- Get link
- Other Apps
Featured Post
EMORO HALISI NI HUYU HAPA TUMBA AYILA, MCHEZA SHOO WA PEPE KALLE ALIYETAMBA KWENYE FILAMU YA ‘MAISHA MATAMU!’
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Tumba Ayila 'Emoro'
Emoro akifanya vitu vyake stejini
Pepe Kalle na Emoro katika poicha ya jalada la albamu.
Na Daniel Mbega,
MaendeleoVijijini Blog
NENO au jina la ‘Emoro’ limekuwa maarufu sana Tanzania,
pengine na ukanda wote wa Afrika Mashariki. Ukisikia neno hilo linatajwa, basi
ujue kwamba watu wanazungumzia mtu au kitu kifupi sana – mbilikimo!
Lakini walio wengi wanatolea mfano wa Emoro bila hata kujua
asili yake – wengi, wa kizazi cha sasa na kilichotangulia kidogo.
Ni sahihi wanapofananisha mtu au kitu kifupi na ‘Emoro’,
lakini ukweli ni kwamba, Emoro mwenyewe ni mtu maarufu ambaye enzi zake
alitamba sana katika tasnia ya muziki na filamu, ingawa alicheza filamu moja
tu!
Wale vijana wenzangu wa zamani wanamkumbuka. Alikuwa mcheza
shoo wa bendi maarufu ya Empire Bakuba iliyokuwa ikiongozwa na jitu la
kimakwelini, jitu la miraba sita – Kabasele Yampanya au Pepe Kalle.
Wanakumbuka vituko vyake alipokuwa stejini jinsi alivyokuwa na
uwezo wa kukata nyonga na kubiduka sarakasi kadiri apendavyo, huku akicheza
kichwa chini miguu juu.
Naam. Jina lake halisi ni Tumba Ayila, na Emoro ni jina la
utani alilopewa enzi zake.
Mimi nilianza kumuona kupitia kwenye video mwaka 1988, siyo
akicheza muziki jukwaani, bali katika filamu moja matata ya La vie est belle,
au ‘Maisha Matamu’ na Waingereza wakatafsiri – ‘Life is beautiful’ au ‘Life is
rosy’.
Mhusika mkuu wa filamu hiyo alikuwa Jules Shungu Wembadia Pene
Kikumba, ambaye wengi walimfahamu kama Papa Wemba. Lakini humo ndani kuna watu
wengine maarufu, akiwemo Pepe Kalle ambaye alicheza kama rafiki mwanamuziki wa
Papa Wemba aliyecheza kama Kourou, kijana kutoka kijijini aliyekwenda mjini
Kinshasa kutafuta maisha ya muziki.
Ukiitazama unaweza kusema ni kama zile filamu mfulilizo za The
gods must be crazy kwa jinsi ilivyo na vituko humo ndani.
Tumba Ayila, au Emoro, ndiye anayetamka mara nyingi maneno ya
La vie est belle ndani ya filamu hiyo, ambamo Papa Wemba, akicheza kama Kourou,
alijua kwamba akienda mjini atakuta maisha rahisi tu, lakini badala yake
ikabidi apitie changamoto nyingi hadi kufanikiwa.
Emoro huyu, akicheza pamoja na rapa mashuhuri wa Empire
Bakuba, Bileku Jean-Pierre Matonet ambaye alifahamika zaidi kama Bileku Mpasi
au Djouna Mumbafu, ndio waliofanikiwa kubadilisha shoo za bendi hiyo ambazo
ziligeuka kuwa kama maonyesho ya sarakasi.
Ukitazama video za albamu za Livre d'or, Dans Masassi calculé
à Abidjan, Adieu Dr. Nico, Obosini Kisomele, Allah, Bakuba Show, Sombokila,
Blanche neige, Nzoto ya chance / 8000 km, maarufu kama Kwassa Kwassa, Joe
Dikando, Pon Moun Paka Bougé, Moyibi, Ya Moseka de l'Empire Bakuba, Show times,
Cé Chalé Carnaval, Feux d'artifice na nyinginezo utaona utukutu wa Emoro ambaye
aliwaacha mashabiki wengi midomo wazi.
Empire Bakuba wakati huo ilikuwa na wanamuziki mahiri kama
Jojo Ikomo, Dilu Walumona na Matolu Dode ambaye wengi walimfahamu kama Papy
Tex. Hawa pamoja na Pepe Kalle ndio walioanzisha Empire Bakuba mwaka 1972.
Lakini pia walikuwepo wapiga solo mahiri kama Kinanga Nanzao maarufu kama
‘Boeing 737’ na Ebuya Lange au ‘Doris’.
