Wakati mwingine mwanamume huyu anaweza akawa amejitapikia na hata kujichafua kusikoelezeka, lakini mwanamke atapiga moyo konde na kumsafisha.
Mwanamke ataficha tabia mbaya ya mumewe na kumwagia sifa kwa majirani zake kwamba mumewe ni bora zaidi! Kama yupo anayeweza kumsema vibaya mumewe hadharani huyo ana matatizo.
Kwa kweli, MWANAMKE NI MAMA AMBAYE AMEAMUA KUISHI NA MTOTO MKUBWA WA KIUME ALIYESHINDIKANA KWA WAZAZI WAKE, HUKU YEYE AKIMWITA MUME MPENZI!
SHIKAMOO MWANAMKE!

Comments