Wakati Empire Bakuba ilipokuja nchini Tanzania kwa mara ya
kwanza mwaka mwaka 1990, nakumbuka nilikuwa shule pale Pugu sekondari. Siku na
fedha ya kiingilio kwenye onyesho lake la Uwanja wa Taifa (sasa Uwanja wa
Uhuru) zaidi ya nauli yangu shilingi 10 na shilingi 5 ya barafu. Usishangae,
wakati huo nauli ya mwanafunzi ilikuwa shilingi 5 tu, hivyo nilikuwa na nauli
ya kwenda na kurudi.
Nilikwenda mapema kama saa tatu nilikuwa nimefika pale. Ingawa
wakati huo bendi hiyo ilikuwa ikitamba na albamu yake ya Pon Moun Paka Bougé,
lakini kama ilivyokuwa kwa mashabiki kwa maelfu waliofurika uwanjani siku hiyo
– ninaamini – lengo langu lilikuwa kuangalia vitu viwili tu – kumuona Pepe
Kalle mwenye urefu wa meta 2.1 na uzani wa takriban kilogramu 150 na dansa
mbilikimo – Tumba Ayila ‘Emoro’!
Niliingia uwanjani, lakini usiniulize niliingiaje, maana
watoto wa kutoka shamba nao wana mbinu nyingi kama hao watoto wa mjini tu.
Nakumbuka wakati wa ziara hiyo ambayo iliratibiwa na kampuni
ya African Music Promoters ya homeboy Anania Sangula ambaye ndiye aliyewaleta
wanamuziki wengi wa Zaire kama Tshala Muana na wengine, ilibidi Emoro atafutiwe
mbilikimo mwenzake wa hapa nchini, nakumbuka jina lake aliitwa Khadija kutoka
Dodoma, ambaye naye alikuwa na uwezo wa kucheza vilivyo jukwaani.
Pepe Kalle aligundua umuhimu wa kumtafuta patna wa Emoro, na
ndipo alipompata Jolie Bébé.
Hata hivyo, miaka miwili baada ya ziara hiyo, yaani mwaka 1992,
Emoro akafariki ghafla wakati bendi ikiwa ziarani Ulaya. Pepe Kalle alilia mno
kwa kifo cha kipenzi chake Emoro na akamtungia albamu maalumu iitwayo Hommage à Emoro.
Baada ya hapo, Jolie Bébé akaongezewa madansa wengine wawili
mbilikimo, mtukutu Dokolos na mbonge nyanya Dominique Mabwa, ambaye uchezaji
wake ulikuwa ukiwaacha wengi hoi.
Mbilikimo wa Congo
Emoro alitokea katika jamii ya Mbilikimo wa Congo (Congo
Pygmies) katika kabila la Bayaka, magharibi mwa Congo DRC.
Mbilikimo hao wa Congo (ambao pia wanajulikana kama Bambenga
au Bayaka) wanaishi katika jamii mbalimbali katika nchi za Rwanda, Burundi,
Congo DRC, Afrika ya Kati, Cameroon, Guinea ya Ikweta, Gabon, Jamhuri ya Congo,
Angola, Botswana, Namibia na Zambia.
Jamii nyingi za Mbilikimo ni wawindaji na walaji matunda
wanaotegemea mazao ya misitu yao. Hata hivyo, wao siyo wakulima, lakini hununua
chakula kutoka kwa wakulima, kwani wanategemea pia mazao ya chakula ndiyo maana
hawawezi kuishi ndani ya misitu ambako hakuna shughuli za kilimo.
Takwimu zinaonyesha kwamba, idadi ya mbilikimo hao ni kati ya
250,000 na 600,000 ambao wanaishi katika misitu ya Congo, ingawa jamii ya
Mbilikimo wa Twamay wanaishi kwenye uwanda wazi na kwenye jangwa.
Mbilikimo wako katika jamii mbalimbali, lakini zinazojulikana
zaidi ni Wambenga (Waka au Wabaka) walioko kusini mwa Bonde la Congo, ambao
wanaongea Kibantu na Kiubangi; Wambuti (waefe) wanaoishi kwenye Misitu Minene
ya Ituri ambao wanaongea Kibantu na lugha nyingine za Sudan ya Kati, Watwa
wanaopatikana katika Maziwa Makuu hasa Burundi na Rwanda ambao wanaongea
Kirundi na Kiga.
Naam. Huyo ndiye Emoro halisi na kwa ufupi tu nimeeleza
historia ya Mbilikimo wa Congo.
Mwenyezi Mungu ampumzishe kwa amani Tumba Ayila Emoro. AMEN.
Comments
Aisee umenikumbusha mbali sana. Wakati nasoma hii makala akili yangu ilihama kabisa nyuma miaka hiyo. Aisee hadi nasisimka aisee.
ReplyDeleteTunahitaji kuweka kumbukumbu, mambo mengi yanasahaulika kutokana na sayansi na teknolojia
DeleteMshana, mambo mengi ya zamani yanasahaulika haraka, hatuweki kumbukumbu na kadiri ulimwengu wa sayansi na teknolojia unavyozidi kusonga tutayasahau mengi.
ReplyDelete